Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumatano, 30 Oktoba 2019

SARATANI YA MATITI YAWEZA KUSHIKA NAMBA MOJA

- Hakuna maoni



Mkurugenzi wa huduma za Kinga ya Saratani  katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI) Dkt. Crispian Kahesa

SARATANI YA MATITI YAWEZA KUSHIKA NAMBA MOJA

Na. Catherine Sungura, WAMJW-DSM

Endapo hatua zisipochukuliwa za  saratani ya matiti inaweza kushika namba moja kwa kuwa na idadi  kubwa ya wagonjwa  nchini.

Hayo yanesemwa na Mkurugenzi wa huduma za Kinga ya Saratani  katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI) Dkt. Crispian Kahesa  alipozungumza na waandishi wa habari  kuhusu mwezi wa uhamasishaji , uelimishaji na uchunguzi wa saratani ambao huadhimishwa kila mwezi oktoba kila mwaka.

“Idadi ya saratani ya matiti  inaonekana kuongezeka nchini ambapo hivi sasa wanawake wenye umri  kuanzia miaka 20 na kuendelea nao wanagundulika  kuugua ugonjwa huu”. Alisema Dkt. Kahesa.

Alisema kuwa endapo hatua zisipochukuliwa  saratani hiyo itazidi kuwa tishio zaidi na kwamba  idadi kubwa ya wagonjwa wanaofika  hospitalini hapo wanatoka katika maeneo ya mjini ambapo mkoa wa Dar es salaam unaonekana kuongoza.

“Tathimini  ya miaka 10 iliyopita saratani hii ilikua inashika nafasi ya tano ,hivi sasa ni ya pili kwa kuwa na idadi kubwa ya wagonjwa,zamani tulikua tunawaona wagonjwa kuanzia miaka 55 ukashuka hadi miaka 50 na sasa tunaona hadi wenye umri wa miaka 20”.

Dkt. Kahesa alisema kuwa kwa mwaka huu pekee wameweza kuona wanawake 1443 ambapo kati ya 342 wamekutwa na uvimbe 170 walikuwa na dalili za awali za saratani.

Kwa upande wa saratani kwa wanaume Dkt. Kahesa alisema kuwa saratani hiyo huathiri asilimia moja kwa wanaume hata hivyo kwa upande wao ni hatari  zaidi na endapo isipogundulika huweza kuathiri mapafu yao kwa haraka.

“Saratani hii huathiri wanawake zaidi  kuliko wanaume kwa asilimia 99 na wanaume ni asilimia 1 tu,ambapo dalili kwa wanaume  ni tofauti  kidogo na wanawake,hivyo kwa mwanaume ni rahisi kugundua kuliko mwanamke kwa kuwa kifua chake kina mafuta mengi.

Aliongeza kuwa kati ya wanawake 170 waliofanyiwa vipimo  zaidi ya 68 waligundulika na vivimbe ambavyo ni ugonjwa wa saratani.

Hapa nchini saratani ya shingo ya kizazi inaongoza ikifuatiwa  na saratani ya matiti,saratani  ya njia ya chakula,saratani ya tezi dume na saratani  nyingine ni zile zinazoathiri  mfumo wa kinga.

Mwisho

Jumanne, 29 Oktoba 2019

MAAMBUKIZI YA VVU NCHINI YASHUKA KWA ASILIMIA 2.3

- Hakuna maoni
 















Na WAMJW- DSM

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu amesema kuwa maambukizi ya VVU yamepungua kutoka asilimia 7 mwaka 2003/4 hadi asilimia 4.7 mwaka 2016/17 .

Waziri Ummy ameyasema hayo leo wakati wa mkutano wa kujadili maendeleo ya utekelezaji wa sera ya pamoja ya ushirikiano na Serikali ya Marekani kupitia PEPFAR cop 19 kuhusiana na VVU na UKIMWI uliofanyika jijini Dar Es Salaam.

“Kuanzia huduma za UKIMWI zianze kutolewa nchini tumeshuhudia mafanikio makubwa kwa upande wa kupunguza maambukizi kutoka asilimia 7 mwaka 2003/4 hadi asilimia 4.7 mwaka 2016/17" alisema Waziri Ummy.

Aliendelea kusema  kuwa Serikali imefanikiwa kutoa huduma za utambuzi na matibabu na sasa dhana ya kwamba UKIMWI ni ugonjwa wa kifo imeisha na kuwa ni ugonjwa unaoweza kudhibitiwa

Aidha,Waziri Ummy amesema kuwa Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo ikiwemo PEPFAR inaendelea kupanga mikakati mbalimbali ya kudhibiti maambukizi ya UKIMWI, kutoa huduma na matibabu kwa watu wanaoishi na virusi.

Mbali  na hayo Waziri Ummy amedai kuwa Serikali imefanikiwa kutoa huduma za utambuzi na matibabu, huku akisisitiza kuwa dhana ya kwamba UKIMWI ni ugonjwa wa kifo imeisha baina ya wananchi

Hata hivyo, Waziri  Ummy amesema, kufikia mwezi Septemba mwaka 2019 idadi ya watu waliopima na kujua afya zao imefikia asilimia 77.2 na kati yao asilimia 98 wanaendelea na huduma za VVU pamoja na matumizi ya ARV.

Hata hivyo Waziri Ummy hakusita kulishukuru shirika la PEPFAR kwa kuendelea kuunga mkono jitihada za Serikali katika mapambano dhidi ya VVU na UKIMWI kwa kudhamini, kuweka malengo na kutoa miongozo katika huduma za VVU nchini.

Kwa upande wake Balozi wa Marekani nchini Dr. Inmi Patterson amesema Serikali ya Marekani itaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika mapambano dhidi ugonjwa wa UKIMWI na ameipongeza Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa jitihada kubwa inazofanya kwa kushirikiana na wadau mbalimbali katika kudhibiti maambukizi na kutoa huduma bora za VVU kwa watu waliogundulika na maambukizi.

Mkutano huo ulijumuisha wadau mbalimbali akiwemo mwakilishi wa Shirika la Afya duniani nchini Tanzania Dkt. Tigest Ketsela pamoja na wataalam kutoka Wizara ya Afya wakiongozwa na Mkurugenzi wa kinga Dkt. Leonard Subi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, Tume ya kudhibiti na kupambana na UKIMWI (TACAIDS) pamoja na Shirika la PEPFAR Tanzania.

Mwisho.

Jumanne, 22 Oktoba 2019

HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA MARA KUKAMILIKA 2020

- Hakuna maoni

Jengo la Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara.




Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Zainab Chaula (kulia) akizungumza na watendaji wake alipotembelea ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara.






Na.WAMJW
Hospitali ya rufaa ya mkoa wa mara inatarajiwa kukamilika  ujenzi wake na kuanza kutoa huduma za afya mwezi agosti 2020

Hayo yamesemwa na na Katibu Mkuu
Katibu Mkuu Dkt. Zainab Chaula wakati  akihitimisha ziara yake mkoani Mara kwa kutembelea ujenzi wa Hospitali hiyo (Kwanga) na kuona maendeleo ya ujenzi ambao ulikua ukisuasua kutokana na sababu mbalimbali.

Dkt. Chaula alisema kuwa  wametoa zaidi ya bilioni 4 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi huo hivyo na kumtaka mkandarasi mkuu Shirika la nyumba nchini (NHC) kuhakikisha mradi huo unakamilika mwezi Agosti mwaka 2020.

"Tunahitaji huduma zianze kutolewa mapema kwani Hospitali hiyo itakua ni mkombozi kwa wananchi wa Musoma na maeneo jirani wanaopata rufaa za kwenda Bugando".Alisema Dkt. Chaula

Katika ziara hiyo.Dkt. Chaula alitembelea Hospitali Teule ya Rufaa ya Mkoa wa Musoma na kuona hali halisi ya utoaji wa huduma za afya Hospitalini hapo kisha kuongea na watumishi.

Aidha, Dkt. Chaula amehitimisha ziara yake mkoani Mara kwa kutembelea Hospitali ya Wilaya ya Butiama na kuridhishwa na majengo mapya ya huduma za mama na mtoto na kisha kutembelea nyumbani kwa Baba wa Taifa na kuweka shada kwenye kaburi lake.

Jumamosi, 19 Oktoba 2019

KATIBU MKUU DKT. CHAULA AHITIMISHA ZIARA YAKE MKOANI MWANZA

- Hakuna maoni











Picha mbalimbali zikimuonesha Katibu Mkuu Dkt. Zainab Chaula alipotembelea Hospitali ya Rufaa ya Sekou Toure kukagua ujenzi wa jengo la ghorofa litakalotoa huduma mbalimbali kisha kutembelea baadhi ya maeneo ya utoaji wa huduma za afya, kuongea na wagonjwa waliofika Hospitalini hapo ili kupata huduma lengo likiwa ni kusikiliza kero zao na kuzitafutia ufumbuzi kisha amehitisha kwa kuongea na watumishi na kutatua baadhi ya kero alizoziona.

Baada ya hapo Dkt. Chaula ametembelea Hospitali ya Rufaa ya Bugando na kuzungumza na Menejimenti ya Hospitali hiyo na kuridhishwa na mafanikio yaliyopatikana ndani ya kipindi cha miaka miwili na kuwezesha hospitali kutoa huduma bora na kuongezeka kwa ukusanyaji wa mapato.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Bugando Prof. Abel Makubi amepongezwa kutokana na ubunifu wake uliowezesha hospitali kuboresha miundombinu na mapato ya ndani.

Dkt. Chaula pamoja na timu aliyoambatana nayo akiwemo Mkurugenzi wa Tiba Dkt. Grace Maghembe imeishauri Hospitali ya Bugando kuendelea kuzijengea hospitali za Mikoa na Wilaya katika kuzalisha maji tiba kwa wagonjwa. Asilimia 50 ya infusion zinazotumika Bugando zinazalishwa na hospitali.

Prof. Kabudi ameishukuru serikali kupitia wizara ya afya  kwa kusaidia kuanzishwa huduma za wagonjwa wa saratani kupitia ujenzi wa jengo la huduma hizo. Pia aliendelea kushukuru kwa hospitali hiyo kuingizwa kwenye mpango wa kupata  mashine ya MRI.

Dkt. Chaula na timu nzima anayoongozana nayo imeondoka jijini Mwanza kuelekea Chato na Geita kuendelea na ziara yake katika mikoa ya kanda ya ziwa.

Alhamisi, 17 Oktoba 2019

DKT. CHAULA ATAKA MAHUSIANO BORA KWA WATUMISHI WA SEKTA YA AFYA

- Hakuna maoni















Na WAJMW-MWANZA

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. Zainab Chaula amezidi kusisitiza mahusiano bora baina ya watumishi walio katika sekta ya afya katika maeneo yao ya kazi na kuwataka kuongeza mapato ili yaweze kuendesha Hospitali na vituo vya afya pamoja na kuboresha hali za watumishi kwa ujumla.

Dkt. Chaula amesema hayo wakati akiendelea na ziara yake katika mikoa ya kanda ya ziwa baada ya leo kutembelea Hospitali ya Wilaya ya Misungwi Jijini Mwanza na kuona hali ya ujenzi wa jengo la huduma za uzazi na kuonekana kuridhishwa na ujenzi huo kisha kuongea na watumishi.

Katibu Mkuu huyo amesema lengo la kutembelea maeneo ya utoaji wa huduma za afya kanda ya ziwa ni pamoja na kuona maendeleo ya utoaji huduma na kuongea na watumishi ili kubaini maendeleo na kupata changamoto zinazowakabili na kuona namna gani ya kuzitatua.

Pamoja na yote yaliyozungumzwa Dkt. Chaula amewaomba watumishi hao kupendana na kufanya kazi kwa moyo ili kuwahudumia wagonjwa wanaofika kupata huduma huku akiwataka kuongeza mapato na kuweza kujilipa motisha kutokana na ufanyaji kazi wao.

 Kabla ya hapo Dkt. Chaula alitembelea kituo cha afya cha Buzuruga na kushirikiana na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza John Mongella katika uzinduzi wa kampeni ya kitaifa ya chanjo za Surua na Ribella kwa watoto wadogo nchini iliyozinduliwa kitaifa Mkoani Morogoro na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu.

Badae Dkt. Chaula akiongozana na Wakurugenzi na viongozi waandamizi kutoka wizara ya afya na ofisi ya Rais TAMISEMI alitembelea ujenzi wa Hospitali mpya ya Wilaya ya Ilemela na kituo cha matibabu ya magonjwa ya hatari na milipuko (Isolation Highly Infectious Unit) cha Buswelu.

MWISHO



Jumanne, 15 Oktoba 2019

MAAMBUKIZI YA VVU YAZIDI KUPUNGUA NCHINI

- Hakuna maoni

Katibu Mkuu Dkt. Zainab Chaula akielezea jambo mbele ya kamati ya bunge ya kudumu ya masuala ya UKIMWI wakati akitoa taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya mpango ya taifa wa kudhibiti UKIMWI katika kipindi cha mwaka 2018/2019 katika ukumbi mdogo wa Bunge jijini Dodoma.


Baadhi ya Wabunge walio katika kamati ya bunge ya kudumu ya masuala ya UKIMWI wakifuatilia uwasilishwaji wa taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya mpango ya taifa wa kudhibiti UKIMWI katika kipindi cha mwaka 2018/2019 katika ukumbi mdogo wa Bunge jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya bunge ya masuala ya UKIMWI Mhe. Oscar Mukasa (kulia) akifafanua jambo wakati taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya mpango ya taifa wa kudhibiti UKIMWI katika kipindi cha mwaka 2018/2019 iliyowasilishwa na Wizara na Afya katika ukumbi mdogo wa Bunge jijini Dodoma.


Baadhi ya Wakurugenzi kutoka idara mbalimbali za Wizara ya Afya wakifuatilia uwasilishwaji wa  taarifa ya utekelezaji wa majukumu ya mpango ya taifa wa kudhibiti UKIMWI katika kipindi cha mwaka 2018/2019 katika ukumbi mdogo wa Bunge jijini Dodoma.

Alhamisi, 3 Oktoba 2019

TAARIFA KUHUSU MWENENDO WA MAGONJWA YA MILIPUKO NCHINI KWA MWEZI SEPTEMBA NA HATUA ZINAZOCHUKULIWA NA SERIKALI KUZUIA NA KUDHIBITI MAGONJWA

- Hakuna maoni


QQ.jpg

Wizara Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imekuwa ikitoa taarifa kwa wananchi mara kwa mara kuhusiana na mwenendo wa magonjwa ikiwemo magonjwa ya milipuko (epidemic diseases) nchini na hatua zinazochukuliwa kuzuia na kudhibiti magonjwa haya. 


Magonjwa yanayofuatiliwa kwa karibu na kutolewa taarifa mara moja pindi yakitokea ni, kumi na nne (14) ambayo ni pamoja na Kipindupindu, Polio, Kimeta, Kuhara Damu, Homa ya Uti wa Mgongo, Mafua makali ya ndege, Surua, Pepopunda ya watoto wachanga, Kichaa cha Mbwa, Ndui, Magonjwa yanayosababishwa na Virusi na Homa yanayosababisha damu kuvuja (Ebola, Marburg, RVF, Homa ya Dengue, Chikungunya), Macho mekundu, Tauni, na Homa ya Virusi ya Manjano. 


Utoaji wa taarifa za magonjwa haya zimerahisishwa, ambapo vituo vyote vya kutoa huduma za Afya nchini kuanzia ngazi ya chini hutoa taarifa hizi kwa kupitia mfumo maalum kwa njia ya simu (Integrated Disease Surveillance and Response - IDSR). Hii hupelekea taarifa zote muhimu kuhusu magonjwa kupatikana kwa haraka na hatua kuchukulia mapema na wizara ili kudhibiti magonjwa haya. 


Kwa kipindi cha mwezi Septemba 2019, Wizara imeendelea kufuatilia magonjwa haya na matukio hatarishi kwa afya, kutoka kwenye mikoa yote nchini. Katika mwezi Septemba, ugonjwa wa Dengue na Surua tu ndio magonjwa ya milipuko yaliyotokea hapa nchini. 


Mwenendo wa Homa ya Dengue nchini. 

Kwa Kipindi cha mwezi Septemba 2019, jumla ya wagonjwa 10 walithibishwa kuwa na Homa ya Dengue na hakukuwa na kifo. Wagonjwa hawa walitolewa taarifa kutoka mikoa 2 ambayo ni Dar es salaam – wagonjwa 4 (Hospitali ya Taifa Muhimbili - 4) na Tanga – wagonjwa 6 (Tanga jiji - 6).


 Ugonjwa huu umeendelea kudhibitiwa kwa kiasi kikubwa nchini na umeendelea kupungua mwezi hadi mwezi. Takwimu za miezi mitatu (Julai, Agosti na Septemba, 2019) zimeonyesha kupungua kwa ugonjwa huu kwa kiasi kikubwa ambapo mwezi Julai 2019 kulikuwa na wagonjwa waliothibishwa 732, mwezi Agosti wagonjwa 92 na mwezi Septemba wagonjwa - 10. 


 Aidha tangu mlipuko huu uanze mwezi Januari 2019 hadi kufikia tarehe 30 Septemba, 2019 kumekuwa na jumla ya wagonjwa waliohisiwa kuwa na Dengue 14,369 na kati yao waliothibishwa ni 6,785 na vifo 13 (Dar-6259, Tanga-365, Pwani-115, Morogoro-22, Lindi-8, Arusha-5, Singida-3, Dodoma-3, Ruvuma-2, Kagera-2 na Kilimanjaro-1). 


Ili kukabiliana na magonjwa yaenezwayo na wadudu dhurifu wakiwemo mbu, Wizara ilizindua mpango mkakati wa kukabiliana na wadudu dhurifu na mbu (National Vector control strategy 2019 - 2023) tarehe 27 Julai 2019, Dar es Salaam. Uzinduzi huu uliambatana na uzinduzi wa kitaifa wa zoezi la upuliziaji wa dawa kupambana na mbu wapevu na unyunyiziaji wa dawa za kuua viluwiluwi wa mbu waenezao magonjwa kama vile Malaria, Dengue na nk,. Dawa za kuangamiza wadudu zilinunuliwa pamoja na mashine kubwa (4) za kupulizia dawa (Fogging Machine) ambazo zilisambazwa katika mikoa iliyoathirika na ugonjwa wa Dengue yaani Dar es Salaam, Tanga pamoja na Dodoma. Wizara imeshaagiza mashine nyingine 4 ili kuweka mkakati endelevu wa zoezi hili. 


Mikoa hii pia (Dar es salaam, Dodoma, Tanga) ilishafanya uzinduzi wa Mkakati wa Kudhibiti Mbu na Wadudu wadhurifu pamoja na kuendesha zoezi la kuangamiza mbu. Hatua hii imesaidia kupunguza maambukizi ya ugonjwa wa Dengue nchini kama inavyoonyeshwa katika takwimu. 


Aidha, zoezi hili la uzinduzi linaendelea kufanyika katika Mikoa yote ili kutokomeza magonjwa yaenezwayo na wadudu hao. Elimu endelevu pia inaendelea kutolewa kwa wananchi juu ya namna kujikinga na kudhibiti ugonjwa huu 


Mwenendo wa Ugonjwa wa Kipindupindu nchini. 

Ugonjwa wa Kipindupindu umedhibitiwa, na kwa sasa HATUNA KABISA mgonjwa wa Kipindupindu nchini. Mara ya mwisho kupata mgonjwa wa Kipindupindu nchini ilikuwa tarehe 14 mwezi Julai 2019. 


Kwa kipindi cha kuanzia tarehe 1 Januari hadi Julai 2019, kulikuwa na jumla ya wagonjwa 424 na vifo 8 vya ugonjwa wa Kipindupindu. Wizara inaendelea kuchukua hatua za kudhibiti ugonjwa huu, ikiwa ni pamoja kufuatilia hatua zinazochukuliwa za kuzuia ugonjwa huu na timu ya Mkoa na Halmashauri ambazo ni pamoja na; Kutoa elimu ya afya kwa wananchi ya namna kujikinga kupata ugonjwa huu, Ufuatiliaji wa usafi wa mazingira. 


Wizara inakamilisha Mpango Mkakati wa Kipindupindu wa mwaka 2019 hadi 2023 ambao utekelezaji wake utajikita katika maeneo yanayotoa wagonjwa mara kwa mara (Hotspot areas) ambayo ni Dar es Salaam (Halmashauri zote), Ngorongoro (Arusha), Simanjiro (Manyara), Handeni na Mkinga (Tanga), Kilwa (Lindi), Ulanga (Morogoro), Mbarali na Chunya (Mbeya), Songwe, Sumbawanga DC (Rukwa), Mpanda (Katavi), Nyasa (Ruvuma) na Iringa DC (Iringa). 


Mpango huu, unalenga kutokomeza Kipindupindu kabisa. Katika mpango huu maeneo yalijikita ni pamoja na: Uratibu na ushirikishwaji wa wadau katika ngazi zote katika kudhibiti ugonjwa, kuimarisha ufuatiliaji na upimaji wa wagonjwa, Kuimarisha utoaji wa matibabu sahihi na mapema kwa wagonjwa, ushirikishwaji wa jamii katika kudhibiti na ugonjwa, kuweka mazingira ya kuwepo kwa maji safi na salama na masuala ya matumizi ya vyoo na vilevile kuimarisha utoaji wa chanjo kwa maeneo sugu na vigezo vitakavyotumika. 


Wizara imeendelea pia na utekelezaji wa Kampeni ya Taifa ya Usafi wa Mazingira yenye kaulimbiu isemayo “USICHUKULIE POA NYUMBA NI CHOO”, ikiwa ni moja ya mikakati ya kutokomeza Kipindupindu na magonjwa ya kuhara. Kampeni hii ambayo ipo katika awamu ya pili, ilizinduliwa rasmi Disemba, 2017 na Mhe. Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. 


Uanzishwaji wa Kampeni hii ni sehemu ya jitihada za serikali kujielekeza katika kutekeleza lengo namba 6.2 la Malengo ya Maendeleo Endelevu (Sustainable Development Goals) pamoja na lengo namba 3 linahusu kuboresha Afya. Katika kipindi cha miaka mitatu ya utekelezaji (2016-2019), jumla ya kaya 2,464,225 zimejenga au kuboresha vyoo kufikia kiwango cha ubora kati ya lengo la kaya 3,360,000. Hii ni sawa na asilimia 73.3. Kwa upande wa taasisi, shule 1,670 kati ya lengo la shule 2,520 zimejenga vyoo bora kwa kuzingatia uwiano. 


Kwa ujumla kaya zenye vyoo bora katika ngazi ya kaya zimeongezeka kutoka asilimia 46 Julai, 2016 hadi asilimia 57.2 Juni, 2019, na kaya zisizokuwa na vyoo zimepungua kutoka asilimia 7.5 hadi asilimia 2.5 katika kipindi hicho. 



Mwenendo wa Ugonjwa wa Surua nchni. 


Katika kipindi cha mwezi Septemba 2019, mlipuko wa ugonjwa Surua ulitokea katika kitongoji cha Kashasha, Kakoma na kijiji cha Kibare wilayani Kyerwa mkoa wa Kagera. Jumla ya wagonjwa 17 walipatikana na ugonjwa wa surua ambapo kati yao; wagonjwa saba walithibitishwa kwa kipimo cha maabara. Mgonjwa wa mwisho kupatwa na dalili za surua katika eneo la Kibare ilikuwa tarehe 14/09/2019. 


Kwa takribani wiki mbili sasa hakuna mgonjwa mwingine aliyepatikana. Wagonjwa wote wamepona na elimu ya jinsi ya kujikinga na ugonjwa wa surua imetolewa na pia kuhamasisha kuwaleta watoto katika kampeni ya kitaifa shirikishi ya chanjo ya surua na rubella, watoto wote chini ya miaka mitano. 


Katika ufuatiliaji wa ugonjwa surua nchini wagonjwa wenye dalili za homa na vipele hufuatiliwa na kuchukuliwa sampuli kupima kubaini kama wana ugonjwa wa surua. Kwa kipindi cha mwezi Septemba 2019, jumla ya sampuli 222 za wagonjwa waliokuwa na dalili ya homa na vipele zilipokelewa na kufangashwa na kuwasishwa maabara ya Taifa kutoka kwenye mikoa 23 ya Tanzania bara. 



Mwenendo wa Ugonjwa wa Polio nchini. 


Hadi sasa hakuna mgonjwa wa Polio aliyethibika hapa nchini tangu mwaka 1996. Hii inatokana na jitihada kubwa za Serikali katika kutoa chanjo na kufuatilia dalili za wagonjwa wenye ugonjwa huu na pia kwa kununua chanjo za Polio ambazo zimeweza kuwafikia watoto wote chini ya miaka mitano (5) kwa zaidi ya asilimia 90%. 


Katika ufuatiliaji wa ugonjwa huu, wagonjwa wote wa dalili za kupooza ghafla (Acute Flaccid Paralysis - AFP) hufuatiliwa na sampuli kuchukuliwa na kupimwa kujua kama wana ugonjwa wa Polio. Kwa mwezi Septemba 2019, jumla ya sampuli 63 za AFP 63 zilifungashwa na kupelekwa maabara kwa ajili ya vipimo. Aidha katika ufuatiliaji wa virusi vya polio katika mazingira, ambapo kirusi hiki pia hukaa kwa muda nao unaendelea na hadi sasa kirusi hiki kimeonekana kuwa hakipo katika mazingira yetu. Ufuatiliaji wa mara kwa mara unaendelea. . 


Katika mpango wa kutokomeza vifo na ulemavu kutokana na magonjwa yanayozuilika kwa chanjo. Wizara ya Afya kupitia Mpango wa Taifa wa Chanjo na kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais - TAMISEMI, itaendesha kampeni ya chanjo dhidi ya Magonjwa ya Surua, Rubella na Polio mnamo tarehe 17 hadi 21 mwezi Octoba 2019. Kampeni hii itafanyika nchi nzima kwa watoto wote lengwa walio na umri wa chini ya miaka mitano. Nawasihi wananchi wote washiriki ili Serikali ifikie lengo la kampeni hii. 


Mwenendo wa Ugonjwa wa Ebola unaoendelea kuripotiwa nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) 


Wizara imekuwa ikifuatilia kwa karibu mwenendo wa ugonjwa wa Ebola unaoendelea kuripotiwa nchini DRC na kuchukua hatua za tahadhari za kuzuia na kukabiliana na ugonjwa huu hususani kwa kuwa kwa sasa ugonjwa huu unaendelea kusambaa na kuingia kusini mwa DRC. Takwimu zinaonyesha kuwa hadi kufikia tarehe 30 Septemba 2019, jumla ya wagonjwa 3,194 walithibitishwa kuwa na ugonjwa huu, na vifo 2133 (CFR 66.8%). Kutokana na ukaribu wa nchi hii na Tanzania, Wizara imeendelea kuchukua hatua za utayari kuzuia na kujiandaa kukabiliana na ugonjwa huu 


Hatua za utayari na kujiandaa kukabiliana na ugonjwa huu nchini ni pamoja na kuimarisha uchunguzi wa Wasafiri kwenye mipaka yetu yote. Kuimarisha utambuzi katika ngazi ya vituo vya kutolea huduma za Afya; Kuhakikisha uwepo vya Vifaa Kinga hususani kwa watumishi wa Afya; Kuimarisha utambuzi wa Ugonjwa na kuendelea kutoa Elimu kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga ugonjwa huu. 


Wizara inayo namba ambayo hutumika bila malipo na wananchi kutoa taarifa za kuwepo kwa tetesi za ugonjwa huu ambazo ni 0800110124 au 0800110125. Kuanzia 2018 hadi sasa, tetesi 28 za wagonjwa wanaohisiwa kuwa na Ebola (washukiwa 2 kwa mwezi Septemba), zimekwisha kutolewa taarifa na uchunguzi kufanyika kwa ukamilifu na kuthibitisha wagonjwa hawa hawakuwa na Ebola, na taarifa zake kupelekwa pia katika Shirika la Afya Duniani. Aidha Wizara imeendelea kufanya pia mazoezi ya kujinoa na kijipima utayari wa kukabiliana na ugonjwa huu (Simulation Exercises) katika mikoa ya Dar es Salaam, Kagera, Kigoma, Kilimanjaro na Arusha. 



NAPENDA KUSISITIZA KUWA HADI SASA HAKUNA MGONJWA ALIYETHIBITISHWA KUWA NA UGONJWA WA EBOLA HAPA NCHINI. WIZARA INAWASIHI WANANCHI KUTOKUWA NA HOFU NA KUPUUZA TAARIFA ZINAZOTOLEWA KILA KUKICHA NA BAADHI YA VYOMBO VYA HABARI NA MITANDAO YA KIJAMII. 



Katika kudhibiti ugonjwa wa Ebola na magonjwa mengine ya milipuko yenye madhara makubwa duniani, nchi yetu kila wakati imekuwa mstari wa mbele ikiwa ni pamoja na kusimamia kwa ukamilifu na kutekeleza Kanuni za Kimataifa za Afya (International Health Regulation - IHR 2005). Mnamo mwaka 2016, Tanzania ilikuwa nchi ya kwanza duniani kuweza kukubali bila kipingamizi kuleta wataalam duniani kuja kupima utayari wa nchi yetu katika kukabiliana na magonjwa haya hatarishi (Joint external evaluation). Hatua hii kubwa na ya uwazi ilifanywa kwa mara ya kwanza Duniani, kama moja ya njia ya kuhakikisha nchi wanachama wa Shirika la Afya Duniani, wanatekeleza Kanuni hizi za Kimataifa (IHR 2005). Aidha nchi nyingine zenye uwezo mkubwa duniani zilisita kufanyiwa tathmini hadi miaka miwili baadae, na nyingine hadi sasa hazijafanya zoezi hili. Hivyo basi, taarifa zinazoenea kuelezea kuhusu Tanzania kutokuweka wazi taarifa za magonjwa hususan uwepo wa ugonjwa wa Ebola nchini, si za kweli na hivyo ziendelee kupuuzwa. Taratibu za utoaji wa taarifa za magonjwa ya milipuko zinajulikana na ninatoa rai kwa sote tuzingatie sheria na taratibu za nchi husika na za kimataifa. 


Ikumbukwe kuwa, ugonjwa wa Ebola ambao unaweza kusambaa kwa haraka, na ambao madhara yake ni makubwa na yanajulikana duniani kote, kamwe hauwezi kufichwa na nchi yetu. Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inatambua madhara makubwa ya kuficha ugonjwa kama huu kwa wananchi. Narudia tena na kuwataka wananchi kutulia na kupuuza taarifa zisizo rasmi kutoka kwenye baadhi ya vyombo vya habari na mitandao ya kijamii, maana HAKUNA UGONJWA WA EBOLA NCHINI TANZANIA. Inaonekana kuna njama ovu za kueneza taarifa hasi dhidi ya nchi yetu. Ninaendelea kuwasihi Wananchi kuwa watulivu na kushikamana kwa pamoja katika kuzuia ugonjwa huu usiiingie nchini. 


Aidha, Serikali inapenda kuwahakikishia Mataifa yote kuwa nchi yetu ni SALAMA na HATUNA UGONJWA WA EBOLA. Nirudie tena kusisitiza kuwa Serikali itaendelea kushirikiana na nchi na mashirika mbalimbali ya kimataifa ikiwemo Shirika la Afya Duniani katika kujenga utayari wa kukabiliana na tishio la ugonjwa wa Ebola. Na endapo kutatokea mtu atakaethibishwa kuwa na ugonjwa wa Ebola nchini tutaendelea kuzingatia miongozo na taratibu za kimataifa ikiwemo kutoa Taarifa WHO kwa mujibu wa Kanuni za Kimataifa za udhibiti wa magonjwa hatari ya kuambukiza (IHR 2005). 


Kipaumbele cha Wizara kwa sasa ni kuendelea kuimarisha utayari wa kukabiliana na ugonjwa huu usiingie nchini na endapo kutatokea kisa cha ugonjwa huu nchini tuweze kukabiliana nao na kuudhibiti mara moja. 


Asanteni sana