Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Habari Picha. Onyesha machapisho yote
Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Habari Picha. Onyesha machapisho yote

Alhamisi, 11 Juni 2020

WAZIRI UMMY AZINDUA BARAZA JIPYA LA MADAKTARI TANGANYIKA

- Hakuna maoni








Na WAJMW-DODOMA

Waziri wa Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu jana amezindua Baraza jipya la Madaktari Tanganyika katika hafla iliyofanyika katika ukumbi wa LAPF jijini Dodoma.

Katika uzinduzi huo Waziri Ummy amelipongeza Baraza jipya linaloongozwa na Mwenyekiti  Prof. David Ngassapa na wajumbe wake wanane walioteuliwa lakini pia hakusita kulishukuru na kutaja baadhi ya mafanikio ya baraza lililopita ambalo lilikua linaongozwa na Prof. Muhammad Kambi ambaye alikua Mwenyekiti.

“Katika kipindi chao cha uongozi, Baraza limepata mafanikio mengi ikiwemo Sheria za Madaktari, Madaktari wa meno wa wataalamu wa Afya shirikishi ya Mwaka 2017, na kuitengenezea kanuni zake tano ambazo ni ya Watarajali, Usajili wa mitihani, Ada na Tozo, pamoja na Uchunguzi wa mashauri ya mafunzo endelevu”. Amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy amesema mabadiliko hayo yameboresha sana muundo wa Baraza na hivyo usimamizi wa taaaluma ya udaktari na udaktari wa meno umeongeza wigo wa usimamizi wa taaluma kwa kuongeza kada za Afya shirikishi ambazo mwanzo zilikua hazina usimamizi.

Waziri Ummy amesema majukumu ya Baraza hilo ni pamoja na kuwatambua wanataaluma inaowasimamia kwa njia ya kuwasajili na kuwapa leseni zinazowaruhusu kufanya kazi hizo na kuwakagua mara kwa mara ili kujiridhisha kuwa wako hai kitaaluma.

Aidha, Waziri Ummy amesema kwa mujibu wa takwimu zilizopo ofisi ya Msajili wa Baraza la Madaktari inaonyesha kuwa jumla ya madaktari wa kada mbalimbali 13,973 wamesajiliwa nchi nzima, hata hivyo madaktari walipo kwenye ajira ni 5568.

Pamoja na hayo, Waziri Ummy amelitaka Baraza jipya chini Mwenyekiti Prof. David Ngassapa kuhakikisha kuwa: Wananchi wanahudumiwa na wanataaluma kwa namna ambayo ni salama, Kuhakikisha kuwa mahusiano kati ya mgonjwa na Daktari yanakuwa ya kuaminiana, Wanataaluma wanapata mafunzo na elimu ya kujiendeleza (CPD) ili waendane sanjari na maendeleo ya sayansi na teknolojia yanayotokea duniani pamoja na Baraza kuhakikisha lina kumbukumbu na taarifa sahihi za wanataaluma linaowasajili na ambazo zinaweza kupatikana kirahisi ili kuhakikisha jamii inapata taarifa sahihi ya wanataaluma wanaoruhusiwa kutoa huduma.

Mwisho, Waziri Ummy amelitaka Baraza hilo kuwa na wajibu wa kutangaza majina ya wanataaluma wenye usajili halali na unaoendana na wakati.

MWISHO

Jumanne, 9 Juni 2020

UGONJWA WA CORONA UNAELEKEA KUISHA NCHINI-WAZIRI UMMY

- Hakuna maoni








Na WAJMW-DOM

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu amesema ugonjwa wa Corona unaelekea kuisha nchini ambapo mikoa zaidi ya 15 haijaripoti mgonjwa yeyote wa Corona kwa zaidi ya wiki.

Waziri Ummy amesema hayo leo wakati alipotembelea kituo cha afya cha Mkonze kilichotengwa kwa ajili ya kuwahudumia watu waliopata maambukizi ya ugonjwa wa Corona jijini Dodoma na kukuta vitanda vikiwa tupu bila kuwa na mgonjwa yeyote kwa zaidi ya wiki.

Waziri Ummy amesema kupitia Waganga wakuu wa Mikoa 15 nchini wamethibitisha kutokua na mgonjwa wa Corona na Mikoa mingine yenye wagonjwa imeripoti kuwa wagonjwa hao wanaendelea vizuri.

Aidha, Waziri Ummy amewashukuru watoa huduma za afya wa kituo cha Mkonze kwa kazi nzuri walioifanya ya kuwahudumia wagonjwa na kuchukua tahadhari zilizosaidia wahudumu hao kutopata maambukizi ya Corona.

Pamoja na hayo Waziri Ummy amesema licha ya ugonjwa wa Corona kuelekea kumalizika nchini, amewataka wananchi kutobweteka na kuendelea kuchukua tahadhari kwa kuzingatia maelekezo yanayotolewa na wataalam wa afya ikiwemo kunawa mikono mara kwa mara kwa sabuni na maji tiririka pamoja na kuvaa barakoa za vitambaa wanapokua kwenye mikusanyiko.

Jumamosi, 30 Mei 2020

HONGERENI WATUMISHI WOTE WA AFYA KWA JINSI MLIVYO PAMBANA KATIKA JANGA LA CORONA.

- Hakuna maoni
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel akisisitiza jambo wakati akiongea na Watumishi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma (hawapo kwenye picha).

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel akiteta jambo na Mkurugenzi wa tiba Wizara ya Afya Dkt. Grace Maghembe, wakati alipofanya ziara ya kuongea na Watumishi wa Sekta ya Afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.

Mkurugenzi wa tiba Wizara ya Afya Dkt. Grace Maghembe akiteta jambo na Mkururugenzi msaidizi anaesimamia hospitali za Rufaa Dkt. Caroline, wakati alipofanya ziara ya kuongea na Watumishi wa Sekta ya Afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.

Baadhi ya Watumishi kutoka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma wakifuatilia neno kutoka kwa Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel pindi alipofanya ziara katika Hospitali hiyo. 

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel akimjulia hali mtoto aliefika na mzazi wake kupata matibabu katika wodi ya watoto, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel akiwa na baadhi ya Watumishi kutoka Wizara ya Afya, katika chumba cha Watoto njiti, katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma. 

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel akimjulia hali mama aliyempeleka mtoto kupata matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma. 

 Picha ya pamoja ikiongozwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel akiwa na viongozi kutoka Wizara ya Afya na Watumishi wa Afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma pindi alipofanya ziara ya kuongea na Watumishi hao.

Jengo la Idara ya magonjwa ya wanawake na uzazi Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.



HONGERENI WATUMISHI WOTE WA AFYA KWA JINSI MLIVYO PAMBANA KATIKA JANGA LA CORONA.

Na WAMJW- DOM

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel amewashukuru Watumishi wote wa Sekta ya Afya nchini kwa namna walivyojitoa katika mapambano dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona.

Dkt. Mollel ameyasema hayo leo, wakati alipofanya ziara ya kuongea na Watumishi wa Sekta ya Afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma na Hospitali ya Rufaa ya kanda ya kati ya Benjamin Mkapa Jijini Dodoma.

"Jinsi ambavyo nyie mmepambana dhidi ya virusi vya Corona na bado mkamuunga mkono Mhe. Rais na ushauri alioutoa yeye na Wataalamu wengine wa Wizara kupitia Waziri wa Afya, nyie mmekuwa mashujaa na jeshi la uzalendo wa hali ya juu, nawashukuru sana" alisema Dkt. Mollel.

Dkt. Mollel aliendelea kwa kukemea tabia za wanasiasa wachache kupotosha Watanzania na Dunia kwa ujumla juu ya kupata maambukizi ya ugonjwa wa Corona kwa Watumishi wa Sekta ya Afya nchini jambo ambalo sio kweli.

"Kuna wanasiasa wanapiga kelele kuhusu Corona kuliko sisi, nawaomba watu tuache kupiga siasa, sisi watumishi wa afya ndio watu wakwanza kukutana na wagonjwa wa Corona laikini leo watumishi mpo 504 je niambieni kuna yoyote amelazwa, watumishi walijibu hapana, kama kweli kuna Watumishi wanakufa basi nyie mngekuwa wa kwanza kuugua na kupoteza maisha" alisema.

Aidha, Dkt Mollel alitoa wito kwa Watumishi wa Sekta ya Afya nchini kufanya kazi kwa bidii katika kuwahudumia wananchi ili kutoa huduma bora, huku akiweka wazi kuwa kazi ya kuwahudumia wananchi ni ya wito na ya uzalendo.

Pia, Mhe Mollel alielezea kuwa Rais alikuwa na maono ya kusitisha matibabu ya nje ya nchi kwa kuboresha huduma za kibingwa nchi na hii imejizihirisha baada ya dunia kupata janga la corona nchi yetu imeendelea kutoa huduma za kibingwa pasipo kutegemea matibabu ya nje kwa wananchi ambao walikuwa na sifa za kutibiwa nje .

Nae Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma Dkt. Ibenzi Ernest ameweka wazi kuwa Hospitali hiyo imeendelea kutoa huduma za Afya bila kutetereka na kutoa elimu kwa umma licha ya kupitia katika kipindi cha mlipuko wa virusi vya Corona ulioikumba nchi.

"Tumeendelea kutoa huduma bora kwa wananchi bila kutetereka hata katika wakati huu wa janga la mlipuko wa maambukizi ya virusi vya Corona ulioikumba nchi, Watumishi wetu wamesimama imara huku wakiendelea kutoa elimu ya kujikinga dhidi ya Corona "alisema.

Jumatano, 20 Mei 2020

WAZIRI UMMY AMESEMA UGONJWA WA KIFUA KIKUU UNAENDELEA KUPUNGUA NCHINI

- Hakuna maoni




Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya Hadubini 7 za kuchunguza kifua kikuu zilizotolewa na Wizara kwa Wilaya ya Chamwino.
Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akiongea jambo na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Bilinith Mahenge wakati wa hafla ya makabidhiano ya Hadubini 57 zilizotolewa na Wizara ya Afya katika Mkoa wa Dodoma. Hafla hiyo ilifanyika Wilayani Chamwino mkoani Dodoma.

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akikabidhi moja ya Hadubini za kuchungua ugonjwa wa kifua kikuu kwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Bilinith Mahenge, Mkuu wa Wilaya ya Chamwino Mhe. Vumilia Nyamaga, Mbunge wa Chilonwa Mhe. Joel Mwaka huku Mkurugenzi wa huduma za kinga Dkt. Leonard Subi akishuhudia.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Bilinith Mahenge na Mkuu wa Wilaya ya Chamwino Mhe. Vumilia Nyamaga wakibeba moja ya Hadubini zilizotolewa na Wizara ya Afya kwa Wilaya ya Chamwino.
Baadhi ya wananchi na wafanyakazi wa kituo cha afya cha Buigiri waliojitokeza kushuhudia makabidhiano ya Hadubini mpya za kupima kifua kikuu zilizotolewa na Wizara ya Afya.


Na WAJMW-Dodoma

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu amesema maambukizi ya Kifua Kikuu (TB) yamepungua nchini kutoka wagonjwa  164,000 mwaka 2015 hadi kufikia wagonjwa 142,000 mwaka 2018.

Waziri Ummy amesema hayo leo wakati akikabidhi Hadubini 57 katika Mkoa wa Dodoma zitakazotumika kufanya vipimo vya ugonjwa wa Kifua Kikuu ambazo zitasambazwa katika Hospitali na Vituo vya Afya mbalimbali mkoani humo.

“Leo nimeanza zoezi la kukabidhi Hadubini 941 zilizonunuliwa na Serikali kwa ufadhili ya Global Fund zenye thamani ya Tsh. Bilioni 3.3 ambapo leo nitamkabidhi Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Binilith Mahenge Hadubini 7 za Wilaya ya Chamwino zitakazosambazwa katika vituo vya Afya mbalimbali”. Amesema Waziri Ummy.

Pamoja na hayo Waziri Ummy ametumia muda huo kueleza mafanikio yaliyofikiwa na Mpango wa Taifa wa Kifua Kikuu na Ukoma ikiwa ni pamoja na kupungua maambukizi mapya kwa asilimia 18 lengo likiwa ni asilimia 20 na vifo vimepungua kwa asilimia 27 lengo likiwa ni asilimia 35.

Aidha, Waziri Ummy amesema ugunduzi wa Kifua Kikuu unaendelea kuimarika ambapo idadi ya wagonjwa waliogundulika na kuwekwa kwenye matibabu imeongezeka kutoka wagonjwa 62,180 mwaka 2015 hadi kufikia 82,,140 mwaka 2019.

Kwa upande wa vituo vya ugunduzi wa tiba, Waziri Ummy amesema katika kipindi cha miaka mitatu vituo vimeongezeka kutoka 662 mwaka 2016 hadi kufikia vituo 1201 mwaka 2019.

Katika kipindi cha miaka idadi ya wagonjwa waliogundulika kuwa na Kifua Kikuu imepungua kutoka wagonjwa 164,000 mwaka 2015 hadi 142,000 mwaka 2018.

Waziri Ummy amesema vifo vinavyotokana na TB vimepungua  kutoka makadirio ya vifo 30,000 mwaka 2015 hadi vifo 22,000 mwaka 2018.

Waziri Ummy ameongeza kuwa Hadubini hizo zitapelekwa katika vituo vipya vya kutolea Huduma za afya 487 ambavyo vimejengwa, Hospitali za Mikoa 3, Hospitali za Wilaya 69 pamoja na vituo vya afya vya zamani 315 pia kubadilisha hadubini zilizoharibika katika vile vituo vyenye uhitaji.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Binilith Mahenge ameishukuru Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa kutambua ulazima wa kuwepo Hadubini hizo katika maeneo mbalimbali ya kutolea huduma za afya lengo likiwa ni kuondoa usumbufu kwa wananchi kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma hiyo.

MWISHO

MSIBWETEKE KATIKA MAPAMBANO DHIDI YA UGONJWA WA CORONA

- Hakuna maoni
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Rashid Mfaume akipokea msaada wa barakoa 17,500 na vipukusi lita 700 kutoka kwa Mwakilishi Mkazi kutoka Shirika lisilo Lakiserikali la Medipeace Tanzania Bi. Sukyung Kim leo Jijini Dar es Salaam.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Rashid Mfaume akiwa ameshika box la barakoa 17,500 na vipukusi lita 700, kulia ni, Mwakilishi Mkazi kutoka Shirika lisilo Lakiserikali la Medipeace Tanzania Bi. Sukyung Kim.



MSIBWETEKE KATIKA MAPAMBANO DHIDI YA UGONJWA WA CORONA.

Na Rayson Mwaisemba, WAMJW- DSM

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Rashid Mfaume ametoa wito kwa wananchi, hususan Jijini Dar es Salaam kutobwete na kuwataka kuendelea kuchukua hatua za tahadhari ili kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona katika kipindi hiki.

Dkt. Rashid Mfaume ametoa wito huo leo, wakati akipokea msaada wa barakoa 17,500 sawa na maboksi 350, na vipukusi (sanitizers) lita 700 ambayo ni sawa na madumu 140 yenye ujazo wa lita 5 kutoka kwa Shirika lisilo Lakiserikali la Medipeace linalohusika na mradi wa mama na mtoto katika Mkoa wa Dar es Salaam.

"Licha ya elimu tunayoendelea kutoa juu ya namna ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona, tunawahamasisha wananchi wasibweteke katika kipindi hiki, ili kuumaliza kabisa ugonjwa huu katika nchi yetu, na hili linawezekana kabisa" alisema

Dkt. Rashid Mfaume aliendelea kusema kuwa, Msaada huo utaelekezwa katika vituo vya kutolea huduma za Afya vya Sinza Hospitali, Vijibweni Hospitali, Rangi Tatu Hospitali, Kituo cha afya Kimara, Kituo cha afya Tandale, Kituo cha afya Mbezi, Kituo cha afya Round table, Kituo cha afya Kimbiji, Kituo cha afya Buguruni, Tegeta Dispensari, Bunju Dispensari.

Aidha, amefafanua kuwa, kumekuwa na ongezeko la wagonjwa katika vituo vya kutolea huduma za Afya, hususan katika Jiji la Dar es Salaam baada ya Serikali kuziteua baadhi ya Hospitali kuwa vituo vya kutolea huduma za Corona, hivyo kuelekezwa msaada huo katika vituo vya Afya kutasaidia mapambano dhidi ya maambukizi mapya ya Corona.

"Sasa hivi tumeona wagonjwa wameongezeka sana katika vituo vya kutolea huduma za Afya, mfano katika Mkoa wa Dar es Salaam baada ya Serikali kuitangaza Hospitali ya Amana kuwa kituo cha kuhudumia wagonjwa wa COVID-19, wagonjwa wengi wamekuwa wakienda katika vituo vingine, hivo msaada huu utasaidia sana kupambana dhidi ya maambukizi mapya" alisema.

Mbali na hayo, Dkt. Mfaume amewataka Wadau wengine kutoka Mashirika mbali mbali nchini kuendelea kuisaidia Serikali vifaa kinga vya kupambana dhidi ya ugonjwa wa Corona ili kuvisaidia vituo vya kutolea huduma za Afya vyiweze kujitosheleza mahitaji hayo, hasa kutokana na vituo vya Afya kuwa sehemu inayopokea watu tofauti kwa wingi.

Hata hivyo, Dkt. Mfaume amewatoa wasi wasi Wananchi kuwa, hali ya Afya katika Mkoa wa Dar es Salaam ni shwari, huku akisisitiza kuwa Serikali inaendelea kuchukua tahadhari za karibu dhidi ya maambukizi hayo ili kuumaliza kabisa ugonjwa huo nchini.

Nae, Mwakilishi Mkazi kutoka Shirika lisilo Lakiserikali la Medipeace Tanzania Bi. Sukyung Kim amesema kuwa, Medipeace inayofadhiliwa na KOICA imekuwa ikishirikiana na Wizara ya Afya pamoja na TAMISEMI katika kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto katika mkoa wa Dar-es-salaam.

Aliendelea kusema kuwa, kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa homa kali ya mapafu unaosababishwa na virusi vya Corona, Shirika hilo linaunga mkono juhudi za Serikali za kupambana dhidi ya maambukizi ya virusi hivyo kwa kutoa vifaa kinga ambavyo vitasaidia kwa Watoa huduma za Afya na wagonjwa wataofika kupata matibabu katika vituo hivyo.

Mwisho.

Jumanne, 12 Mei 2020

SAFISHA VITASA KATIKA MAENEO YA BIASHARA NA MAKAZI YETU

- Hakuna maoni
Mfanyabiashara wa duka la dawa baridi, eneo la Tabata Jijini Dar es Salaam akisafisha kitasa na kioo cha duka lake ikiwa ni sehemu ya maeneo hatarishi kupata virusi vya Corona kutoka na kushikwa mara kwa mara na wateja.

 Dereva boda boda eneo la Bagamoyo mjini. Bw. Octavian Leonard Nyoni akisafisha mikono yake kwa maji safi yanayotiririka na sabuni ikiwa ni sehemu ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona.

 Timu ya uhamasishaji kutoka Wizara ya Afya, kwa kushirikiana na Wadau kutoka Shirika lisilo Lakiserikali la Project CLEAR wakiendelea na uhamasishaji kwa wananchi wa eneo la kituo cha mabasi cha Bagamoyo Mkoa wa Pwani, jinsi ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona.

Sfaff sergeant (S/Sgt ) Valentine Ngowi, akitoa maelekezo namna ya kukaa mita moja au zaidi baina ya mtu mmoja na mwingine katika eneo la kituo cha mabasi ya Bagamoyo, ikiwa ni moja ya njia ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona.

Abiria katika kituo cha mabasi cha Kisarawe Mkoa wa Pwani wakisafisha mikono kwa sabuni na maji safi yanayotiririka na wengine kwa kutumia sanitizer kabla ya kupanda basi na kuanza safari, wamefanya hivo ikiwa ni sehemu ya mapambano dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona.

Balozi wa kampeni ya Mikoni safi, Tanzania salama, Msanii Mrisho Mpoto (Mjomba), akimkabidhi vipeperushi vya elimu juu ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona kwa Afisa Afya wa Wilaya ya Kisarawe Mkoa wa Pwani, Kulia ni Mkuu wa Kitengo cha maji na usafi wa mazingira, Wizara ya Afya, Ndg. Anyitike Mwakitalima.

Ofisi za Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe Mkoa wa Pwani.


SAFISHA VITASA KATIKA MAENEO YA BIASHARA NA MAKAZI YETU

Na WAMJW- PWANI

Mkuu wa Kitengo cha maji na usafi wa mazingira, Wizara ya Afya, Ndg. Anyitike Mwakitalima ametoa wito kwa Watanzania wote kujenga tabia ya kusafisha vitasa na maeneo yote yanayoshikwa mara kwa mara katika maeneo ya shughuli za kila siku na makazi yetu.

Ndg. Anyitike ameyasema hayo wakati akitoa elimu kwa wakazi wa Kisarawe na Bagamoyo Mkoa wa Pwani, kuhusu kuchukua tahadhari za kujikinga dhidi ya maambukizi ya homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya Corona katika maeneo ya biashara na makazi.

"Tuhakikishe tunasafisha maeneo yote tunayoyashika mara kwa mara kwa maji yenye sabuni, sanitizer au spirit, futa maeneo yote yanayoshikwa mara kwa mara, lakini kumbuka kufuta sehemu za vitasa vya mlango na meza " alisema

Pia, alisisitiza kuwa, ni muhimu kujenga tabia ya kufuta katika maeneo yote ambayo watu wanapendelea kukaa kama vile maeneo ya viti, meza na vioo katika maeneo ya biashara bila kusahau milango.

Aidha, Ndg. Anyitike Mwakitalima ametoa rai kwa wananchi hususan vinyozi katika maeneo ya saluni kuhakikisha wanavaa Barakoa (mask) pindi wanapokuwa katika maeneo yao ya kazi, ili kuvunja mnyororo wa maambukizi Corona kutoka mtu mmoja kwenda kwa mwingine endapo utakuwepo.

"Unapoenda saluni usikubali kinyozi yoyote akunyoe nywele kama hajavaa Barakoa hali itayosaidia kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa Corona katika maeneo ya kazi na kuvunja mnyororo wa maambukizi ya virusi hivyo" alisema.

Nae, Sfaff sergeant (S/Sgt ) Valentine Ngowi, ameendelea kuwakumbusha wazazi na walezi, kuhakikisha wanawalinda Watoto dhidi ya ugonjwa wa Corona, kwa kuwapa elimu, na kuhakikisha hawazululi hovyo mtaani, hasa katika kipindi hiki ambacho shule zimefungwa ili kuepusha misongamano inayoweza sababisha kusambaa kwa ugonjwa wa Corona.

"Tuhakikishe Watoto wanakaa nyumbani, Watoto wasiende kuzulula hovyo, ni rahisi Watoto kupata maambukizi ya Corona kwasababu ya ufahamu na uelewa wao juu ya madhara ya ugonjwa huu wa Corona " alisema.

Kwa upande wake, Balozi wa kampeni ya Mikoni safi, Tanzania salama, Msanii Mrisho Mpoto (Mjomba) amewaasa wafanyabiashara wa Barakoa kutoruhusu wateja kujaribu barakoa na kuzirudisha, hali inaweka wanunuzi wengine katika hatari yakupata maambukizi ya virusi vya Corona.

" kwa wauzaji wa Barakoa, chonde chonde usiruhusu mtu ajaribu Barakoa alafu akaiacha, hii itasaidia kuvunja mnyororo wa maambukizi ya virusi vya Corona kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mtu mwingine endapo atatokea mtu mwenye maambukizi" alisema.

Timu ya Wizara ya Afya na Wadau kutoka Shirika lisilo Lakiserikali la Project CLEAR kupitia kampeni ya Mikono Safi, Tanzania Salama imeendelea kutoa elimu ya kujikinga dhidi ya maambukizi ya virusi vya Corona katika, Wilaya ya Bagamoyo, Wilaya ya Kisarawe na Wilaya ya Kibaha Mkoa wa Pwani.

Mwisho.

Ijumaa, 8 Mei 2020

SERIKALI ITAENDELEA KUTOA TAKWIMU ZA MWENENDO WA UGONJWA WA CORONA

- Hakuna maoni



Picha mbalimbali zikimuonesha Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akiangalia namna watoa huduma wanavyopokea simu kutoka kwa wananchi kwa ajili ya kupata elimu kuhusu ugonjwa wa Corona

Waziri Ummy Mwalimu akiongea na mwananchi  kupitia kituo cha afya cha huduma kwa wateja mara baada ya kukizindua
Picha ya pamoja ikionesha Waziri Mhe. Ummy Mwalimu akiwa na viongozi na wafanyakazi wa kituo cha afya cha huduma kwa wateja.

Na. WAMJW,Dar es Salaam.

Serikali itaendelea kutoa takwimu za mwenendo kuhusu Ugonjwa wa Corona mara baada ya kukamilika kwa maboresho ya kiufundi ya Maabara ya Taifa ya Afya ya Jamii.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati akizindua kituo cha Afya cha huduma kwa wateja (Afya call center) kilichopo eneo la Chuo cha Afya ya Sayansi ya Jamii Muhimbili (MUHAS), upanga Dar es Salaam.

“Takribani siku Saba sasa hatukuweza kutoa taarifa za takwimu za maabara  kuhusu mwenendo wa Corona nchini kwa sababu sasa hivi tunafanya maboresho  ya  maabara ya taifa ya afya ya jamii,hivyo niwatoe hofu wananchi kwamba ndani ya siku chache zoezi litakamilika na tutaendelea kutoa taarifa kwa umma mara kwa mara”, alisema.

Waziri Ummy amesema kuwa Corona ipo na itaendelea kuwepo kwa  miezi kadhaa,pia kumekuwepo na vifo kutokana na ugonjwa huu, hivyo wananchi wanapaswa kujua namna ya kuishi na ugonjwa huo kwa kujikinga na maambukizi.

 “Ninawasihi wananchi muondoe hofu na muendelee kuchukua tahadhari  ya kujikinga kwani ugonjwa wa Corona bado upo Tanzania, wagonjwa wapo na vifo vinavyotakana na COVID-19  vipo, ni muhimu kutambua kuwa ugonjwa huu utaendelea kuwepo kwa miezi kadhaa hivyo lazima mchukue tahadhari ya kujikinga kama magonjwa mengine”Alisisitiza Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy amewataka wananchi kuendelea na  shughuli zao za ujenzi wa Taifa za kila siku pamoja na kuchukua tahadhari kwa  kuepuka  mikusanyiko isiyo ya lazima, kunawa mikono kwa sabuni na maji yanayotiririka, na kukaa umbali wa mita moja kati ya mtu na mtu mwingine.

Kuhusu Uvaaji wa barakoa, Waziri huyo amewataka wananchi kuendelea kuvaa   barakoa za vitambaa ili kujikinga na maambukizi ya ugonjwa huo na kuwa barakoa za viwandani ziachwe zitumike kwa ajili ya watoa huduma za afya.

Amewashauri wananchi kufua na kupiga pasi barakoa za vitambaa kabla ya kuzitumia na kusisitiza kuwa zinapaswa kuwa safi kabla ya kuvaliwa.

MWISHO

Alhamisi, 7 Mei 2020

DKT. NDUGULILE AIAGIZA NIMR KUFANYA UTAFITI KUHUSU UGONJWA WA CORONA

- Hakuna maoni

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Faustine Ndugulile akizungumza katika mkutano na watafiti wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR juu ya maambukizi ya ugonjwa wa Corona.
Waziri wa Afya, Dkt. Ndugulile akifafanua jambo baada ya kumalizika kwa mkutano kujadili jinsi ya kupambana na Covid-19 nchini. Kushoto ni Mkurugenzi Mkuu wa NIMR, Prof. Yunus Mgaya.






Dkt. Ndugulile akijadiliana jambo pamoja na watafiti wa taasisi hiyo mara baada ya kumalizika kwa mkutano huo.

WAMJW- Dar es Salaam                                                                           

Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeitaka Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) kufanya utafiti kuhusu ugonjwa wa Corona (Covid-19) kwa kuwa kuna tofauti kubwa ya dalili zilizojitokeza kwa wagonjwa hapa nchini ukilinganisha na wagonjwa waliopo nje ya  nchi.

Agizo hilo limetolewa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Faustine Ndugulile wakati alipokutana na watafiti wa taasisi hiyo wakati  wakijadili maambukizi ya ugonjwa wa Corona na aina ya matibabu ambayo wagonjwa wanatakiwa kupatiwa hasa baada ya kubainika kuwa dalili za ugonjwa huo zinatofautiana na dalili za wagonjwa wa mataifa mengine.

“Kuna mambo mengi ambayo tunapaswa kuyafanyia utafiti wa kisanyansi, moja ni uelewa wa jamii, tunataka kujua wagonjwa wanaougua Corona ni wagonjwa wa namna gani, wana magonjwa ya aina gani, dalili zinazowapata wagonjwa ni za aina gani.  Hapa tunataka tupate uwelewa,” amesema Dkt. Ndugulile.

Pia, amesema kupitia utafiti huo wanataka kujua aina za matibabu ambayo wagonjwa wanatakiwa kupatiwa ili kuhakikisha ugonjwa wa Covid-19 unadhibitiwa hapa nchini.

“Kutokana na muitikio mkubwa wa tiba asili na tiba mbadala, kupitia kikao hiki nawaelekeza wataalamu wetu wajipange kufanya utafiti na kutoa majibu ya tiba ya maambukizi ya virusi vya Corona,” amesema Dkt. Ndugulile.

Amesema wamekubaliana na watafiti hao kufanyia kazi maagizo hayo ndani ya muda mfupi na kutoa majibu sahihi ambayo yatasaidia katika mapambano ya ugonjwa wa Corona.

Naye Mkurugenzi Mkuu  wa NIMR, Prof. Yunus Mgaya amesema mapambano dhidi ya ugonjwa Covid-19  ni vita ambayo inapaswa kufanyiwa utafiti ambao utasaidia kupatikana kwa njia sahihi za kukabiliana na maambukizi ya ugponjwa huo.

“Tunafahamu kwamba jamii za kiafrika zina utaalamu katika miti shamba. Katika hili kuna tafiti mbalimbali zinaendelea ili kuchunguza uwezo wa miti shamba kwa lengo la kupunguza makali ya Covid-19.

Mwisho

Jumanne, 5 Mei 2020

VIFO VYA WATOTO WACHANGA VIMEPUNGUA KUTOKA 25 KWA KILA VIZAZI HAI 1000 HADI SABA KWA KILA VIZAZI HAI 1000

- Hakuna maoni
Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akizungumza wakati akipokea msaada wa vifaa kinga,vipeperushi,mabango na vifaa vya kutoa elimu kwa umma kwa ajili ya watoa huduma za afya na waandishi wa habari nchini

Waziri Ummy Mwalimu ameishukuru UNESCO na bank ya Absa kwa msaada wao.Kutoka kulia ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya Prof. Mabula Mchembe na kulia kwa Waziri  ni Mkurugenzi wa Rasiliamali watu kutoka banki ya Absa Tanzania Ltd. Patrick Foya

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto-Idara Kuu Afya Prof.Mabula Mchembe akiongea wakati wa kupokea msaada kutoka UNESCO na Benki ya Absa Tanzania Ltd


Mwakilishi Mkazi wa UNESCO nchini Tanzania, Tirso Dos Santos akikabidhi msaada wa vifaa kinga pamoja na vifaa vya elimu kwa umma kwa ajili ya waandishi wa habari


Na WAMJW – Dar es Salaam

Vifo vya watoto wachanga wenye umri wa chini ya siku 28 vimepungua kutoka 25 kwa kila vizazi hai 1000 kwa mwaka 2015/16 na kufikia saba  kwa kila vizazi hai  1000 kwa mwezi Machi mwaka huu.

Hayo yamesemwa leo  jijini  jijini Dar es Salaam na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati akipokea msaada wa vifaa kinga, mabango,vipeperushi na vifaa vya  kutoa elimu kwa Umma kuhusu ugonjwa wa Corona kutoka kwa Benki ya Absa Tanzania Ltd na Shirika  la UNESCO.

Waziri Ummy alisema kupungua kwa vifo hivyo kumetokana na jitihada zilizofanywa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli  katika kuimarisha sekta ya afya hapa nchini hii ni pamoja na kuboresha vituo vya kutolea huduma za afya, upatikanaji wa dawa, vifaa na vifaa tiba.

“Kwa namna ya kipekee niwapongeza na kuwashukuru wakunga wote hapa nchini kwa kazi kubwa na nzuri wanayoifanya kila siku ya kuwahudumia akina mama wajawazito na watoto  wenye umri chini ya miaka mitano”,.

“Pamoja na kuwa maambukizi ya Virusi vinavyosababisha ugonjwa wa Corona (COVID-19) yapo na watu wanaumwa ugonjwa huu, lakini tusisahau kuwa kina mama wajawazito wanajifungua kila siku na wakunga  wanaendelea kuwahudumia kinamama hawa”, alisisitiza Waziri Ummy.

Waziri huyo aliwahakikishia wananchi kuwa pamoja na kuwa ugonjwa wa Corona upo   huduma zingine zinaendelea kama kawaida  katika vituo vituo vyote vya kutolea huduma za afya zikiwemo huduma za kliniki za akina mama wajawazito na watoto, upimaji wa magonjwa mbalimbali pamoja na upasuaji.

 “Ninawashukuru wadau mliotoa vifaa hivi, ninawaomba wadau wengine waendelee kuiunga mkono Serikali katika kupambana na ugonjwa wa Corona ambao ni janga la Dunia”,.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa wizara  hiyo Prof. Mabula Mchembe alisema  vifaa hivyo vitaboresha  utoaji wa huduma za afya katika vituo vilivyopo Dar es Salaam pamoja na maeneo mengine nchini.

“Ninawahakikishia wananchi pamoja na wadau mliotoa vifaa hivi kuwa  vitatumiwa na wataalamu wetu katika kutoa huduma mbalimbali za matibabu kwa wagonjwa wanaotibiwa katika vituo vyetu vya afya”, alisema Prof. Mchembe.

Akikabidhi vifaa hivyo Mkurugenzi wa  Rasiliamali watu wa benki ya Absa Tanzania Ltd. Patrick Foya alisema vifaa kinga walivyovitoa vyenye thamani ya milioni 20 ambavyo ni glovu, barakoa na vitakasa mikono vitawasaidia watoa huduma za afya wakati wanawahudumia wagonjwa.

Mwisho