Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumanne, 29 Januari 2019

TAMKO LA MHE. UMMY MWALIMU (MB) KATIKA KUADHIMISHA SIKU YA UKOMA DUNIANI


TAMKO LA MHE. UMMY MWALIMU (MB) WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO KATIKA KUADHIMISHA SIKU YA UKOMA DUNIANI TAREHE 27/01/2019
KIGAMBONI, DAR ES SALAAM

Ndugu wanahabari,
Siku ya Ukoma Duniani huadhimishwa ulimwenguni kote kila Jumapili ya mwisho ya mwezi Januari. Kwa mwaka huu, siku hii itaadhimishwa tarehe 27 Januari, 2019. 

Lengo kuu la maadhimisho haya ni kukumbusha umma wa watanzania juu ya ugonjwa huu. Ni dhahiri kuwa ugonjwa wa Ukoma umekuwa ukiogopwa sana katika jamii yetu toka enzi na enzi hasa kutokana na ukweli kwamba unasababisha ulemavu wa kudumu mwilini na kufanya waathirika kuwa tegemezi na kutothaminiwa.

Sanjali na madhimisho haya, hapa Tanzania tunaadhimisha miaka 60 ya uwepo wa Shirika la Ujerumani linaloshughulikia masuala ya Kifua kikuu na Ukoma (GLRA). Shirika hili limekuwa mstari wa mbele katika kuisaidia serikali kuhakikisha Ukoma unatokomezwa kwa kufadhili shughuli mbali mbali ikiwa ni pamoja na kutoa vyombo vya usafiri kwa waratibu wa Kifua kikuu na Ukoma nchi nzima.



Ndugu wanahabari,
Siku ya Ukoma Duniani inatupa fursa ya kutathmini mwelekeo wa jitihada zetu nchini na zile za kimataifa katika kupambana na ugonjwa huu. Kauli mbiu katika maadhimisho ya mwaka huu ni “TUTOKOMEZE UBAGUZI, UNYANYAPAA NA CHUKI DHIDI YA WAATHIRIKA WA UKOMA”. Ni kweli kuwa waathirika wengi wa Ukoma wananyanyapaliwa na kubaguliwa katika maeneo mengi, takriban asilimia 50 ya wagonjwa wa Ukoma hupatwa na sonona na huishi maisha ya huzuni na wasi wasi mkubwa. Haya yote husababishwa na mtazamo hasi wa jamii dhidi ya waathirika wa ugonjwa wa Ukoma. Mtazamo huu hasi ndio kikwazo kikubwa katika vita ya kutokomeza Ukoma duniani na hapa nchini. 

Serikali, wadau na wananchi wote wanahimizwa kuungana na kuongeza nguvu katika kupinga matukio vyote vya ubaguzi na unyanyapaa ikiwa ni pamoja na kuhakikisha hakuna sheria kandamizi kwa watu walioathirika na ugonjwa wa Ukoma. Kwa kufanya kazi pamoja na kupinga kwa nguvu zote vitendo hivi itatusaidia kupiga hatua mbele kuelekea kutokomeza Ukoma.

Ndugu wanahabari,
Pamoja na kwamba nchi yetu ilifikia viwango vya utokomezaji wa Ukoma kitaifa mnamo mwaka 2006 kwa kiwango cha chini ya mgonjwa 1 kati ya watu 10,000, Ukoma bado unaendelea kuwa tatizo la kiafya miongoni mwa jamii nchini kwetu. Kwa mujibu wa takwimu za Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua kikuu na Ukoma (NTLP) za mwaka 2017, jumla ya wagonjwa wapya 1,933 waligunduliwa na hivyo kufanya kiwango cha ugunduzi kuwa watu 4 kwa kila watu 100,000. Takwimu hizi zinaifanya Tanzania kuendelea kuwa miongoni mwa nchi 22 zenye wagonjwa wengi wa Ukoma duniani nchi nyingien ni pamoja na India, Indonesia, Brazil, Ethiopia, Msumbiji, Nigeria na DRC Kongo. Hivi sasa bado kuna mikoa kumi ambayo inagundua wagonjwa wapya wa Ukoma wengi zaidi kila mwaka na kuchangia karibia 80% ya wagonjwa wote. Mikoa hiyo ni pamoja na: Lindi, Rukwa, Mtwara, Morogoro, Pwani; Tanga, Geita, Dodoma, Tabora na Kigoma. 

Aidha, bado zipo wilaya 20 ambazo kiwango cha ukubwa wa tatizo la Ukoma lipo juu sana na bado hazijafikia lengo la utokomezaji, nazo ni Liwale,  Lindi vijijini, Nachingwea, Ruangwa, Nanyumbu, Masasi mjini,  Pangani, Mkinga, Korogwe,  Mvomero, Kilombero, Morogoro vijijini, Ulanga, Shinyanga manispaa,  Mafia, Rufiji, Kilwa, Chato, Nkasi,  na Mpanda. 

Ndugu wanahabari,  
Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto kwa kushirikiana na Wizara ya TAMISEMI inatekeleza shughuli mbali mbali katika kuhakikisha Ukoma unatokomezwa  kabisa. Shughuli hizo ni pamoja na : 
Kuhakikisha dawa za kutibu Ukoma zinaendelea kupatikana wakati wote na bila malipo yoyote, 
Kuendesha kampeni za uibuaji wa wagonjwa wapya ngazi ya jamii kwa kuwashirikisha watoa huduma ngazi ya jamii ( Leprosy Elimination Campaigns) hasa katika wilaya zenye kiwango kikubwa cha wagonjwa wa Ukoma,
Kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu dalili za Ukoma na upatikanaji wa huduma kwa kutumia vifaa vya habari, Elimu na mawasiliano kama vile vipeperushi, mabango na mikanda ya video, 
Utekelezaji wa shughuli za kuzuia ulemavu unaotokana na Ukoma ikiwemo kutathmini wagonjwa wenye vidonda, kufanya upasuaji maalum, huduma za kitaalam za macho na utoaji wa viungo bandia pamoja na viatu maalum.

Ndugu wanahabari,
Pamoja na hatua zinazochukuliwa na serikali na mafanikio zipo changamoto kubwa mbili ambazo ni jamii kuendelea kushikilia imani potofu juu ya Ukoma kuwa ni ugonjwa wa kurithi au kulogwa; na wagonjwa kuchelewa kujitokeza kupata matibabu hadi wanapopata ulemavu. Ukoma ni ugonjwa wa kuambukizwa unaosababishwa na vimelea vinavyoshambulia mishipa ya fahamu na huambukizwa kwa njia ya hewa pekee.

Nitoe rai kwa jamii, wazazi na walezi kuwa sote tujenge tabia ya kuchunguza miili yetu na ya watoto wetu. Endapo utaona mojawapo ya dalili za Ukoma ambazo ni baka au mabaka mwilini yenye rangi ya shaba na hayana hisia, vijinudu kwenye ngozi au mishipa ya fahamu kuvimba. Dalili nyingine ni ganzi kwenye mikono na miguu. Unashauriwa kwenda kwenye kituo cha tiba kilicho karibu nawe kwa uchunguzi bila kuchelewa. Hii itawawezesha wataalam wa afya kuchunguza na kubainisha kama mgonjwa ana Ukoma ili apate tiba sahihi mapema na hivyo kuzuia maambukizi na ulemavu wa kudumu unaoweza kuzuilika.

Ugonjwa wa Ukoma unatibika. Mgonjwa aliyeanza tiba hawezi kuambukiza mtu mwingine na hivyo hakuna sababu ya kumtenga na anaweza kuendelea na shughuli za kawaida za maisha.

Tiba ya Ukoma inapatikana nchini kote na hutolewa bila malipo kwa wagonjwa wote.
Nirudie tena kuwa, pale tunapoona mabadiliko yoyote yanajitokeza kwemye miili yetu twende mapema katika vituo vyetu vya huduma kuchunguzwa ili tupate matibabu stahili. 

Ndugu wanahabari,
Aidha, napenda kuwashukuru watoa huduma katika vituo vya huduma za afya kote nchini kwa juhudi wanazofanya kila siku kuhakikisha ugonjwa huu si tatizo la kiafya tena nchini. Pia wanahabari kwa kuendelea kuendelea kuelimisha jamii kuhusu magonjwa mbalimbali.

Pia nachukua nafasi hii kwa niaba ya serikali ya awamu ya tano ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kuyashukuru mashirika mbali mbali ya ndani na nje yanayounga mkono juhudi zetu za kutokomeza Ukoma nchini kama vile Norvatis Foundation ya Uswisi, Germany Leprosy and Tuberculosis Relief Association (GLRA) ya Ujerumani, Nippon Foundation chini ya  Sasakawa Memorial Health Initiative ya Japani na Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa michango yao ya hali na mali katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa Ukoma hapa nchini Tanzania. 
“TUTOKOMEZE UBAGUZI, UNYANYAPAA NA CHUKI DHIDI YA WAATHIRIKA WA UKOMA”.


Asanteni kwa kunisikiliza!



0 on: "TAMKO LA MHE. UMMY MWALIMU (MB) KATIKA KUADHIMISHA SIKU YA UKOMA DUNIANI"