Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Ijumaa, 21 Desemba 2018

WANANCHI WAASWA KUPIMA UGONJWA WA HOMA YA INI

- Hakuna maoni

Mwanafunzi wa chuo cha Mt. Joseph (kushoto) akipata chanjo ya homa ya ini kutoka kwa mtaalam wa afya toka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (kulia)

Mratibu wa chanjo ya Homa ya Ini kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road Dkt. Kandali Samuel (kushoto) akizungumza jambo na Mhadhiri wa Chuo cha Mt. Joseph Prof. Fred Mhalu (kulia) wakati wa zoezi la uchunguzi na utoaji chajo ya homa ya ini kwa wafanyakazi na wanafunzi wa Chuo cha Mtakatifu Joseph.

Dkt. Kandali Samuel akizungumzia kuhusu ugonjwa wa homa ya ini na athari zake kwa waandishi wa habari wakati wa zoezi la uchunguzi na utoaji chajo ya homa ya ini kwa wafanyakazi na wanafunzi wa Chuo cha Mtakatifu Joseph.

Wanafunzi wa chuo cha Mt. Joseph Jijini Dar Es Salaam wakijitokeza kupata elimu, uchunguzi wa afya zao na chanjo ya homa ya ini katika zoezi liliondeshwa na madaktari kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road.


Na WAMJW - Dar Es Salaam

Wananchi watakiwa kupima afya zao mara kwa mara kubaini magonjwa mbali mbali nyemelezi ikiwemo ungojwa wa homa ya ini ambao watu wengi bado hawana uelewa nao.

Hayo yamesemwa na Mratibu wa Chanjo ya Homa ya Ini kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Dkt Kandali Samuel alipokuwa katika Chuo cha Sayansi ya Afya Cha Mtakatifu Jospeh Jijini Dar Es Salaam wakati wa uchunguzi na utoaji wa chanjo ya homa ya ini kwa wafanyakazi na wanafunzi wa chuo hicho.

Akizungumza na wanahabari, Dkt. Kandali Samuel amesema kuwa wamefika katika Chuo hicho kutoa huduma ya uchunguzi wa virusi aina ya Hepatitis B vinavyosababisha ugonjwa wa Homa ya Ini.

 “Kirusi cha Hepatitis B ni miongoni mwa virusi vinavyoshambulia ini na kusababisha homa ya ini, kirusi hiki ni hatarai na kinaweza kupelekea magonjwa mbalimbali ya ini ambayo hudhoofisha ini na kusababisha magonjwa ya ziada na kushusha utendaji kazi wa ini” amesema Dkt. Kandali.

Hata hivyo Dkt. Kandali amesema kuwa mtu anaweza kuishi muda mrefu bila kugundua kuwa ana ugonjwa huo ambao dalili zake huwa hazijionyeshi kwa kipindi cha muda mfupi kulingana na kinga ya mtu. “Virusi hivyo huweza kusabababisha athari kubwa kwenye mwii wa binadamu na hadi kusababisha saratani ya ini” alisema Dkt. Kandali.

Dkt Kandali amesema kuwa takwimu za ugonjwa huo nchini zinaonyesha kuwa asilimia 4.4 ya watanzania wanaishi na maambukizi ya virusi vya Hepatitis B ambapo kati ya watu 20 mmoja ana virusi hivyo.

Akifafanua namna maambukizi ya ugonjwa huo hutokea, Dkt Kandali amesema kuwa ugonjwa wa homa ya ini huambukizwa kupitia maji maji na damu kutoka kwa mtu mwenye virusi vya Hepatitis B kwenda kwa mtu mwingine kwa njia ya kujamiina, kutumia vitu vyenye ncha kali kwa zaidi ya mtu mmoja au kutoka kwa mama mzamzito kwenda kwa mtoto wakati wa kujifungua.

Aidha Dkt. Kendali amesema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Afya inaandaa mwongozo ambao utawezesha uchunguzi wa mgonjwa toka amepata maambukizi ili kuwezesha tafiti kubaini athari nyinginezo zinazoweza kuambatana na ugonjwa huo huku taasisi ya Saratani Ocean Road kwa sasa ikijikita katika utoaji wa kinga dhidi ya ugonwja huo.

“Watu wengi wanajua kazi ya ini ni kuchuja sumu, endapo ini likifeli hata ufanyaji kazi ya kuchuja sumu na madawa mwilini pia huathirika. Ini pia linachangia katika kutengeneza chembe nyekundu za damu kwa kutengeneza protini” Alisema Dkt. Kendali na kuwataka wananchi kuchunguza afya zao mara kwa mara.

Naye Mhadhiri kutoka Idara ya Mikrobailojia na Kinga chuoni hapo Profesa Fred Mhalu amesema kuwa kinga ni bora zaidi kuliko tiba kwani hutusaidia kwa kutukinga na maradhi yanayoletwa na vimelea au virusi nyemelezi.  “Ugonjwa wa ndui umekwisha na polio karibia inakwisha ni kutokana na utaratibu mzuri wa kingatiba uliowekwa wa kujikinga na magonjwa hayo kupitia chanjo” alifafanua Profesa Mhalu.

Kwa upande wake Bw. Bonaventure Mattogo, Rais Serikali ya wanafunzi chuoni hapo amesema kuwa zoezi hilo limepokelewa kwa furaha na wanafunzi wote na kuishukuru Serikali kupitia Taasisi ya Saratani ya Ocean Road kuja na mpango huo. 

“Magonjwa yanayosababishwa na virusi yapo mengi lakini ugonjwa huu wa homa ya ini chanjo  yake inapatikana, ni vyema watu wakajitokeza katika hospitali zetu kupata chanjo hii ambayo hutolewa mara moja ambayo hukupa ulinzi dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa homa ya ini kwa kipindi cha maisha yako yote” alisema Bw. Mattogo

Mwisho.

Jumanne, 18 Desemba 2018

TFDA YAFIKIA NGAZI YA TATU YA UDHIBITI WA DAWA KIMATAIFA.

- Hakuna maoni
 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu (kulia) akipokea waraka wa utambuzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa-TFDA ya kufikia ngazi ya nne ya udhibiti wa bidhaa za dawa kutoka kwa Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania Dkt. Tigest Ketsela Mengestu (kushoto).

 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu (kulia) akipokea waraka wa utambuzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa-TFDA ya kufikia ngazi ya nne ya udhibiti wa bidhaa za dawa kutoka kwa Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania Dkt. Tigest Ketsela Mengestu (kushoto).
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akifafanua jambo kwa waandishi wa habari (hawapo pichani) kuhusu hali ya udhibiti wa bidha za dawa chini ya TFDA.


Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) Dkt. Tigest Ketsela Mengestu akisoma taarifa ya hali ya udhibiti wa dawa nchini kwenye kikao na waandishi wa habari (hawapo pichani) katika ofisi za Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA)

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini Bw. Adam Fimbo (aliyesimama) akisema jambo kwenye mkutano na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati wa kupokea waraka wa utambulisho wa mamlaka hiyo kufikia ngazi ya nne ya udhibiti wa dawa nchini.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akisoma waraka kwa utambuzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa-TFDA ya kufikia ngazi ya nne ya udhibiti wa bidhaa za dawa. aliye upande wa kushoto ni Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania Dkt. Tigest Ketsela Mengestu.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (kushoto) akisikiliza maoni toka kwa mteja Bw. Fareh Abdul mkazi wa Dar es Salaam aliyefika katika ofisi za Mamlaka ya Chakula na Dawa kupata huduma.

Picha ya pamoja Mgeni Rasmi, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu aliye meza kuu katikati akiwa na viongozi mbali mbali pamoja na wajumbe wa mkutano.


Na WAMJW - Dar Es Salaam.


Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini (TFDA) imetambuliwa rasmi na Shirika la Afya Duniani (WHO) kufikia ngazi ya tatu ya ubora wa mifumo ya udhibiti wa dawa na kuifanya Tanzania kuwa nchi ya kwanza barani Afrika kufikia hatua hiyo.

Hayo yamejiri leo wakati Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari wakati upokeaji wa waraka wa utambulisho wa ngazi ya tatu kwa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) toka WHO.

“Tunaposema ngazi ya tatu ya udhibiti wa bidhaa za dawa maana yake ni kuwa Tanzania sasa tumepiga hatua katika upatikanaji wa dawa bora, zilizo salama na zenye ufanisi pale tuu ambapo zitakapo kuwa zimethibitishwa na TFDA” amesema Waziri Ummy.

Waziri huyo amesema kuwa dawa yoyote ambayo imetengenezwa aidha ndani au nje ya Tanzania na kuthibitishwa, kukaguliwa na kupewa cheti na TFDA maana yake dawa hiyo ni bora, salama na yenye ufanisi uliokusudiwa kwa matumizi ya binadamu.
 “Kama ni dawa ya kutibu ugonjwa wa malaria basi ni dawa ya kutibu malaria kweli na si vinginevyo” alisema Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy ameipongeza TFDA kwa kufikia hatua hiyo na kusema serikali itaendelea kuboresha mifumo iliyopo ili kuondoa dawa zisizofaa kwa matumizi ya binadamu.

Naye Mwakilishi Mkazi wa Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzaina Dkt. Tingest Ketsela Mengestu amesema kuwa ni jambo la kujivunia kwa Tanzania kuwa nchi ya kwanza barani Afrika kuwa na mfumo mzuri wa udhibiti wa bidhaa za dawa.

“Nachukua nafasi hii kuipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kuweka mazingira mazuri yaliyoleta mafanikio haya. TFDA imefanya maboresho makubwa kwa kuhakikisha dawa zilizopo katika soko ndani ya Tanzania zina usalama, ubora na ufanisi wa hali ya juu kwa matumizi ya binadamu” amesema Dkt. Tingest.

Tangu kuanzishwa kwake mnamo mwaka 2003, Mamlaka ya Chakula na Dawa nchini (TFDA) imekuwa ikijiwekea mikakati ya kuboresha mifumo ya utendaji ili kuweza kutoa huduma bora kwa wananchi.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA) Bw. Adam Fimbo amesema kuwa Tathimini mbalimbali zimefanyika kutoka taasisi tofauti duniani kukagua mifumo ya umahiri katika ukaguzi wa vyakula na dawa hivyo kupelekea mamlaka hiyo kufikia ngazi ya tatu.

“Nchi nyingi bado zinasita kuwaita WHO kuwafanyia tathimini lakini sisi tuliamini tunaweza kufanyiwa tathimini kutokana na mifumo mizuri tuliyoiweka” alisema Bw. Fimbo na kuendelea kwa kusema kuwa “hatua hii ni kubwa, sasa Tanzania imeingia katika kundi la nchi chache duniani ambazo zimefikia ngazi ya tatu”

Mwisho

WAZIRI UMMY AGAWA BIMA ZA MATIBABU KWA WATOTO 900 NCHINI

- Hakuna maoni
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu akisisitiza jambo mbele ya Watoto wanaoishi katika Mazingira magumu na Walezi wao (hawapo kwenye picha) wakati wa kukabidhi Bima za Matibabu kwa Watoto hao wanaoishi katika Mazingira magumu Mkoani Dar es salaam

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu akiteta jambo na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Dkt. Grace Magembe wakati wa kukabidhi Bima za Matibabu kwa Watoto wanaoishi katika Mazingira magumu Mkoani Dar es salaam

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu akimkabidhi Bima ya Matibabu mmoja kati ya watoto wanaoishi katika Mazingira magumu wakati wa sherehe za kukabidhi Bima za Matibabu kwa Watoto wanaoishi katika Mazingira magumu jijini Dar es salaam.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu akiwa katika picha ya pamoja na Watoto wanaoishi katika Mazingira magumu wakati wa saherehe za kukabidhi Bima za Matibabu kwa Watoto hao leo katika makao ya Watoto UMRA, Magomeni Mikumi jijini Dar es salaam.




Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu akiwa na wafanyakazi wa Benki ya  Stanbinc, wakati wa sherehe za kukabidhi Bima za Matibabu kwa Watoto wanaoishi katika Mazingira magumu jijini Dar es salaam.


Na WAMJW - DSM
 
HOTUBA MGENI RASMI WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO, MHESHIMIWA UMMY ALLY MWALIMU (MB) KATIKA SHEREHE YA KUKABIDHI BIMA ZA MATIBABU KWA WATOTO WANAOISHI KATIKA MAZINGIRA MAGUMU MKOANI DAR ES SALAAM: MAKAO YA WATOTO UMRA, MAGOMENI 

TAREHE 17/12/2018

Ndugu Dkt. John Jingu  Katibu Mkuu, WAMJW, Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii;
Ndugu Ken Cockkerill - Afisa Mtendaji Mkuu wa Stanbic Bank; 
Mganga Mkuu Mkoa wa Dar es Salaam;
Ndugu Bernard Konga  Mkurugenzi Mtendaji wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya; 
Afisa Ustawi wa Jamii Mkoa wa Dar es Salaam;
Ndugu Francisca Makoye Afisa Ustawi wa Jamii Mkuu  Manispaa ya Ilala, Dar es Salaam;
Viongozi  wa Siasa na Watendaji Wakuu wa Serikali;
Ndugu Rahma Juma Kishumba  Kiongozi Mlezi wa Makoa ya Watoto UMRA;
Ndugu Viongozi na Waratibu wa Huduma za Ustawi wa Jamii kutoka Manispaa za Mkoa wa Dar es Salaam;
Ndugu Viongozi wa Makao na Taasisi za Malezi ya Watoto Wanaishi katika Mazingira Magumu;
Ndugu Wanahabari na Wasanii;
Ndugu Wageni Waalikwa;
Ndugu Wananchi.

Asalaam Aleykum, 
Watotoooooo  (Wataitikia  Kwanzaaaaa!!)

Ndugu Wananchi; 
Awali ya yote, naomba tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana hapa Makao ya Watoto UMRA Magomeni. Leo ni siku kubwa na muhimu kwa watoto wote nchini na hususan kwa Watoto Wanaoishi Katika Mazingira Magumu. Hivyo basi inatupasa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa dhati kwa kutupatia Fursa hii ambapo LEO kwa Msaada wa Benki ya STANBIC tunawapatia Bima za Matibabu Jumla ya Watoto 900 nchini. Kati yao, Mkoa wa Dar es Salaam tunawapatia Bima za Matibabu Jumla ya Watoto 500.

Ndugu Wananchi; 
Napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru kwa dhati Benki ya Stanbic kwa moyo wao wa kizalendo wa kuamua kuwalipia Bima za Afya Watoto Wanaoishi Katika Mazingira Hatarishi. Msaada huu ni muhi sana kwao katika kuhakikisha kuwa wanapata malezi na makuzi bora, hivyo kujiwekea hazina yenye afya bora kwa taifa letu miaka inayokuja.

Vile vile ninawashukuru kwa dhati wenzetu wa Mfuko wa Bima ya Afya kwa kuchukua hatua za haraka katika kupokea, kuchambua na kuhakiki na kupitisha orodha ya majina ya watoto ambayo Wizara yangu iliyapendekeza kupatiwa vitambulisho vya Bima ya Afya. Kasi na umakini mlio onyesha katika kukamilisha zoezi hili inaakisi sawa sawa kauli Mbiu ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ya Hapa ni Kazi Tu!

Ndugu Wananchi;
Leo ni siku maalumu kwa watoto wetu wapendwa. Kwa msingi huu sijanuia kutoa hotuba ndefu za kitaalamu kama ambavyo huwa ninafanya katika hadhira nyingine za watu wazima. Hata hivyo ngoja nieleze mambo machache ya msingi hapa chini.

Ndugu Wananchi;
Kupitia Sera ya Afya 2007, Serikali imeendelea kutoa kipaumbele katika huduma za afya zenye ubora na zinazowafikia wananchi wote ili kuboresha afya zao. Serikali inatambua umuhimu wa afya bora kwa wananchi wake kwani afya bora ni raslimali muhimu kwa maendeleo. Kitendo cha kuwapatia Bima ya Afya Watoto wetu leo hii, ni mojawapo ya jitihada za Serikali kwa kukushirikiana na Wadau kama STANBIC BANK katika kuhakikisha kuwa wananchi wote iwemo wale wa makundi maalumu ya uhitaji wanapata Huduma Bora za Afya.

Ndugu Wananchi;
Napenda kuchukua fursa kusisitiza kuwa Maendeleo ya Taifa letu la Tanzania yataletwa na wananchi wenye afya na wenye uwezo wa kuzalisha mali. Katika kuhakikisha kuwa wananchi wana afya bora, Serikali imeendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kutoa huduma za afya kwa kuzingatia sera na miongozo iliyopo. 

Ndugu Wananchi;
Hivyo basi naomba nitoe Wito kwa wengine wa Maendeleo and Sekta Binafsi hapa nchini kuiga mfano wa moyo wa kujitolea kwa kuwasaidia Watanzania wenzetu wasiojiweza kupata mahitaji yao ya msingi ikiwemo uhakika wa kupata huduma bora za afya.

Ndugu Wananchi;
Kama Waziri mwenye dhamana wa kusimamia uendeshaji wa Makao ya Kulelea Watoto Wenye Shida, nachukua fursa hii pia kuueleza Umma wa Watanzania na Wamiliki wa Makao haya juu umuhimu wa kuzingatia Sheria na Kanuni husika. Hili likifanyika vyema, litasaidia kuwa na Makao yanayotoa huduma bora za malezi na makuzi kwa watoto ambao wametoka kwenye shida nyingi maishani mwao. 

Ndugu Wananchi;
Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto inalojukumu la uratibu wa uanzishwaji na uendeshaji wa Vituo vya Kulelea Watoto Wadogo Mchana na Makao ya Watoto walio katika mazingira hatarishi kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto Na. 21 ya mwaka 2009. Lakini, Pamoja na uwepo wa sheria hii kumekuwepo na changamoto ya uanzishaji na uendeshaji wa Vituo na Makao usiozingatia  sheria na kanuni za uanzishaji wa huduma hizi.

Ndugu Wananchi; 
Katika kuhakikisha kuwa Tanzania inakuwa na Makao Bora ya watoto wenye shida, yenye uwezo wa kuwapatia mahitaji yao ya msingi kama vile Afya Bora ninatoa maelekezo yafuatayo;
Natoa tamko kuwa mamlaka husika katika kila Halmashauri kwa uratibu wa Maafisa Ustawi wa Jamii, wavifunge mara moja Vituo vyote, Makao yote yanayoendeshwa kinyume na sheria. 
Wamiliki wa Vituo na Makao haya watii matakwa ya sheria ya kuwasilisha taarifa za utekekezaji za Mwezi, Robo Mwaka na Mwaka kama ilivyoanishwa katika Kanuni;
Kuanzia sasa ni marufuku kwa mtu yoyote au Shirika kuanzisha Vituo vya Kulelea Watoto Wachanga Mchana na  Makao ya Watoto bila kibali cha Mamlaka husika; 
Wakurugenzi wa Majiji, Manispaa na Halamashauri za Wilaya kupitia kwa Maafisa Ustawi wa Jamii kufanya Ukaguzi wa Vituo hivi na kuwasilisha taarifa za ukaguzi kila mwezi kwa Msajili ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa, ikiwemo kufunga Vituo visivyokidhi vigezo.
Wamiliki wa Vituo hivi kuzingatia Sheria na Kanuni katika utoaji wa huduma na kujiepusha kutumia huduma hii kwa manufaa binafsi;
Jamii inapaswa kuelewa kuwa familia ndiyo mahala salama kwa malezi ya watoto. Hivyo baba, mama na walezi wa watoto hawana budi kuwajibika ipasavyo kulea watoto wao.

Ndugu Wananchi; 
Kama nilivyotangulia kusema awali leo ni siku muhimu wa Watoto Wanaoishi Katika Mazingira Magumu, na watoto wote kwa ujumla katika nchi yetu. Maelekezo ya kuzingatia sheria na taratibu husika niliyotoa hapo juu yanatosha kuwafungua masikio wakorofi wachache wasiopenda kufuata taratibu. 

MWISHO

Ndugu Wananchi;
Narudia tena kuwashukuru kwa dhati Benki ya STANBIC KUWAPATIA ZAWADI BORA YA KRISTMASI WATOTO WETU KWA KUWAPATIA BIMA ZA AFYA.

ASANTENI SANA KWA KUNISIKILIZA SASA NIPO TAYARI KUWAKABIDHI KADI ZA BIMA YA AFYA WATOTO WETU WAPENDWA.

WAZIRI UMMY AZINDUA BODI MPYA YA WAFAMASIA

- Hakuna maoni
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu akisisitiza jambo mbele ya Wajumbe na viongozi wa Baraza la Wafamasia (Hawapo kwenye picha) wakati wa uzinduzi wa Baraza jipya la Famasia leo katika Ofisi ndogo za  Wizara jijini Dar es salaam

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu akimkabidhi zawadi mmoja kati ya  Wajumbe wa Baraza la Wafamasia wakati wa uzinduzi wa Baraza jipya la Famasia leo katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es salaam

Wajumbe wa Baraza la Wafamasia wakiwa katika kikao cha uzinduzi wa Baraza jipya la Famasia kilichofunguliwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu leo katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es salaam.

Wajumbe wa Baraza la Wafamasia wakifuatilia kwa makini maelekezo kutoka kwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy Mwalimu wakati kikao cha uzinduzi wa Baraza jipya la Famasia, leo katika Ofisi ndogo za Wizara jijini Dar es salaam.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Na Watoto, Mhe. Ummy katika picha ya pamoja na Sekretarieti ya Baraza la Wafamasia baada ya kikao cha uzinduzi wa Wajumbe wapya wa Baraza la Famasi katika Ofisi ndogo za Wizara Jijini Dar es salaam.


Na WAMJW-DSM 

HOTUBA YA MHE. UMMY MWALIMU (MB) WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO WAKATI WA UZINDUZI WA BARAZA JIPYA LA FAMASI
KATIKA UKUMBI WA WIZARA TAREHE 17 NOVEMBA, 2018

Mwenyekiti wa Baraza la Famasi uliyemaliza muda na wa sasa; 
Wajumbe wa Baraza la Famasi waliomaliza muda na wanaoingia kazini;
Wakurugenzi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na  Wazee;  
Msajili wa Baraza la Famasi;
Wasajili kutoka Bodi na Mabaraza chini ya Wizara;
Watumishi wa Wizara pamoja na Sekretarieti ya Baraza;
Wageni waalikwa;
Wanahabari;
Mabibi na Mabwana.

Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kutukutanisha siku hii ya leo. Pili nitoe shukrani zangu za dhati kwa kunipa nafasi ya kukutana na kuzungumza pamoja nanyi na  kuzindua Baraza Jipya la Famasi ambalo ni la awamu ya nne (4) tangu Baraza hili kuanzishwa rasmi mwaka 2003.

Aidha, nichukue nafasi hii kwa niaba yangu binafsi na ya Wizara kuupongeza uongozi wa Baraza chini Mwenyekiti Ndugu Legu Mhangwa kwa moyo wa kujitolea na kufanya kazi nzuri pamoja na changamoto zilizokuwepo.  Ni ukweli usiofichika kwamba mmefanya kazi nzuri katika kulijenga Baraza la Famasi.

Nimesikiliza kwa makini mafanikio mbalimbali ambayo Baraza limeyapata kufuatia maelezo yaliyotolewa na Mwenyekiti aliyemaliza muda wake pamoja na Msajili wa Baraza na kwamba, pamekuwepo na umuhimu wa kufanya mapitio ya kanuni na miongozo mbalimbali ambayo imeonekana imepitwa na wakati ili kwenda sambamba na mabadiliko ya sasa.

Katika muda wa miaka mitatu (3) mliyotumika, Baraza limeonyesha uwezo mkubwa wa kudhibiti taaluma na wanataaluma, kusimamia na kudumisha maadili na miiko ya taaluma ya famasi, pamoja na usimamizi wa utoaji wa huduma za dawa na hivyo kuendeleza na kuboresha uhai wa fani ya famasi.

Pamoja na maboresho hayo niwapongeze kwa kupandishwa hadhi kwa Baraza na kuwa taasisi inayojitegemea.  Hii inaonesha jinsi mlivyoweza kuweka juhudi katika kujisimamia na kuongeza ufanisi kiutendaji katika majukumu yenu. Kwa kuwa baadhi yenu mmemaliza wajibu wenu leo, ninawasihi kutokana na uzoefu mlioupata katika kipindi cha miaka mitatu, muendelee kutoa ushauri kwa wajumbe wapya ambao wanakabidhiwa majukumu haya ili kufanikisha malengo na madhumuni ya kuwepo kwa Baraza hili.


Mabibi na Mabwana,
Kwa moyo wa dhati nawapongeza wajumbe wapya ambao mnakabidhiwa majukumu hivi leo, Wizara yangu na Serikali kwa ujumla tuna matarajio makubwa katika kipindi hiki cha miaka mitatu (3) ambacho mtakuwa na jukumu hili kubwa la kuishauri Wizara katika mambo kadha wa kadha ya taaluma hii na hatimaye kuboresha utoaji wa huduma za dawa katika vituo na sehemu mbalimbali zinazofanya shughuli hizi kwa mujibu wa Sheria.

Mabibi na Mabwana, 
Ni imani yangu kubwa kuwa wengi wenu katika Baraza lililotangulia na hili la sasa mnafahamu fika majukumu yenu kama yalivyoainishwa katika Sheria ya Famasi, Sura 311 inayounda Baraza hili. Sitakuwa na sababu ya kuyataja, ila nashauri muweze kurejea kwenye sheria hiyo ambayo katika hayo nisisitize kushirikiana na taasisi mbalimbali ambazo kwa namna moja au nyingine zinagusa masuala ya taaluma hii ikiwa ni pamoja na mafunzo ya wanataaluma wa fani hii ili kutosababisha migongano ya kiutendaji ya ndani na nje ya Wizara zinazohusika.

Mabibi na Mabwana,
Pamoja na kazi nilizozitaja hapo juu, jukumu la Baraza la Famasi ni kuleta msukumo wa utoaji huduma bora ya afya kwa mtanzania.  Hili linawezekana kwa kuhakikisha kuwa wanataaluma wanazingatia maadili na nidhamu ya taaluma katika ununuaji, utunzaji na matumizi sahihi ya dawa na vifaa tiba vilivyo salama na ubora wa hali ya juu. 
Vile vile, napenda nisisitize kuwa Baraza lione umuhimu wa kuweka msukumo wa pekee kwenye masuala ya kuboresha mafunzo na elimu ili  tuwe na wanataaluma  wenye uwezo wa utendaji wa kiwango cha hali ya juu katika nchi yetu katika maeneo yote ikiwamo uzalishaji wa dawa Viwandani ili kwenda sambamba na adhima ya Serikali kuelekea uchumi wa Viwanda.

Mabibi na Mabwana,
Napenda kuwahakikishia kuwa, jamii ya watanzania wanahitaji huduma hii, hali inaonesha kuwa, kupitia takwimu mbalimbali zaidi ya 40% ya wananchi wanapopata tatizo la afya huanza kwenda kupata huduma ya awali kwenye maduka ya dawa (famasi na maduka ya dawa muhimu), hivyo basi kushindwa kuwa na huduma bora katika maeneo hayo  na inahatarisha kwa kiasi kikubwa maisha ya wananchi. 

Wizara inalitambua hili na umuhimu wa kuwepo kwa fani hii hapa nchini. Kwa kushirikiana na kada nyingine za afya huduma za afya zitaendelea kuboreka na kuthaminiwa katika maeneo yetu ya kazi. 

Mabibi na Mabwana,
Wataalam wa fani ya famasia ndio wahusika wakuu katika masuala yote yanayohusu dawa katika kuhakikisha kuwa dawa zinapatikana katika hospitali na vituo vyote vya kutolea huduma za afya nchini. Serikali kwa upande wake imeongeza bajeti ya Dawa kutoka Shilingi bilioni 30 mwaka 2015/2016 hadi Tsh 270 Bilioni mwaka 2018/2019, hivyo ni Wataalamu hawa wa Famasi wanaotakiwa kuhakikisha kuwa ongezeko la bajeti linaenda sambamba na upatikanaji wa dawa na matumizi sahihi kwa kuzingatia miongozo ya tiba. Ni dhahiri kuwa utaalamu wa kutengeneza, uagizaji, usafirishaji, usambazaji, utoaji dawa sahihi  kwa wagonjwa, utunzaji na utoaji mafunzo yahusuyo dawa ndiyo msingi mkubwa wa taaluma hii. Hivyo basi Baraza ambalo ndilo lililopewa dhamana ya kusimamia kazi za utendaji wa taaluma hii kuongeza nguvu za usimamizi na udhibiti wa sheria na miongozo  na kuhakikisha kazi za wataalamu hawa zinafuata miiko na taratibu za kitaaluma zilizowekwa na zinafanyika kwa uangalifu; na kuchukua hatua zinazostahili pindi inapogundulika kuna ukiukwaji wa Sheria na taratibu

Pia ni wajibu wa wanataaluma kuwa mfano mzuri kwa jamii wanayoihudumia ili kujenga imani na kudumisha uhusiano mzuri na jamii wanazozihudumia.  

Wageni Waalikwa,
Kuhusu migogoro ambayo nimekuwa nikiisikia kati ya Baraza na Wafanya biashara wa Maduka ya Dawa ni vyema tuchukue hatua za haraka ili kuondoa changmoto hizo na katika hili naelekeza Baraza tufanya yafuatayo:
Maduka ya Dawa yasiyo na vibali yaliyopo katika maeneo yasiyoruhusiwa kuendesha maduka ya ADDO, kwa sasa yapewe muda wa mpito wa miaka miwili (2) kuanzia tarehe ambayo utatoa taarifa hiyo kwa umma;
Katika kipindi hicho maduka hayo yauze dawa zisizohitaji cheti cha Daktari (general sales medicines) kwa utaratibu ambao utaandaliwa na Baraza la Famasi kwa masharti kwamba endapo watakiuka utaratibu huo hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yao;
Baada ya muda huo kupita, maduka haya yatatakiwa aidha kufungwa, kupandishwa hadhi kuwa Famasi au kuhamia maeneo yanyoruhusiwa ADDO na kuendelea kutoa huduma hiyo; na
Wamiliki wa Maduka ya Dawa ambayo yapo katika maeneo yanayoruhusiwa kuendesha ADDO wayapandishe hadhi maduka yao mara moja.

Mabibi na Mabwana,
Napenda kuwahakikishia kuwa yote yatawezekana kama sisi sote tutakubaliana kusimamia na kutekeleza suala la uwazi na ukweli (Transparency & Good Governance). Nawasihi kuendelea kushirikiana na nchi nyingine ili kupata uzoefu zaidi wa namna bora ya kusimamia taaluma hii ya Famasia.

Hitimisho,
Mwisho ningependa kuwahakikishia kwamba Wizara ipo tayari kuwasaidia katika mipango iliyopo na ile mtakayoipendekeza kwa serikali kulingana na hali halisi ya uwezo. Niwatakie Baraza jipya linalozinduliwa leo utekelezaji mzuri wa majukumu yenu. 

Baada ya kusema hayo machache, sasa natamka kuwa Baraza la Famasi limezinduliwa rasmi. 

Asanteni kwa Kunisikiliza.

Alhamisi, 13 Desemba 2018

WAZIRI UMMY AZUNGUMZA NA WAZIRI WA AFYA WA FALME YA MOROCCO




Picha mbalimbali zikimuonesha Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu-Tanzania leo akikutana na kufanya mazungumzo  na waziri wa Afya wa Falme ya Morocco, Prof. Anass Doukkali ambapo wamezungumzia masuala mbalimbali ya ushirikiano kwenye sekta ya Afya baina ya nchi hizo.

WAZIRI UMMY MWALIMU AHUDHURIA MKUTANO UNAOJADILI AFYA YA MAMA NA MTOTO NCHINI INDIA



Picha mbalimbali zikimuonesha Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akishiriki mkutano maalum wa mawaziri wa afya kuhusu afya ya mama na mtoto unaofanyika jijini New Delhi nchini India ulioanza tarehe 12-14 Desemba 2018. Mkutano huo unajadili afya ya mama na mtoto "4th Partnership for Maternal, Newborn and Child Health 2018".

SERIKALI YATOA RAI KWA WANANCHI KUJITOKEZA KUPATA DAWAKINGA YA MATENDE NA MABUSHA

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Faustine Ndugulile akisisitiza jambo mbele ya waandishi wa Habari (Hawapo kwenye picha) wakati akitoa tamko kuhusu kampeni ya kumeza dawa kingatiba ya magonjwa ya minyoo ya Tumbo, Usubi, Trakoma na Matende na Mabusha katika mikoa saba hapa nchini.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Faustine Ndugulile akitoa tamko kuhusu kampeni ya kumeza dawa kingatiba ya magonjwa ya minyoo ya Tumbo, Usubi, Trakoma na Matende na Mabusha katika mikoa saba hapa nchini, pembeni yake ni mratibu wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Dkt. Upendo Mungila

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Faustine Ndugulile akitoa tamko kuhusu kampeni ya kumeza dawa kingatiba ya magonjwa ya minyoo ya Tumbo, Usubi, Trakoma na Matende na Mabusha katika mikoa saba hapa nchini, pembeni yake ni mratibu wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Dkt. Upendo Mungila


TAMKO LA MHE. DKT. FAUSTINE NDUGULILE (MB.) NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO KUHUSU KAMPENI YA KUMEZESHA DAWA  KINGATIBA YA MAGONJWA YA MINYOO YA TUMBO, USUBI, TRAKOMA, MATENDE NA MABUSHA KATIKA MIKOA SABA (7) HAPA NCHINI. 

Ndugu Wananchi
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ikishirikiana na wadau itafanya kampeni ya kugawa dawa za Kingatiba ya magonjwa ya minyoo ya tumbo, usubi, trakoma, matende na mabusha katika mikoa saba (7) hapa nchini, ambayo ni Dar es Salaam katika Manispaa zote, Iringa wilaya ya Mufindi DC, Mtwara wilaya ya Masasi, Pwani wilaya ya Kibaha na Mafia, Rukwa wilaya ya Kalambo, Songwe wilaya ya Songwe na Tanga wilaya ya Mkinga na Korogwe. 
Lengo kuu la kufanya kampeni ni kutibu na kuzuia maambukizi ya magonjwa ya minyoo ya tumbo, Usubi, Trakoma, Matende na mabusha au Ngirimaji. Aidha, dawa hizi au kingatiba hii, zitasaidia kupungua kwa ulemavu na adha za magonjwa haya. Kuna faida kubwa kwa wananchi wakishiriki katika zoezi hili la umezaji kinga tiba hii. Faida hizo ni:
Kukinga upungufu wa damu.
Kumuepusha mtu kupata upofu.
Kupunguza maambukizi kutoka mtu mmoja kwenda kwa mwingine.
Kuua vimelea vya Magonjwa haya.
Kukinga na kupunguza maumivu na madhara yanayosababishwa na Magonjwa haya.
Kupungua kwa Magonjwa ya ngozi.
Kuongeza virutubisho bora mwilini.
Kuboresha nguvukazi katika jamii.
Kuwezesha watoto kukua vizuri.
Kuongeza uelewa wa watoto wawapo shuleni.

Ugonjwa wa Minyoo ya tumbo huathiri zaidi jamii maskini na husababishwa na mtu kula mayai ya minyoo kutoka katika udongo au minyoo hii kupenya kwenye ngozi. Aidha, Kuna minyoo ya aina tatu ambayo husababisha ugonjwa huu,minyoo mviringo,minyoo mijeledi  na minyoo ya safura. Pamoja na kutoa dawa za kutibu ugonjwa huu lakini pia jambo la msingi ni vyema wananchi mkaweka maeneo yanu katika hali ya usafi na kula vyakula vilivyopikwa vizuri na kuiva. 
Ugonjwa wa Usubi husababishwa na minyoo inayoitwa Onchocerca volvulus, huenezwa na inzi weusi wadogo wanaokaa kandokando ya mito yenye maji yaendayo kasi. Athali za ugonjwa huu ni ngozi kuwasha,  ngozi kuwa na mabakamabaka kama ya chui, ngozi kuwa na muonekano wa kenge, pia uono hafifu na upofu. 

Trakoma au vikope ni ugonjwa sugu unaoshambulia macho na kusababisha kope kupinda na kugusa kioo cha jicho ambapo husababisha makovu juu ya kioo cha jicho na hupunguza uwezo wa kuona na kusababisha upofu usiotibika. Ugonjwa huu husababishwa na bakteria aina ya Chlamydia trachomatis. 
Juhudi kubwa za kutokomeza ugonjwa wa Trakoma au Vikope zimefanyika na kuweza kupunguza kiwango cha maambukizi. Kati ya Wilaya 71 zilizokuwa na uambukizo, Wilaya 63 sawa na Asilimia Themanini na Tisa (89%) zimeweza kufikia kiwango cha chini  ya asilimia 5% ambayo inaruhusu kusimamisha zoezi la kingatiba ya Trakoma  katika ngazi ya Jamii. Katika mwaka huu wa 2018 ni Wilaya 8 tu ndio zinaendelea na zoezi la  Kingatiba ya  ugonjwa wa Trakoma kwa kutumia dawa aina ya Zithromax. 
Ugonjwa wa Matende na Mabusha husababishwa  na minyoo midogo midogo ambayo huenezwa na mbu wa aina zote kutoka kwa mtu mmoja kwenda kwa mwingine. 
Dalili za ugonjwa huu ni homa kali ambayo huchukua siku 3 – na huambatana na baridi kali, Kichefuchefu, kutapika, kuvimba kwa mitoki, kubabuka ngozi, kuvimba kwa miguu, mikono, matiti au sehemu za siri kwa jinsia zote.
Mafanikio katika kutokomeza ugonjwa wa Matende na mabusha yameanza kuonekana, kati ya Wilaya 120 ambazo zilikuwa na uambukizo, Wilaya 98 ambazo ni sawa na asilimia sabini na Saba (77) zimeweza kupunguza maambukizi ya ugonjwa huo na hivyo kufikia kiwango cha kusimamisha ugawaji wa kingatiba kwa jamii katika Wilaya hizo. 

Hii ina maana kwamba kwa mwaka huu 2018 ni wilaya 28 tu ndizo zitakuwa na zoezi la umezeji kingatiba kwa ajili ya kukinga na kutibu ugonjwa wa Matende na mabusha katika ngazi ya jamii. Magonjwa haya yasipopatiwa tiba haraka mtu anaweza kupata madhara kama:-
Maumivu ya muda mrefu na wakati mwingine ulemavu mkubwa.
Umaskini na kudumaza uchumi wa kaya na hatimaye Taifa.
Kudhoofisha ukuaji hasa kwa watoto wenye umri mdogo kimwili na kiakili.
Utapia mlo kwa watoto
Utumbo kujisokota 
Hatimae kifo kama mgonjwa hakutibiwa.

Ndugu Wananchi
Pamoja na kwamba ugawaji wa dawa utafanyika katika mikoa saba (7) hapa nchini, napenda nijikite sana katika kuelezea umezaji wa dawa katika mkoa wa Dar es Salaam kwa mwaka huu wa 2018. Hii siyo mara ya kwanza kwa mkoa huu kufanya zoezi la umezaji wa dawa Kingatiba ya minyoo ya tumbo, matende na mabusha. Zoezi hili kwa mkoa wa Dar es Salaam lilianza mwaka 2013 na limekuwa likitekezwa kila mwaka. Katika mwaka wa kwanza watu wapatao 3,028,828 walijitokeza na kupatiwa kingatiba hii. Idadi hii imekuwa ikiongezeka kila mwaka zoezi linapotekelezwa na kwa mwaka jana 2017, watu waliojitokeza kupatiwa kingatiba walikuwa 4,914,351 ambayo ni sawa na asilimia 86 (86%) ya lengo lililotarajiwa.  
Ingawa kiwango cha umezaji wa dawa hizi kwa jamii kimeendelea kuwa juu, lakini idadi ya watu wanaojitokeza kwenye zoezi hili bado haijaridhisha sana kutuwezesha kutangaza kwamba tutatokomeza magonjwa haya katika mkoa wa Dar es Salaam, bado maambukizi yapo juu ya kiwango cha asilimia mbili (2%). Lengo la mwaka huu ni kugawa dawa watu wapatao 5,376,207 katika Manispaa zote tano (5) za Mkoa wa Dar es Salaam. 

Kama wizara tumeweza kuwezesha rasilimali za dawa na fedha za utekekelezaji wa kampeni hi muhimu. Aidha tumeweza kusaidiana na wenzetu wa TAMISEMI kufanya uhamasishaji kwa ngazi mbalimbali kwa viongozi wa jamii, kata na mitaa. Kampeni hii itawapa fursa wanajamii kupunguza uambukizo wa magonjwa haya na hatimaye kuwa jamii kuwa huru na vimelea vya magonjwa haya kwa vizazi vijavyo. 
Kampeni hii kwa mwaka huu, itahusisha wakazi wote wa Mkoa wa Dar es Salaam na wageni waliopo katika Jiji hili wenye umri wa kuanzia miaka mitano (5) na kuendelea. Dawa zitakazotolewa ni aina Albendazole kidonge kimoja (kitatafunwa) na Ivermectin (Mectizan)  ambayo itatolewa kulingana kimo chake . 
Ndugu Wananchi
Napenda kuwataarifu kuwa kampeni hii itaendeshwa kuanzia tarehe 15  hadi 20 mwezi Disemba, 2018 kwa watu wenye umri uliotajwa hapo juu. Napenda kusisitiza kuwa viongozi wa ngazi zote ikiwa ni pamoja na ngazi ya jamii wanawajibika kutoa taarifa hii na kuhamasisha wananchi wote washiriki kikamilifu katika kampeni. Aidha, katika kufanikisha zoezi hili nawasishi wananchi na viongoziu wote kutumia njia mbalimbali za mawasiliano kama vile vyombo vya habari, kuhamasisha wananchi makanisani na misikitini  kujitokeza kushiriki zoezi hili.
Aidha, wanachi mtambue kuwa vituo vya kutolea huduma hizi vimesogezwa karibu jamii ili kurahisisha upatikanaji wa huduma. Ambapo Jumla ya vituo mia tisa kumi na tano (915) ambavyo ni pamoja na Zahanati, Vituo vya afya, Hospitali, stendi za mabasi, masoko, ofisi za serikali za mitaa, ofisi za taasisi mbalimbali pamoja na kambi za Majeshi yetu na Magereza vitatoa huduma hiin a takribani wagawa dawa Elfu moja mia nane thelathini (1,830) waliopatiwa mafunzo watahusika katika kutoa huduma hiyo kwenye vituo Mwisho napenda kutoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam na wa mikoa mingine ambayo zoezi hili litafanyika  kushiriki kikamilifu katika umezaji dawa hizi. Zoezi hili ni muhimu kwani magonjwa haya yanaathiri sana jamii yetu. Kwa viongozi wenzangu na wanahabari tunaomba muendelee kuelimisha umma kuhusu magonjwa haya na umuhimu wa umezaji wa kingatiba hii. 

LINDA, OKOA MAISHA, ZUIA ULEMAVU JITOKEZE KUMEZA DAWA-KINGATIBA’


Jumapili, 9 Desemba 2018

HOSPITALI MPYA 67 ZA WILAYA KUJENGWA NCHINI

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Faustine Ndugulile (wakati kati) akishuhudia makabidhiano ya mabenchi yakukalia, wakwanza kulia ni Meneja wa NMB kanda ya Dar es salaam Bw. Badru Idd  akimpa mkono Mwakilishi wa Mkurugenzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili Dkt. John Rwegasha katika tukio la makabidhiano ya mabenchi yakukalia 52 lililofanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es salaam.

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Faustine Ndugulile akiteta jambo na Meneja wa NMB kanda ya Dar es salaam Bw. Badru Idd katika tukio la makabidhiano ya mabenchi yakukalia 52 yenye thamani ya Mikioni 10, lililofanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es salaam.

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Faustine Ndugulile akikagua mabenchi hayo baada ya makabidhiano leo, katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es salaam.

Naibu Waziri wa Afya Dkt. Faustine Ndugulile akimuaga Meneja wa NMB kanda ya Dar es salaam Bw. Badru Idd  baada ya tukio la makabidhiano ya mabenchi yakukalia 52 yenye thamani ya shilingi Milion 10, lililofanyika katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es salaam.

Jengo la mahala pakupimzikia la Kitengo cha Dharura, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili


HOSPITALI MPYA 67 ZA WILAYA KUJENGWA NCHINI

Na WAMJW - Dar es salaam.

SERIKALI kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee ma Watoto inatarajia kujenga Hospitali za Wilaya 67, ikiwa ni mkakati na jitihada za Serikali kuboresha Huduma za Afya na kupunguza adha kwa wananchi kupata huduma za afya.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile leo wakati akipokea viti kwaajili yakupumzikia hospitalini, kutoka benki ya NMB katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili jijini Dar es salaam.

Dkt. Ndugulile amesema kuwa kwa sasa zipo Hospitali za Wilaya 80, hivyo Serikali imeamua kuongeza hospitali za Wilaya takribani 67 ikiwa ni mkakati wa kuboresha huduma za Afya hususani huduma za mama na mtoto.

"Mwaka huu tunajenga Hospitali za Rufaa, Mikoa ambayo haina, tunajenga Hospitali za Wilaya 67, na tunahospitali kama 80 za Wilaya," alisema Dkt. Ndugulile.

Dkt. Ndugulile aliendelea kusema kuwa Serikali imeboresha vituo vya Afya takribani 200 ili kusaidia kutoa huduma za upasuaji, hivyo kusaidia kupunguza msongamano wa wagonjwa kupata huduma katika Hospitali za Wilaya na za Rufaa za Mkoa.

Sambamba na hayo Dkt. Ndugulile ameishukuru Benki ya NMB kwa kutenga Asilimia 1 ya mapato yanayotoka kwenye faida kuelekeza kwenye Jamii ya Watanzania hususani katika huduma za Afya.

"Niwashukuru sana NMB bank, kwa kutenga mapato yenu na faida yenu kuielekeza kwenye jamii, na nimefurahi zaidi, kusikia kwamba mmewekeza zaidi katika huduma za Jamii, Sisi kama Serikali tunawapongeza" alisema Dkt Ndugulile

Dkt. Ndugulile aliendelea kusema kuwa vitawasaidia sana wagonjwa ambao wanatoka sehemu mbali mbali ya nchi kupata maeneo mazuri yakuweza kukaa wakati wagonjwa wao wakipata huduma za Afya, hivyo niwaombe sana msiishie hapo kwani bado kuna maeneo mengi yanahitaji msaada.

Nae Meneja wa NMB Kanda ya Dar es Salaam Bw. Badru Idd amesema kuwa benki ya NMB huwa inalipa fadhira kwa Jamii baada ya kupata faida, kwa kuleta maendeleo, ikiwemo kujenga miundombinu, na kuboresha huduma za Jamii ili watanzania waweze kunufaika na kutoka Benki yao ya NMB.

"Kwa mujibu wa taratibu za Benki ya NMB huwa tunatoa Asilimia 1% kwenye pato ambalo tumepata kwa mwaka huo, mathalani mwaka Jana tumeingiza milioni 94, hivyo tunatoa Asilimia 1% ya Milioni 94 na kuirudisha kwa Jamii" alisema Bw. Badru Idd.

Bw. Badru Idd aliendelea kusema kuwa hiyo Asilimia 1% ipo kwenye mafungu makubwa 3, kundi la kwanza NMB inapenda sana kutoa huduma kwenye sekta ya Afya, kundi la pili ni Sekta ya Elimu na kundi la tatu ni huduma kwenye majanga yanayotokea.

Mwisho.

Ijumaa, 7 Desemba 2018

WAUGUZI WANAOVUNJA MAADILI YA KAZI KUKIONA CHAMOTO

- Hakuna maoni
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe.Ummy Mwalimu akisisitiza jambo mbele ya wananchi wa Nanyumbu (hawapo kwenye picha), wakati wa ziara yake ya kukagua hali ya utoaji wa huduma za Afya na uhamasishaji kwa wananchi kujiunga na Bima ya Afya Mkoa wa Mtwara.
Waziri wa Afy, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe.Ummy Mwalimu akisoma cheti cha mtoto aliyefikishwa na baba yake Hospitali ya Wilaya Nanyumbu ili kupata huduma za Afya.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe.Ummy Mwalimu akiwasalimia wanafunzi wa shule ya awali pindi tu alipowasili kwaajili ya mkutano wa hadhara na wananchi wa Nanyumbu ili kusikiliza kero zao na kuwaeleza Maendeleo ya Sekta ya Afya kwaujumla.

Wananchi wa Nanyumbu wakiongozwa na Wazee waliojitokeza kumsikiliza Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe.Ummy Mwalimu pindi alipokuwa katika ziara yake ya kukagua hali ya utoaji wa huduma za Afya na uhamasishaji kwa wananchi kujiunga na Bima ya Afya Mkoa wa Mtwara.

Na WAMJW - Nanyumbu, Mtwara

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe.Ummy Mwalimu ametoa onyo Kali kwa Wauguzi wote kwenye vituo vya  kutolea huduma za afya nchini wanaovunja maadili na miiko ya kazi za uuguzi ikiwemo matumizi ya lugha chafu kwa wagonjwa na wanaowapiga akina mama wajawazito wakati wakijifungua.

Ameyasema hayo  wakati alipotembelea Hospitali ya Wilaya Nanyumbu, akiwa katika ziara yake Mkoani Mtwara ya kukagua hali ya utoaji huduma za Afya na uhamasishaji kwa wananchi juu ya umuhimu wa kujiunga na Bima ya Afya hasa katika msimu huu wa Biashara ya Korosho.

Waziri Ummy alisema kuwa Serikali kupitia Baraza la Uuguzi litawafutia usajili Muuguzi yeyote atakayegundulika ametenda kosa la kumpiga mama mjamzito au kumtolea lugha chafu wakati wa kujifungua.

"Tunataka kumjua huyo, ambae ni hodari sana wakupiga wanawake wajawazito, makofi wakati wakujifungua, kwa kweli huyo ni wa kumfukuza kazi, Mimi mkiniletea namfutia Leseni yake kabisa, hafanyi kazi Serikalini, hafanyi kazi Sekta Binafsi" alisema Waziri Ummy.

Pia, Waziri Ummy alitoa Maagizo kwa Mganga Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi wa Wilaya ya Nanyumbu Mhe.Hamis Dambaya kuhakikisha  Wauguzi na Watumishi wote wanavaa vitambulisho vya kazi wakati wote wakiwa eneo la kazi ili wananchi wanaokwenda kupata huduma za Afya waweze kuwatambua majina yao.

"Tumewaambia wavae vitambulisho, ili mtusaidie kutaja jina la Wauguzi wanaovunja maadili ya kazi zao, hapa naomba nisiwahukumu wote, Mganga Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi mpo hapa, nikirudi tena nisisikie kuna Muuguzi anapiga makofi wajawazito wanaokuja kujifungua" alisema Waziri Ummy.

Kwa upande mwingine Waziri Ummy amesema kuwa Serikali kupitia Wizara ya Afya italeta mashine mpya ya kisasa ya digitali ya X-Ray ndani ya miezi mitatu itayosaidia wananchi wa Nanyumbu hasa kutokana na Wilaya hiyo kuwa katika Bara bara kuu ya kutoka Masasi hadi Songea.

Aidha, Waziri Ummy ametoa Rai kwa wananchi wa Nanyumbu kuhakikisha kabla ya kufika Disemba 31 mwaka huu, kaya zote katika eneo hilo lazima liwe limejenga na kutumia choo bora ili kupunguza magonjwa ya Bakteria yanayoigharimu Serikali pesa nyingi katika matibabu na Dawa.

"Ndugu zangu nendeni pale Hospitali, katika kila Wagonjwa 100, Wagonjwa 60 wana magonjwa ya kuhara,magonjwa ya tumbo, magonjwa yanayohusiana na kiwango duni cha usafi, nimekuwa nikiimba wimbo huu tangu nikiwa Waziri wa Afya, na hapa tulipofikia ni agizo la Waziri Mkuu pindi alipokutana na maafisa Afya wa Halmashauri na Mkoa jijini Dodoma" alisema Waziri Ummy

Waziri Ummy aliendelea kusema kuwa akiwa kama Waziri wa Afya kazi kubwa aliyonayo ni kuhakikisha anawakinga watu wasiumwe na pale wanapoumwa waweze kupata Huduma Bora za Afya, lazima niwe mkali kwenye kinga, mimi ni Waziri wa Afya sio Waziri wa Wagonjwa" alisema Waziri Ummy.

Mwisho.

Alhamisi, 6 Desemba 2018

WAZIRI UMMY AAGIZA AFISA AFYA WA WILAYA ACHUNGUZWE KWA TUHUMA YA RUSHWA

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akisisitiza jambo kwenye kikao.  
Waziri wa Afya, Mhe.Ummy Mwalimu akikagua wodi ya akina mama na watoto.

Na WAMJW-NEWALA, MTWARA

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amemwagiza Mkuu wa Wilaya ya Newala Mhe. Aziza Mangosongo, Kumchunguza Afisa Afya wa Wilaya hiyo maarufu kwa jina la Mama Flora kwa tuhuma ya rushwa aliyochukua kutoka kwa Bw.Shaib Mussa kama adhabu  ya kutupa taka  hovyo.

Hayo yamefuatia baada ya Mwananchi aliyejitambulisha kwa jina na Shaibu Musa kutoa malalamiko yake mbele ya Mhe.Waziri ya kilipishwa  shilingi elfu 50,000 na Bibi Afya huyo  mwaka Jana.

Waziri Ummy alisema kuwa Watumishi wa Serikali hasa wa Sekta ya Afya ni lazima wajiepushe na vitendo vya Rushwa na kuacha tamaa zinazopelekea kuminywa kwa haki kwa baadhi Wananchi wanaotaka kupata huduma.

"Namtafuta mmoja ili nimtolee mfano kwa Tanzania nzima, bahati nzuri Mimi ni Mwanasheria, Kosa LA jinai halina muda, hata kama ni 2017, tunataka huyu mtu afuatiliwe, achunguzwe kama kweli shilingi 50,000 iliingizwa kwenye Halmashauri au haijaingia, tunataka Mazingira masafi lakini ile hela iende Serikalini" alisema Waziri Ummy.

Nae Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Bw. Bernard Konga amesema kuwa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) umeanza rasmi kampeni ya uandikishaji ya kijiji kwa kijiji katika Mikoa ya Mtwara na Lindi ili kuwawezesha wananchi hao kuwa kwenye utaratibu mzuri wa kupata huduma za matibabu.

Bw. Bernard Konga  aliendelea kusema kuwa, Wananchi wamekuwa wakiingia katika umasikini mkubwa kwa kulazimika kuuza mali za familia kwa lengo la kupata fedha za kugharamia huduma za matibabu.

"Nikuhakikishie Mheshimiwa Waziri na wananchi wote walioko hapa, timu yangu inaanza rasmi kampeni ya kijiji kwa kijini kuanzia wiki ijayo kwa lengo la kumfikia kila mkulima aliyeko katika Mkoa wa Mtwara na Lindi ili wananchi hawa wawe kwenye mfumo bora wa kupata huduma za matibabu wakati wowote, alisema Bw. Konga.

Konga  aliendelea kusema kuwa zaidi ya asilimia 80 ya wananchi wote wako kwenye sekta ya kilimo hususan maeneo ya vijijini na kwa kutambua umuhimu wa kulitunza kiafya kundi hili, Mfuko ulianzisha mpango maalum unaojulikana kwa jina la Ushirika Afya unaowawezesha kujiunga na huduma za NHIF kwa gharama nafuu.

Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto yupo Mkoani Mtwara  kwa ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma za Afya Pamoja na  uhamasishaji kwa Wananchi kujiunga na mfuko wa Bima ya Afya ya Taifa (NHIF) na Leo hii yupo Wilayani ya Newala.

Mwisho