Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Alhamisi, 17 Desemba 2020

WATAALAM WA TIBA ASILI WATAKIWA KUFANYA UTAFITI WENYE USHAHIDI

Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya Bw. Edward Mbanga akiongea na wataalam wa tiba asili/mbadala kutoka taasisi za serikali na vyuo vikuu mbalimbali vinavyojishughulisha na tafiti za dawa za tiba asili nchini.

 
Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali Dkt.Eliud Eliakimu  akizungumza wakati wa kikao hicho

 
Mkemia Mkuu wa Serikali kutoka Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali Dkt.Fidelice Mafumiko na Msajili wa Baraza la Tiba Asili/Mbadala Dkt. Ruth Suza wakifuatilia ufunguzi wa kikao kazi hicho.
 
Kaimu Katibu Mkuu Edward Mbanga (katikati) na Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Eliud Eliakimu(kulia) na Mkurugenzi wa Idara ya Tiba Dkt. Grace Maghembe  wakifuatilia uwasilishaji wa mada kwenye kikao cha kujadili

 
Washiriki wa kikao kazi cha siku mbili  cha kujadili muelekeo wa tiba asili nchini kinachofanyika kwenye ukumbi wa ofisi za wizara zilizopo Area D jijini Dodoma


Picha ya pamoja ya mgeni rasmi na washiriki wa kikao kazi cha kujadili muelekeo wa tiba asili na tiba mbadala nchini.


WATAALAM WA TIBA ASILI WATAKIWA KUFANYA UTAFITI WENYE USHAHIDI

Na. Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Wataalam wa tiba asili na tiba mbadala nchi wametakiwa kufanya utafiti ambao utakuwa na  ushahidi wa usalama wa dawa pamoja na ufanisi wa wa dawa hizo kwa watumiaji.

Rai hiyo imetolewa na Kaimu Katibu Mkuu wizara ya Afya, Maendeleo ya jamii, Jinsia, wazee na watoto-Idara kuu Afya Bw. Edward Mbanga wakati wa kikao cha pamoja cha wizara na  wataalam hao kutoka taasisi za Serikali na Vyuo Vikuu mbalimbali nchini kilichofanyika kwenye ukumbi wa wizara jijini Dodoma.

Mbanga amesema kuwa ushahidi huonekana kwenye utafiti hivyo warudi nyuma na kujiuliza wamekosea wapi na nini kifanyike ili kuwa na uelewa wa pamoja kwani kizazi kijacho kinahitaji kuelezwa na kuelewa tiba asili.

“Lazima tuulizane tunataka kufikia wapi na kuweka mikakati  ya kuyafikia,nashauri tutambue nini kifanyike,tuna changamoto zipi na tunafikaje huko kwa kushirikiana kwa pamoja  ili tutambue kwanini hatufiki hivyo lazima tujikite kwenye utafiti wenye ushahidi”.Alisisitiza.

Aliongeza kuwa katika kikao hicho wataalam hao wanatakiwa kutafuta majibu ambayo tiba asili itaendelea hata baada ya kipindi hiki,na wawe na matamanio kama nchi nyingine ili tiba asili itolewe kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

“Tumekuwa tukifanya utafiti wa masuala ya tiba asili na tiba mbadala  kuanzia miaka ya sitini, sasa tujiulize  tangu tutafiti hadi sasa matokeo yanafanana?,bado kuna changamoto ya watu kushindwa kuthamini vya kwao hasa katika matumizi ya tiba asili kwa kuamini vinavyotoka nje ya nchi vina ubora zaidi kuliko vya kwao.

Hata hivyo Kaimu katibu mkuu huyo aliwataka katika kikao hicho watoke na mkakati wa kuanzisha vituo vya uendelezaji   vya tiba asili kwenye halmashauri zote kwa kuwapatia ujuzi na motisha wataalam wa tiba asili pamoja na kufanyia tafiti dawa zao na mwisho wa utafiti kuwe na haki miliki.

Kwa upande wake Kaimu Mganga Mguu wa Serikali Dkt. Eliud Eliakimu amesema kuwa kama nchi wameamua kuendeleza tiba asili kwa umoja ili kuwe na spidi ambayo italeta mafanikio yenye tija nchini.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Tiba kutoka Wizara ya afya Dkt. Grace Maghembe amesema  tiba asili zipo na zinatumika  kutibu magonjwa mbalimbali  na malighafi ya kutengeneza dawa hizo zipo hapa nchini hivyo uwezo wa kutengeneza katika viwango kama nchini nyingine inawezekana endapo kutawekwa msukumo na hivyo kusaidia kuinua uchumi wa nchi na wa wakulima wa hapa nchini.

Mwisho

Jumatano, 16 Desemba 2020

TIMIZENI WAJIBU WENU KWA WELEDI NA MAADILI.

 
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akifungua Mkutano wa Maafisa Afya mazingira uliofanyika Jijini Dodoma.

 
Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali, ambae pia ni Mkurugenzi wa huduma za Kinga Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi akiwasilisha maelekezo ya Mganga Mkuu wa Serikali kwa Maafisa Afya mazingira katika ufunguzi  wa Mkutano wa tathmini wa Maafisa Afya mazingira uliofanyika Jijini Dodoma.
 
 
Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe TAMISEMI Dkt. Paul Chawote akitoa neno kwa Maafisa Afya mazingira (hawapo  kwenye picha) walio hudhuria Mkutano wao wa tathmini, uliofanyika Jijini Dodoma.

 
Mwenyekiti wa Maafisa afya mazingira nchini Bw. Evans Simkoko akitoa salam za Maafisa Afya mazingira kwa Mgeni rasmi ambae ni Katibu Mkuu Wizara ya Afya (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa tathmini wa Afya mazingira uliofanyika Jijini Dodoma.
 
 
Maafisa Afya kutoka maeneo ya mipaka wakifuatilia kwa makini neno kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa tathmini wa Afya mazingira uliofanyika Jijini Dodoma.
 
Maafisa  Afya mazingira wakifuatilia kwa makini neno kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa tathmini wa Afya mazingira uliofanyika Jijini Dodoma.


TIMIZENI WAJIBU WENU KWA WELEDI NA MAADILI.

Na Rayson Mwaisemba, WAMJW- DOM.

KATIBU Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Idara kuu ya Afya Prof. Mabula Mchembe amewataka Maafisa Afya ngazi zote kufanya kazi zao kwa weledi na kufuata maadili wakati watimizapo majukumu yao katika jamii.

Prof. Mchembe ameyasema hayo, wakati akifungua Mkutano wa Maafisa Afya mazingira wenye kauli mbiu ya "Zingatia mahitaji ya Jinsia kwa usafi wa mazingira endelevu " uliofanyika Jijini Dodoma.

"Tusimamie maadili sana, usitende kitu kwa kufikiria kwamba unamfanyia fulani, natambua changamoto zipo katika baadhi ya sehemu, lakini tunahitaji kutimiza wajibu wetu kwa maadili na uwaminifu wa hali ya juu" alisema Prof. Mchembe.

Pia, Prof. Mchembe amewataka Maafisa Afya mazingira kusimamia usafi katika maeneo ya huduma za vyoo katika jamii, hususan katika ofisi na vituo vya daladala ambavyo huudumia Jamii kwa kiasi kikubwa ili kuikinga Jamii dhidi ya magonjwa ya milipuko.

Aidha, Prof. Mchembe amewaagiza Maafisa Afya mazingira nchini kusimamia usafi na ubora wa vyakula katika maeneo yote yanayotoa huduma za vyakula, yakiwemo maeneo ya migahawa na hoteli ili kuikinga jamii na magonjwa ya tumbo na kuhara.

Mbali na hayo Prof. Mchembe ametoa wito kwa Maafisa afya mazingira kujiepusha na vitendo vya Rushwa wakati wa wakitimiza majukumu yao na kuhakikisha usafi wa mazingira unaendelea kufuatwa katika ngazi zote za Jamii.

"Tuachane na Rushwa, inawezekana baadhi ya sehemu unafika pale, unapewa 10,000 au unapewa bia mbili au tatu unaondoka zako, kitu ambacho hakina maana, sasa kama wewe ni Mtaalamu wa Afya simama kwenye maadili yako" alisema Prof. Mchembe.

Hata hivyo, Prof. Mchembe amewaagiza Maafisa afya mazingira nchini, kusimamia udhibiti wa takataka zinazotokana na utoaji wa huduma za afya ili kuendelea kuikinga jamii dhidi ya maambukizi yatokanayo na taka hizo.

Naye Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali, ambae pia ni Mkurugenzi wa huduma za Kinga Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi amewaagiza Waganga wakuu wa mikoa  kutoa elimu mara kwa mara kwa watendaji wao juu ya maadili badala ya kusubiri kuchukua hatua baada ya kosa kujitokeza.

"Kutoa elimu mara kwa mara kuhusu maadili, badala ya kusubiri kuchukua hatua kwa Maafisa Afya au wana taaluma wenu, wanapokiuka au kufanya makosa mbali mbali " alisema Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Subi.

Aliendelea kusema kuwa, baadhi ya maeneo hususan mijini bado kuna hali ya usafi wa mazingira usioridhisha, na kuelekeza kuanza kampeni ya usafi wa mazingira ya muda wa miezi miwili, huku akiwataka kuanza oparesheni hiyo kwa kuzingatia Sheria na kanuni za afya ya mwaka 2009.

Hata hivyo, Kaimu Mganga Mkuu wa Serikali amewaagiza Maafisa Afya mazingira, kukagua suala la usafi wa mazingira kwenye shule, mabweni, maofisi na maeneo yote yenye mikusanyiko ili kuhakikisha usafi wa mazingira unapewa mkazo ili kuikinga jamii dhidi ya maambukizi ya magonjwa ya mlipuko.

Wakati huo huo Mwenyekiti wa Maafisa afya mazingira nchini Bw. Evans Simkoko ameiomba Serikali kuipa kipaumbele kada ya Maafisa Afya mazingira kwenye ajira mpya, ili kuongeza ufanisi katika utoaji huduma kwa wananchi, kisha kuikinga Jamii dhidi ya maambukizi ya ugonjwa ya milipuko.

Mwisho.

TANZANIA YAVUKA VIWANGO VYA KIMATAIFA VYA UTOAJI WA CHANJO

Prof. Mabula Mchembe, 
Katibu Mkuu 
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Dkt. Leonard Subi
Mkurugenzi wa Huduma za Kinga
Wizara ya Afya


 Na. Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendheleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe amewapongeza viongozi na watumishi wa huduma za chanjo ngazi zote nchini kwa  utendaji bora wa utoaji wa chanjo kwa bidii na kuhakikisha kuwa malengo yaliyowekwa kitaifa na kimataifa yanafikiwa.

Pongezi hizo zimetolewa leo wakati akifungua mkutano wa mwaka wa tathimini wa huduma za chanjo Tanzania unaofanyika kwenye ukumbi wa Mt. Gasper jijini Dodoma.

"Niwapongeze kwa jitihada zenu na kuifanya nchi kufanikiwa katika utoaji wa huduma za chanjo kwa kuvuka kiwango cha asilimia 90 kilichowekwa kimataifa, hivyo nawataka mkubaliane na kupanga mbinu na mikakati ya kudumisha na kuboresha zaidi viwango vya chanjo nchini".

Hata hivyo katibu Mkuu huyo alisema licha cha kufanikiwa huko Serikali kupitia Wizara yake itaendelea kudumisha  kiwango cha chanjo nchini na ana uhakika takwimu za mwaka 2020  zitakapotolewa na Shirika la Afya Duniani(WHO)  itafikia asilimia 98 au zaidi.

Licha ya pongezi hizo Prof. Mchembe  amewaagiza viongozi wa afya ngazi za Mikoa na wilaya  kuhakikisha kuwa huduma za chanjo zinapewa kipaumbele  ili usitokee tena mkoa utakaoshindwa kudumisha kiwango kilichofikiwa kwani ili watoto waendelee kuwa na afya njema hakuna budi kuwapa chanjo bora za kuwakinga dhidi ya maradhi.

"Nchi yetu imekuwa na utekelezaji wa mkakati wa Fikia kila Wilaya,Fikia kila mtoto apate chanjo,nawasisitiza waratibu wa huduma za chanjo kuhakikisha kuwa mikoa inayofanya vibaya inatumia mkakati huu ili  kuhakikisha kuwa watoto na walengwa wote wanafikiwa katika kupata haki yao ya msingi ya chanjo".

Aidha, Prof. Mchembe aliwashukuru wadau wote wa maendeleo kwa michango yao mbalimbali  katika kuhakikisha kwamba watoto  wanapatiwa chanjo bora  ambayo inaleta kinga dhidi ya maradhi ambayo yanaweza kusababisha ulemevu na vifo kwa watoto.

Naye Mkurugenzi wa Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI  Dkt. Ntuli kapologwe amewapongeza Waganga Wakuu wa Mikoa pamoja na waratibu wa huduma za chanjo nchini kwa kuwa kinara wa utoaji wa chanjo na kuweza kuwafikia walengwa wote nchini na kuongoze kuwa TAMISEMI inaipa uzito mkubwa suala la chanjo kwani kinga ya mtoto inaanza na chanjo.

Kwa upande wake  Mwakilishi wa Mganga Mkuu wa Serikali ambaye pia ni  Mkurugenzi wa Idara ya kinga Kutoka Wizara ya afya, Dkt. leonard Subi amesisitiza kuwa wizara ya afya inasimamia ubora na usalama wa huduma wanazozitoa hasa upande wa chanjo ambao mara kadhaa umekua na mapokeo tofauti,hivyo amesisitiza kuwa wizara ipo makini zaidi na afya za wananchi

Wakati huo huo Mwakilishi wa wadau wa maendeleo ambaye anatoka WHO Nassoro Mohamed  ameipongeza Wizara ya afya pamoja na viongozi wa mikoa kwa kuhakikisha watoto wote nchini wanafikiwa  licha ya changamoto za hapa na pale hivyo kama wadau wanashiriki ili kuhakikisha Serikali inafikia malengo waliyojiwekea katika kutoa huduma za chanjo.

-MWISHO-

Alhamisi, 10 Desemba 2020

DKT. GWAJIMA AWATAKA VIONGOZI WA WIZARA YA AFYA KUSHIRIKIANA ILI KUONGEZA UFANISI KAZINI

 
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima akifurahia jambo na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel baada ya kuwasiri katika ofisi za Wizara ya Afya Jijini Dodoma.
 
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima akisaini kitabu pindi alipowasiri katika ofisi za Wizara ya Afya Jijini Dodoma.
 
 
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin  Mollel akisaini kitabu baada ya kuwasiri katika ofisi za Wizara ya Afya Jijini Dodoma.
 
Katibu  Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula  Mchembe akisisitiza  jambo mbele ya Watumishi wa Afya wakati  wa mapokezi ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na Naibu Waziri wake katika ofisi za Wizara ya Afya Mtumba Jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin  Mollel akisalimiana na Watumishi wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto pindi alipowasiri katika ofisi za Wizara ya Afya Mtumba Jijini Dodoma.

 

Watumishi wa Wizara ya Afya na Wakurugenzi wake, wakifuatilia kwa makini maelekezo kutoka kwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto katika ofisi za Wizara ya Afya Mtumba Jijini Dodoma.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima pamoja na Naibu Waziri wake Dkt. Godwin Mollel, wakiwa na Katibu Mkuu Idara ya Afya, Prof. Mabula Mchembe (wanne kutoka kushoto) na Katibu Mkuu Idara ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu (wakwanza kushoto).

Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima pamoja na Naibu Waziri wake Dkt. Godwin Mollel, wakiwa na Katibu Mkuu Idara ya Afya, Prof. Mabula Mchembe (wanne kutoka kushoto) na Katibu Mkuu Idara ya Maendeleo ya Jamii Dkt. John Jingu (wakwanza kushoto), pamoja na Watumishi na Wakurugenzi kutoka Idara Kuu ya Afya.


 

DKT. GWAJIMA AWATAKA VIONGOZI WA WIZARA YA AFYA KUSHIRIKIANA ILI KUONGEZA UFANISI KAZINI

Na WAJMW-Dodoma

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima amewataka Wakurugenzi na watumishi wa Wizara ya Afya kushirikiana ili kuweza kufikia lengo la kuboresha huduma za afya nchini.

Dkt. Dorothy amesema hayo leo wakati akiongea na Wakurugenzi pamoja na viongozi mbalimbali waliompokea mara baada ya kuapishwa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli kuwa Waziri wa Wizara hiyo mapema katika hafla iliyofanyika Ikulu-Chamwino, Jijini Dodoma.

Dkt. Gwajima amesema ili sekta ya afya iweze kusonga mbele na kuwafikia wananchi katika kiwango cha hali ya juu inategemea na ushirikiano utakaokuwepo baina ya viongozi wa Wizara pamoja na watumishi mbalimbali wa sekta ya afya.

“Wapeni ushirikiano makatibu wakuu, mambo mengi yanafanywa na wataalam kwa kushirikiana na makatibu wakuu, tukikubaliana kufanya jambo basi wote tufunge mikanda kuhakikisha tukamalisha kwa wakati lengo likiwa kutimiza dhamira ya Mhe. Rais ya kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya nchini”. Amesema Dkt. Gwajima.

Aidha, Waziri Gwajima amewataka viongozi wa idara mbalimbali wanapotembelea maeneo mbalimbali ya Sekta kuja na ripoti ya ziara zao na kukabidhi kwa Katibu Mkuu ili ziweze kufanyiwa kazi na kutoa miongozo halikadhalika amewataka makatibu wakuu kutofungia ripoti hizo makabatini bali wazifanyie kazi na kutatua changamoto zinazozikabili sekta ya afya.

“Nawataka Viongozi wa Wizara mnapoenda 'Supervision' mrudi na ripoti na pia nawaomba Makatibu Wakuu msizipuuze ripoti mnazoletewa ili tuone zinaleta faida gani kwenye ofisi zetu na pia katika kuboresha huduma za afya nchini”. Ameongeza Dkt. Gwajima.

Waziri huyo amesema kwa kufanya hivyo itaongeza ufanisi kwa kila kiongozi atakayeenda ili kujua aanzie wapi na siyo kila mmoja kwenda na jambo lake huku akiendelea kusisitiza viongozi hao kushirikiana ili kutatua kero na changamoto zilizopo.

Pamoja na hayo Waziri Dorothy amezitaka Taasisi, Hospitali na vituo vya afya kutoa taarifa za mapato na matumizi na ameagiza kutengenezwa mfumo utakaosaidia kupata taarifa hizo ili ziweze kusaidia kutoa muelekeo wa uboreshaji wa huduma za afya.

Pia ametaka utengenezwe muongozo wa huduma kwa wateja ili utolewe kwa watumishi wa sekta ya afya ili wabadilike na kuwathamini wagonjwa wanaofika katika maeneo ya kazi ili kupata huduma.

Kwa upande wake Katibu Mkuu Prof. Mabula Mchembe amewapongeza na kuwashukuru Waziri Dorothy pamoja na Naibu Waziri Dkt. Godwin Mollel kwa kuchaguliwa kuiongoza Wizara hiyo na kuahidi kutoa ushirikiano.

MWISHO

Jumatatu, 7 Desemba 2020

"WATUMISHI WA AFYA MSHIKIRI KATIKA KUCHANGIA MAENDELEO YA SEKTA YA AFYA" - MGANGA MKUU WA SERIKALI

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi

 


Na WAMJW – Mwanza.

 Mganga mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi amewata watumishi wa afya kushiriki kikamilifu katika kuchangia Maendeleo ya sekta ya afya na si kuiachia Serikali na Jamii pekee.

 

Amesema hayo akiwa kwenye kikao kazi na timu ya uongozi wa afya ndani ya Mkoa wa Mwanza kilichofanyika Wilayani Misungwi kujadali mikakati ya uboreshaji wa huduma za afya mkoani humo.

 

“Kwanini tushindwe kuchangia uboreshaji wa huduma za afya, lazima tuwe na moyo wa kujitoa kuchangia, hizi ni mali zetu sote sisi pamoja na watoto wetu sote tutatibiwa huko” Ni lazima sasa Hospitali zetu zianze kuwa na jicho la kutoa huduma huku zilijenga uwezo wa kifedha na kupunguza utegemezi toka serikali, bila kuathiri huduma kwa wananchi wasio na uwezo wa kulipia.. amesema Prof. Makubi.

 

Amesema hatuwezi kuitegemea Serikali na wafadhili pekee kutuletea Maendeleo ya huduma za afya katika maeneo yetu hivyo na watumishi wanapaswa kushiriki katika kuboresha huduma hizo katika maeneo waliyopo.

 

Aidha Prof. Abel Makubi alitumia nafasi hiyo pia kuendesha shughuli ya michango kwa ajili ya uboreshaji wa huduma za afya ndani ya Mkoa huo ambapo juma ya Tsh 6,850,000/= fedha ambayo itaenda kutumika katika ujenzi wa jengo kwa ajili ya huduma kwa watoto waliolazwa mahututi (NICU)

 

Prof. Makubi amesema kuwa Mkoa wa Mwanza una uhitaji mkubwa wa huduma hiyo hivyo ufinyu wa eneo katika Hospitali ya Bugando unasababisha watoto walio wagonjwa kukosa huduma kwa wakati.

 

“Hospitali ya Budango inaendelea kupata wingi wa watoto ambao hawajafikia umri wa kuzaliwa na wengi wakiletwa bugando kunakuwa na shida ya kupata eneo la kuwahudumia, kwa michango hiyo itasaidia kuboresha huduma hizo kwa kuongeza eneo” amesema Prof. Makubi

 

Hata hivyo Prof. Makubi amesisitiza suala la uongozi imara kwa viongozi waliopewa dhamana ya kusimamia taasisi za afya na kuwasisitiza  kuwajibika ipasavyo katika utumishi wao kwa kuhakikisha watumishi walio chini yao wanatoa huduma bora kwa wananchi.

 

Mwisho

HOSPITALI ZENYE WATAALAM BINGWA ZATAKIWA KUTOA HUDUMA ZA MKOBA KWA WANANCHI WALIO MBALI NA HUDUMA

 

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Makubi akisema jambo kwenye kikao na kamati tendaji ya Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Bugando



Dkt. Caroline Damian Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Tiba anayesimamia Hospitali za Rufaa za Mikoa akisema jambo kwenye kikao na kamati tendaji ya Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Bugando

Kaimu Mkurugenzi Msaidizi Hosptali ya Rufaa ya Kanda ya Ziwa Dkt. Fabian Massaga (aliyesimam) akisema jambo katika kikao kazi cha kamati tendaji ya Hospitali hiyo na Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi 


Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akimpima mapigo ya moyo mgonjwa kwa kutumia kipimo cha Echo-Cadiogram katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda Bugando

Na Englibert Kayombo, WAMJW - Mwanza

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi ametoa wito kwa Hospitali zenye wataalam wanaotoa huduma za kibingwa kuwa na huduma za mkoa “Outreach Services” endelevu ili wananchi walio mbali na huduma hizo nao waweze kuhudumiwa karibu na maeneo waliyopo.

Prof. Makubi ametoa amesema hayo akiwa katika ziara ya kikazi katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Bugando ambapo alikwenda kujionea hali ya utoaji wa huduma na kuzungumza na viongozi na kamati tendaji ya hospitali hiyo.

“Nitoe wito kwa Hospitali zote za Kanda, Maalum na ya Taifa ambazo tunazo nchini, zianze ama kama wameashaanza waendele kushuka chini kwenda kutoa huduma za mkoba kwenye hospitali zetu” amesema Prof. Makubi

Prof. Abel Makubi amesema kuwa Hospitali hizo zina wajibu wa kuwajengea uwezo wataalam waliopo kwenye Hospitali ngazi ya chini yao kuanzia Hospitali za Rufaa za Mikoa, Wilaya hadi ngazi ya chini ili waweze kutoa huduma kwenye maeneo yao na kuwapunguzia gharama wananchi kwenda umbali mrefu kwa ajili ya kupata huduma za matibabu.

Amesema kuwa wananchi wengi hawapati huduma za kibingwa katika maeneo yao kutokana na kukosokana kwa wataalam hao na pamoja na miundombinu ya vifaa wezeshi vya huduma hizo katika Hospitali za Wilaya hivyo ni vyema wakawa na mipango ya huduma hizo kwenye maeneo ya karibu na wananchi.

Prof. Makubi amesema kuwa huduma za mkoa zinawasaidia pia wataalam waliopo kwenye Hospitali za Wilaya kuongeza ujuzi wa kazi hasa kwenye kuwahudumia wananchi wenye uhitaji wa huduma za kibingwa ambazo hazipatikani kwenye maeneo yao.

Aidha Prof. Makubi ameipongeza Hospitali ya Kanda ya Bugando kwa kuwa na program endelevu ya huduma za mkoa na kuwahimiza wasiache kutoa huduma hizo kwa wananchi huku akizitaka Hospitali nyingine kuiga kutoka hospitali hiyo.

“Watu wanaona umuhimu wa Bugando kwamba ipo pamoja na wao, kwa hiyo ni vizuri na nyie mkatimiza huo wajibu wa kuendelea kushikamana na viongozi kuanzia ngazi ya Mikoa, Wilaya, Vituo vya afya mpaka kwenye zahanati”Amesema Prof. Makubi

Amemtaka Mkurugenzi pamoja na kamati tendaji ya hospitali hiyo na hospitali nyingine za Kanda na Taifa kukaa pamoja kwa muda wa miezi 3 ijayo kuona ni jinsi gani kuziendeleza huduma hizo za mkoba katika Mikoa 8” Amesisitiza Prof. Makubi

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Bugando Dkt. Fabian Massaga amesema hospitali hiyo inaendela kutoa na kuboresha huduma zaidi ili wananchi wengi waweze kupata huduma bora katika kanda ya ziwa.

Amesema Hospitali hiyo imekuwa ikitoa huduma za mkoba pamoja na ‘camp’ za huduma za kibingwa kwa wananchi hivyo kuwapunguzia gharama ya kwenda umbali mrefu kufuata matibabu bugando.

Amebainisha kuwa hospitali hiyo katika mwezi huu wa desemba kuazia tarehe 18 itaendesha ‘camp’ ya huduma za upasuaji wa moyo pamoja na upasuaji kwa watoto ambapo wataalam bigwa wa huduma hizo kutoka Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Bugando na Daktari kutoka nchi ya Uganda.

Ijumaa, 4 Desemba 2020

“VITA YA MAGONJWA YASIYO YA KUAMBUKIZA INAHITAJI JUHUZI ZA KILA MMOJA WETU” – MGANGA MKUU WA SERIKALI

- Hakuna maoni

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akisema jambo kwa viongozi wa Mkoa wa Geita katika kikao cha kujadili miundombinu ya Sekta ya Afya

Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhe. Robert Gabriel akisema jambo kwenye kikao cha mkoa kujadili miundombinu ya sekta ya afya


Na Englibert Kayombo WAMJW - GEITA


Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi amesema juhudi za kila mwananchi mmoja mmoja zinahitajika ili kupambana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwa kubadili mtindo bora wa maisha, ulaji wa chakula bora pamoja na kufanya mazoezi.


Prof. Makubi amesema hayo akiwa kwenye kikao cha viongozi ndani ya Mkoa wa Geita kilichofanyika mkoani huyo kujadili miundombinu ya sekta ya afya na elimu.


“Sasa tumeingia katika vita nyingine ya kupambana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza, magonjwa haya hayana dalili ya kukushtua kwenda Hospitali, haya ni hatari zaidi kuliko yale magonjwa ya kuambukiza” amesema Prof Makubi.


Amesema dalili magonjwa yasiyo ya kuambukiza huwa hazijitokezi kwa haraka zaidi hivyo mtu huwa anajiona kuwa yuko salama ili hali akiwa mgonjwa ambapo dalili huja baadae kwa uzito mkubwa na mtu huwa amechelewa kuanza kupata matibabu.


“Magonjwa ambayo ni ya kuambuzika yana dalili, utajisikia homa au uchovu, magonjwa yasoyo ya kuambukiza hayana hizo dalili za kukushtua kwenda hospitali, utaanza kuona matatizo baadae na kugundua moyo au figo imefeli, hizo ndo dalili za kwanza” amefafanua Prof. Makubi


Prof. Makubi amesema ni lazima tuelewe magonjwa hayo kama vile presha, moyo, kisukari, kufeli kwa figo na kifua ni hatari kuliko hata yale ya kuambuza yakiwemo Malaria, Ukimwi na Kifua Kikuu ambapo mtu asipojitambua mapema kufanya vipimo, kubadilisha tabia, mwenendo wa chakula huishia kuathirika kiuchumi yeye na familia yake kwa kuwa magonjwahayo yana gharama kubwa za matibabu.


“Usijitambua mapema kufanya vipimo, kubadilisha tabia na mwenendo wa chakula utajikuta uko kijana wa umri wa miaka 30 hadi 50 unapata matatizo ambayo yatakufanya ushindwe kushikiri katika majukumu yako ya uzalishaji na kuiingiza serikali katika gharama kubwa ya kukuhudumia” amesema Prof. Makubi


Amesisitiza wananchi kubadili mtindo wa maisha, mwenendo wa chakula na kuzingatia kufanya mazoezi ya mara kwa mara ili kupambana na magonjwa hayo ambayo yameshika kasi hasa kwa vijana na watu wazima.


“Zamani tulikuwa tunafanya mazoezi, tunalima, tunaendesha baiskeli, kutembea sasa hivi hatufanyi hivyo na ndio maana tumejikuta tunapata haya matatizo ya magonjwa yasiyo ya kuambukiza kwa haraka sana, tufanye mazoezi na kubadilisha mtindo wa maisha yetu tunayoishi sasa na kuzingatia mwenendo bora wa vyakula vyetu” amesisitiza Prof. Makubi


Aidha amewataka viongozi hao kuendelea kutoa elimu ya afya kwa wananchi ili kuweza kubadilisha mtindo wa maisha na wananchi hao waanze kwenda hospitalini kufanya vipimo ili kutambua dalili za haraka za magonjwa hayo.


Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Geita Mhandisi. Robert Gabriel amewataka wananchi kuzingatia mtindo bora wa maisha na kufanya mazoezi ya mara kwa mara ili kuepukana na magonjwa hayo


“Tumeambiwa maisha yamebadilika, mazoezi ndio mpango mzima wa afya, tumekuwa ‘busy’ mno kila siku kwenye magari maisha yamebadilika na magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza huja na mtetemo mkubwa na kupona huwa ni shida, tukumbushane na kubadilika ili tuweze kupambana na magonjwa hayo” Amesisitiza Mkuu wa Mkoa wa Geita.


Mhe. Robert Gabriel ametoa wito kwa wananchi kufanya mazoezi ya mara kwa mara na kubadili mtindo wa maisha kuepukana na magonjwa hayo ambayo amesema huathiri uchumi wa familia na nchi kuingia gharama kubwa ya matibabu.

Mwisho

 

"VIFO VYA MAMA WAJAWAZITO HAVIVUMILIKI TENA" – MGANGA MKUU WA SERIKALI

- Hakuna maoni
Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akisema jambo kwa timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kilichofanyika Wilaya ya Misungwi.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Dkt. Thomas Rutachuzibwa akisema jambo kwa timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kilichofanyika Wilaya ya Misungwi.

Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Tiba anayesimamia Hospitali za Rufaa za Mikoa Dkt. Caroline Damian (kulia) pamoja na Katibu wa Mganga Mkuu wa Serikali Bi. Maurine Kunambi (kushoto) wakiwa kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga Mkoa wa Mwanza.

Timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza wakiwa kwenye kikao cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.

Timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza wakiwa kwenye kikao cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.


VIFO VYA MAMA WAJAWAZITO HAVIVUMILIKI TENA" – MGANGA MKUU WA SERIKALI

Na Englibert Kayombo WAMJW - MWANZA.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi amesema kuwa Serikali haitovumia tena vifo vya akina mama wajawazito vinavyosababishwa na uzembe wa watumishi kazini.

Prof. Makubi ametoa kauli hiyo alipokuwa akifunga kikao kazi cha timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza kilichofanyika Wilayani Misungwi kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.

"vifo vya akina mama wajawazito havivumiliki tena kwa sasa hivi kwenye hii dunia ambapo tumeingia uchumi wa kati, ni lazima tutafute mbinu mpya na nzuri tuweze kuziendeleza na kuhakikisha kwamba ambaye amekuja kuleta maisha asifariki” amesema Prof. Makubi.

Amesema siyo vifo vya akina mama wajawazito tuu ndio vizuiwe bali hata vya watoto wachanga wanaozaliwa pia vidhibitiwe kwa wataalam wa afya kuhakikisha watoto hao wanazaliwa salama pia.

Prof. Makubi amesema Serikali imewekeza rasilimali nyingi kwenye sekta ya afya hivyo ni vyema matunda ya uwekezaji huo yakaenda kuonekana kupitia uboreshwaji wa huduma bora za afya ikiwemo kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga.

Amesema anashangazwa na vifo vingi vya akina mama wajawazito kutokea katika vituo vya kutolea huduma za afya na sio kwenye Jamii na kuwataka watumishi hao kujitafakari ni sehemu gani kuna changamoto ili zifanyiwe kazi na kudhibiti vifo hivyo.

“Nimefurahishwa kuona mmekutana hapa kutafakari, kwa hiyo mmeshaliona tatizo hamkusubiri Wizara ya Afya kuja kuwaambia mfanye nini, hilo ndio linanipa moyo mmejitambua na mmeamua kuchukua hatua wenyewe” amepongeza Prof. Makubi wa timu ya uongozi wa afya ya Mkoa wa Mwanza kwa kuanza kuchukua hatua.

Aidha,Prof. Makubi ametoa wito kwa Mikoa mingine iendeleze kile ambacho mkoa wa Mwanza imeanza kufanya kwa kufanya vikao vya tathimini na kuweka mikakati ya kudhibiti vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga. 

“Kabla ya mwezi wa kwanza haujaisha kila Mkoa uwe umeshakaa, ukishirikisha viongozi wote wa Mkoa, Wilaya na Halmashauri vituo vya afya mpaka zahanati wawe na wawakilishi ili mjadili mbinu ambazo zinaweza kupunguza vifo vya akina mama wajawazito kwa kiasi kikubwa zaidi”

 Amesisitiza Prof. Makubi akitoa agizo hilo kwa timu za uongozi wa afya kwa mikoa yote.“Tuondoke hapa tulipo kwa sababu wananchi wanatamani twende tupige hatua moja mbele ili tukaboreshe huduma zetu, kwa mikakati mliyoweka tukiitekeleza naamini tunaweza tukatoka kwenye tatizo hili” Amesisitiza Prof. Makubi.

Naye Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Dkt. Thomas Rutachuzibwa amesema kuwa wameyapokea maelekezo yote aliyoyatoa Mganga Mkuu wa Serikali na watayafanyia kazi kuhakikisha vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga vinadhibitiwa mkoani humo.

“Ninakuahidi ndani ya miezi mitatu tutaanza kupata mabadiliko, tutakaa kwa muda uliobaki kuweka mpango kazi kuhakikisha tunaenda kutekeleza yale yote tuliyopanga ili kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga” amesema Dkt. Rutachuzibwa.

Dkt. Rutachuzibwa amesisitiza suala la wajibikaji kwa watumishi wa afya wakiwa kwenye maeneo yao ya kazi kwa kutambua wana wajibu upi na kuhakikisha wanatoa huduma bora kwa wananchi na kupunguza changamoto zilizopo maeneo yao ya kazi.

“Kila mmoja ajitambue, tutoe huduma kwa wananchi, kuanzia leo naomba wote tuanze upya, kila mtu awajibike kwa kipande chake” amesisitiza Mganga Mkuu wa Mkoa Dkt. Thomas Rutachuzibya.

Mwisho

Alhamisi, 3 Desemba 2020

MABARAZA YA KITAALUMA YAPEWA SIKU 14 KWENDA MKOA WA MWANZA KUZUNGUMZA NA WATUMISHI

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi aliyesisimama akisema jambo kwenye kikao na watumishi wa afya katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba

Watumishi wa afya katika Hospitali ya Wilaya ya Kwimba wakiwa kwenye kikao na Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi (hayupo pichani)

NA Englibert Kayombo WAMJW - Mwanza

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi ametoa muda wa siku 14 kwa baraza la madaktari pamoja na baraza la wauguzi kwenda Mkoa wa Mwanza kuzungumza na watumishi wa kada wanazosimamia ili kurekebisha na kuwajengea uelewa zaidi wa maadili ya taaluma zao.

Prof. Makubi ametoa agizo hilo akiwa Wilayani Kwimba alipokuwa ziara ya kikazi kukagua hali ya utoaji wa huduma na kuzungumza na watumishi wa kada ya afya. 

“Mabaraza mengi yamekuwa yanabaki huko makao makuu kuhukumu watu, wamejiondoa kabisa kwenye kazi ya kuwajenga watumishi, badala ya kupita huku na kuwaelekeza watumishi, wao wanasubiri kupokea malalamiko” amesema Prof. Makubi

Amesema ni lazima mabaraza yahakikishe watumishi hawafanyi makosa kwa kuwaweka katika maadili mema bila kufanya hivyo tutakuwa na watumishi wasio na sifa.

Prof. Makubi amesisitiza kuwa mabaraza yote 10 yanatakiwa kutelekeza majukumu yao ipasavyo na yote wajiwekee utaratibu wa kuzunguka na kuzungumza na watumishi kuanzia ngazi ya Mikoa hadi Wilayani

Mwisho.

Jumatano, 2 Desemba 2020

WATUMISHI KADA YA AFYA WAASWA KUDHIBITI VIFO VITOKANAVYO NA UZAZI NA WATOTO WACHANGA.

Mkurugenzi wa Huduma za Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe kutoka Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt. Ntuli Kapologwe akisema jambo kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na Uzazi na Watoto wachanga Mkoa wa Mwanza

Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Emmanuel Tutuba akisema jambo wakati wa kikao kazi cha kujadili ivifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kwa mkoa huo

Mganga Mkuu Mkoa wa Mwanza Dkt. Thomas Rutachuzibwa akisema jambo wakati wa kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga katika mkoa huo

Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Tiba anayesimamia Hospitali za Rufaa za Mikoa Dkt. Caroline Damian (kushoto) pamoja na mwakilishi kutoka Ofisi ya Mganga Mkuu wa Serikali Bi. Maurine Kunambi (kulia) wakiwa kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga Mkoa wa Mwanza.

Mkurugenzi Mtendaji Taasisi ya Benjamin Mkapa (kulia) Dr. Ellen Mkondya- Senkoro pamoja na viongozi wengine wakiwa kwenye kikao kazi cha kujadilii vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga Mkoa wa Mwanza.

Wajumbe wa timu ya afya ya Mkowa wa Mwanza wakiwa kwenye kikao cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga katika Mkoa wa Mwanza.

Na Englibert Kayombo, WAMJW - MWANZA

Watumishi wa kada ya afya nchini wameaswa kuhakikisha wanadhibiti vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kwa kuwajibika ipasavyo wakiwa kazini na kuepukana na tabia za uzembe.

Kauli hiyo imetolewa na na Mkurugenzi wa Huduma za Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe kutoka Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Dkt. Ntuli Kapologwe alipokuwa akizungumza na timu ya afya ya Mkoa wa Mwanza kwenye kikao kazi cha kujadili vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga kwa mkoa huo.

“Suala la vifo, pasipokuwepo na uwajibikaji na umoja ni vigumu sana kuweza kulifanikisha, kuchukua hatua imekuwa changamoto kwa timu nyingi hivyo kupelea kuongezeka kwa vifo” amesema Dkt. Ntuli.

Ameendelea kusema kuwa wataalam wa afya hawatakiwi kuoneana aibu endapo mjumbe wa timu hatofanya kazi yake ipasavyo kwa uzembe wake mwenyewe achukuliwe hatua za kinidhamu ili kuweza kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na kupunguza vifo vya akina mama na watoto wachanga.

Amesema kuwa wataalam wa afya wanapaswa kuwa wamoja na kushirikiana kikamilifu wakiwa kazini na kuacha kusubiri wataalam kutoka ngazi ya juu kuja kutoa maamuzi ya vitu ambavyo vingewezwa kufanywa na viongozi katika eneo husika.

Kwa upande wake Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Emmanuel Tutuba amesema vifo vitokanavyo na uzazi na watoto wachanga vimekuwa viongezeka mkoani humo na kuwataka watumishi wa kada ya afya kuhakikisha wanapunguza kiwango cha vifo hivyo kwa mkoa huo ambao ni kinara wa huduma bora za afya katika Kanda ya Ziwa.

Akitaja takwimu za vifo hivyo, Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza Bw. Tutuba amesema katika kipindi cha miaka mitano kuanzia mwaka 2015 vifo vilikuwa 145, mwaka 2016 vifo 151, mwaka 2017 vifo 193, mwaka 2018 vifo 151, mwaka 2019 vifo 171 na kwa mwaka huu mpaka kufikia mwezi Septemba vimetokea vifo 142.

“Lazima tukae tutafakari, licha ya uwekezaji mkubwa ambao Serikali imefanya lakini vifo vinaongezeka, tunapokutana hivi tusiishie tuu kupashiana, ni lazima tutimize wajibu wetu” amesisitiza Bw. Tutuba.

Hata hivyo Bw. Tutuba amepongeza watumishi wa kada ya afya mkoani humo kwa juhudi zao wanazofanya kuhakikisha wanaokoa maisha ya watanzania pamoja na raia wa kigeni wanaokuja mkoani humo kwa ajili ya huduma za matibabu.

“Tumejitahidi kufanya mazuri mengi, lakini badi hatujatekeleza kwa asilimia 100, tumefanya vizuri lakini bado tungeweza kufanya vizuri zaidi endapo kila mmoja angetimiza wajibu wake” amesema Bw. Tutuba.

Mwisho

Jumanne, 1 Desemba 2020

WANAOFANYA MAPENZI NA WASICHANA WENYE UMRI MDOGO WAONYWA

- Hakuna maoni
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akihutubia Wananchi kwenye maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa Kimataifa, Tujumuike Pamoja".

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akitoa taarifa ya hali ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI mbele ya mgeni rasmi (Hayupo kwenye picha) wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akiteta jambo na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro. 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akipeana mkono na Mkurugenzi wa TACAIDS Dkt. leonard Maboko baada ya kuhutubia wananchi, wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro. 
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akipata taarifa kutoka kwa Mkuu wa kitengo cha tiba na matunzo Dkt. Anath Rwebemberwa katika banda la Mpango wa Taifa wa kupambana na UKIMWI (NACP) ulio chini ya Wizara ya Afya, maendeleo ya jamii, jinsia, Wazee na watoto.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe na Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi wakiwa na Mkurugenzi wa Kinga Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi (watano kutoka kushoto) Meneja NACP Dkt. Beatrecy Mutayoba (wamwisho), wakwanza kushoto ni Mkuu wa kitengo cha tiba na matunzo Dkt. Anath Rwebemberwa na wapili kushoto ni Mkuu wa kitengo cha Kinga (NACP) Dkt. Magreth Kagashe.


Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akiwa na viongozi wengine Wakiserikali, wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa Kimataifa, Tujumuike Pamoja".


WANAOFANYA MAPENZI NA WASICHANA WENYE UMRI MDOGO WAONYWA. 

Na Rayson Mwaisemba WAMJW- Kilimanjaro 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa ametoa onyo kali kwa wanaofanya mapenzi (ngono) na wasichana wenye umri mdogo, hali inayosababisha kuwaharibia malengo yao ya baadae. 

Mhe. Kassim Majaliwa ameyasema hayo leo wakati akiwahutubia wananchi kwenye maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa Kimataifa, Tujumuike Pamoja".

"Nataka niwakumbushe na kutoa tahadhari kwa wale watu wazima mnaofanya mapenzi na vijana wadogo wa kike, ole wenu, ole wenu, ole wenu " ameyasema Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.
Alisema kuwa, takwimu za maambukizi mapya ya VVU zinaonesha kwamba asilimia 40 ya maambukizi hutokea kwa vijana na katika hao asilimia 80 ni vijana wa kike, huku akiweka wazi kuwa, vijana ni kundi linalokabiliwa na changamoto ya maambukizi mapya ya VVU nchini.

Aliendelea kusema, kundi la vijana na hasa wa kike lipo kwenye hatari kubwa zaidi ya kupata maambukizi mapya, huku akidai uchambuzi wa kimazingira kuhusu takwimu hizi unaonesha kuwa sababu za vijana kuwa katika hatari ya maambukizi mapya ya VVU ni pamoja na kuanza ngono katika umri mdogo, vijana wadogo wa kike kuwa na mahusiano ya kingono na wanaume wenye umri mkubwa Matumizi yasiyo sahihi na endelevu ya mipira ya kike na kiume.

Aidha, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, ametoa wito kwa vijana kujitambua na kuthamini maisha yao kwa kujikinga na maambukizi mapya ya VVU, huku akiwakumbusha kuwa vijana ndio nguvu kazi ya Taifa, na kuwataka wale wanaoishi na VVU waendelee kutumia dawa za ARV kwa ufuasi sahihi bila kuacha ili kufubaza VVU na kuimarisha afya zao. 

"Natoa wito kwa vijana kujitambua na kuthamini maisha yao kwa kujikinga na maambukizi mapya ya VVU kwa kuwa ninyi ni nguvu kazi na Taifa linawategemea. Na wale wanaoishi na VVU waendelee kutumia dawa za ARV kwa ufuasi sahihi bila kuacha ili kufubaza VVU na kuimarisha afya zao", alisema Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa. 

Nae Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe amesema kuwa, Tanzania na Dunia kwa ujumla imepiga hatua kubwa katika jitihada za kukabiliana na janga la VVU na UKIMWI.

Aliendelea kusema kuwa, kama nchi inavyoelekea kufikia malengo ya Tisini Tatu, changamoto, na vipaumbele vimeendelea kubadilika kutokana na mafanikio ya mwitikio wa mapambano.
Takwimu zinaonesha kuwa wanaume, watoto, vijana wanaopevuka na vijana wadogo, na watu wanaofanya tabia hatarishi, wako nyuma kutambua hali zao, ufuasi hafifu wa tiba, na ufubazaji wa VVU usioridhisha. 

Hata hivyo, Prof. Mabula Mchembe amesema kuwa, Serikali inaendelea na jukumu la kutafiti, kuandika na kusambaza taarifa za kitaalamu zinazochambua na kutoa masuluhisho ya changamoto zitazotumika kuhuisha sera, miongozo na taratibu za huduma na afua za VVU na UKIMWI. 

"Tunalo jukumu sasa, la kutafiti, kuandika na kusambaza taarifa za kitaalamu zinazochambua na kutoa masuluhisho ya changamoto hizi ili sasa yatumike kuhuisha sera, miongozo na taratibu za huduma na afua za VVU na UKIMWI", amesema Prof. Mchembe 

Mwisho.