Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Afya. Onyesha machapisho yote
Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Afya. Onyesha machapisho yote

Jumatano, 19 Agosti 2020

HUDUMA ZA AFYA YA UZAZI NA MTOTO ZIMEENDELEA KUIMARIKA NCHINI

- Hakuna maoni




 


 Na WAJMW-Dodoma

 Huduma za Afya kwa mama na mtoto zimeendelea kuimarika nchini baada ya uboreshwaji wa huduma za afya nchini katika kipindi cha miaka mitano toka 2015 hadi 2020.

 Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakati akiongea na wadau mbalimbali wa maendeleo katika sekta ya afya Pamoja na watumishi mbalimbali wa Wizara hiyo waliokutana jijini Dodoma.

 Waziri Ummy amesema kuimarika kwa huduma hizo zimetokana na kuimarishwa miundombinu ikiwa ni pamoja na kuongezeka vituo vya kutolea huduma 1797 ambavyo Zahanati 1198, Vituo vya Afya 487, Hospitali za Halmashauri 99, Hospitali za Mikoa 10 ikiwemo Hospitali ya Mkoa wa Mara ya Mwalimu Nyerere Memorial Hospital ambayo ujenzi wake iliasisiwa na Mwalimu J.K Nyerere mwaka 1977.

 “Uwekezaji huu mkubwa uliofanywa na Serikali ya awamu ya tano kwenye miundombinu ya utoaji wa huduma za afya umeongeza umeongeza vituo vya huduma za upasuaji wa dharura wa kumtoa mtoto tumboni kutoka vituo 192 (Vituo vya afya 115 na Hospitali za Halmashauri 77) mwaka 2015 hadi vituo 586 (Hospitali za Halmashauri 99 na vituo vya 487) mwaka 2020 ikiwa ni sawa na ongezeko la vituo 394”. Amesema Waziri Ummy.

 Waziri Ummy amesema Serikali imeongeza idadi ya Vituo vya huduma kwa ajili ya Watoto wachanga wanaozaliwa wakiwa na shida ya kupumua, uzito pungufu na maambukizo ya Bakteria (Neonatal Care Units) kutoka 14 mwaka 2015 hadi kufikia 104 mwaka 2020.

 Aidha, Serikali imeongeza upatikanaji wa huduma kwa ajili ya Watoto mahututi (Paediatric ICU) katika Hospitali za Rufaa za kanda mbili mwaka 2015 hadi Hospitali za kanda sita ambazo ni Muhimbili, Bugando, KCMC, Mbeya, Benjamin Mkapa na Mloganzila.

 Waziri Ummy amesema upanuzi huu umesogeza huduma muhimu kwa ajili ya dharura ya uzazi na Watoto karibu na wananchi kupitia uimarishaji wa vituo vya afya ya msingi, hivyo kuwaondolea kero na gharama kubwa walizokua wanazitumia kufuata huduma hizi mbali na maeneo yao na hivyo kuboresha Maisha.

 Kutokana na maboresho yaliyofanyika katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya tano, viashiria vikuu vya mwenendo wa huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto vimeendelea kuimarika ikiwa ni Pamoja idadi ya wanawake wanaotumia huduma afya ya uzazi kabla ya ujauzito na baada ya kujifungua imeongezeka kutoka asilimia 32 mwaka 2015/16 hadi asilimia 43 mwaka 2020, ongezeko la akinamama kuhudhuria kliniki imeongezeka kutoka asilimia 39 hadi asilimia 81 kufikia mwezi Juni 2020, kiwango cha wajawazito wanaojifungua kwenye vituo vya kutolea huduma kimeongezeka kutoka asilimia 64 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 83 Juni 2020 na hivyo kuvuka lengo la Mpango Mkakati wa Afya ya Uzazi na Mtoto (2016-2020).

 Waziri Ummy amesema hali hii inaashiria utafiti wa hali ya vifo vitokanavyo na uzazi na watoto nchini utakapofanyika mwaka 2021, kiwango cha vifo vitaokanavyo na uzazi kitakuwa chini ya vifo 190 kwa vizazi hai 100,000 ukilinganisha na vifo 556 kwa vizazi hai 100,000 iliyotolewa mwaka 2015/16.

MWISHO

 

 

 

 

 


Jumamosi, 8 Agosti 2020

WAZIRI UMMY APIGA MARUFUKU WANAFUNZI KUPEWA VIDONGE VYA FOLIC ACID MASHULENI

- Hakuna maoni











Picha mbalimbali zikimuonesha Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akiambatana na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Loata Ole Sanare, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Martine Shigela pamoja viongozi mbalimbali wakipita katika mabanda yaliyopo kwenye maonesho ya Nanenane kanda ya Mashariki yanayofanyika Mkoani Morogoro kuona bidhaa na huduma katika mabanda hayo.


NA EMMANUEL MALEGI-MOROGORO

 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto amepiga marufuku shule zote nchini kuwapa wasichana dawa aina ya Folic Acid na badala yake shule zimetakiwa kulima kuwajengea uwezo wa kulima maboga na mbogamboga katika bustani za shule.

 Waziri Ummy amesema hayo leo wakati alipokua akihitimisha kilele cha Maonesho ya Nanenane kanda ya Mashariki inayojumuisha Mikoa ya Dar Es Salaam, Pwani, Tanga na Morogoro ambayo yamefanyika mkoani Morogoro.

 Waziri Ummy amesema kuwa ni marufuku kuwapa wanafunzi na wasichana balehe vidonge vya Folic Acid, badala yake fedha hizo zinazotolewa kwa ajili ya dawa hizo zitumike kuanzisha bustani shuleni ili kuzalisha vyakula vinavyotoa madini hayo.

 

“Mbali na kuanzishwa kwa bustani shuleni lakini pia fedha hizo zinaweza kupelekwa kwa vijana ili waanzishe miradi ya bustani za mboga kwa ajili ya kuzalisha mazao yanayozalisha asidi hiyo yakiwemo maboga, matunda na hata karoti badala ya kutoa vidonge kwa wanafunzi”. Amesema Ummy.

 

Kuhusu unywaji wa maziwa mashuleni, Waziri Ummy amesema kuwa atamwandikia barua ya pendekezo Waziri wa Elimu Profesa Joyce Ndalichako ili kuanzia Septemba mosi mwaka huu kila shule iwe na kibanda cha maziwa kwa ajili ya wanafunzi kununua.

 Aidha, Waziri Ummy amesema kuwa  utafiti wa Shirika la Afya Duniani (WHO) unaonesha kwamba kila mtu anatakiwa kunywa nusu lita ya maziwa sawa na lita 180 kwa mwaka, lakini kwa sasa kila mtu anakunywa lita 40 kwa mwaka sawa na vijiko 10 vya chai kwa siku.

 Pia Waziri amesema udumavu kwa watoto wa chini ya miaka mitano umepungua nchini kutoka asilimia 34.4 mwaka 2014 hadi asilimia 31.8 mwaka 2018 licha ya kuwa jitihada zinatakiwa kuendelea kuchukuliwa.

 Pamoja na hayo Waziri Ummy ameupongeza mkoa wa Morogoro kwa kuwa mwenyeji wa maonesho hayo ambayo yamekua chachu ya ukuaji wa kilimo, uvuvi, ufugaji na ujasiriamali nchini na amewataka waratibu wake kutoishia hapo na badala yake ujuzi huo upelekwe vijijini kwa ajili ya kuendeleza sekta hiyo muhimu ambayo kwa kiasi kikubwa inachangia pato la taifa.


Jumatatu, 3 Agosti 2020

WAUGUZI NA WAKUNGA WATAKIWA KUTUMIA UTAALAMU WAO KWA AJILI YA USTAWI WA TAIFA

- Hakuna maoni




Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto-Idara Kuu Afya Edward Mbanga akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi kwenye ukumbi wa Cathedral jijini Dodoma.

Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsai, wazee na Watoto akiongea na viongozi  hao wakati wa kikao cha mafunzo ambapo aliwataka kuweka dhamira na malengo  ya dhati  katika kuboresha maadili katika taaluma ya uuguzi na ukunga.

Muuguzi Mkuu kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI Charles Kadugushi akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi, Jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Idara ya Uuguzi na Ukunga kutoka Wizara ya Afya Bi. Ziana Sellah akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi, Jijini Dodoma.

Msajili wa Baraz a la Uuguzi na Ukunga Agnes Mtawa akiwasilisha mada wakati wa kikao kazi hicho kinachofanyika jijini Dodoma.

Picha ya pamoja ya mgeni rasmi na wasajili wa mabaraza ya kitaaluma yaliyopo chini ya wizara ya afya.

Mgeni rasmi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wauguzi wakuu wa Wilaya mara baada ya ufunguzi.


WAUGUZI NA WAKUNGA WATAKIWA KUTUMIA UTAALAMU WAO KWA AJILI YA USTAWI WA TAIFA

Na.Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Wauguzi na Wakunga nchini wametakiwa kutoa huduma kwa kuzingatia miongozo iliyopo wakati wakitoa huduma kwa weledi ili kufikia malengo na matumaini ya wateja kwa ajili ya ustawi wa Taifa.

Rai hiyo imetolewa leo na Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto – Idara Kuu ya Afya Bw. Edward Mbanga wakati wa ufunguzi wa  kikao kazi  cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi wauguzi wakuu wa wilaya kinachofanyika jijini Dodoma.

Bw. Mbanga amesema  kuwa wauguzi na wakunga ndio watendaji wakuu katika vituo vya afya kwenye ngazi ya jamii hadi Taifa hivyo uwajibikaji mzuri na utawala bora utaboresha utendaji hali itayosaidia kufikia malengo mbalimbali waliyojiwekea katika ngazi zote.

"Viongozi mnatakiwa kuwa wabunifu, wachapa kazi, wenye nidhamu na mfano bora wa kuigwa katika utekelezaji wa majukumu yenu,kwahiyo  ni lazima msimamie utoaji wa huduma uliyo mzuri na wenye heshima na utu.”Alisema

Aidha, Kaimu Katibu Mkuu huyo aliwakumbusha  washiriki hao kuwa, suala la huduma za uuguzi na ukunga ni suala la  ubinadamu zaidi na kuvaa viatu vya wagonjwa wao.

“Hakuna aliyegongwa muhuri wa kuugua  au kuwa mgonjwa akalazwa ,sisi sote ni wagonjwa watarajiwa kwahiyo kama ambavyo sisi tungependa kuuguzwa vizuri, kijibiwa kwa kauli nzuri basi tuhakikishe tunasimamia maadaili ya kazi”.Alisisitiza Mbanga.

Hatahivyo alisema kuwa, Serikali inawahakikishia itaendelea kufanya kazi pamoja na waauguzi  kwa kutoa miongozo thabiti na kuhakikisha upatikanaji wa nyenzo muhimu katika hospitali na vituo vya kutolea huduma ya afya na kuboresha mazingira ya kazi yaliyo bora na salama.

Aliendelea kusema kuwa, hivi karibuni kumekuwa na malalamko  mbalimbali ya kiutendaji  na kitaaluma kutoka kwa wateja  wanaofika kupata huduma za afya na hivyo kuleta taswira mbaya  kwa taaluma yao na kuonyesha hakuna usimamizi mzuri wa utoaji huduma za uuguzi na ukunga.

“Tungependa  wateja wetu watoe sifa  badala ya malalamiko hivyo kikao hiki mje na mipango ya kuondokana na malalamiko kwani taaluma yenu ni zaidi taaluma." alisema.

Hata hivyo, amewakumbusha  viongozi hao kuwa mstari wa mbele kupambana dhidi  ya rushwa na kuhakikisha inatokomezwa katika maeneo yao ya kazi kwani rushwa imekuwa ikilalamikiwa na kuripotiwa katika kada ya afya nchini.

-MWISHO-

Ijumaa, 12 Juni 2020

DKT. MOLLEL ATETA NA MADEREVA WA MALORI, NAMANGA

- Hakuna maoni
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel akiongea na madereva malori mpaka wa Tanzania na Kenya Namanga Jijini Arusha, lengo kuwasikiliza changamoto zao.





Baadhi ya madereva wa malori waliokwama katika mpaka wa Tanzania na Kenya Namanga Jijini Arusha wakimsikiliza Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel.




DKT. MOLLEL ATETA NA MADEREVA WA MALORI, NAMANGA 

Na WAMJW- Arusha. 

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel amefanya ziara katika mpaka wa Tanzania na Kenya Namanga Jijini Arusha na kuzungumza na madereva wa malori yanayokwenda Kenya ili kusikiliza changamoto zinazowakumba. 

Dkt. Mollel amefanya ziara hiyo leo, ikiwa ni sehemu ya kutafuta ufumbuzi wa changamoto zinazowakumba madereva hao, katika kipindi hiki ambacho Dunia imekumbwa na maambukizi ya homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya Corona. 


Dkt. Mollel amesema kuwa, Serikali imeliona tatizo hilo na kuweka wazi kuwa itaongeza kasi katika kuhakikisha inapata suluhu ya changamoto wanazokumbana nazo madereva hao katika eneo la mpaka wa Namanga. 

"Nimekuja kuwaambia poleni, lakini Serikali yetu itaenda kwa kasi ya ajabu kuhakikisha kwamba hili tatizo lenu katika mpaka huu linatatuliwa " alisema. 

Aidha, Dkt. Mollel amewataka madereva hao kuwa wavumilivu katika kipindi hiki ambacho, Serikali inatafuta utatuzi wa changamoto yao, huku akiwapa salamu kutoka kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt. John Pombe Magufuli na kusema anawapenda sana.

Mbali na hayo Dkt. Mollel alisema kuwa changamoto hii iliyojitokeza katika mpaka wa Namanga ni suala mtambuka ambalo linahusisha Wizara zaidi ya moja, huku akiweka wazi kuwa suala hili lina uhusiano wa kibiashara na uchumi baina ya nchi hizo.

Nae, dereva wa malori yanayokwenda nchini Kenya Bw. Abdullah Hassan amesema kuwa, kama madereva hawakubaliani na majibu ya vipimo wanavyopewa kutoka Kenya kutokana na vipimo hivyo kuonesha idadi kubwa ya madereva kuwa na ugonjwa wa Corona jambo ambalo sio kweli.

"Tunaishi maisha magumu sana kutokana na hali iliyojitokeza, na kunachosikitisha zaidi, sisi hatukubaliani na vipimo ambavyo tunapimwa upande wa pili. 

Kwa upande wake, Japhet Jeremiah alisema kuwa, wamekuwa wakiombwa kiasi cha shilingi 2000 za Kenya ili kuandikiwa kuwa hawana Corona, hali aliyeweka wazi kuwa ni uonevu kwa madereva kutoka Tanzania. 

"Sisi kero yetu, tumekuwa tukipima Kenya tumeambiwa tuna Corona, na mimi wiki mbili nilipima nikapewa cheti nina Corona lakini ukweli ni kwamba sina Corona na sijawai tumia dawa yoyote mpaka sasahivi" alisema 

Mwisho.

Ijumaa, 14 Februari 2020

HOSPITALI YA WILAYA MWANGA YAPEWA WIKI MBILI KUJA NA MKAKATI WA UPATIKANAJI WA VIPIMO MUHIMU VYA AFYA

- Hakuna maoni
 Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akikagua kadi ya bima ya afya ngazi ya jamii iliyoboreshwa kutoka kwa mgonjwa aliyefika hospitali ya Wilaya ya Mwanga kupata huduma za afya.

 Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile (kulia) akifafanua jambo kwa watumishi  wa Wilaya ya Mwanga (hawapo pichani) kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Bw. Thomas Apson.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile (kushoto)  akisalimiana na Mkuu wa Wilaya ya Mwanga Bw. Thomas Apson (kulia) mara baada ya kuwasili katika ofisi za Mkuu wa Wilaya ya Mwanga.



HOSPITALI YA WILAYA MWANGA YAPEWA WIKI MBILI KUJA NA MKAKATI WA UPATIKANAJI WA VIPIMO MUHIMU VYA AFYA

Na WAMJW - Mwanga, Kilimanjaro.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile ameutaka uongozi wa Hospitali ya Wilaya ya Mwanga kuandaa mkakati madhubuti utakaowawezesha kuwa na vipimo muhimu vya afya.

Dkt Ndugulile ametoa agizo hilo leo alipotembelea Hospitali ya Wilaya ya Mwanga kujionea hali ya utoaji huduma na kubaini kuwa hospitali hiyo haina vipimo vya damu, vipimo vya kemia pamoja vipimo vya CD4.

”Kwa miaka miwili sasa hakuna vipimo vya msingi katika hospitali hii, tunawakosesha huduma wananchi” amesema Dkt. Ndugulile

”Haiwezekani Hospitali kubwa ndani ya Wilaya kukosa vipimo vya msingi, haiwezekani mtu hapa sasa hivi anahitaji kipimo cha damu atoke hapa aende Hospitali ya Mawenzi Moshi kwa ajili ya vipimo” amesema Naibu Waziri Ndugulile.

Katika hatua za kutafuta ufumbuzi wa changamoto hiyo, Waziri Ndugulile ameushauri uongozi wa afya ndani ya Wilaya kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Mwanga kuhakikisha wanatenga fedha kwa ajili ya kununua vifaatiba hivyo ili wananchi waweze kupata huduma za vipimo ndani ya Wilaya ya Mwanga.

Aliendelea kushauri kuwa kupitia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) wao wanatoa mkopo wa majengo na vifaa kwa taasisi za umma na binafsi, mnaweza kuwafikia NHIF na kujadili kuhusu suala hili.

”Huko kwingine wanazitumia hizo fursa, kaeni na watu wa NHIF, Meneja wa NHIF kaa na viongozi wa Hospitali hii ikiwezekana mkubaliane hivyo vitu vipatikane kwa haraka” ameshauri Dkt. Ndugulile.

”Naamini mna wadau wa maendeleo ambao mnashirikiana nao katika mambo mbalimbali, timu ya afya ndani ya mkoa, wilaya pamoja na hospitali nawaombeni sana tuwe tunaomba vitu ambavyo vina manufaa kwa wananchi” amesisitiza Dkt. Ndugulile.

Awali akitoa salamu za wananchi wa Wilaya ya Mwanga, Mbunge wa Jimbo la Mwanga Profesa Jumanne Maghembe amesema kuwa changamoto ya kijiografia ndani ya Wilaya hiyo inachangia wananchi kukimbilia hospitali za Wilaya jirani ili kuweza kupata huduma.

”Wilaya yetu hii ina upande wa mlimani na huku tambarare, wananchi wengi walio huku tambarare wanaona ni bora kwenda Moshi kwa ajili ya matibabu kuliko kwenda juu mlimani iliko Hospitali” amesema Prof. Maghembe.

Hata hivyo Prof. Maghembe amesema kuwa tayari ndani ya Wilaya wameshaanza taratibu za kujenga Hospitali nyingine eneo la chini (tambarare) ili wananchi wanaoishi maeneo hayo waweze kupata huduma za afya ndani ya Wilaya ya Mwanga.

-Mwisho-

Jumatano, 5 Februari 2020

MAAMBUKIZI MAPYA YA MALARIA YAMEPUNGUA KWA ASILIMIA 27

 Katibu wa Chama cha TAPAMA Mhe. Raphael Chegeni akionesha kadi ya tathmini ya Malaria, wakati wa kikao cha uraghabishaji kwa Wakurugenzi na Wakuu wa vitengo wa Wizara ya Afya.

Mkurugenzi wa Kinga Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi akisikiliza maoni ya washiriki, wakati kikao na umoja wa wabunge wa kupambana na malaria na magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Tanzania(TAPAMA) na Alma (African Leaders Malaria Alliance).

Mwakilishi wa Alma Tanzania Bw. Diego akiwasilisha mada kuhusu namna namna ya kuingia kwenye mfumo wa simu/kompyuta ya kadi ya tathmini ya Malaria ili kujionea utendaji wa Mkoa au hatua zinazochukuliwa kutatua matatizo ya eneo husika.

Picha ya pamoja kati ya Watumishi wa Wizara ya Afya na wabunge wa kupambana na Malaria na magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Tanzania(TAPAMA) na viongozi wa Alma (African Leaders Malaria Alliance) waliofika Wizara ya Afya kufanya uraghibishaji wa  kadi ya tathimini ya malaria  kwa ajili ya uwajibikaji na utendaji kwa viongozi wa wizara jijini hapa.


MAAMBUKIZI MAPYA YA MALARIA YAMEPUNGUA KWA ASILIMIA 27

Na WAMJW - Dodoma.

Maambukizi mapya ya ugonjwa wa malaria yamepungua nchini   kwa asilimia 27 na hiyo ni kutokana na kuboreka kwa utoaji huduma za mapambano ya ugonjwa huo ukilinganisha na waginjwa 164 kati ya watu 1000 mwaka 2015 hadi wagonjwa 119 kati ya watu 1000 mwaka 2018.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Kinga Dkt. Leonard Subi wakati akitoa taarifa kwa umoja wa wabunge wa kupambana na malaria na magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Tanzania(TAPAMA) na Alma (African Leaders Malaria Alliance) waliofika wizara ya afya kufanya uraghibishaji wa  kadi ya tathimini ya malaria  kwa ajili ya uwajibikaji na utendaji kwa viongozi wa wizara jijini hapa.

Dkt. Subi amesema kuwa mafanikio hayo yametokana na jitahada za viongozi wa Serikali inayoongozwa na Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli na muhimili wa Bunge katika ushirikiano mzuri na wadau pamoja ma wananchi katika kupambana na ugonjwa huo.

Amesema kuwa viongozi wa nchi za afrika wanawajibika kwa afya za wananchi na hivyo kwa Tanzania vifo vitokanavyo na Malaria vimepungua  kwa asilimia 63 kutoka vifo 6,737 mwaka 2015  hadi 2,540 mwaka 2018.

“Ingawa hivi sasa tupo kwenye kudhibiti ila  tunalengo la kutokomeza,hivyo tuna imani kwamba tanzania tunao uwezo mkubwa wa kufikia huko kwani kuaniza Mh. Rais Wetu hadi muhimbili kama Bunge nao wako mstari wa mbele kuondosha malaria nchini”.

Aidha, amesema kuwa hivi sasa kumekuwa na mabadiliko makubwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini kwa kupungua kwa wagonjwa wanaougua malaria kupungua pia hata kwa watoto chini ya miaka mitano vifo vimepungua.

“Tanzania tumeamua kupambana na wadudu dhurifu kuanzia ngazi ya viluilui hadi mbu wapevu waenezao maradhi, hivyo kila mwananchi anawajibu wa  kuchukua hatua, hivyo ni vyema tukaungana ili kuiondosha Malaria nchini”.Amesema Dkt. Subi

Naye Katibu wa TAPAMA Mhe. Raphael Chegeni amesema kuwa msingi wa taifa ni kuwa na afya ,hivyo wanafarijika na afua zinazochukuliwa na wizara ya afya katika kupambana na malaria nchini “Malaria inaua hivyo tunajivunia kuona tanzania inazidi kupambana kutokomeza ugonjwa huu.

Kadi ya tathimini ya malaria ni kitendea kazi cha usimamizi kilichotolewa na wizara ya afya kinachoonyesha takwimu za utendaji wa viashiria vya malaria vilivyopewa kipaumbele katika ngazi ya mikoa na wilaya  ambayo inaleta urahisi katika kutambua wapi kuna tatizo ili hatua za kuokoa maisha ziweze kuchukuliwa.

Mwisho

Jumapili, 26 Januari 2020

KINU CHA KUFUA OKSIJENI KCMC KUWA MSAADA KWA WENYE MATATIZO YA UZAZI

Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kaskazini (KCMC) Dkt. Sarah Urasa akizungumza katika Mkutano wa Maafisa Habari wa Wizara ya Afya na Taasisi zake katika kampeni ya "TumeboreshaAfya".

Bibi Catherine Mushi akiendesha  kinu cha kuzalisha hewa safi (Oxygen plant) katika hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kaskazini KCMC.

 Mtaalam wa kutengeneza baskeli za magurudumu matatu(wheelchair) Bw. Samson Shirima akiwa katika kiwanda cha kuzalisha bidhaa hizo katika hospitali ya rufaa ya KCMC.

Madaktari pamoja na wauguzi wakiwahudumia watoto  njiti katika wodi maalum ya watoto hao   KCMC.

Mtaalam kutoka Idara ya ngozi Bw. Maghembe Juma katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Kilimanjaro KCMC akitengeneza dawa na mafuta maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa ngozi katika Hospitali hiyo.

Grace Manyika akiweka alama za ukomo wa matumizi ya mafuta maalum kwa watu wenye ulemavu wa ngozi (albinism) katika kiwanda hicho  kilichopo hospitali ya KCMC, Kilimanjaro.

Mtambo wa kinu cha kisasa cha kuzalisha hewa safi (oxygen plant)wenye uwezo wa kuzalisha mitungi 400 kwa siku ambao upo katika hospitali ya Rufaa ya kanda ya kaskazini KCMC.

KCMC



KINU CHA KUFUA OKSIJENI KCMC KUWA MSAADA KWA WENYE MATATIZO YA UZAZI

Na Mwandishi wetu, KILIMANJARO.

IMEELEZWA kuwa uwepo wa kinu kipya na cha kisasa chenye uwezo wa kufua hewa ikiwemo hewa safi ya Oxygen na ile ya  Naitrojeni kitakuwa msaada kwa wenye tatizo la uzazi nchini.

Akizungumzia hospitalini hapo ikiwa ni utekelezaji wa kampeni ya Tumeboresha sekta ya Afya yenye lengo la kuonyesha mafanikio makubwa yaliyopatikana katika uwamu ya tano ndani ya Wizara ya afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Kaimu Mkurugenzi wa KCMC Dkt. Sarah Urasa alisema:

"Uhifadhi wa mbegu za kiume  na kike upo mbioni kuanza hapo baadae. Hatua hiyo kwani tayari tumeanzisha klininiki maalumu kwa ajili ya watu wenye matatizo ya uzazi ambayo tunaonana na wagonjwa kwa wiki mara moja  ambapo huwahudumia watu 10 mpaka 12." Alisema.

Mbali na kazi hiyo  kinu hicho kinauwezo wa kufua hewa ya Oksijeni ambayo kwa kiwango kikubwa hutumika kuwasaidia watu wenye matatizo ya kupumua ambapo kwa siku mitungi 400 hufuliwa katika kinu hicho.

Dkt. Sarah Urasa aliongeza kuwa: "Hii ni hospitali ya kwanza kuwa na kinu ya kufua hewa ya oksijeni na Nitrogen  hapa nchini.

Hewa ya Oksijeni pia inatumika kwa wale wagonjwa wanaopewa dawa za usingizi kwaajili ya upasuaji, hewa ya nitrogen inatumika kuhifadhi sampuli kutoka kwa wagonjwa,tiba kwa magonjwa ya ngozi vile vile hutumika kukata matokeo kwenye ngozi au kwenye viungo vya uzazi" alisema.
 
Huduma hiyo ambayo imeanza mwaka huu Dkt. Sarah alisema ununuzi wa mitungi ya gesi ya oksijeni pekee ulikuwa ukiwagharimu takribani milioni tatu kwa wiki huku gharama za usafirishaji ikiwa haijajumuishwa hatua ambayo imeokoa gaharama za uendeshaji hospitalini hapo.

Dkt.Sarah alieleza kuwa kwa kadiri uzalishaji unavyoongezeka katika kinu hicho wataanza kutumia mfumo wa kuunganisha gesi moja kwa moja hadi katika kitanda cha mgonjwa.

"Tumeona uharibifu mkubwa unaotokana namitungi hii ya gesi sakafu yetu imekuwa ikiharibika kutokana na uzito wa mitungi yenyewe kwahiyo mfumo tutakapkuja kuutumia utakuwa bora zaidi tofauti na sasa "alisema.

Mafanikio mengine aliyoyataja Dk.Sarah alisema katika utawala wa Rais Dk.John Magufuli wamefanikiwa kuanza kutengeneza maji tiba 'dripu' kwaajili ya kuwasaidia wagonjwa ndani na nje ya hospitali.

"Hii inetusaidia kwa kiwango kikubwa hata hospitali zingine zimekuwa zikifika hapa kwaajili ua kujifunza namna ya kutengeneza maji tiba "alisema.

Pia alisema KCMC ndio kituo pekee inayotambulika kimaitafa kutoa mafunzo ya magonjwa ya ngozi na zinaa kwa nchi zote za Afrika Mashariki.

"Kituo hiki ndio kinachozalisha mafuta ya ngozi kwaajili ya watu wenye ualbino na tayari tumeingia makubaliano na Bohari kuu ya Dawa MSD kwaajili ya kusambaza dawa na tayari tumefikia mikoa 25 kwa kutumia mfumo wetu wa usambazaji na sasa MSD watatuongezea nguvu ili kusambazwa nchi mzima "alisema

Kwa upabde wake,  Mhandisi KCMC Dustan Kanza alisema mgonjwa mmoja hutumia mtungi mmoja lengo kuepukana na maambukizi.

Alisema katika kinu hicho kwa saa 24 inauwezo wa kuzalisha mitungi 400 na mpaka sasa tayari zaidi ya mitungi 600 imezalishwa tangu kuanza kufanya kazi kwa kinu hicho januari mwaka huu.

Mwisho.




Jumatatu, 16 Desemba 2019

MAOFISA AFYA WATAKIWA KUWAKINGA WANANCHI DHIDI YA MAGONJWA-DKT. SUBI

Mkurugenzi wa Kinga, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi akieleza jambo mbele ya Maafisa Afya wa Mikoa na Halmashauri, wakati wa ufunguzi wa Maadhimisho ya Wiki ya usafi wa mazingira.

Afisa kutoka Idara ya Mazingira Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee naWatoto Bw. Anyitike Mwakitalima akieleza mafanikio mbali mbali yaliyopatikana kutokana na afua mbali mbali za usafi wa mazingira zinazotekelezwa na Wizara ya Afya kwa kushirikiana na Wadau.

Maafisa Afya kutoka Mikoa, Halmashauri na Wadau wakifuatilia kwa makini neno kutoka kwa Mkurugenzi wa Kinga, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi.


MAOFISA AFYA WATAKIWA KUWAKINGA WANANCHI DHIDI YA MAGONJWA-DKT. SUBI

Na Catherine Sungura, WAMJW - Dodoma

Maofisa afya wa mikoa na halmashauri wametakiwa kusimamia afya ya jamii kwenye maeneo yao ili wananchi wajikinge dhidi ya magonjwa yakuambukiza na yele yasiyoambukiza.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa kinga Dkt. Leonard Subi wakati akiongea na maofisa hao ambao wanakutana jijini hapa  kwa  kikao kazi cha siku tatu wakijadili utekelezaji wa maazimio yaliyotolewa kwenye mkutano mkuu wa kwanza mwaka jana  na  Waziri Mkuu wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa.

“Mkutano huu ni wa pili mwaka huu,ni mkutano muhimu kwa maofisa afya kwani ndio wasimamizi wa shughuli za afya katika ngazi za jamii kwa kuhakikisha wananchi wanajikinga na maradhi, kula chakula bora kuishi makazi bora,usafi wa mazingira pamoja na kuwa vyoo bora”.Amesema Dkt. Subi

Aidha, amesema katika mkutano huu mambo mbali mbali yatajadiliwa ikiwemo  afya mazingira,usafi na uchafuzi wa mazingira na kila kinachotumiwa na kumzunguka  mwananchi ,pia wataangalia mabadiliko ya tabia nchi na kupata taarifa kutoka ngazi za mikoa ni jinsi gani walivyotekeleza majukumu yao.

“Maafisa afya muendelee kuishauri wizara kwa kutumia takwimu kwani tunatarajia mkutano huu mtabadilishana uzoefu  kutoka sehemu zenu za kazi,kama wizara tumekua tukitengeneza sera na miongozo mbali mbali ya kudhibiti maradhi yote yanayoweza kuathiri afya za binadamu hivyo kazi ya wizara ni kukusanya taarifa,kuchakata na kuzitolea miongozo na maelekezo”. Aliongeza Dkt. Subi.

Hata hivyo amesema maofisa hao wana majukumu ya kusimamia na  kulinda afya mipakani ili kusiingie magonjwa ya milipuko kutoka nje hususan  nchi za jirani pamoja na utoaji wa chanjo ambapo Tanzania ipo vizuri.

Mkutano huo ambao utafunguliwa kesho na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu umebeba Kauli mbiu isemayo “Huduma bora za afya mazingira na usafi ni kichocheo muhimu cha uchumi endelevu.


Alhamisi, 12 Desemba 2019

SERIKALI YAAGIZA HOSPITALI ZOTE NCHINI KUANZISHA MFUKO WA FEDHA ZA DAWA.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Mhe Ummy Mwalimu akieleza jambo wakati wa kikao cha kuzindua Bodi ya ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Sekou-Toure.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Mhe Ummy Mwalimu akiteta  jambo na Mwenyekiti mpya wa Bodi ya ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Sekou-Toure  Prof. Abel Makubi wakati wa kikao cha kuzindua Bodi hiyo.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Mhe Ummy Mwalimu akikata  utepe ikiwa kama ishara ya uzinduzi wa Bodi mpya ya ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Sekou-Toure, Kulia kwake ni Mwenyekiti mpya wa Bodi Prof. Abel Makubi, kushoto kwake ni Kaimu RMO Mkoa Mwanza Dkt. Silas Wambura.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Mhe Ummy Mwalimu na Mwenyekiti mpya wa Bodi ya ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Sekou-Toure wakiwa wamebeba kitabu cha mwongozo wa Bodi ya ushauri,  wakati wa kikao cha kuzindua Bodi hiyo.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto Mhe Ummy Mwalimu akimkabidhi mwongozo mmoja kati  ya wajumbe wa Bodi mpya ya ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza Sekou-Toure, katikati ni Kaimu Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt. Silas Wambura.

Baadhi ya Watumishi wa Hospitali  ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza Sekou-Toure waliofika kushuhudia uzinduzi wa Bodi mpya ya ushauri ya Hospitali hiyo, uliofanywa na Waziri wa Afya Mhe.@umwalimu katika ukumbi wa RMO Mkoa wa Mwanza.

Baadhi ya Watumishi wa Hospitali  ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza Sekou-Toure na Wajumbe wa Bodi ya zamani  ya ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza Sekou-Toure, waliofika kushuhudia uzinduzi wa Bodi mpya ya ushauri ya Hospitali hiyo, uliofanywa na Waziri wa Afya Mhe.@umwalimu katika ukumbi wa RMO Mkoa wa Mwanza.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri wa Afya Mhe.@umwalimu, akiwa na wajumbe wa Bodi mpya ya ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza Sekou-Toure baada ya uzinduzi wa Bodi hiyo.


SERIKALI YAAGIZA HOSPITALI ZOTE NCHINI KUANZISHA MFUKO WA FEDHA ZA DAWA.

Na Rayson Mwaisemba, WAMJW- MWANZA

Serikali kupitia Wizara ya Afya imeagiza Waganga Wakuu wa Vituo vya Afya na Hospitali zote nchini kuanzisha mfuko wa fedha za Dawa kupitia makusanyo ya fedha za ndani, ili kuweza kukabiliana na changamoto ya upatikanaji wa dawa nchini endapo itatokea.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe Ummy Mwalimu katika kikao cha uzinduzi wa Bodi mpya ya ushauri ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza.

"Kuanzia Vituo vya Afya, Hospitali zote za Halmashauri, za Mikoa , kuanzisha mfuko wa fedha za dawa, na vyanzo vikuu vya mifuko hii ni mapato yatokanayo na mauzo ya dawa, huduma za Maabara, huduma za mionzi" alisema Waziri @umwalimu.

Amesema, Bodi hiyo ya ushauri lengo lake kubwa ni kuhakikisha inaboresha huduma za kinga na tiba katika Hospitali, huku ikihakikisha huduma hizo zinaifikia wananchi kwa ubora na gharama nafua.

Aliendelea kusema, Sera ya Afya nchini inawataka Wananchi kuchangia huduma kwa gharama nafuu isipokuwa kwa makundi yote ya msamaha, wakiwemo Wazee, Watoto walio chini ya miaka mitano na mama wajawazito, hivyo kuwataka kuweka mifumo mizuri ili kurahisisha utoaji huduma.

Mbali na hayo, Waziri Ummy ameiagiza Bodi hiyo kuhakikisha inaboresha huduma za dharura na ajali, ili kuokoa vifo vitokanavyo weza kuepukika kupitia huduma za dharura, keisha kuwashauri kujenga jengo jipya la wagonjwa wa nje (OPD) ili kuboresha huduma kwa wananchi.

"Watu wengi wanakufa wakiwa getini Mwa Hospitali, wakati utaalamu upo, kwamba mkiboresha huduma za dharura na ajari, tunaweza kuokoa maisha ya watu wengi " alisema Waziri @umwalimu.

Aidha, Waziri Ummy ameeleza majukumu ya Bodi hiyo ni kushauri, kutengeneza, kusimamia na kupitisha miongozo, malengo na mipango mikakati ya Hospitali kulingana na Sera na miongozo ya Serikali.

Nae Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Sekou-Toure Dkt. Dkt. Graham Mtui ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kuendelea kuboresha huduma za Afya katika Hospitali hiyo kwa kuleta mashine ya uchunguzi wa figo na ini, mashine ya kusafisha figo ambazo zinatarajia kuanza kutoa huduma Januari 2020.

Kwa upande mwingine amesema, Hospitali inatarajia kupokea mashine sita ikiwemo CT Scan, X- ray yakidigitali, vifaa vya mifupa na mashine zinazosaidia kupumulia kutoka MSD.

Hata hivyo, amesema kuwa, idadi ya Wagonjwa wanaofika kupata huduma, kutoka wastani wa wagonjwa 350 kwa siku kwa mwaka 2015 hadi kufikia wagonjwa kati ya 500 mpaka 700 kwa Mwaka huu 2019, huku akiweka wazi kupunguza Rufaa za kwenda Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Bugando kwa asilimia 50.

"Kutokana na mafanikio hayo, idadi ya wagonjwa wanaopata huduma katika Hospitali imeongezeka, kutoka wastani wa wagonjwa 350 kwa siku ambayo ilikuwa mwaka 2015, na kufikia wastani wa wagonjwa kati ya 500 hadi 700 kwa mwaka huu 2019", alisema Dkt. Graham Mtui.

Mwisho.