Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumanne, 6 Desemba 2022

TANZANIA NA COMORO KUIMARISHA ZAIDI USHIRIKIANO KWENYE SEKTA YA AFYA

Katibu Mkuu Wizara ya Afya Prof. Abel Makubi (kulia) akimkabidhi zawadi Balozi wa Comoro Nchini Tanzania Dkt. Ahamada El Badaoui  mara baada ya kufanya kikao kilicholenga  kuboresha ushirikiano katika maendeleo ya Sekta ya Afya baina ya Tanzania na Comoro

Katibu Mkuu Wizara ya Afya Prof. Abel Makubi

Picha ya pamoja ya Katibu Mkuu Wizara ya Afya Prof. Abel Makubi (aliye mstari wa mbele kushoto), Watumishi wa Wizara pamoja na wageni kutoka Ubalozi wa Comoro wakiongozwa na Balozi wa Comoro nchini Tanzania Dkt. Ahamada El Badaoui (mwenye suti rangi ya bluu)  mara baada ya kufanya kikao kilicholenga  kuboresha ushirikiano katika maendeleo ya Sekta ya Afya baina ya Tanzania na Comoro.


Na WAF – Dar Es Salaam 

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Prof. Abel Makubi leo amekutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Comoro nchini Tanzania Dkt. Ahamada El Badaoui kujadili namna ambavyo nchini hizo zinaweza kushirikiana katika maendeleo ya Sekta ya Afya. 

Katika mazungumzo yao viongozi hao wamekubaliana kuendelea kushirikiana kuboresha uhusiano wa kutoa tiba kwa wagonjwa wanaotoka Comoro na kuja kupata matibabu ya Kibingwa katika Hospitali za Taifa na kanda. 

Prof. Makubi amesema Serikali ya Comoro imepanga kufanya maonesho ya kimataifa ya sekta ya afya ambayo yatashirikisha Tanzania na nchi nyingine yatayayofanyika januari mwakani na kwamba hiyo itakua fursa kwa watoa huduma za afya ikiwemo hospitali na kampuni za dawa na wananchi kwa ujumla kujumuika kwa pamoja katika maonesho ili kutangaza shughuli zinazofanywa na sekta ya afya nchini. 

“Hii ni fursa nzuri nawaomba watanzania wajiandae ili kuweza kuonesha ni huduma zipi tunatoa na azma yetu kama Serikali kuifanya Tanzania iwe chombo cha kutoa utaalamu na vilevile kutoa huduma kwa maana ya Medical Tourism, tunataka kuhakikisha kwamba vituo vyetu vinakua na huduma iliyobora ambayo itavutia wagonjwa kutoka nchi zingine” amesema Prof. Makubi 

Aidha amesema taasisi za serikali na sekta binafsi zitaendelea kushirikiana na Comoro kwa kuwapatia mafunzo wataalamu mbalimbali ambao wanapenda kuja kusomea hapa nchini. 

Kwa upande wake Balozi wa Comoro nchini Dkt. Ahamada El Badaoui ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kukubali kuendelea kushirikiana na nchi hiyo na kueleza kuwa uhusiano kati ya Tanzania na Comoro ni wa muda mrefu na wenye manufaa. Amefafanua kuwa Comoro imekua pia ikishirikiana na hata Hospitali binafsi zilizopo nchini na yote hiyo imetokana na kuwa na mahusiano mazuri baina ya pande zote mbili.

Jumatano, 17 Agosti 2022

WAZIRI UMMY MWALIMU AWAKARIBISHA WAWEKEZAJI KUTOKA INDIA NA FALME ZA KIARABU KUWEKEZA KWENYE SEKTA YA AFYA NCHINI

- Hakuna maoni
Na Englibert Kayombo WAF, Dar Es Salaam. Waziri wa Afya Mhe.Ummy Mwalimu leo amekutana na kufanya mazungumzo na Wawekezaji kutoka India pamoja na Umoja wa Falme za Kiarabu (United Arab Emirates) kujadili na kuwakaribisha kwenye fursa za uwekezaji katika Sekta ya Afya nchini. Waziri Ummy amepongeza nchi hizo kwa kuonyesha nia ya kutaka kuwekeza kwenye Sekta ya Afya na kuongeza ushirikiano katika kusaidia maendeleo ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuboresha ubora wa huduma za afya. “Tumekuwa tukishirikiana na India kwenye mambo mengi kuhusu Sekta ya Afya, tuna madaktari wetu watanzania wanasoma masuala ya udaktari huko India, tuna wawekezaji kutoka India hapa nchini, ushirikiano huu ni mzuri na una tija kwa Serikali na Watanzania”. Amesema Waziri Ummy na kuipongeza Umoja wa Falme za Umoja wa Kiarabu kwa kuvutiwa kuwekeza kwenye Sekta ya Afya hapa nchini. Waziri Ummy amesema kuwa kipaumbele cha Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwenye Sekta ya Afya ni ubora wa huduma, hivyo kuwakaribisha wawekezaji hao kuwekeza hapa nchini ili Watanzania na raia kutoka nchi Jirani waweze kupata huduma za kibingwa za matibabu. Aidha, Waziri Ummy ametoa wito kwa wawekezaji hao kuweka mkazo zaidi katika fursa za uwekezaji kwenye upande wa kuboresha mifumo ya TEHAMA kwenye Sekta ya Afya nchini huku akisema kuwa bado kuna changamoto nyingi kwenye mifumo ya TEHAMA ndani ya Sekta ya Afya. Bw. Lav Aggarwal ambaye ni Kiongozi wa wawekezaji kutoka India, amesema kuwa lengo kufika nchini ni kuboresha zaidi ushirikiano baina ya nchi husika na wanatarajia kuendela kushirikiana na Tanzania katika kuboresha zaidi upatikanaji wa huduma bora za matibabu hapa nchini. Naye Balozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu hapa nchini Balozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu hapa nchini Bw. Khalifa Al Marzooqi amesema ziara ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mhe. Samia Suluhu Hassan katika Umoja wa Falme za Kiarabu imefungua zaidi milango ya uwekezaji kutoka Falme za Kiarabu na kufika hapa kuja kuona nini cha kuwekeza kwenye Sekta ya Afya.

Alhamisi, 4 Agosti 2022

ENDELEENI KUTOA HUDUMA BORA KWA WANANCHI-DKT. SICHALWE

- Hakuna maoni

Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Aifello Sichalwe alipotembelea Hospitali Misheni ya Haydom iliyoko Mkoani Manyara kujionea hali ya utoaji wa huduma za afya ili kuleta ufanisi mzuri katika kutoa huduma.


Na. WAF – Manyara

Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Aifello Sichalwe ameupongeza Uongozi wa Hopsitali ya Misheni ya Haydom iliyoko Mkoani Manyara kwa kazi nzuri wanayofanya katika kuwahudumia wanachi na kuwataka kuendelea kutoa huduma  bora za afya. 

Dkt. Sichalwe ameyasema hayo  Mkoani Manyara alipotembelea Hospitali hiyo kujionea hali ya utoaji wa huduma za afya ambapo amewataka kuwa na dawati la huduma kwa mteja ili kuleta ufanisi mzuri katika kutoa huduma.

Aliendelea kusisitiza kuwa, sababu za hospitali nyingi kushindwa kufanya  vizuri  ni pamoja na kukosekana uongozi mzuri katika utendaji, kutobadili fikra na tabia zinazodumaza maendeleo katika utoaji huduma kwa wananchi. 

“Nahitaji wataalamu wa afya mrudi katika miiko yenu na weledi wenu hii itaturudishia hadhi ya taaluma na kuleta ufanisi mzuri wakati wa kutoa huduma kwa wananchi."Amesema. 

Hata hivyo Dkt. Sichalwe amewakumbusha watumishi katika hospitali hiyo kutumia fursa iliyotolewa na Serikali ya kujiendeleza kielimu ili kuendelea kupata ujuzi zaidi katika taaluma zao.

Aidha amewataka kuwasimamia vizuri na kwa karibu madaktari watarajali wanaofanya mazoezi kwa vitendo (Interns), kwa kuwaelekeza miiko ya taaluma na kufanya  kazi kwa juhudi na ufanisi ili wapate ujuzi mzuri wa kulitumikia Taifa utaoleta matokeo chanya.

Mwisho


SERIKALI KUJA NA MIKATABA YA KUPUNGUZA VIFO VYA MAMA NA MTOTO.

Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Aifello Sichalwe akiongea katika kikao cha Wadau wa Sekta ya Afya kwenye eneo la mama na mtoto pamoja na Lishe kilichofanyika Mkoani Singida.


Na.Rayson Mwaisemba,WAF- SINGIDA 

Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Aifello Sichalwe alisema, Serikali kupitia Wizara ya Afya na OR-TAMISEMI imejipanga kupunguza vifo vya Wajawazito na watoto kupitia mikataba itakayobeba viashiria vya Wajawazito na lishe inayotarajiwa kusainiwa na Wakuu wa Mikoa. 

Dkt. Sichalwe alisema hayo katika kikao cha Wadau wa Sekta ya Afya kwenye eneo la mama na mtoto pamoja na Lishe kilichofanyika Mkoani Singida.

"Tumekubaliana kutekeleza maagizo ya Mhe. Rais aliyoyatoa ya kuja na mkataba mmoja ambao utakuwa umebeba viashiria vya utendaji vya akina mama wajawazito pamoja na masuala ya Lishe ikiwa ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kupambana dhidi ya vifo vya Wajawazito na watoto wachanga".Alisema Dkt. Sichalwe 

Aliendelea kusema kuwa, pamoja na hayo Serikali kwa kushirikiana na wadau imekubaliana kuanza kutekeleza matumizi ya kanzi data, yatakayotoa fursa ya kujua viashiria vya hatari vya mjamzito endapo anavyo kutokana na maswali atayoulizwa na Mtaalamu wa afya.

Sambamba na hilo Dkt. Sichalwe alisema, kwa upande mwingine Serikali kwa kushirikiana na wadau wamekubaliana utekelezaji wa azimio la vikao vya kujadili vifo vya mama na mtoto vilivyoanzishwa na Wizara ya Afya kikanda. 

Aidha, Dkt. Sichalwe alieleza kuwa, kwa pamoja kama Wadau wa Sekta ya Afya wamekubaliana kutekeleza mfumo wa kusimamia magari ya kubebea Wajawazito (M-MAM) unaorahisisha mfumo wa rufaa nchini kama sehemu nyingine ya mkakati wa kupambana dhidi ya changamoto ya vifo vya Wajawazito na watoto. 

Mbali na hayo, Dkt. Sichalwe aliwashukuru Wadau waliojitokeza katika kikao hicho cha Kimkakati na kuweka wazi kuwa, maazimio yote ya kikao hicho yatawasilishwa kwenye uongozi wa Wizara ya Afya na TAMISEMI kwaajili ya utekelezaji na Wadau wote walioshiriki kikao hicho na wasio shiriki watakuwa katika utekelezaji. 

Hata hivyo, aliweka wazi kuwa, wamekubaliana kuleta mipango yao, namna walivyotekeleza na changamoto wanazokutana nazo wakati wa utekelezaji wa mipango hiyo na wanaishauri nini Serikali ili kwa pamoja kuona namna gani wanaweza kushirikiana kuzitatua kwa lengo la kuongeza kasi ya kupunguza vifo vya mama na mtoto katika jamii.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Dkt. Ntuli Kapologwe alisema, katika kikao hicho wamepitia viashiria mbalimbali vinavyolenga masuala ya mama na mtoto ambavyo vitasaidia kuongeza uwajibikaji kwa viongozi mbalimbali ngazi ya Mkoa na kupima matokeo ya uwajibikaji huo kwa kupungua kwa vifo vya Wajawazito na watoto. 

Pia, Dkt. Ntuli amesema kuwa, Serikali ilifanya uwekezaji mkubwa wa miundombinu ambapo vituo vya afya 650  ambavyo vinatoa huduma za upasuaji vimejengwa, huku hospitali mpya za Halmashauri 130 zikijengwa, hivyo uwekezaji huo ni lazima uende sambamba na huduma bora zitazosaidia kupungua kwa vifo vya Wajawazito na watoto. 

"Serikali imefanya uwekezaji mkubwa wa miundombinu, katika kipindi cha miaka mitano vituo vya afya 650 vinavyotoa huduma za upasuaji, sambamba na hilo hospitali mpya za Halmashauri 130, sasa uwekezaji huo lazima uende sambamba na huduma." Alisema Dkt. Ntuli.

Mwisho.

 

Jumamosi, 25 Juni 2022

BILIONI 4.4 ZATOLEWA NA SERIKALI KUBORESHA HUDUMA ZA RADIOLOJIA NA UZALISHAJI WA HEWA YA OKSIJENI HOSPITALI RUFAA YA JESHI LUGALO

- Hakuna maoni

 



Serikali kupitia Wizara ya Afya imetoa kiasi cha Bilioni 4.4 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya kutolea Huduma za Radiolojia, jengo la kufua hewa ya oksijeni pamoja na uboreshaji wa huduma za dharura na wagonjwa mahututi katika Hospitali Rufaa ya Jeshi Lugalo.


 

Prof. Abel Makubi Katibu Mkuu Wizara ya Afya.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya Prof. Abel Makubi mara baada ya kutembelea miradi hiyo ya ujenzi inayoendelea kutekelezwa ndani ya Hospitali hiyo iliyopo Jijini Dar Es Salaam.
“Shilingi Bilioni 4.4 zimetolewa na Serikali chini ya Mhe Rais Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya miradi ya ujenzi hapa Lugalo, lakini pia tumetoa zaidi ya Bilioni 4.8 kwa utekelezaji wa miradi ya afya kwenye Idara nyingine za Ulinzi na Usalama ikiwemo Jeshi la Polisi na Jeshi la Magereza.” amesema Prof. Makubi na kuongezea kuwa Wizara ya Afya itaendelea kushirikiana na Wizara na Taasisi nyinginezo kuboresha huduma za Afya.

Prof. Makubi ameipongeza Hospitali hiyo kwa usisamizi hodari wa miradi hiyo huku akiwataka viongozi kuhakikisha miradi hiyo inakamilika ndani ya wakati ili wananchi waanze kupata huduma.

“Tunamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuiwezesha Jeshi la Wananchi wa Tanzania kutoa huduma za afya kwa wananchi lakini pia kwa kutoa fedha za UVIKO-19 kwa ajili ya kuboresha huduma za afya nchini” amesema Prof. Makubi ambaye pia alifikisha salaam za Waziri wa afya , Mhe Ummy Mwalimu kwa Uongozi wa Hospitali ya Lugalo.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa Dkt. Faraji Mnyepe amesema kuwa Wizara yake itaendela kushirikiana na Wizara ya Afya kuhakikisha wanaendelea kutoa huduma bora za matibabu kwa wananchi.

Ujenzi wa jengo la Huduma za Radiolojia.

"Tunajenga hivi kwa ajili ya nchi wala sio kwa ajili ya jeshi pekee, huduma hizi tunazifanya kwa manufaa ya nchi” amesema Dkt. MnyepeKwa upande wake Mkuu wa Hospitali ya Jeshi Lugalo Brig. Jenerali Agatha Katua amesema kuwa Hospitali ya Jeshi Lugalo ilipokea fedha kiasi cha Shilingi Bilioni 4.4 ambapo mpaka sasa tayari wameshanunua mashine ya kufua hewa ya oksijeni kutoka Borahi Kuu ya Dawa, huku ujenzi wa jengo la kuwekea mashine hizo na kutoa huduma ukiwa unaendelea.

Ujenzi wa jengo la kufua hewa ya oksijeni.

Brigedia Jenerali Agatha Katua amesema kuwa wanaendelea na ujenzi wa jengo la Radiolojia ambapo wataweka huduma zote za radiolojia sehemu hiyo kwa kuweka mashine za CT, Scan, MRI, X-Ray, Ultra Sound.
Awali akitoa taarifa ya utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa jengo la radiolojia na jengo la kufua hewa ya oksijeni, Mkurugenzi Mtendaji wa SUMA JKT Kanali Petro Ngata amesema ujenzi wa jengo la radiolojia umefikia asilima 62 huku wakitarajia kukamilisha ujenzi ifikapo Mwezi Septemba 2022 huku Jengo la kufua hewa ya oksijeni ujenzi umefikia asilimia 45 na wanatarajia kukamilisha ifikapo Mwezi Agosti 2022.

Mwisho

Jumatatu, 20 Juni 2022

WADAU WA MAENDELEO KUCHAGIA BILIONI 98.1 KUPITIA MFUKO WA AFYA WA PAMOJA

Waziri wa Afya, Mheshimiwa Ummy Mwalimu akisema jambo kwenye Mkutano na Wadau wa Maendeleo wanaochangia kwenye Mfuko wa Afya wa pamoja (hawapo pichani) uliofanyika Jijini Dar Es Salaam.
Naibu Waziri Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Dkt. Festo Dugange akisema jambo kwenye Mkutano na Wadau wa Maendeleo wanaochangia kwenye Mfuko wa Afya wa pamoja (hawapo pichani) uliofanyika Jijini Dar Es Salaam.





Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu (wa kushoto) akisema jambo na wadau wa maendeleo wanaochangia fedha kwenye Mfuko wa Afya wa pamoja (Health Basket Fund)


Na Englibert Kayombo - Dar es Salaama

Wadau wa Mfuko wa Afya wa pamoja nchini (Health Basket Fund) wamepanga kuchangia kiasi cha shilingi Bilioni 98.1 kwa ajili ya kuboresha utoaji wa huduma za afya nchini kwa mwaka 2022/2023.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa afya Mhe. Ummy Mwalimu wakati wa kikao cha kujadili uboreshaji wa mfuko huo kupitia ushirikiano wa pamoja  kati ya Serikali na wadau Jijini Dar Es Salaam.

“Kwa niaba ya Serikali tunawashukuru wadau wetu wanaochangia kwa pamoja kwenye Mfuko wa Afya na tunatarajia kwa Mwaka wa fedha ujao wa 2022/23 wadau wetu kwa pamoja kuchangia Shilingi Bilioni 98.1 na fedha hizo zitaingizwa moja kwa moja kwenye akaunti za Vituo vya kutolea huduma za Afya nchini” amesema Waziri Ummy Mwalimu

Waziri Ummy amesema katika mwaka wa fedha uliopita wadau kupitia Mfuko walichangia kiasi cha shilingi bilioni 74.3 ambapo asilimia 90 ya fedha zimekwenda kwenye Halmashauri na zimeingizwa moja kwa moja kwenye Zahanati, Vituo vya Afya pamoja na Hospitali za Wilaya nchini.

Aidha Waziri Ummy Mwalimu amesema upo umuhimu kwa wadau wa maendeleo kuchanga fedha kwa pamoja na kuweka kwenye Mfuko wa Afya wa pamoja na kusema kuwa kufanya hivyo ni kuzingatia Mifumo na taratibu za Serikali za kutoa fedha kwa ajili ya Huduma za Afya nchini pamoja na kuwekeza fedha kwenye maeneo ya vipaumbele vya Serikali.

“Fedha zinazoingizwa nchini kwa ajili ya kusaidia shughuli mbalimbali za afya tunapenda ziingizwe kwenye Mfuko wa Afya wa pamoja ili tuweke kushirikiana kufanya kazi pamoja na kupata matokea ya haraka kwa pamoja.

mapendekezo yetu wadau wengine wachangia kupitia mfuko huo kwani tumeona mafanikio makubwa" amefafanua Waziri Ummy Mwalimu.

Kwa upande wake Naibu Waziri kutoka Ofisi ya Rais TAMISEMI Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange ameshukuru wadau hao kwa kuendela kutoa ushirikiano na Serikali na kutoa fedha kwa ajili ya kuboresha utoaji wa huduma katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

Mhe. Dugange amepongeza wadau hao kwa kuongeza kiwango cha fedha kutoka Shilingi Bilioni 74.3 mwaka wa fedha 2021/22 hadi Bilioni 98.1 kwa mwaka wa fedha 2022/23 na kusema kuwa kupitia mchango huo pamoja na uwekezaji mkubwa uliofanyika, Serikali kufanya mapinduzi makubwa kwenye ubora wa huduma za afya kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

Mhe. Dkt. Dugange amesema kuwa asilimia 33.3 ya fedha hizo hutumika kwenda kununua dawa, vifaatiba na ‘reagents’ kwa ajili ya vipimo vya maabara ikiwa na pamoja kuboresha huduma za mama na mtoto katika vituo vya kutolea huduma za afya.

“Kwa mwaka huu wa fedha 2022/23 vituo zaidi ya 175 vimepata vifaatiba kwa ajili ya huduma za upasuaji, lakini kwa mwaka ujao wa fedha, tunatarajia vituo zaidi ya 225 vitapata vifaatiba” amefafanua Mhe. Dugange

Akizungumza kwa niaba ya Wadau wanaochangia katika Mfuko wa Afya wa pamoja, akizungumza na vyombo vya Habari Dkt. Peter Nyela Meneja wa Program ya Afya kutoka Ubalozi wa ‘Ireland’ wanafanya hivyo kusaidia Serikali ili kuhakikisha Vituo vya kutolea huduma za afya nchini vinakuwa na dawa, kurahisisha huduma nyinginezo ikiwemo huduma za rufaa, pamoja na motisha kwa watoa huduma za afya nchini.

Huu ni ushirikiano mzuri sana baina ya Serikali na Wadau wa Maendeleo kuweza kufanya kazi kwa pamoja kuweza kusaidia kuboresha huduma za Afya nchini, Sisi kama Wadau kwa pamoja tutaendelea kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kuboresha Sekta ya Afya nchini” amefafanua Dkt. Nyela.

Mfuko wa Afya wa Pamoja umedumu kwa miaka 23 hadi kufikia leo ambapo ni muunganiko wa pamoja baina ya Serikali na Wadau wa Maendeleo kutoka Denmark, Korea, Ireland, Switzerland, Canada, UNFPA, UNCEF na Benki ya Dunia ambao huchangia katika huduma za afya nchini kwa kutoa fedha na kuziweka kwenye akaunti moja na fedha hizo kutolewa moja kwa moja kwenye vituo vya  kutolea huduma za afya nchini.

Ijumaa, 17 Juni 2022

WAZIRI UMMY AKUTANA NA MWAKILISHI MKAZI KUTOKA UN-WOMEN

- Hakuna maoni

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akiwa na Mwakilishi Mkazi kutoka UN-WOMEN Bi. Hodan Addou baada ya kumalizika kwa kikao chao kilichofanyika katika Ofisi za Wizara ya Afya Jijini Dodoma.

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akiwa katika picha ya pamoja na Mwakilishi Mkazi kutoka UN-WOMEN Bi. Hodan Addou aliyeambatana na wenzake.

Picha ikionesha kikao kati ya Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu na Mwakilishi Mkazi kutoka UN-WOMEN Bi. Hodan Addou aliyeambatana na wenzake kutoka UN-WOMEN


 Kutoka Dodoma, Juni 17, 2022.

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu leo Juni 17,2022 amekutana na kufanya mazungumzo na mwakilishi kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa upande wa wanawake (UN - WOMEN) katika ofisi za Wizara Jijini Dodoma. 

Katika mazungumzo yao kwa pamoja wamekubaliana kushirikiana katika masuala ya afya, hususan katika kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto na usawa wa kijinsia katika Sekta ya Afya. 

Waziri ummy amempongeza Mwakilishi huyo kwa kazi nzuri anazoendelea kufanya na ameahidi kuendelea kushirikiana nae ili kufikia malengo ya kuboresha huduma za afya hasa zinazowahusu wanawake katika Sekta ya Afya. 


#AfyaKwanza 

#JaliAfyaYako

Jumanne, 10 Mei 2022

HATUWEZI KUWA NA WATUMISHI BORA WA AFYA KWA KUVUMILIA VYUO VINAVYOFANYA UDANGANYIFU - PROF. MAKUBI

Wakuu wa vyuo vya Afya wakifuatilia neno kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Wakuu wa vyuo vya afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya akieleza jambo wakati akifungua Mkutano wa Wakuu wa vyuo vya afya, Jijini Dodoma

Mkurugenzi wa Mafunzo na Rasilimali watu Wizara ya Afya Dkt. Saitore Laizer akieleza jambo mbele ya mgeni rasmi (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Wakuu wa vyuo vya afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Mwakilishi wa Katibu Mtendaji wa NACTVET Bw. Twaha Twaha akitoa salamu kutoka taasisi yake wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Wakuu wa vyuo vya afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Baadhi ya Wakuu wa vyuo vya Afya wakifuatilia neno kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Wakuu wa vyuo vya afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Baadhi ya Wakuu wa vyuo vya Afya wakifuatilia neno kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Wakuu wa vyuo vya afya uliofanyika Jijini Dodoma.


Na WAF - DOM 

KATIBU MKUU Wizara ya Afya Prof. Abel Makubi amesema kuwa, Serikali haitaendelea kuvumilia tabia ya udanganyifu unaofanywa na baadhi ya vyuo vya afya nchini, kwani tabia hizo hupelekea kupata Watumishi wasio na ubora na kurudisha nyuma jitihada za Serikali za kuboresha huduma kwa wananchi. 

Prof. Makubi amesema hayo leo Mei 10, 2022 wakati akifungua Mkutano wa Wakuu wa vyuo vya afya wenye kauli mbiu ya  "Huduma bora za Afya ni matokeo ya uwepo wa vyuo bora nchini," uliofanyika Jijini Dodoma. 

"Hatuwezi kuwa na Watumishi bora wa Afya kwa kuvumilia baadhi ya vyuo vinavyoendekeza tabia ya udanganyifu kwenye uendeshaji wa mafunzo, hali hii inarudisha nyuma juhudi za Serikali za kuboresha huduma kwa wananchi." Amesema Prof. Makubi. 

Amesema, hali ya udanganyifu ni kinyume cha Sheria, maadili, utaratibu na mbaya zaidi udanganyifu huu umeendelea hadi kwenye mazoezi ya mitihani ya ndani na ile ya Kitaifa kwa kuwahusisha baadhi  ya wanafunzi na walimu katika maeneo yao, hii haikubaliki. 

Sambamba na hilo, Prof. Makubi amewaelekeza Wasajili wa Mabaraza ya kitaaluma kuchukua hatua hatua stahiki kwa wakufunzi wanaoshiriki kwenye udanganyifu kwa kuwafutia leseni na hatua nyingine kwa mujibu wa Sheria za nchi. 

Aliendelea kusisitiza kuwa, Wizara haitasita kuchukua hatua kali kwa chuo chochote kitachoenda kinyume na utaratibu wa uendeshaji wa mafunzo na upimaji wa wanafunzi, ikiwa na sehemu ya uboreshaji wa utoaji huduma. 

Katika kulinda ubora wa Wahitimu, Prof. Makubi ameelekeza kusitisha usajili kwa vyuo ambavyo havijakidhi utaratibu kama vile kutokuwa na miundombinu ya kufundishia ikiwemo hospitali na maabara za mafunzo kwa vitendo,  msongamano wa vyuo vingi katika eneo moja hali inayopelekea wanafunzi kukosa eneo la kufanyia mafunzo kwa vitendo. 

Aidha, amewapongeza Wakuu wa vyuo kwa kazi nzuri wanayoendelea kuifanya licha mazingira magumu yanayokutana nayo katika maeneo yao ya utendaji, na kuahidi kuendelea kutoa ushirikiano katika utatuzi wa changamoto hizo ili kuboresha huduma kwa wananchi. 

Mbali na hayo, amewataka Wakuu wa vyuo kuwa Wazalendo na kuzingatia misingi ya uongozi bora kwa kushirikisha viongozi wengine katika ngazi ya maamuzi, ikiwemo katika matumizi ya fedha ili kuondoa misuguano inayoweza kuepukika. 

Hata hivyo,  ametoa wito kwa Wakuu wa vyuo kuwa wabunifu katika utendaji wao, ikiwemo kushirikiana na Wadau mbalimbali wanaopatikana katika maeneo yao jambo litakalosaidia kupunguza changamoto katika vyuo vyao. 

Naye,Mkurugenzi wa Mafunzo na rasilimali watu Wizara ya Afya Dkt. Saitore Laizer amemshukuru Katibu Mkuu kwa kuendelea kusaidia vyuo vya mafunzo, na kuahidi kutekeleza maelekezo yote aliyotoa ili kufikia lengo la Serikali la kuboresha huduma kwa wananchi. 

Mwisho.


Ijumaa, 6 Mei 2022

WARATIBU WA TIBA ASILI WAELEKEZWA KUKEMEA RAMLI CHONGANISHI.

 

KAIMU Mkuregenzi Msaidizi anayeshughulikia Tiba Asili na Tiba Mbadala Wizara ya Afya Bi. Lucy Mziray akieleza jambo wakati wa ufunguzi wa mafunzo ya Waratibu wa tiba asili wa baadhi ya Halmashauri nchini, mafunzo yaliyofanyika Jijini Mwanza.

Kaimu Msajili wa Baraza la Tiba asili na Tiba mbadala Bw. Ndehani Msigwa akieleza majukumu ya Baraza la Tiba asili na Tiba mbadala katika ufunguzi wa mafunzo ya Waratibu wa tiba asili wa baadhi ya Halmashauri nchini yaliyofanyika Jijini Mwanza.

Baadhi ya Waratibu wa Tiba asili walioshiriki mafunzo ya huduma za tiba asili yenye lengo la kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo juu ya shughuli mbalimbali za tiba asili nchini, mafunzo yaliyofanyika Jijini Mwanza.

Baadhi ya Waratibu wa Tiba asili walioshiriki mafunzo ya huduma za tiba asili yenye lengo la kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo juu ya shughuli mbalimbali za tiba asili nchini, mafunzo yaliyofanyika Jijini Mwanza.

Baadhi ya Waratibu wa Tiba asili wakiendelea na mafunzo ya huduma za tiba asili yenye lengo la kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo juu ya shughuli mbalimbali za tiba asili nchini, mafunzo yaliyofanyika Jijini Mwanza.

Picha ya pamoja ya Waratibu wa tiba asili ngazi ya Halmashauri wakiwa pamoja na viongozi kutoka Wizara ya Afya na Baraza la Tiba asili na Tiba mbadala baada ya mafunzo ya huduma za tiba asili  yaliyofanyika Jijini Mwanza.



WARATIBU WA TIBA ASILI WAELEKEZWA KUKEMEA RAMLI CHONGANISHI. 

Na WAF - MWANZA. 

KAIMU Mkuregenzi Msaidizi anayeshughulikia Tiba Asili na Tiba Mbadala Wizara ya Afya Bi. Lucy Mziray ametoa wito kwa Waratibu wa Tiba asili na Tiba mbadala ngazi ya Halmashauri kukemea ramli chonganishi zinazofanywa na baadhi ya Waganga wa tiba asili wasio waaminifu. 

Bi. Lucy ametoa wito huo leo Mei 6 katika ufunguzi wa mafunzo ya Waratibu wa tiba asili wa baadhi ya Halmashauri nchini, mafunzo yenye lengo la kubadilishana uzoefu na kujengeana uwezo juu ya shughuli mbalimbali za tiba asili nchini, mafunzo yaliyofanyika Jijini Mwanza. 

Amesema, wapo baadhi ya Waganga wa tiba asili wanafanya ramli chonganishi jambo ambalo ni kinyume cha taratibu, Sheria na miongozo ya Serikali, hali inayopelekea uminywaji wa haki na uvunjifu wa amani katika ngazi ya familia na jamii kwa ujumla. 

"Nitoe wito kwa Waratibu wote wa tiba asili na tiba mbadala nchini, kuhakikisha wanakemea ramli chonganishi zinazofanywa na baadhi ya Waganga, na hali hii hupelekea kutotenda haki na inaweza kupelekea uvunjifu wa amani katika ngazi zote ikiwemo ngazi ya familia na jamii." Amesema. 

Sambamba na hilo, amesema kuwa, kuanzia mwaka 2018 Kitengo cha Tiba Asili kwa kushirikiana na Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala na baadhi ya vyuo vya kitaaluma imefanikiwa kuwapa mafunzo Waganga wa tiba asili 200 kuhusu miiko ,maadili na usafi katika kuandaa dawa za  asili. 

Aidha, ametoa rai kwa Waratibu wa Tiba asili wote waliohudhuria kupeleka ujuzi kwa kuwafundisha na kuwahamasisha waganga wa tiba asili na tiba mbadala juu ya ya sheria, miiko na maadili ya kazi wanazofanya katika jamii na uzingatiaji wa usafi na usalama katika utoaji wa huduma zao, ikiwa pamoja na uandaaji salama wa dawa za asili. 

Kwa upande wake Kaimu Msajili wa Baraza la Tiba asili na Tiba mbadala Bw. Ndehani Msigwa amewapongeza Waratibu wa Tiba asili na Tiba mbadala kwa kuhudhuria mafunzo yenye lengo la kuchochea utoaji wa huduma bora na salama ili kuilinda Afya ya Watanzania. 

Aliendelea kwa kutoa wito kwa Waratibu wa Tiba asili kuhakikisha wanasajili Waganga wote katika maeneo yao na kusajili vituo vyao wanavyotolea huduma ili Watambulike na Wizara pamoja na Baraza linalowasimamia kwa mujibu wa Sheria na taratibu. 

"Bado tunao Wataalamu wengi kwenye maeneo yetu ambao hawajasajiliwa na kwa waliosajiliwa bado vituo vyao havijasajiliwa, hii ni changamoto kubwa ambayo naamini baada ya kutoka kwenye mafunzo haya tutakwenda kuitatua." Amesema Bw. Msigwa. 

Nae, Katibu wa Afya kutoka Balaza la Tiba asili na Tiba mbadala Bw. Patrick Seme amewataka Waratibu wa Tiba asili na Tiba mbadala ngazi ya Halmashauri kuratibu matangazo ya tiba asili kwenye vyombo vya habari, na kuchukua hatua kwa wanaotoa na wanaorusha matangazo hayo ambayo hayajapewa kibali na Wizara kupitia Baraza la Tiba asili na Tiba mbadala kwani matangazo mengi hupotosha umma juu ya uwezo wa kutibu. 

"Mkakemee vitendo vibaya vinavyofanywa na baadhi ya Waganga wa Tiba Asili  ambavyo vinakiuka sheria ya Tiba Asili ya 2002 ikiwa ni pamoja na utoaji wa matangazo ya huduma za tiba asili ambayo hayajapekuliwa na kupewa kibali na Baraza la Tiba Asili na utoaji wa huduma za tiba asili bila kusajiliwa." Amesema. 

Mwisho.





Jumatano, 13 Aprili 2022

ASILIMIA 26 YA WATU WAZIMA WANASHINIKIZO LA JUU LA DAMU.

- Hakuna maoni
Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Aifello Sichalwe akipima msukumo wa damu katika Zahanati ya Makole Jijini Dodoma, baada ya kuzindua mradi wa Healthy Heart Africa (HHA) unaoratibiwa na AstraZeneca katika Mikoa ya Dodoma na Dar es salaam.

Wananchi walioshiriki tukio la uzinduzi wa mradi wa Healthy Heart Africa (HHA) unaoratibiwa na AstraZeneca katika Mikoa ya Dodoma na Dar es salaam, wakifuatilia kwa makini neno kutoka kwa Mganga Mkuu wa Serikali aliyeongoza zoezi la uzinduzi wa mradi huo

Picha ya pamoja ikiongozwa na Mganga Mkuu wa Serikali Dkt. Aifello Sichalwe.



ASILIMIA 26 YA WATU WAZIMA WANASHINIKIZO LA JUU LA DAMU. 

Na Rayson Mwaisemba WAF- DOM.

MGANGA Mkuu wa Serikali Dkt. Aifello Sichalwe amebainisha kuwa asilimia 26 ya watu wazima wenye umri wa miaka kati ya 25 hadi 64 wana shinikizo la juu la damu, hali inayosababishwa na mtindo wa maisha ikiwemo ulaji wa vyakula vya mafuta mengi, matumizi ya pombe kupita kiasi na kutofanya mazoezi. 

Dkt. Sichalwe amebainisha hayo leo Aprili 13, 2022 wakati akifungua Mradi wa Healthy Heart Africa tukio lililofanyika katika zahanati ya Makole Jijini Dodoma. 

"Tumefanya utafiti mwaka 2012 na kukagundua kwamba asilimia 26 ya watu wazima kati ya miaka 25 na 64 wana shinikizo la juu la damu na tatizo hili linatarajia kuongezeka kwa kiasi kikubwa endapo hatutachukua hatua." Amesema Dkt. Sichalwe. 

Aliendelea kusema kuwa, tafiti zinaonesha kuwa, zaidi ya asilimia 75% ya Wagonjwa hao wenye shinikizo la juu la damu hawatumii tiba yoyote, huku akiweka wazi kuwa zaidi ya robo tatu kati yao hawajui kama wana shinikizo la juu la damu. 

Aidha, Dkt. Sichalwe amesema kuwa, taarifa za utafiti zilizofanywa katika baadhi ya hospitali za Rufaa zimebaini kuwa, wastani wa watu 19 katika kila watu 100 wanaolazwa kwa tatizo la shinikizo la juu la damu hufariki Dunia. 

Sambamba na hilo, ameweka wazi kuwa, hali ni mbaya zaidi kwa wagonjwa wa kiharusi, ambapo katika kila watu 100 wanaolazwa, watu 39 wanafariki kwa tatizo hilo la shinikizo la juu la damu, hivyo Serikali kupitia Wizara ya Afya itaendelea kutoa elimu na kuhamasisha jamii ili kuongeza nguvu za kupambano dhidi ya ugonjwa huo. 

Mbali na hayo Dkt. Sichalwe ameendelea kusisitiza juu ya kuzingatia utoaji huduma za afya kwa kufuata miongozo, huku akisisitiza weledi na umahiri wakati wa kutoa huduma ili kuepusha malalamiko yanayoweza kuzuilika kutoka kwa wananchi. 

Naye, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Rashid Mfaume amewashukuru Wadau wa PATH kwa kuendelea kushirikiana na Serikali katika mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo ugonjwa wa Shinikizo la juu la damu. 

Amesema, Ukuaji wa miji, Maendeleo ya Sayansi na teknolojia na mabadiliko ya mtindo wa maisha kwa kiasi kikubwa yanaendana na ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo ugonjwa wa shinikizo la juu la damu, hivyo kuwaomba Wadau kuendelea kushirikiana na Serikali katika mapambano dhidi ya magonjwa hayo hasa katika miji inayoendelea kwa kasi ikiwemo Dodoma, Dar es Salaam, Arusha, Mwanza na Mbeya. 

Mpango wa Healthy Heart Africa (HHA) ni mpango wa miaka miwili unaoratibiwa na AstraZeneca katika Mkoa wa Dodoma (HF 13) na Dar es salaam (HF 22), na unajumuisha jumla ya vituo vya kutolea huduma za afya 35 (zahanati 25 na hospitali 10). Mradi huu unashughulikia magonjwa ya moyo na mishipa, haswa Shinikizo la damu (HTN). 


Mwisho.