Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumatatu, 31 Agosti 2020

SIMAMIENI USAJILI WA DAWA ZA ASILI KWA KUTOA ELIMU YAKUTOSHA KWA WATENGENEZAJI - PROF. MCHEMBE.

- Hakuna maoni

KATIBU MKUU Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto - Idara Kuu ya Afya Prof. Mabula Mchembe akisema jambo  kwa wadau (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa Siku ya Tiba ya Asili kwa Mwafrika

Dkt. Grace Magembe Mkurugenzi wa Huduma za Tiba kutoka Wizara ya Afya

Mzee Issa Mdoe Mwakilishi wa Wagaga wa Tiba asili kutoka Mkoa wa Dodoma






Na WAMJW- DOM 

KATIBU MKUU Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto - Idara Kuu ya Afya Prof. Mabula Mchembe amewaagiza Baraza la Tiba Asili na Tiba mbadala na Mamlaka zote katika Mikoa na Halmashauri nchini kusimamia usajili wa dawa za asili kwa kutoa elimu ya kutosha kwa waganga na watengeneza dawa wa tiba asili. 

Prof. Mchembe ameyasema hayo leo wakati akifungua maadhimisho ya siku ya tiba asili ya Mwafrika yaliyofanyika katika viwanja vya Mwl. Nyerere Jijini Dodoma, yenye kauli mbiu ya "Miongo miwili ya Tiba Asili Afrika 2001 mpaka 2020 Nchi zina mafanikio gani".

"Kwa maana hiyo basi nawaagiza Baraza la Tiba Asili na tiba mbadala na Mamlaka zote katika Mikoa na Halmashauri nchini kusimamia usajili wa dawa za asili kwa kutoa elimu ya kutosha kwa waganga na watengeneza dawa wa tiba asili" alisema Prof. Mabula Mchembe. 

Aliendelea kusisitiza kuwa, ni vyema Baraza la tiba asili na Mamlaka zote nchini, kushirikiana na taasisi zote zinazohusiana na tiba asili hususan Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, kutokana na kuwepo kwa kitengo kinachohusiana na mimea. 

Prof. Mchembe amesema kuwa, katika kuadhimisha miaka 18 ya siku ya tiba asili ya Mwafrika, Serikali kupitia Wizara ya Afya imefanya mambo mengi ikiwemo, kuitambua huduma ya tiba asili katika Sera ya Afya kuanzia, kutungwa kwa Sheria ya tiba asili na tiba mbadala Namba 23 ya mwaka, kutengenezwa kwa kanuni na miongozo mbalimbali ya Tiba Asili na Tiba Mbadala mwaka, kuanza kutoa mafunzo kwa Waratibu na watoa huduma wa tiba asili nchini.

Aidha Prof. Mchembe, ameliagiza Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala na Mamlaka zote katika Mikoa na Halmashauri nchini kusimamia usajili wa dawa za asili kwa kutoa elimu ya kutosha kwa waganga na watengeneza dawa wa tiba asili.

Mbali na hayo Prof. Mchembe ametoa wito kwa Wataalamu wa tiba asili na tiba mbadala nchini kutumia fursa kwa kuanzisha viwanda vidogo na vya kati vya kuchakata dawa za asili kwa lengo la kuongeza ubora na hivyo thamani yake. 

"Nitoe wito kwa Waganga na wadau wa Tiba Asili kutumia fursa iliyopo ya Tanzania ya Viwanda kwa kuanzisha viwanda vidogo na vya kati vya kuchakata dawa za asili kwa lengo la kuongeza ubora na hivyo thamani yake" alisema Prof. Mchembe 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe amesema kuwa, kupitia maadhimisho ya tiba asili kama nchi tumepata mafanikio mengi sana ikiwemo kuongezeka idadi kubwa ya wananchi wanaotumia dawa za asili hususan katika kipindi cha mlipuko wa virusi vya Corona. 

"Kupitia maadhimisho ya tiba asili, tangu tumeanza kama nchi, Luna mafanikio mengi sana yameweza kupatikana, lakini kubwa naloweza kulisemea, ni kuongezeka kwa idadi ya wananchi wanaotumia dawa zetu za asili pamoja na tiba mbadala, na mfano mzuri ni katika kipindi cha mlipuko wa ugonjwa wa Corona, kama nchi tunaweza kusimama kifua mbele na kusema tiba zetu za asili zimetutoa kwa kiwango kikubwa, " alisema. 

Aliendelea kusema kuwa, pamoja na kuendelea na utafiti wa dawa mbali mbali za asili ambazo zilitumika katika kipindi cha mlipuko wa ugonjwa wa Corona, takribani zaidi ya watu 100,018 walitumia dawa za asili, ikiwemo njia ya kujifukiza (nyungu), na kuonesha mafanikio kwa kiasi kikubwa. 

Nae Kaimu Msajili Baraza la tiba asili na tiba mbadala Wizara ya Afya Ndg. Patrick Seme amesema kuwa, hadi sasa Baraza la tiba asili na tiba mbadala limeshasajili dawa 30, huku akiweka wazi kuwa kiasi hiki cha dawa zilizosajiliwa ni kidogo ukilinganisha na uhalisia, huku akiweka wazi kuwa Baraza linaendelea kuhakikisha linasajili dawa nyingi zaidi kwa kufuata kanuni na taratibu. 

"Kama mnavyofahamu kuwa mwaka 2017 tulianza kusajili dawa za asili kupitia Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala na kuwa hadi sasa dawa 30 zimesajiliwa. Kiasi hiki cha dawa zilizosajiliwa nichache sana ukilinganisha na uhalisia." Alisema. 

Akiwawawakilisha Waganga wa tiba asili Mkoa wa Dodoma Mzee Issa Mdoe amesema kuwa, Baraza la tiba asili na tiba mbadala kwa kushirikiana na Waganga wa tiba asili limekuwa na mafanikio mengi yakiwemo kutoa elimu mara kwa mara kwa Waganga kujua dhana ya tiba asili ikiwemo kujiepusha na mauaji ya vikongwe na mauaji ya albono na mauaji ya watoto wadogo. 

Mbali na hayo Mzee Issa Mdoe ameweka wazi kuwa, baadhi ya changamoto zinazowakumba, zikiwemo gharama za usajili wa dawa kuwa juu, hivyo kuwafanya Waganga wengi kushindwa kisajili dawa zao, elimu ndogo ya malipo ya njia ya elektroniki inayopelekea baadhi ya Waganga katapeliwa na watu wasio waaminifu.

Mwisho.

Alhamisi, 27 Agosti 2020

SERIKALI KUSAINI HATI YA UTEKELEZAJI YA SHILINGI BILIONI 125.69 KWA AJILI YA KUIMARISHA HUDUMA ZA AFYA NGAZI YA MSINGI

- Hakuna maoni

Prof. Mabula Mchembe Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto

Na. WAMJW-Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendelo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo wanaochangia sekta ya afya kupitia Mfuko wa Afya wa Pamoja (Health Basket Fund imeridhia kuweka saini Hati ya Shilingi Bilioni 125.69 kwa ajili ya kuimarisha huduma za afya katika ngazi ya msingi nchini 

Akiongea wakati wa kuidhinisha makubaliano hayo,  Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Prof. Mabula Mchembe amesema kuwa lengo kuu la Mfuko huo tangu kuanzishwa kwake mwaka 1999 ni Kuimarisha huduma za afya katika ngazi ya msingi (halmashauri) zote nchini. 

Amesema katika utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2020/21  Wadau nane (8) watachangia jumla ya USD 53.84 sawa na Shilingi bilioni 125.69 kwa kipaumbele cha kuimarisha huduma za afya katika vituo vya afya kwenye halmashauri zote 184 nchini.

“Shilingi bilioni 105.32  zitatumika kwa ajili ya kuimarisha utoaji wa huduma za afya katika vituo vya afya vipatavyo 5,533 kwenye halmashauri zote 184 nchini ikiwa ni pamoja na ununuzi wa dawa, vifaa na vifaa tiba, uendeshaji wa vituo, ukarabati mdogo na huduma za chanjo na vikoba.

 “Fedha hizo zitapelekwa moja kwa moja vituoni kwa utaratibu wa ‘Direct Health Facility financing” Alisema Prof.. Mchembe.
Aidha, Prof Mchembe alisema Shilingi bilioni 4.29 zitatumika kwa ajili ya kuziwezesha Timu za Afya za Mikoa 26 kufanya ufuatiliaji na usimamizi shirikishi katika halmashauri zote nchini na Shilingi bilioni 2.09 zitawezesha Ofisi ya Rais– TAMISEMI kusimamia na kutoa msaada wa kitalaam katika halmashauri na mikoa yote nchini. 

Aliongeza kuwa Shilingi bilioni 5.13 zitawezesha Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kutekeleza masuala ya sera, mikakati na miongozo kwa ajili ya kuhakikisha huduma za afya zinatolewa kwa kiwango na ubora stahiki na Shilingi bilioni 8.86 zitakuwa kwa ajili ya kutekeleza maeneo mengine ya kipaumbele katika sekta.

“Vipaumbele tulivyoidhinisha  na kamati ni pamoja na kutoa mafunzo kwa wataalam 620 wa dawa za usingizi; kununua machine za kisasa za kutolea dawa za usingizi katika vituo vya afya ngazi ya halmashauri na kufanya ukarabati mkubwa katika vyuo vinne (4) vya kutolea mafunzo ya watalaam wa afya”.

Prof. Mchembe alitaja maeneo mengine ya kipaumbele yaliyoidhinishwa na Kamati Kuu ya Mfuko huo kuwa ni kuhuisha Mkataba wa Makubaliano (MOU) baina ya pande zote mbili kwa kipindi cha 2021 – 2026, kununua mashine za kutolea dawa za usingizi katika vituo vya kutolea huduma za afya pamoja na kuvijengea uwezo vituo vya afya katika kusimamia na kutumia fedha kwa kuzingatia miongozo na taratibu mbalimbali. 

Maazimio ya uwekaji saini Hati hiyo yamefanyika kwenye ofisi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto iliyoko mji wa Serikali Mtumba ambapo ulihudhuriwa na watalaam kutoka Wizara ya  Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Wizara ya Fedha na Mipango, OR – TAMISEMI, Bohari ya Dawa na Wadau wa Maendeleo wanaochangia Mfuko huo kutoka Canada, Denmark, KOICA, Ireland, Switzerland UNICEF, UNFPA na Benki ya Dunia. walioshiriki kwa njia ya ‘video conference’. 
-Mwisho-


 

Ijumaa, 21 Agosti 2020

TUSHIRIKIANE KUPAMBANA DHIDI YA MAGONJWA YASIYO AMBUKIZA - MGANGA MKUU WA SERIKALI.

- Hakuna maoni

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi (watatu kutoka kushoto) akikagua taarifa za mgonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Kaskazini KCMC, pindi alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma katika Hospitali hiyo.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi (watatu kutoka kushoto) akipokea taarifa za hali ya mgonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Kaskazini KCMC, pindi alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma katika Hospitali hiyo.

Kiwanda cha uzalishaji mitungi ya oksijeni kilichopo katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya kaskazini KCMC. 

Baadhi ya mashine za uzalishaji wa gesi ya oksijeni inazotumika katika matibabu  ya wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya kaskazini KCMC.


TUSHIRIKIANE KUPAMBANA DHIDI YA MAGONJWA YASIYO AMBUKIZA - MGANGA MKUU WA SERIKALI.

Na WAMJW- KILIMANJARO

MGANGA Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi ametoa wito kwa watoa huduma za Afya kushirikiana kwa pamoja kwa kutoa elimu, katika mapambano dhidi ya magonjwa yasiyo ambukiza yanayosababishwa na mtindo wa maisha ikiwemo ulaji usiofaa, matumizi ya vileo na kutofanya mazoezi.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Makubi ametoa rai hiyo wakati alipotembelea Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Kaskazini KCMC kukagua hali ya utoaji huduma za Afya katika Hospitali hiyo kwa wananchi.

Prof. Makubi amesema kuwa, ni muhimu watoa huduma za afya kuungana kwa pamoja kushirikiana kwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu magonjwa yasiyo ambukiza (NCD), kwa njia ya kuwafuata wagonjwa katika maeneo yao, jambo ambalo litasaidia kupunguza mzigo wa wagonjwa katika hospitali za Rufaa nchini.

"Mshirikiane kwa pamoja kutoa Elimu ya ufahamu, na kupima angalau mara 2 kwa mwaka juu ya  magonjwa yasiyo ambukiza  kupitia njia ya kuwafuata wateja katika maeneo yao na kuwafanyia upimaji (outreach program)" alisema Prof. Makubi.

Hata hivyo, Prof. Makubi ametoa rai kwa watoa huduma za afya kuhakikisha wanatoa huduma kwa wakati kwa wagonjwa ili kuepusha msongamano unaoweza sababisha mlipuko wa magonjwa mengine katika hospitali na kupunguza usumbufu kwa wagonjwa.

Aidha, Prof. Makubi ameridhishwa kwa kiasi kikubwa hali ya utoaji huduma katika Hospitali hiyo, huku akiwataka kuongeza jitihada ili kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi na kupunguza malalamiko yanayoweza kuepukika kwa urahisi.

"Mimi kwa KCMC, sipati malalamiko mengi sana, simamìeni katika ubora huo, na mhakikishe mnaongeza Juhudi zaidi, na kwa hilo nawapongèza sana sana" alisema Prof. Abel Makubi.

Hata hivyo, Prof. Makubi amewapongeza watumishi wa Hospitali ya KCMC wakiongozwa na Mkurugenzi wao Prof. Gileard Masenga kwa kuanzisha mradi wa uzalishaji wa gesi ya oksijeni, jambo linalosaidia kuongeza mapato na kuokoa kiasi kikubwa cha pesa ambacho kingetumika kununua mitungi ya gesi, na pesa hizo kuelekezwa katika kuboresha huduma kwa wananchi.

Naye, Mkurugenzi wa huduma za tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Maghembe amewataka watumishi kutobweteka, katika kuwahudumia wananchi, licha ya kazi nzuri ambayo inaendelea kufanywa na uongozi kwa kushirikiana na Mkoa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa uhakika ubora huduma Wizara ya Afya Dkt. Eliakim Eliud amewataka watoa huduma kuhakikisha wanafuata miongozo ya kujikinga ya utoaji huduma (IPC guidelines) wakati wa kuhudumia wagonjwa ili kujikinga wao na wagonjwa wanaowahudumia.

Mwisho.

Alhamisi, 20 Agosti 2020

HATUNA UHABA WA CHANJO NCHINI- DKT. LEONARD SUBI

- Hakuna maoni

Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto Dkt. Leonard Subi, akisisitiza jambo mbele ya Waandishi wa habari wakati alipofanya ziara katika ghala la chanjo lililopo katika Hospitali ta Rufaa ya Mkoa wa Dodoma-General.


HATUNA UHABA WA CHANJO NCHINI: DKT. LEONARD SUBI

Na. Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesema kuwa, haina upungufu wa chanjo wa aina yeyote hivyo kuwataka wazazi/walezi kuwapeleka watoto wao kuwapatia chanjo katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi wakati alipotembelea ghala ya kuhifadhia chanjo iliyopo hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma kukagua hali ya chanjo katika mkoa huo.

Dkt. Subi amesema kuwa, chanjo zote aina tisa ambazo zinakinga dhidi ya magonjwa kumi na tatu zipo kwenye ghala hilo“tulikua na upungufu wa aina mbili za chanjo nchini kati ya tisa ambazo tumekuwa tukizitoa lakini, sasa hivi chanjo zote zipo, kwani zimeshawasili hapa nchini na usambazaji unaendelea”, amesema Dtk. Subi

Hata hivyo Dkt. Subi amesema kuwa, upungufu huo wa chanjo ulitokea baada ya Dunia kukumbwa na janga la mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19 ambapo anga zote zilifungwa kwani chanjo husafirishwa kwa mnyororo baridi, kwahiyo huitaji usafiri wa anga.

“Tunamshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa kulifungua anga la Tanzania ambapo,  chanjo sasa zimeanza kuingia nchini na hadi sasa mikoa kumi na tatu(13) chanjo hizi zimeshapokelewa kati ya mikoa 26, na mikoa mingine kumi na tatu  ya Tanzania Bara usambazaji unaendelea kupitia Bohari ya Dawa (MSD)”.

Aidha, Dkt. Subi alisema kuwa, usambazaji wa chanjo hizo mbili ambazo wananchi walikua wanazikosa, umeshaanza na watazipata kwa uhakika, huku akielekeza bohari ya dawa nchini (MSD) kuhakikisha chanjo zote  zimefika katika mikoa iliyosalia ya Tanzania Bara ifikapo mwishoni mwa wiki hii.

“Waganga Wakuu wa Mikoa na Halmashauri wote nchini hakikisheni chanjo hizo mnazipeleka kwenye vituo vyetu  vya kutolea huduma za afya na muwajulishe wananchi kwamba chanjo zipo na zinapatikana bila malipo yeyote, wazazi na walezi pelekeni watoto wenu kupata chanjo katika mikoa yenu”Alisisitiza Dkt. Subi.

Kwa upande wa taarifa iliyotolewa na moja ya chombo cha habari hapa nchini kwa kukosekana kwa chanjo ya kuzuia kuhara (Rota) Dkt. Subi alifafanua kuwa, nchi ya Tanzania haijawahi kukosa chanjo hiyo,huku akiweka bayana kuwa, chanjo zilizopungua kwa mwezi mmoja na nusu ni chanjo ya Polio na Surua-Rubella hali iliyosababishwa na mlipuko wa Covid-19 Duniani, huku akisisitiza kuwa serikali imekua ikinunua chanjo hizo kutoka nchi za Ulaya na Asia.

Aliendelea kusema kuwa, Serikali inaendelea kutoa fedha za chanjo, na kuweka wazi kuwa hadi sasa  imetoa zaidi ya  shilingi bilioni 18 kwa ajili ya ununuzi wa chanjo  na kuifanya  Tanzania kuendelea kuwa katika kiwango cha juu cha utoaji wa chanjo kwa zaidi ya asilimia 98 kwa miaka sita mfululizo.

Hata hivyo, Dkt. Subi amesema kuwa, Tanzania haijawahi kupata mgonjwa wa kupooza tangu mwaka 1996, jambo linalotokana na  uwepo wa hali nzuri ya upatikanaji wa chanjo, huku akidai kuwa nchi ya Tanzania tayari imepata cheti cha utambuzi kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) mwaka 2015.

 

MWISHO.

Jumatano, 19 Agosti 2020

HUDUMA ZA AFYA YA UZAZI NA MTOTO ZIMEENDELEA KUIMARIKA NCHINI

- Hakuna maoni




 


 Na WAJMW-Dodoma

 Huduma za Afya kwa mama na mtoto zimeendelea kuimarika nchini baada ya uboreshwaji wa huduma za afya nchini katika kipindi cha miaka mitano toka 2015 hadi 2020.

 Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakati akiongea na wadau mbalimbali wa maendeleo katika sekta ya afya Pamoja na watumishi mbalimbali wa Wizara hiyo waliokutana jijini Dodoma.

 Waziri Ummy amesema kuimarika kwa huduma hizo zimetokana na kuimarishwa miundombinu ikiwa ni pamoja na kuongezeka vituo vya kutolea huduma 1797 ambavyo Zahanati 1198, Vituo vya Afya 487, Hospitali za Halmashauri 99, Hospitali za Mikoa 10 ikiwemo Hospitali ya Mkoa wa Mara ya Mwalimu Nyerere Memorial Hospital ambayo ujenzi wake iliasisiwa na Mwalimu J.K Nyerere mwaka 1977.

 “Uwekezaji huu mkubwa uliofanywa na Serikali ya awamu ya tano kwenye miundombinu ya utoaji wa huduma za afya umeongeza umeongeza vituo vya huduma za upasuaji wa dharura wa kumtoa mtoto tumboni kutoka vituo 192 (Vituo vya afya 115 na Hospitali za Halmashauri 77) mwaka 2015 hadi vituo 586 (Hospitali za Halmashauri 99 na vituo vya 487) mwaka 2020 ikiwa ni sawa na ongezeko la vituo 394”. Amesema Waziri Ummy.

 Waziri Ummy amesema Serikali imeongeza idadi ya Vituo vya huduma kwa ajili ya Watoto wachanga wanaozaliwa wakiwa na shida ya kupumua, uzito pungufu na maambukizo ya Bakteria (Neonatal Care Units) kutoka 14 mwaka 2015 hadi kufikia 104 mwaka 2020.

 Aidha, Serikali imeongeza upatikanaji wa huduma kwa ajili ya Watoto mahututi (Paediatric ICU) katika Hospitali za Rufaa za kanda mbili mwaka 2015 hadi Hospitali za kanda sita ambazo ni Muhimbili, Bugando, KCMC, Mbeya, Benjamin Mkapa na Mloganzila.

 Waziri Ummy amesema upanuzi huu umesogeza huduma muhimu kwa ajili ya dharura ya uzazi na Watoto karibu na wananchi kupitia uimarishaji wa vituo vya afya ya msingi, hivyo kuwaondolea kero na gharama kubwa walizokua wanazitumia kufuata huduma hizi mbali na maeneo yao na hivyo kuboresha Maisha.

 Kutokana na maboresho yaliyofanyika katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya tano, viashiria vikuu vya mwenendo wa huduma za afya ya uzazi, mama na mtoto vimeendelea kuimarika ikiwa ni Pamoja idadi ya wanawake wanaotumia huduma afya ya uzazi kabla ya ujauzito na baada ya kujifungua imeongezeka kutoka asilimia 32 mwaka 2015/16 hadi asilimia 43 mwaka 2020, ongezeko la akinamama kuhudhuria kliniki imeongezeka kutoka asilimia 39 hadi asilimia 81 kufikia mwezi Juni 2020, kiwango cha wajawazito wanaojifungua kwenye vituo vya kutolea huduma kimeongezeka kutoka asilimia 64 mwaka 2015 hadi kufikia asilimia 83 Juni 2020 na hivyo kuvuka lengo la Mpango Mkakati wa Afya ya Uzazi na Mtoto (2016-2020).

 Waziri Ummy amesema hali hii inaashiria utafiti wa hali ya vifo vitokanavyo na uzazi na watoto nchini utakapofanyika mwaka 2021, kiwango cha vifo vitaokanavyo na uzazi kitakuwa chini ya vifo 190 kwa vizazi hai 100,000 ukilinganisha na vifo 556 kwa vizazi hai 100,000 iliyotolewa mwaka 2015/16.

MWISHO

 

 

 

 

 


Jumatano, 12 Agosti 2020

WATOA HUDUMA WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA WELEDI KWA KUZINGATIA MAADILI.

- Hakuna maoni

Mkurugenzi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akiwasalimia wagonjwa waliokuwa wakisubiri huduma katika eneo la wagonjwa wa nje (OPD) katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.

Mkurugenzi wa tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akimjulia hali moja kati ya wagonjwa waliofika kupata huduma za Afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara, pindi alipofanya ziara katika Hospitali hiyo.

Mkurugenzi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe (wa katikati) akiwa pamoja na  Mkurugenzi wa uhakiki ubora wa huduma kutoka Wizara ya Afya Dkt.  Eliakim Eliud wakikagua muongozo  wa utoaji huduma kwa kwa Wauguzi, pindi walipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma za Afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.


Mkurugenzi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akiwa na Wataalamu wa Maabara katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.
 
Mkurugenzi wa tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akiwa na Wataalamu wa Maabara katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara,  wakati alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma za Afya katika Hospitali hiyo.

Mkurugenzi Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe akikagua kadi inayoonesha hali ya idadi ya dawa zilizopo (Bin Card) katika chumba cha kuhifadhia dawa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.

 

WATOA HUDUMA WATAKIWA KUFANYA KAZI KWA WELEDI KWA KUZINGATIA MAADILI.

Na Rayson Mwaisemba, WAMJW- MANYARA

MKURUGENZI wa tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Magembe ametoa wito kwa Watoa huduma za Afya nchini kufanya kazi kwa weledi kwa kuzingatia maadili wakati wa kumhudumia mgonjwa.

Dkt. Grace Magembe ametoa rai hiyo leo, wakati alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma za afya, na ujenzi wa miundombinu katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara.

Dkt. Grace amesema kuwa, kwa kiasi kikubwa Serikali imewekeza kwenye ujenzi wa miundombinu, vifaa tiba na hali ya upatikanaji wa dawa, ikiwa ni sehemu ya maboresho ya utoaji huduma za afya bora kwa mwananchi katika jamii.

"Serikali imewekeza kwenye miundombinu, kwenye vifaa tiba, hali ya upatikanaji wa dawa, lakini Watumishi wanatakiwa wafanye kazi kwa weledi kwa kuzingatia maadili ya kazi zao wakati wa kumuhudumia mgonjwa " alisema Dkt. Grace.

Aliendelea kusema kuwa, Serikali imekuwa ikisisitiza sana, kuhusu maadili mazuri wakati wa utoaji huduma kwa wateja, pindi wanapokuja kupata huduma, hii inajumuhisha mapokezi yake, muda anaotumia kusubiri huduma, muda wa kurejesha majibu yake na kauli zinazotumika wakati wa utoaji huduma.

Hata hivyo, Dkt. Grace ametoa wito kwa viongozi wa hospitali kuwa na mpango madhubuti wa matengenezo ya vifaa tiba ili kuepuka ewezekano wa kusimama kwa baadhi ya huduma, hali itayopelekea wananchi kukosa huduma na upotevu wa mapato.

"Kitu kingine ambacho tunasisitiza katika hospitali ni kuwa na mpango madhubuti wa matengenezo ya vifaa tiba, vifaa ambavyo vimenunuliwa na Serikali ni vya gharama kubwa mnoo, fedha nyingi sana zimetumika, kwahiyo tunasisitiza kuwa na mpango wa matengenezo" alisema

Aidha, Dkt. Grace kwa kiasi kikubwa ameridhishwa na hali ya upatikanaji wa dawa katika maeneo alipofanya ziara, huku akitoa rai kwa Watoa huduma kuhakikisha mgonjwa anapoandikiwa dawa azipate dawa alizoandikiwa lakini pia azipate kwa kwa muda sahihi.

" tumeangalia tena suala la upatikanaji wa dawa, namna dawa inavyohifadhiwa, namna dawa inavyotumika, namna dawa inavyotoka chumba cha kuhifadhia mpaka inapomkuta mhitaji wodini, hii yote tumeifanyia kazi kwasababu tunataka hizo dawa zitumike kulingana na mahitaji yaliyotakiwa" alisema Dkt Grace.

Mbali na hayo, Dkt. Grace amesisitiza agizo la Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi juu ya kufanya kazi kwa juhudi na ushirikiano ili kupunguza vifo vya mama na mtoto, huku akisisitiza kuwa, kuweka mikakati thabiti katika mapambano dhidi ya vita hii, na kuweka wazi kuwa vifo vya mama na mtoto vitakuwa ni kigezo cha kuangalia uwajibikaji na utendaji kazi wa Waganga Wakuu wa Mikoa, Wilaya na Waganga wafawidhi.

"Hatutaki kuona mama wa Kitanzania anakufa wakati analeta kiumbe Duniani, vifo vingi vinasababishwa na sababu ambazo zinaweza kuzuilika, lazima kila Mtumishi afanye kazi, kuanzia Mganga Mkuu wa Mkoa, Mganga Mkuu wa Wilaya, hospitali zote zilizopo ndani ya Mkoa wake, wote wafanye kazi kwa kushirikiana, wake na mkakati, sisi kama Wizara kwa kushirikiana na TAMISEMI tutaendelea kufuatilia tuone kama vifo vinapungua au la na hatua zitachukuliwa " alisema.

Nae, Mkurugenzi wa uhakiki ubora huduma Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Eliakim Eliud amesisitiza kuwa, kuongeza kazi za utoaji huduma kwa kuzingatia ubora wa huduma na kufuata miongozo ya kujikinga wakati wa kuwahudumia wagonjwa.

Kwa upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Manyara Dkt. Damas Kayera ameweka wazi kuwa, Mkoa wa Manyara umeendelea kuwa ma rekodi nzuri juu ya hali ya upatikanaji wa dawa muhimu wa kufikia wastani wa 91%, jambo lililosaidia kupunguza malalamiko kwa wananchi wanaokuja kupata huduma.

"Mkoa unaendelea kuwa na rekodi nzuri ya ongezeko la dawa muhimu, zinazofuatiliwa na Wizara ya afya kwa kila kituo, ambapo kwa kipindi cha nusu mwaka 2020 kumekuwa na wastani wa 91%" amesema.

Mwisho.

Jumamosi, 8 Agosti 2020

WAZIRI UMMY APIGA MARUFUKU WANAFUNZI KUPEWA VIDONGE VYA FOLIC ACID MASHULENI

- Hakuna maoni











Picha mbalimbali zikimuonesha Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akiambatana na Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Loata Ole Sanare, Mkuu wa Mkoa wa Tanga Martine Shigela pamoja viongozi mbalimbali wakipita katika mabanda yaliyopo kwenye maonesho ya Nanenane kanda ya Mashariki yanayofanyika Mkoani Morogoro kuona bidhaa na huduma katika mabanda hayo.


NA EMMANUEL MALEGI-MOROGORO

 Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto amepiga marufuku shule zote nchini kuwapa wasichana dawa aina ya Folic Acid na badala yake shule zimetakiwa kulima kuwajengea uwezo wa kulima maboga na mbogamboga katika bustani za shule.

 Waziri Ummy amesema hayo leo wakati alipokua akihitimisha kilele cha Maonesho ya Nanenane kanda ya Mashariki inayojumuisha Mikoa ya Dar Es Salaam, Pwani, Tanga na Morogoro ambayo yamefanyika mkoani Morogoro.

 Waziri Ummy amesema kuwa ni marufuku kuwapa wanafunzi na wasichana balehe vidonge vya Folic Acid, badala yake fedha hizo zinazotolewa kwa ajili ya dawa hizo zitumike kuanzisha bustani shuleni ili kuzalisha vyakula vinavyotoa madini hayo.

 

“Mbali na kuanzishwa kwa bustani shuleni lakini pia fedha hizo zinaweza kupelekwa kwa vijana ili waanzishe miradi ya bustani za mboga kwa ajili ya kuzalisha mazao yanayozalisha asidi hiyo yakiwemo maboga, matunda na hata karoti badala ya kutoa vidonge kwa wanafunzi”. Amesema Ummy.

 

Kuhusu unywaji wa maziwa mashuleni, Waziri Ummy amesema kuwa atamwandikia barua ya pendekezo Waziri wa Elimu Profesa Joyce Ndalichako ili kuanzia Septemba mosi mwaka huu kila shule iwe na kibanda cha maziwa kwa ajili ya wanafunzi kununua.

 Aidha, Waziri Ummy amesema kuwa  utafiti wa Shirika la Afya Duniani (WHO) unaonesha kwamba kila mtu anatakiwa kunywa nusu lita ya maziwa sawa na lita 180 kwa mwaka, lakini kwa sasa kila mtu anakunywa lita 40 kwa mwaka sawa na vijiko 10 vya chai kwa siku.

 Pia Waziri amesema udumavu kwa watoto wa chini ya miaka mitano umepungua nchini kutoka asilimia 34.4 mwaka 2014 hadi asilimia 31.8 mwaka 2018 licha ya kuwa jitihada zinatakiwa kuendelea kuchukuliwa.

 Pamoja na hayo Waziri Ummy ameupongeza mkoa wa Morogoro kwa kuwa mwenyeji wa maonesho hayo ambayo yamekua chachu ya ukuaji wa kilimo, uvuvi, ufugaji na ujasiriamali nchini na amewataka waratibu wake kutoishia hapo na badala yake ujuzi huo upelekwe vijijini kwa ajili ya kuendeleza sekta hiyo muhimu ambayo kwa kiasi kikubwa inachangia pato la taifa.


Jumatatu, 3 Agosti 2020

WAUGUZI NA WAKUNGA WATAKIWA KUTUMIA UTAALAMU WAO KWA AJILI YA USTAWI WA TAIFA

- Hakuna maoni




Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto-Idara Kuu Afya Edward Mbanga akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi kwenye ukumbi wa Cathedral jijini Dodoma.

Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsai, wazee na Watoto akiongea na viongozi  hao wakati wa kikao cha mafunzo ambapo aliwataka kuweka dhamira na malengo  ya dhati  katika kuboresha maadili katika taaluma ya uuguzi na ukunga.

Muuguzi Mkuu kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI Charles Kadugushi akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi, Jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Idara ya Uuguzi na Ukunga kutoka Wizara ya Afya Bi. Ziana Sellah akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi, Jijini Dodoma.

Msajili wa Baraz a la Uuguzi na Ukunga Agnes Mtawa akiwasilisha mada wakati wa kikao kazi hicho kinachofanyika jijini Dodoma.

Picha ya pamoja ya mgeni rasmi na wasajili wa mabaraza ya kitaaluma yaliyopo chini ya wizara ya afya.

Mgeni rasmi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wauguzi wakuu wa Wilaya mara baada ya ufunguzi.


WAUGUZI NA WAKUNGA WATAKIWA KUTUMIA UTAALAMU WAO KWA AJILI YA USTAWI WA TAIFA

Na.Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Wauguzi na Wakunga nchini wametakiwa kutoa huduma kwa kuzingatia miongozo iliyopo wakati wakitoa huduma kwa weledi ili kufikia malengo na matumaini ya wateja kwa ajili ya ustawi wa Taifa.

Rai hiyo imetolewa leo na Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto – Idara Kuu ya Afya Bw. Edward Mbanga wakati wa ufunguzi wa  kikao kazi  cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi wauguzi wakuu wa wilaya kinachofanyika jijini Dodoma.

Bw. Mbanga amesema  kuwa wauguzi na wakunga ndio watendaji wakuu katika vituo vya afya kwenye ngazi ya jamii hadi Taifa hivyo uwajibikaji mzuri na utawala bora utaboresha utendaji hali itayosaidia kufikia malengo mbalimbali waliyojiwekea katika ngazi zote.

"Viongozi mnatakiwa kuwa wabunifu, wachapa kazi, wenye nidhamu na mfano bora wa kuigwa katika utekelezaji wa majukumu yenu,kwahiyo  ni lazima msimamie utoaji wa huduma uliyo mzuri na wenye heshima na utu.”Alisema

Aidha, Kaimu Katibu Mkuu huyo aliwakumbusha  washiriki hao kuwa, suala la huduma za uuguzi na ukunga ni suala la  ubinadamu zaidi na kuvaa viatu vya wagonjwa wao.

“Hakuna aliyegongwa muhuri wa kuugua  au kuwa mgonjwa akalazwa ,sisi sote ni wagonjwa watarajiwa kwahiyo kama ambavyo sisi tungependa kuuguzwa vizuri, kijibiwa kwa kauli nzuri basi tuhakikishe tunasimamia maadaili ya kazi”.Alisisitiza Mbanga.

Hatahivyo alisema kuwa, Serikali inawahakikishia itaendelea kufanya kazi pamoja na waauguzi  kwa kutoa miongozo thabiti na kuhakikisha upatikanaji wa nyenzo muhimu katika hospitali na vituo vya kutolea huduma ya afya na kuboresha mazingira ya kazi yaliyo bora na salama.

Aliendelea kusema kuwa, hivi karibuni kumekuwa na malalamko  mbalimbali ya kiutendaji  na kitaaluma kutoka kwa wateja  wanaofika kupata huduma za afya na hivyo kuleta taswira mbaya  kwa taaluma yao na kuonyesha hakuna usimamizi mzuri wa utoaji huduma za uuguzi na ukunga.

“Tungependa  wateja wetu watoe sifa  badala ya malalamiko hivyo kikao hiki mje na mipango ya kuondokana na malalamiko kwani taaluma yenu ni zaidi taaluma." alisema.

Hata hivyo, amewakumbusha  viongozi hao kuwa mstari wa mbele kupambana dhidi  ya rushwa na kuhakikisha inatokomezwa katika maeneo yao ya kazi kwani rushwa imekuwa ikilalamikiwa na kuripotiwa katika kada ya afya nchini.

-MWISHO-