Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumapili, 27 Januari 2019

TAASISI ZA DINI NI WADAU WAKUBWA WA SEKTA YA AFYA NCHINI

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Faustine Ndugulile(mwenye shati jeupe) akikata utepe wakati wa uzinduzi wa Zahanati ya St. Mary's Mivumoni wilayani Pangani, Tanga. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Pangani Bi. Zainab Abdallah Issa, aliye kulia ni Mhashamu Baba Askofu Anthony Banzi wa Kanisa Katoliki Jimbo la Tanga.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Faustine Ndugulile (kushoto) akipokea pongezi toka kwa Mhashamu Baba Askofu Athony Banzi wa Jimbo Katoliki Tanga (kulia) mara baada ya kuzindua Zahanati ya St. Mary's Mivumoni iliyopo katika Wilaya ya Pangani Mkoani Tanga

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Faustine Ndugulile akipokea baraka toka kwa Mhashamu Baba Askofu Banzi wakati wa misa ya kubariki Zahanati ya St. Mary's Mivumoni iliyoko Wilayani Pangani, Tanga.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Faustine Ndugulile akikagua vifaa katika Zahanati ya St. Mary's Mivumoni iliyoko WIlayani Pangani, Tanga mara  baada ya kuizindua.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Faustine Ndugulile (kushoto) akisalimiana na Mkuu wa WIlaya ya Pangani Bi. Zainab Abdallah Issa (kulia) mara baada ya kuwasili wilayani humo tayari kwa ziara ya kikazi.

NA WAMJW - Pangani, TANGA.

Pamoja na juhudi zinazofanywa na Serikali kuboresha sekta ya afya nchini, Taasisi za Dini bado ni wadau wakubwa wanaotegemewa na Serikali kuboresha Sekta hiyo kutokana na uwekezaji mkubwa wa miundombinu pamoja na utoaji wa  huduma ya afya nchini.

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile alipokuwa akizindua Zahanati ya St. Mary Mivumoni, inayomilikiwa na Masista wa Mtakatifu Francis wa Capuchin katika Kata ya Bushiri, Wilayani Pangani, Mkoa wa Tanga.

Dkt Ndugulile amesema kuwa Taasisi za Dini zina mchango mkubwa kwa maendeleo ya wananchi, kutokana na huduma za kijamii kama vile elimu na afya ambazo zimekuwa zikitolewa na madhebeu ya dini mbalimbali nchini na kusema kuwa Serikali itaendelea kutoa ushirikiano wa kutosha kuhakikisha ushirikiano uliopo unaleta manufaa kwa wananchi.

Akitaja takwimu za idadi ya vituo vya kutolea huduma za afya nchini, Dkt Ndugulile amesema kuwa “Takwimu zinaonyesha kuwa katika Sekta ya Afya, makanisa yana zahanati zaidi ya 791, vituo vya afya 160 pamoja na hospitali 116” na kuendelea “huu ni mchango mkubwa sana ambao haupaswi kupuuzwa bali kuenziwa na sisi tunashukuru sana” alisikika akisema Dkt. Ndugulile.

Aidha baada ya ukaguzi wa jengo hilo la zahanati, Dkt Ndugulile amefurahishwa kuona zahanati hiyo ina vifaa vya kisasa ambavyo vinaifanya kituo hicho kuvuka sifa za kuwa zahanati kutaka mchakato wa kuipandisha kuwa kituo cha afya huku uongozi wa zahanati hiyo ukiombwa kushughulikia suala la kuboresha miundombinu ya majengo ili kupata wodi za kulaza wagonjwa.

“Zahanati mliyojenga ni kubwa, nzuri na ina nafasi, tutakuwa hatujatenda haki kama tutaiacha ikiwa katika ngazi ya zahanati, tuweke malengo ya kuifanya kuwa kituo cha afya unaanza ili huduma nyingi za matibabu ziwe zinapatikana katika eneo hili” Alisema Dkt Ndugulile.

Kwa upande wake Mhashamu Baba Askofu Anthony Banzi wa Jimbo Katoliki Tanga amesema kuwa ni jambo la faraja kuona Taasisi za Dini zikishirikiana na Serikali katika kutoa huduma kwa jamii.

“Tunaishukuru sana Serikali kwa kutoa nafasi kwa mashirika ya dini kuweza kushirikiana na Serikali katika kutoa huduma kwa jamii zikiwemo elimu, afya pamoja na huduma nyingine” alisema Mhashamu Baba Askofu Anthony Banzi.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Pangani Bi zainab Abdallah Issa amesema kuwa uwepo wa zahanati hiyo itawasaidia wakazi wa mivumoni na Tarafa ya Madanga kwa ujumla kupata huduma za afya karibu na maeneo yao tofauti na awali ambapo walikuwa wanatumia muda mwingi kusafiri umbali mrefu kufata huduma za afya.

Kwa upande mwingine Dkt Ndugulile ametumia jukwaa hilo kuzungumzia mikakati iliyopo katika kuboresha sekta ya afya kwa upande wa bima ya afya ambapo amesema kuwa Serikali iko mbioni kuboresha mifumo ya bima ya afya itakayoiwezesha mwananchi mmoja na mwenza pamoja na wategemzi wanne kupata huduma za afya kwa gharama za shilingi 30,000, fedha ambayo itawaweza kupata huduma za matibabu kuanzia ngazi ya zahanati hadi hospitali ya Mkoa na kutoa rai kwa wananchi kujitokeza kwa wingi kukata bima ya afya pindi utaratibu huo utakapo anza  rasmi.

Jumamosi, 26 Januari 2019

5. HALI YA HUDUMA ZA AFYA NCHINI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2018

Naibu Waziri wa Afya, ,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akikagua vifaa vya kupima ugonjwa wa Ebola pindi alipotembelea uwanja wa ndege wa Mwalimu Nyerere jijini Dar Es Salaam.

5. Magonjwa ya Mlipuko

#Tanzania imeendelea kuwa salama licha ya tishio la kuwepo kwa Ugonjwa wa Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.

#Wizara imechukua tahadhari za kulinda mipaka yake. Hivyo, hakukuwa na mgonjwa yeyote aliyegundulika kuwa na Ebola nchini kwa mwaka 2017 na 2018.

#Aidha, Serikali imeendelea na mapambano dhidi ya ugonjwa wa Kipindupindu ambapo Mwaka 2018 kulikuwa na wagonjwa 4,706 na vifo 84 ikilinganishwa na wagonjwa 4,626 na vifo 93 mwaka 2017.

#Ugonjwa wa Dengue watu 226 waliathirika mwaka 2018 ikilinganishwa na watu 65 mwaka 2017. Hakuna kifo kilichosababishwa na ugonjwa huu.

#Vilevile kulikuwa na wagonjwa 6 wa Chikungunya ambao walipatiwa matibabu mwaka 2018 na hakuna kifo kilichotokea.

Imetolewa na;
Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto
26/01/2019

JUMLA YA WAGONJWA WAPYA 1,933 WALIGUNDULIWA NA UKOMA NCHINI


Waziri Ummy Mwalimu akitoa tamko la siku ya ukoma Duniani ambapo aliwasisitiza wananchi kujenga tabia ya kuchunguza miili yao pamoja na watoto kama kuna mabaka rangi ya shaba  yasiyo na hisia na kuwahi hospitalini mara waonapo dalili hizo.




Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu  akipeana mkono na Mzee Mohamed Ally ambaye ni muhanga wa Ugonjwa wa Ukoma anayeishi katika Makao ya Wazee Nunge kama ishara ya kupinga vitendo vya kuwanyanyapaa wangonjwa wa ukoma.



Waziri  wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akiwapa mikono waathirika wa ugonjwa wa mikono wanaoishi makazi ya Nunge wilayani Kigamboni ikiwa ni ishara ya kuondoa unyanyapaa kwa waathirika wa ukoma.
Waziri Ummy Mwalimu baada ya kutoa tamko la maadhimisho ya siku ya ukoma Duniani ambayo itafanyika kesho akiwakabidhi waathirika wa ukoma chakula kwenye makazi yaliyopo Nunge wilayani Kigamboni.Siku ya ukoma Kitaifa itafanyika kesho makazi ya watu waishio na ukoma Wilayani Mvomero Mkoani Morogoro.

Tanzania ilifikia viwango vya utokomezaji wa Ukoma kitaifa mnamo mwaka 2006 kwa kiwango cha chini ya mgonjwa 1 kati ya watu 10,000 lakini Ukoma bado unaendelea kuwa tatizo la kiafya miongoni mwa jamii nchini kwetu.

 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amesema hayo leo katika Tamko lake la leo alilolitoa mbele ya vyombo vya habari  kuhusu hali ya Ukoma Nchini katika Makao ya Wazee Nunge Kigamboni Jijini Dar es Salaam.

 Waziri Mwalimu amesema kuwa kwa mujibu wa takwimu za Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua kikuu na Ukoma (NTLP) za mwaka 2017, jumla ya wagonjwa wapya 1,933 waligunduliwa na hivyo kufanya kiwango cha ugunduzi kuwa watu 4 kwa kila watu 100,000.

 Aidha ameongeza kuwa takwimu hizi zinaifanya Tanzania kuendelea kuwa miongoni mwa nchi 22 zenye wagonjwa wengi wa Ukoma duniani nchi nyingien ni pamoja na India, Indonesia, Brazil, Ethiopia, Msumbiji, Nigeria na DRC Kongo.

 ‘’Hivi sasa bado kuna mikoa kumi ambayo inagundua wagonjwa wapya wa Ukoma wengi zaidi kila mwaka na kuchangia karibia 80% ya wagonjwa wote. Mikoa hiyo ni pamoja na: Lindi, Rukwa, Mtwara, Morogoro, Pwani; Tanga, Geita, Dodoma, Tabora na Kigoma’’ Alongeza Waziri Ummy.

 Amezitaja Wilaya zenye kiwango kikubwa cha ugonjwa wa ukoma kuwa ni  20 ambazo kiwango cha ukubwa wa tatizo la Ukoma lipo juu sana na bado hazijafikia lengo la utokomezaji, nazo ni  amabazo ni Liwale,  Lindi vijijini, Nachingwea, Ruangwa, Nanyumbu, Masasi mjini,  Pangani, Mkinga, Korogwe,  Mvomero, Kilombero, Morogoro vijijini, Ulanga, Shinyanga manispaa,  Mafia, Rufiji, Kilwa, Chato, Nkasi,  na Mpanda.

 Waziri Ummy aidha amesema Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto kwa kushirikiana na Wizara ya TAMISEMI zimendelea kuhakikisha Ukoma unatokomezwa kabisa kwa Kuhakikisha dawa za kutibu Ukoma zinaendelea kupatikana wakati wote na bila malipo yoyote.

 Amezitaja juhudi nyingine kuwa ni kuendesha kampeni za uibuaji wa wagonjwa wapya ngazi ya jamii kwa kuwashirikisha watoa huduma ngazi ya jamii (Leprosy Elimination Campaigns) hasa katika wilaya zenye kiwango kikubwa cha wagonjwa wa Ukoma.

 Amesema pamoja na hatua zinazochukuliwa na serikali na mafanikio zipo changamoto kubwa mbili ambazo ni jamii kuendelea kushikilia imani potofu juu ya Ukoma kuwa ni ugonjwa wa kurithi au kulogwa na wagonjwa kuchelewa kujitokeza kupata matibabu hadi wanapopata ulemavu.

 ‘’Natoa rai kwa jamii, wazazi na walezi kuwa sote tujenge tabia ya kuchunguza miili yetu na ya watoto wetu na endapo utaona mojawapo ya dalili za Ukoma ambazo ni baka au mabaka mwilini yenye rangi ya shaba na hayana hisia, vijinudu kwenye ngozi au mishipa ya fahamu kuvimba. Dalili nyingine ni ganzi kwenye mikono na miguu. Unashauriwa kwenda kwenye kituo cha tiba kilicho karibu nawe kwa uchunguzi bila kuchelewa’’. Alisisitiza Mwalimu.

Ameongeza kuwa kupima afya kutawawezesha wataalam wa afya kuchunguza na kubainisha kama mgonjwa ana Ukoma ili apate tiba sahihi mapema na hivyo kuzuia maambukizi na ulemavu wa kudumu unaoweza kuzuilika uku akitaka jamii kifahamu kuwa ugonjwa wa Ukoma unatibika.

 Siku ya Ukoma Duniani huadhimishwa ulimwenguni kote kila Jumapili ya mwisho ya mwezi Januari. Kwa mwaka huu, siku hii itaadhimishwa tarehe 27 Januari,2019.Hapa Tanzania maadhimisho haya kitaifa yatafanyika wilayani Mvomero,Mkoani Morogoro.

Ijumaa, 25 Januari 2019

4.MAPAMBANO DHIDI YA VVU/UKIMWI, MALARIA NA KIFUA KIKUU

- Hakuna maoni



 Waziri wa Afya, maendeleo ya jamii, Jinsia, wazee na watoto Mhe. Ummy Mwalimu.
 
 
HALI YA HUDUMA ZA AFYA NCHINI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2018

4.MAPAMBANO DHIDI YA VVU/UKIMWI, MALARIA NA KIFUA KIKUU


#Mapambano Dhidi ya VVU/UKIMWI
Katika kuhakikisha kuwa Tanzania ina kuwa salaama kutokana na maambukizi mapya ya VVU, kuwapunguzia makali ya virusi vya UKIMWI na kuzuia waathirika wasishambuliwe na magonjwa nyemelezi, Sekta ya Afya ikishirikana na Wadau inatekeleza mpango wa Kimatatifa wa 90-90-90.

# Mpango huo unazitaka nchi kuwatambua wenye VVU kwa asilimia 90 ifikapo mwaka 2020 miongoni mwa watanzania wote wanaoishi na VVU wanaokadiriwa kuwa 1,500,000 nchi nzima, hatua ya pili ni kuhakikisha kuwa asilimia 90 ya wanaogundulika kuwa na VVU wanaanza dawa za ARV na kati ya wanaoanza dawa za ART asilimia 90 wanaimarisha kinga zao za mwili ili kuzuia wasishambuliwe na magonjwa nyemelezi.

#Hadi kufikia mwisho wa Mwezi Septemba 2018, Wizara kupitia Mpango wa Taifa wa Kudhibiti UKIMWI iliweza kuwaandikisha katika tiba ya kufubaza virusi vya UKIMWI, jumla ya wagonjwa 1,087,382 kati ya hao watoto walikuwa ni 58,908. 

#Idadi hii ya wagonjwa walio katika tiba ni asilimia 72 ya watu 1,500,000 wanaokadiriwa kuishi na VVU nchini kote ikilinganishwa na asilimia 70 mwaka 2017.

#Lengo la 90 ya pili ni kuhakikisha asilimia 90 ya waliokutwa na VVU wanaanzishiwa dawa za ART, lengo hili limefikiwa ambapo Watanzania 1,068,282 sawa na asilimia 98.2 wanatumia dawa za ART.

# Na lengo la 90 ya tatu ni kuhakikisha asilimia 90 ya wanaoanzishiwa dawa za ARV kinga zao za mwili zinaimarika (Viral road suppression), ambapo lengo hili limefikiwa kwa asilimia 87. 

# Mapambano dhidi ya Malaria nchini
mwaka 2018 idadi ya 5,769,837 waligundulika kuwa na ugonjwa wa malaria ikilinganishwa na watu 5,595,916 mwaka 2017.

# Matumizi ya kipimo cha haraka cha malaria (mRDT) yaliiongezeka kutoka asilimia 79 mwaka 2017 hadi kufikia asilimia 86 mwaka 2018  


#Mapambano dhidi ya Kifua Kikuu Nchini
Wizara kwa kushirikiana na wadau wa sekta ya afya iliendelea na mapambano dhidi ya ugonjwa wa kifua kikuu ambapo katika mwaka 2018 jumla 47,967 waligundulika kuwa na vijidudu vya Kifua kikuu ikilinganishwa na wagonjwa 44,714 waliogunduliwa mwaka 2017. 

#Huduma kwa Wagonjwa wa TB wanaogundulika kuwa na HIV 2017 na Mwaka 2018 
Katika kuimarisha tiba dhidi ya Kifua Kikuu na VVU, wagonjwa wote wanaogundulika kuwa na kifua kikuu, hupimwa kama wanamaambukizi ya VVU. 
 
*Hii inawawezesha wagonjwa kutibiwa TB na VVU. Katika kipindi cha mwaka 2018 asilimia 99 ya wagonjwa waliogundulika kuwa na maambukizi ya Kifua Kikuu walipimwa VVU ambapo asilimia 31 kati yao walikutwa na VVU ikilinganishwa na mwaka 2017 ambapo asilimia 97 ya wagonjwa wa TB waliopima VVU kati yao asilimia 34 waligundulika kuwa na VVU.

#Kwa wale waliogundulika kuwa na VVU asilimia 93 walianzishiwa dawa za ARV. 

#Kiwango cha maambukizi ya VVU kwa wagonjwa walio na TB kiko juu sana hivyo Sekta ya Afya inahakikisha kuwa wagonjwa wote wanaogundulika kuwa na VVU/UKIMWI wanaanzishiwa dawa za ART.   
   

#Kitaifa zaidi ya asilimia 93 ya wagonjwa wote wa TB wliogundulika kuwa na VVU walianzishiwa dawa za ART

Imetolewa na;
Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto
25/01/2019

Alhamisi, 24 Januari 2019

SERIKALI YATOA BILIONI 2.5 KWA AJILI YA UJENZI WA JENGO LA MAMA NA MTOTO HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA SHINYANGA

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akikagua jengo la wagonjwa wa nje (OPD) ambalo limekamilika  katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga. Kushoto ni Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Bi. Jasinta Mboneka na kulia ni Katibu Tawala wa Mkoa huo Bw. Albert Msosela.

Jengo la Wagonjwa wa nje (OPD) na utawala katika Hopitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akioneshwa ramani ya majengo ya kituo cha afya cha Kambarage na Mganga Mkuu wa Wilaya Dkt. Lusajo Mwakajoko wakati alipotembelea kituo hicho leo kilichopo manispaa ya  Shinyanga.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akimjulia hali mtoto mchanga aliyezaliwa katika kituo cha afya cha Kambarage mjini Shinyanga.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akipanda mti wa kumbukumbu katika kituo cha afya cha Kambarage kilichopo katika manispaa ya  Shinyanga.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto akiangalia kichanga kilicholazwa katika chumba maalum cha uangalizi wa watoto mahututi na wale waliozaliwa kabla ya siku (njiti) katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga. Kushoto ni daktari bingwa wa watoto Dkt. Mwita Ngutunyi.

NA WAMJW-SHINYANGA

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imetoa kiasi cha shilingi bilioni 2.5 zitakazotumika katika ujenzi  wa jengo la mama na mtoto katika Hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, lengo likiwa ni kutoa huduma za kibingwa kwa akina mama wajawazito na watoto wachanga.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakati alipotembelea ujenzi wa Hospitali hiyo na kukuta jengo la wagonjwa wa nje (OPD) na Utawala likiwa limekamilika.

Waziri Ummy amesema fedha hizo zitafika katika Hospitali hiyo ndani ya wiki mbili ili ziweze kuchochea kasi ya ujenzi na lengo  ifikapo mwezi Septemba 2019 Hospitali hiyo ianze kutoa huduma za afya.

“Ninaahidi kutoa shilingi bilioni 2.5 ndani ya wiki mbili ziweze kutumika katika ujenzi wa jengo la mama na mtoto, lengo la serikali ni kuhakikisha kila mama mjamzito anapofika Hospitalini kujifungua atoke akiwa salama yeye na kichanga chake”. Amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy amefikia uamuzi huo baada ya kupokea ripoti ya mkoa kuhusu vifo vitokanavyo na uzazi kutoka kwa Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt. Mfaume Rashid, ambapo kwa mwaka 2016/2017 kulikua na vifo 73, na mwaka 2017/2018 vikiwa ni vifo 56, hali ambayo Waziri huyo ameonekana kutoridhishwa nayo.

Hata hivyo Waziri Ummy ameahidi kuongeza fedha zingine kiasi cha shilingi bilioni 3 ndani ya mwezi mmoja, zitakazotumika katika ujenzi wa jengo kwa ajili ya huduma za uchunguzi ikiwemo huduma za maabara, X-ray na CT-Scan pia jengo hilo litakua na vyumba vitatu vya upasuaji.

Waziri Ummy amesisitiza ujenzi wa jengo hilo utumike wa  mfumo wa Force Account ambao utahakikisha wananchi wanashiriki kwa asilimia 100 katika kufanikisha ujenzi huo na huduma za afya zianze kutolewa mapema.

Wakati huo huo, Waziri Ummy ametembelea kituo cha afya cha Kambarage katika Manispaa ya  Shinyanga kuona hali ya miundombinu ya kituo hicho na utoaji wa huduma za afya huku kwa kiasi kikubwa akionekana kuridhishwa na kasi ya ujenzi wa majengo ya huduma mbalimbali.

Kuhusu uhaba wa watumishi wa kada za afya Waziri huyo ameahidi kutatua changamoto hiyo hali inayopelekea kuwepo kwa msongamano wa wagonjwa.

Aidha, Waziri Ummy amehitimisha ziara yake katika mikoa ya kanda ya ziwa kwa kutembelea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga na kuridhishwa kwa kiasi kikubwa na hali ya utoaji wa huduma za afya hasa katika jengo la huduma za mama na mtoto na pia katika jengo la kuhifadhia watoto wachanga wenye uhitaji wa uangalizi maalumu (NICU).

-Mwisho-

UPATIKANAJI WA DAWA MUHIMU KATIKA VITUO VYA KUTOLEA HUDUMA ZA AFYA NCHINI


HALI YA HUDUMA ZA AFYA NCHINI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2008

3.UPATIKANAJI WA DAWA MUHIMU KATIKA VITUO VYA KUTOLEA HUDUMA ZA AFYA NCHINI

#Hali ya upatikanaji wa Dawa muhimu katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini imeendelea kuimarika tokea kuingia madarakani kwa Serikali ya awamu ya Tano. 

#Serikali imeongeza bajeti ya dawa kutoka Shilingi Milioni 31 mwaka 2015/16 hadi kufikia Shilingi milioni 251 mwaka 2016/17 na Shilingi 270 mwaka 2018/19. 

#Hali hii imewezesha takribani vituo vyote vya kutolea huduma nchi kuwa na dawa zote muhumu na kuwezesha wananchi kupata dawa karibu na maeneo wanayoishi. 

# Mwaka 2015 hali ya upatikanaji wa dawa ilikuwa asilimia 46 kutokana na ongezeko la bajeti pamoja na usimamizi mzuri wa usambazaji dawa, mwaka 2016/17 hali upatikanaji wa dawa iliongezeka na kufikia asilimia 89 na mwaka 2018 ilifikia asilimia 94 kwa dawa dawa muhimu zinazosambazwa na Bohari ya Dawa nchini (MSD). 

Imetolewa na;
Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto
24/01/2019

HOSPITALI YA MKOA WA GEITA YAPEWA SIKU 60 KUFUNGUA DUKA LA DAWA

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akiongozana na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Geita Bw. Josephat Maganga (kulia) wakitoka kukagua jengo la hospitali ya rufaa ya mkoa wa Geita.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akimjulia hali mtoto aliyekuja kupata matibabu katika Hospitali ya Mkoa wa Geita. Katikati ni mama wa mtoto huyo Bi. Jenista Benedicto.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akiangalia ramani ya majengo za majengo ya Hospitali ya rufaa ya Geita wakati alipotembelea ujenzi huo. Pembeni ni msimamizi wa ujenzi huo Injinia Grace Elias.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akiangalia mashine mpya ya X-ray ya kidigitali iliyifungwa katika Hospitali ya wilaya ya Chato wakati alipoitembelea hospitali hiyo kuona hali ya utoaji huduma za afya.


 HOSPITALI YA MKOA WA GEITA YAPEWA SIKU 60 KUFUNGUA DUKA LA DAWA

Na WAMJW-GEITA
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu ameuagiza uongozi wa Hospitali ya mkoa wa Geita kuhakikisha wanafungua duka la dawa ili kutoa huduma karibu na wananchi pia kuongeza mapato ya Hospitali.
Waziri Ummy ametoa agizo hilo mapema leo wakati alipoitembelea hospitali hiyo ili kuona hali ya miundombinu pamoja na utoaji wa huduma za afya.
“Tumeshaagiza Hospitali zote nchi nzima kuwa na maduka ya dawa ya Hospitali, kwanini hapa hamjafungua duka lenu? Alihoji Waziri Ummy na kuongeza “sasa nawapa miezi miwili uongozi wa Hospitali kuhakikisha mnafungua duka la dawa la Hospitali ili liweze kuwasaidia kupandisha mapato lakini pia kusogeza huduma karibu na wananchi. Alisema Waziri huyo.
Pamoja na hayo Waziri Ummy ameonekana kuridhishwa na hali ya upatikanaji wa dawa wa zaidi ya asilimia 90 na uboreshwaji wa huduma za afya zinazotolewa katika Hospitali hiyo.
Kabla ya hapo Waziri Ummy alitembelea ujenzi wa Hospitali Teule ya Mkoa wa Geita ambapo alishuhudia ujenzi huo ukiwa umekamilika kwa asilimia 54 lakini amemtaka mkandarasi anayesimamia ujenzi  huo ambaye ni wakala wa ujenzi (TBA) kufanya kazi usiku na mchana ili Hospitali hiyo ianze kufanya kazi ifikapo Mwezi Julai 2019.
Waziri Ummy amekamilisha ziara yake ya mkoa wa Geita kwa kutembelea Hospitali ya Wilaya ya Chato ili kujiridhisha na hali ya utoaji wa huduma za afya na miundombinu pamoja na kuhakikisha kama vifaa na vifaa tiba vinapatikana Hospitalini hapo.
Waziri Ummy ameridhishwa na utolewaji wa huduma za afya lakini ameitaka Hospitali hiyo kuwa na chumba maalum chenye vifaa maalum vya uangalizi wa watoto wachanga mahututi na wale waliozaliwa kabla ya siku (watoto njiti) lengo likiwa ni kupunguza vifo vya watoto wachanga nchini.
Aidha, waziri huyo ameagiza uongozi wa Hospitali hiyo kuanzisha kitengo cha huduma za wagonjwa wa dharura na wale waliopata ajali ikiwa ni agizo la serikali kwa hospitali zote za wilaya na mikoa nchi nzima.
Huo ni muendelezo wa ziara za Waziri Ummy katika mikoa ya kanda ya ziwa kutembelea Hospitali mbalimbali kuangalia hali ya miundombinu na utoaji wa huduma za afya.

Jumatano, 23 Januari 2019

HALI YA HUDUMA ZA TIBA NCHINI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2018


Jengo la wagonjwa wa dharura katika Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kaskazini KCMC.

Mwaka 2018 jumla ya mahudhurio ya wagonjwa ilikuwa 42,411,276 katika vituo vya kutolea huduma za tiba nchini ikilinganishwa na 54,478,926 kwa mwaka 2017 Kati ya hao wagonjwa wa wa nje (OPD) ilikuwa 41,052,012 na wagonjwa wa kulazwa (IPD) ilikuwa 1,359,264.

1. Wagonjwa waliohudumiwa katika Hospitali za Halmashauri, Vituo vya Afya na Zahanati katika ngazi ya msingi.
Ø Katika mwaka 2018 jumla ya wagonjwa wa nje (OPD) ilikuwa 36,376,967 walipatiwa huduma katika hospitali za Halmashauri, hospitali nyingine, vituo vya afya na zahanati ikiwa ni 18,194,619 hudhurio la kwanza na 18,182,348 mahudhurio ya marudio. Mwaka 2017, jumla ya wagonjwa wa nje (OPD) ilikuwa 47,650,158 ambapo 30,174,341 hudhurio la kwanza na 15,809,971 mahudhurio ya marudio.
Wakati huo huo wagonjwa wa Kulazwa mwaka 2018 walikuwa 404,659 ikilinganishwa na wagonjwa 523,587 mwaka 2017

2. Wagonjwa waliohudumiwa katika Hospitali za Rufaa za Mikoa mwaka 2018
Ø Kwa kipindi cha Januari hadi Desemba 2018 Hospitali za Rufaa za Mikoa zilihudumia jumla ya wagonjwa 3,526,503 ambapo wagonjwa wa nje walikuwa 3,054,318 na wagonjwa wa ndani walikuwa 472,185 ikilinganishwa na wagonjwa 4,781,999 waliohudumiwa kwa kipindi cha Januari hadi Desemba 2017.

3. Mahudhurio ya wagonjwa katika Hospitali ya Taifa, Hospitali Maalum na Hospitali za Rufaa za Kanda
Ø Katika kipindi cha Januari hadi Desemba 2018, Hospitali hizi zilihudumia jumla ya wagonjwa   2,103,147 ambapo wagonjwa wa kulazwa walikuwa 482,420 na wagonjwa wa nje walikuwa 1,620,727. Ikilinganishwa na idadi ya wangonjwa 2,046,769 kwa kipindi cha Januari hadi Desemba 2017. Ambapo idadi ya wagonjwa wa kulazwa ilikuwa 711,766 na wagonjwa wa nje 1,335,003. 


Imetolewa na;
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Jumanne, 22 Januari 2019

HALI YA HUDUMA ZA AFYA NCHINI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2018

- Hakuna maoni
 
 
HALI YA HUDUMA ZA AFYA NCHINI KATIKA KIPINDI CHA MWAKA 2018

1. Afya ya Uzazi,Mama na Mtoto

#Katika mwaka 2018, jumla ya wajawazito 2,086,930 walihudhuria na kuandikishwa kliniki, ikilinganishwa na wajawazito 2,009,879 mwaka 2017. Mwongozo wa utoaji huduma za afya ya uzazi na mtoto unaelekeza wajawazito kuanza huduma mapema kabla ya majuma 12 ya ujauzito na kuhudhuria kliniki angalau mara nne katika kipindi cha ujauzito ili waweze kupata huduma zote muhimu.

#Asilimia 25 ya wajawazito nchini waliweza kufanya *hudhurio la kwanza kliniki kabla ya majuma 12* ikillinganishwa na asilimia 18 mwaka 2017.

#Ongezeko la *wajawazito kujifungulia katika vituo vya kutolea huduma za afya* Mwaka 2018 asilimia 73 ya wajawazito walijifungulia katika vituo vya kutolea huduma za afya ikilinganishwa na asilimia 70 mwaka 2017.

#Huduma ya *kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto* imeendelea kutolewa ambapo mwaka 2018 asilimia 97 ya wajawazito walipima VVU ikilinganishwa na asilimia 95 mwaka 2017. 

#Katika wajawazito waliopima VVU, asilimia 3.9 waligundulika kuwa na VVU na kati ya hao waliogundulika asilimia 99 walianzishiwa dawa za ART. Katika mwaka 2017, Asilimia 4.2 ya wajawazito waligundulika kuwa na maambukizi ya VVU na kati yao asilimia 99 walianza dawa za ART. 

#Hali ya upatikanaji wa chanjo kwa watoto nchini imeendelea kuwa katika kiwango cha juu kwa asilimia 85 katika kipindi cha mwaka 2018 na mwaka 2017

Imetolewa na ;
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto
Chanzo: District Health Information System 2 (DHIS2).

TBA WAPEWA WIKI MBILI KUPELEKA FEDHA ZA UJENZI WA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA SIMIYU

- Hakuna maoni
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akitoa maelekezo kwa Injini mkuu wa TBA Simiyu Bw. Likimaitare Naunga wakati akipotembelea ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Simiyu. Kulia ni Mkuu wa mkoa huo Bw. Anthony Mtaka.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akimsalimia ndugu wa mgonjwa aliyelazwa (jina halijafahamika) katika hospitali teule ya Somanda alipotembelea hospitali kuona hali ya utaoaji huduma za afya. Kulia ni Mwenyekiti wa CCM wilaya Bi. Juliana Mahongo na Daktari zamu.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akisisitiza jambo wakati alipotembelea wodi za Hospitali ya rufaa ya mkoa wa Simiyu. Kushoto ni Mganga Mkuu wa mkoa Dkt. Mageda Kihulya, Mbunge wa bunge la Afrika Mashariki Bi. Happines Lugiko na Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Bw. Anthony Mtaka.




Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akitembelea ujenzi wa jengo la uchunguzi na mama na mtoto katika Hospitali ya Rufaa ya mkoa wa Simiyu. Waliongozana nae ni viongozi waandamizi wa mkoa wakiongozwa na Mkuu wa mkoa huo Anthony Mtaka.



TBA WAPEWA WIKI MBILI KUPELEKA FEDHA ZA UJENZI WA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA SIMIYU


Na WAMJW-SIMIYU

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu ameiagiza wakala wa ujenzi (TBA) kupeleka fedha za ujenzi zilizotolewa na Serikali katika ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu kuhakikisha zinafika ndani ya wiki mbili.

Agizo hilo limetolewa  leo wakati alipotembelea ujenzi wa jengo la Uchunguzi na jengo la Mama na Mtoto na kutoridhishwa na kasi ya ujenzi huo huku sababu kubwa inayopelekea kusuasua ikitajwa  ni fedha kidogo zilizopokelewa na wakala wa ujenzi wa mkoa wa Simiyu kiasi cha Shilingi Milioni 430 wakati serikali imetoa Bilioni 1.064 kwa ajili ya ujenzi huo.

“Ninawashngaa TBA kwanini wanakaa na fedha wakati wanajua mradi wa ujenzi unaendelea huku, serikali imetoa Bilioni 1.064 ili zitumike katika ujenzi wa Hospitali hii lakini TBA wameleta milioni 430 tu, hizo fedha zingine ziko wapi?”. Alihoji waziri Ummy.

Kufuatia hali hiyo Waziri Ummy ameahidi kushughulikia suala hilo na kuahidi fedha hizo zitafika katika mradi huo ndani ya wiki mbili ili ziweze kusaidia kuongeza kasi ya ujenzi wa majengo hayo ambapo yanatarajiwa kukabidhiwa na kuanza kutoa huduma kuanzia mwezi Juni mwaka huu.

Kwa upande wake Injinia mkuu wa TBA anayesimamia ujenzi huo Bw. Likimaitare Naunga amesema fedha zilizoletwa katika mradi huo hazitoshi na ndiyo sababu kubwa inayochangia kusuasua kwa mradi huo huku akitaka wakala wa ujenzi (TBA) kuhakikisha fedha hizo zinafika mapema ili zisaidie kuongeza kasi ya mradi na kufikia lengo.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Bw. Anthony Mtaka amemuahidi Waziri Ummy kuwa atasimamia kwa karibu upatikanaji wa fedha hizo zilizopo TBA zinafika katika mradi na kuhakikisha mradi unakamilika ndani ya muda uliopangwa ili huduma muhimu za kibingwa zianze kutolewa Hopitalini hapo.

Wakati huo huo waziri Ummy ametembelea Hospitali teule ya Somanda iliyopo wilayani Bariadi na kuonekana kutoridhishwa na huduma zinazotolewa katika jengo la Mama na Mtoto ambapo alishuhudia huduma mbaya zinazotolewa kwa akinamama wajawazito na watoto wachanga.

Pia Waziri Ummy ameshangazwa baada ya kuona hakuna chumba cha kuhifadhia watoto wenye uhitaji wa huduma maalum kama huduma za joto kwa watoto waliozaliwa kabla ya muda (Njiti) na kuitaka Hospitali hiyo kuwa na chumba hicho muhimu.

Aidha, Waziri Ummy ameshangazwa na kutokuwepo kwa huduma za upasuaji katika jengo hilo huku sababu ikitajwa kutokuwepo kwa Sinki, hali inayosababisha usumbufu mkubwa kwa akinamama wajawazito wanaofika kupata huduma hospitalini hapo.

Kufuatia hali hiyo waziri huyo ametoa siku tatu kwa uongozi wa Hospitali hiyo chini ya Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt. Mageda Kihulya kuhakikisha wananunua sinki hilo na huduma za upasuaji zianze kutolewa mara moja katika jengo hilo.

Waziri Ummy yupo Mkoani hapa katika  ziara  ya kikazi ya kutembelea mikoa ya Simiyu, Geita na Shinyanga ili kuweza kuona hali ya miundombinu na utoaji huduma katika hospitali za rufaa za mikoa.