Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumamosi, 29 Juni 2019

HUDUMA ZA DHARURA KWA WAJAWAZITO ZAENDELEA KUSAMBAA NCHINI

- Hakuna maoni
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akisisitiza  jambo mbele ya wananchi (hawapo kwenye picha) wakati wa matembezi ya hisani yanayolenga kuwezesha uwepo wa Wakunga kwa uzazi salama.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (Watatu kushoto) akiteta jambo na Waziri wa Afya wa Serikali ya Zanzibar Bw. Hamad Rashid Mohamed wakati wa matembezi ya hisani yanayolenga kuwezesha uwepo wa Wakunga kwa uzazi salama,  Kulia kwa Waziri Ummy ni Mkurugenzi wa Amref Health Africa nchini Bi. Florence Temu

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu pamoja na Waziri wa Afya wa Serikali ya Zanzibar Bw. Hamad Rashid Mohamed wakinyoosha viungo muda mfupi baada ya kumaliza matembezi ya hisani yanayolenga kuwezesha uwepo wa Wakunga kwa uzazi salama, yaliyofanyika katikati viwanja vya farasi Jijini Dar es Salaam.

 Mkurugenzi wa Amref Health Africa nchini Bi. Florence Temu akiwasilisha taarifa ya mradi wa  SUAM mbele ya Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu (hayupo kwenye picha) wenye lengo la kuwezesha uwepo wa Wakunga kwa uzazi salama

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (wakatikati) pamoja na Waziri wa Afya wa Serikali ya Zanzibar Bw. Hamad Rashid Mohamed wakimkabidhi zawadi ya cheti Mkurugenzi Mtendaji wa Azania Bank, Charles Itembe kwa mchango mkubwa walioutoa kufanikisha matembezi hayo ya hisani yanayolenga kuwezesha uwepo wa wakunga kwa uzazi salama nchini.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto pamoja na Waziri wa Afya wa Serikali ya watu wa Zanzibar Bw. Hamad Rashid Mohamed wakati wa matembezi ya hisani yanayolenga kuwezesha uwepo wa Wakunga kwa uzazi salama, yaliyofanyika katikati viwanja vya farasi Jijini Dar es Salaam.


Na WAMJW- DSM 

Serikali kupitia Wizara ya Afya, yaendelea kuboresha huduma za Afya za dharura nchini kwa kuviwezesha vituo vya Afya kuweza kutoa huduma za uzazi wa dharura ikiwemo upasuaji wa kumtoa mtoto tumboni ili kuokoa vifo vitokanavyo na matatizo ya uzazi pingamizi. 

Hayo yamesemwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe Ummy Mwalimu leo wakati wa matembezi ya hisani yanayolenga kuchangia Juhudi za kupunguza na kuepusha vifo vya wajawazito na Watoto wachanga vitokanavyo na uzazi, katika viwanja vya farasi Jijini Dar es Salaam. 

Waziri Ummy amesema kuwa wakati Serikali ya awamu ya tano inaingia madarakani ilikuwa vituo vya Afya takribani 109 sawa na asilimia 19 ya vituo vya Afya ambavyo vilikuwa na uwezo wa kutoa huduma za upasuaji za dharura pamoja na kumtoa mtoto tumboni, huku sasa kuongezeka hadi kufikia takribani vituo 460.

Aidha, Waziri Ummy aliendelea kusema kuwa kila mwaka Wanawake 11,000 hufariki nchini, sawa na wanawake 900 kila mwezi, ikiwa ni sawa na wanawake 30 kila siku hufariki wakiwa wanatimiza wajibu wao wa msingi wakuleta kiumbe Duniani, hivyo ni lazima Juhudi za ziada ziendelee kuchukuliwa. 

Kulingana na takwimu zilizofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu zinaonesha kwamba vifo katika kila vizazi hai 100,000 wanawake 556 hufariki, huku wanawake wajawazito nchini wakiwa Milioni 2 kwa mwaka

Mbali na hayo, Waziri Ummy amesema kuwa Serikali imeweza kuongeza bajeti ya dawa hadi kufikia takribani Bilioni 260, ikilinganishwa na bajeti ya Bilioni 30 iliyokuwepo kabla ya Serikali ya awamu ya tano kuingia madarakani, huku dawa kama ’magnesium sulfate' kwa ajili ya kifafa cha mimba zikipatikana bila malipo.

"Tumeweza kuongeza bajeti ya dawa, wakati tunaingia madarakani ilikuwa takribani Bilioni 30, sasa hivi tunazungumzia bajeti ya dawa ya Bilioni 260, huku dawa kama magnesium sulfate kwa ajili ya kifafa cha mimba zinapatikana bure bila malipo yoyote katika vituo vyetu vya kutoa huduma za Afya " alisema Waziri Ummy. 

Hata hivyo, Waziri Ummy amesema kuwa licha ya maboresho makubwa yanayoendelea kufanywa bado kuna changamoto ya Watoa huduma za Afya, hivyo amelipongeza Shirika la Amref kwa jitihada za kuajiri baadhi ya Watoa huduma jambo linalosaidia kupunguza changamoto katika Sekta ya Afya. 

"Tunauhitaji wa watumishi wa Afya takribani 200,008 katika vituo vya Afya vya Serikali kuanzia ngazi ya Zahanati mpaka ngazi ya Hospitali za rufaa za mikoa, huku watumishi waliopo ni takribani 98,000, hivyo pengo likiwa ni Asilimia 52, huku Zahanati zikiwa ndio waathirika wakubwa" alisema Waziri Ummy

Nae Waziri wa Afya wa Serikali ya watu wa Zanzibar Bw. Hamad Rashid Mohamed amewataka wakina mama kuwai katika vituo vya kutolea huduma za Afya pindi waonapo dalili za ujauzito, ili kuokoa vifo ambavyo vinaweza zuilika wakati wa kujifungua.

"Katika zile siku 12 za mwanzo wajitahidi kufika katika vituo vya Afya kupata uangalizi, na vifo vingi ndio huanza kutokea hapa, kwahiyo ningeomba sana wakinamama kuwahi katika vituo vya Afya, kuonana na wakunga waliopata elimu ili wapate huduma kwa wakati " alisema Hamad Rashid.

Mwisho

Jumatano, 26 Juni 2019

BODI ZA HOSPITALI ZA RUFAA ZATAKIWA KUTATUA CHANGAMOTO

- Hakuna maoni
Katibu Mkuu Wizara ya Afya akisema jambo kwa wajumbe wa Bodi ya Ushauri wa Hospitali za Rufaa za Mikoa (hawako pichani) katika Kikao kazi kilichofanyika jana Jijini Dodoma.

Wajumbe wa Bodi ya Ushauri wa Hospitali za Rufaa za Mikoa wakiwa katika kikao kazi.


Wajumbe wa Bodi ya Ushauri wa Hospitali za Rufaa za Mikoa wakiwa katika kikao kazi.

Na.WAMJW,Dodoma

Wajumbe wa bodi za ushauri za hospitali za rufaa nchini wametakiwa kutatua changamoto zilizopo kwenye hospitali zao ili wananchi wapate huduma zilizo bora

Rai hiyo imetolewa na Katibu Mkuu,Wizara ya Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Dkt.Zainabu Chaula wakati akifungua kikao kazi cha uhamasishaji wa wajumbe wa bodi za ushauri za hospitali za rufaa za mikoa kinachofanyika jijini hapa

Dkt.Chaula alisema wizara inawategemea na kuwathamini wajumbe hao  katika kuleta mabadiliko ya uimarishaji wa huduma za afya katika hospitali za mikoa zilipo katika maeneo yao hivyo wanatakiwa kuwa wabunifu.

“Nyie ndio macho yetu kule,tumewapa wajibu hivyo tunawategemea mtushauri na kuleta mafanikio katika maeneo yenu".Alisisitiza Dkt.Chaula

Aidha,aliwataka wabuni katika kuongeza vyanzo vya mapato ili hospitali hizo ziweze kuwahudumia wananchi ipasavyo na si kwenda hospitali za ngazi za juu“madaktari bingwa wanatengenezwa wananchi hawapaswi kwenda hospitali kubwa bali hospitali za rufaa"alisema Dkt.Chaula

Wakati huo huo Mganga Mkuu wa Serikali Prof.Mohhamad Bakari Kambi alisema wanatarajia mabadiliko makubwa katika rasiliamali watu hususan kwenye sekta ya afya  kwa kuwa wabunifu.

"Tutawapima kwa utendaji  na mafanikio yenu na hivyo tutapenda baadae muwe bodi tendaji ili muwe na uwezo mkubwa wa kufanya maamuzi na si ushauri kama ilivyo sasa.Alisema Prof.Kambi

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Tiba Dkt.Grace Maghembe alisema wanatambua mchango wa bodi hizo kwani ndio walezi kwenye hospitali za rufaa za mikoa hivyo watasaidiana panapotokea mapungufu ili kuweza kurekebisha kwa haraka.

Dkt.Maghembe aliwataka wajumbe hao kusaidia kwa utashi katika kuimarisha  na kusimamia vyanzo vyanzo vya mapato yanayokusanywa pamoja na matumizi yake na kuzifanya hospitali za rufaa za mikoa kupunguza rufaa za hospitali kubwa na kuzifanya ziwe sehemu za kwanza za rufaa na kupunguza gharama za matibabu.

Kikao kazi hicho kinakutanisha wajumbe wa bodi za ushauri za hospitali za rufaa za mikoa kutoka mikoa kumi  kutoka Tanzania bara

Jumanne, 25 Juni 2019

WAZIRI WA AFYA ASISITIZA UBORA WA BIDHAA KATIKA KIWANDA KIPYA CHA DAWA NA VIFAATIBA SIMIYU.

- Hakuna maoni
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (kushoto) akimkabidhi vitendea kazi Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kiwanda cha Dawa na Vifaatiba kwa Profesa Olipa David Ngassapa (kulia)

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akisema jambo wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kiwanda cha Dawa na Vifaatiba cha Simiyu leo Jijini Dodoma.

Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kiwanda cha Dawa na Vifaatiba cha Simiyu wakimsikiliza Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (hayupo pichani) wakati akizindua bodi hiyo.
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt. Zainab Chaula akisema jambo wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kiwanda cha Dawa na Vifaatiba cha Simiyu leo Jijini Dodoma.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akisema jambo wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kiwanda cha Dawa na Vifaatiba cha Simiyu leo Jijini Dodoma.

Picha ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akiwa na Watendaji Wakuu ndani ya Wizara ya Afya na Taasisi za Afya pamoja na Wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Kiwanda cha Dawa na Vifaatiba cha Simiyu.

Na.WAMJW.Dodoma

Bodi ya wakurugenzi wa kiwanda cha dawa na vifaa tiba cha Simiyu(SIMIYU MEDICAL PRODUCTS) wametakiwa  kuzalisha bidhaa zenye viwango na kukidhi mahitaji ya ndani nan je ya nchi.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati wa uzinduzi wa bodi ya wakurugenzi wa kiwanda hicho uliofanyika leo jijini hapa.

Waziri Ummy amesema kuwa bidhaa zenye viwango itasaidia kuuza nje ya nchi na watanzania kuzitumia kwani lengo la serikali ya awamu ya tano ni ya kukuza uchumi wa viwanda 

“Lakini mhakikishe maamuzi yeyote mtakayofanya mjiridhishe je ni kwa ajili ya maslahi ya Taifa na je yatatufikisha kule tunapotaka kufika,jiridhisheni katika kuhakikisha mnatumia fedha hizi chache tulizonazo katika kuleta matokeo ya haraka haya ndiyo ya kuyazingatia”.Alisisitiza Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy aliitaka bodi hiyo kuhakikisha wanaongeza thamani ya mazao ya nchi kwa kuzalisha bidhaa nchini na kuondokana na uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi,kuongeza ajira na hata kuondokana na uagizaji wa bidhaa kutoka nje ya nchi.

Hata hivyo aliwataka wasiangalie bidhaa zinazotakana na pamba hivyo kwa baadae  ni bora wakaangalia bidhaa zingine zinazohitajika ambazo zinanunuliwa kwa haraka sana kutoka MSD kwani bohari ya Dawa hivi sasa imepata mkataba wa kununua bidhaa za hospitali kwa niaba ya nchi kumi na sita za nchi ya SADC hivyo wahakikishe bidhaa zinazozalishwa zina viwango na ubora na uzalishaji unakidhi soko la ndani nan je ya Tanzania.

Katika hatua nyingine Waziri Ummy amempongeza Mtanzania Dkt. Aswar Hilonga kwa kutunukiwa tunzo na Shirika la Afya Duniani kutokana na Ubunifu wake wa kutengeneza mtambo wa kuchuja na kusafisha maji.

Mtambo huo unaotumia nanotechnology una uwezo wa kuchuja maji na kuyafanya yawe safi na salama kwa matumizi ya binadamu na kuondoa bakteria, kemikali na taka katika maji.

"Asilimia 60 ya wagonjwa wa nje wanaokwenda Hospitalini  wanatokana na kiwango duni cha hali ya usafi  ikiwenyo unywaji wa maji yasiyo safi na salama. Hivyo kupitia teknolojia hii tunaweza kuokoa fedha za Serikali kwa ajili ya kutibu wagonjwa" amesema Waziri Ummy.

Kwa upande wake Dkt. Hilonga ameiomba Serikali kuweza kuunganisha mtambo huo wa maji ambao unauzwa kwa bei nafuu katika Taasisi za Umma ambao unachuja maji kwa kuondoa batkeria na kemikali na taka katika maji ndani ya muda mfupi.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (kushoto) akimpongeza Dkt. Askwar Hilonga (kulia) kwa kutunukiwa tuzo kutoka Shirika la Afya Duniani kwa  ubunifu wa mtambo wa kuchuja na kusafisha maji unaotumia nanotechnology kuondoa bakteria, kemikali na taka kwenye maji.

Mwisho.



DKT. CHAULA AWAFUNDA WAKUU WA VYUO VYA AFYA VYA SERIKALI

- Hakuna maoni
Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Zainab Chaula akieleza jambo wakati akifungua Mkutano wa Wakuu wa Vyuo vya Afya vya Serikali uliofanyika Jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Mafunzo Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Laizer akifuatilia maelekezo kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt Zainab Chaula (hayupo kwenye picha) pindi alipofungua Mkutano wa Wakuu wa Vyuo vya Afya vya Serikali uliofanyika Jijini Dodoma.

Mwakilishi wa Wakuu wa Vyuo vya Afya vya Serikali akisoma Risala mbele ya mgeni rasmi ambae ni Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. Zainab Chaula wakati wa ufunguzi wa mkutano wa Wakuu wa Vyuo vya Afya vya Serikali, uliofanyika jijini Dodoma.

 Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. Zainab Chaula akiteta jambo na Mkurugenzi wa Mafunzo Wizara ya Afya Dkt Laizer wakati wa ufunguzi wa mkutano wa Wakuu wa Vyuo vya Afya vya Serikali, uliofanyika jijini Dodoma.

Baadhi Wakuu wa Vyuo vya Afya vya Serikali wakifuatilia kwa makini maelekezo kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya Dkt. Zainab Chaula wakati alipofungua Mkutano wa Wakuu wa Vyuo vya Afya vya Serikali uliofanyika Jijini Dodoma.

Jopo la Wakuu wa Vyuo na Makaimu Wakuu wa vyuo vya Afya vya Serikali wakifuatilia maelekezo kutoka kwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Dkt Zainab Chaula wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa Wakuu  wa vyuo vya Serikali uliofanyika Jijini Dodoma.


Na WAMJW- DOM

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Zainab Chaula amefungua Mkutano wa Wakuu wa Vyuo vya Afya vya Serikali uliofanyika Jijini Dodoma. 

Katika Mkutano huo Dkt. Zainab Chaula amewataka Wakuu wa vyuo kuongeza ubunifu katika utoaji huduma kwenye taasisi zao na kuboresha miundombinu jambo litakalosaidia kuinua kiwango cha elimu katika maeneo yao.

Kwa upande mwingine, Dkt. Chaula amewataka Wakuu hao wa vyuo vya Afya kuondoa dhana ya kuitegemea Serikali katika kila jambo ili kuwaletea Maendeleo, huku akisisitiza uanzishwaji wa vitega uchumi katika vyuo hivo jambo litalosaidia kupambana dhidi ya ukata wa fedha.

Aidha, Dkt Zainab Chaula amekemea vitendo vya uvunjaji wa maadili vinavyofanywa na baadhi ya Wakuu wa vyuo ikiwemo suala ya Rushwa, kufelisha wanafunzi, mambo yanayopelekea kutia doa Maendeleo ya taasisi hizo. 

"Mkuu wa Chuo ni kama mzazi, kuna baadhi ya maeneo unakuta Mkuu wa chuo anatongoza wanafunzi, wengine wanafukuzisha wanafunzi, mnaharibu Watoto wa wenzenu, kwa hali hii tutazipata wapi baraka za Mwenyezi Mungu " alisema Dkt Chaula 

Mbali na hayo, Dkt Zainab amewapongeza Wakuu hao wa Vyuo kwa Juhudi wanazoendelea kuchukua katika kuboresha vyuo hivo licha ya changamoto lukuki wanazoendelea kukumbana nazo.

Dkt. Chaula aliendelea kusema kuwa, Serikali inatambua Juhudi kubwa zinazofanywa na Wakuu wa vyuo vya Afya nchini na kuahidi kupokea changamoto zote na kuendelea kutafutia ufumbuzi kadiri inavyowezekana.

Ijumaa, 21 Juni 2019

KAULI YA SERIKALI KUHUSU MLIPUKO WA UGONJWA WA HOMA YA DENGUE NCHIN

- Hakuna maoni




KAULI YA SERIKALI KUHUSU MLIPUKO WA UGONJWA WA HOMA YA DENGUE NCHINI

1.   UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni Na. 49 Ibara ya (1), (2) na (3) ya Kanuni za Kudumu za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Toleo la Mwaka 2016, naomba kutoa Kauli ya Serikali kuhusu mlipuko wa Homa ya Dengue nchini.

Mheshimiwa Spika, ugonjwa wa Dengue sio ugonjwa mpya. Ugonjwa huu ulianza kutolewa taarifa hapa nchini tangu mwaka 2010, na kutolewa tena mwaka 2013, 2014, 2018 na mwaka huu (2019). Kidunia inakadiriwa watu milioni 390 huugua ugonjwa wa homa ya Dengue kila mwaka huku vifo vitokanavyo na ugonjwa huo vikiwa 40,000 kwa mwaka ikilinganishwa na ugonjwa wa Malaria ambapo watu 216 Million huugua ugonjwa huo kwa mwaka huku vifo vikiwa 450,000. Kama ilivyo katika nchi  nyingi duniani zinazoathirika na mlipuko wa ugonjwa huu, mara nyingi hutokea nyakati za mvua hasa katika maeneo ya mijini ambayo kuna mazalia mengi ya mbu kutokana na kutuwama kwa maji. Ugonjwa huu huenezwa na mbu aina ya Aedes ambae ni mbu mweusi mwenye madoadoa meupe ya kung’aa na ambaye hupendelea kuuma hasa wakati wa asubuhi, mchana na jioni.

Mheshimiwa Spika, dalili za ugonjwa huu ni pamoja na homa ya ghafla, kuumwa na kichwa hususan sehemu za macho, maumivu ya viungo na uchovu. Dalili hizi huanza kujitokeza kati siku ya 3 hadi 14 tangu mtu alipoambukizwa virusi vya homa ya Dengue. Wakati mwingine dalili za ugonjwa huu zinaweza kufanana sana na dalili za ugonjwa wa Malaria. Aidha, mara chache hutokea mgonjwa wa homa ya Dengue, anapata vipele vidogovidogo, anavilia damu kwenye ngozi na wengine kutokwa na damu sehemu za fizi, mdomoni, puani, kwenye macho na pia kwenye njia ya haja kubwa au ndogo. 

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2019, ugonjwa huu umeanza kutolewa taarifa katika vituo vya kutolea huduma za Afya hapa nchini kuanzia mwezi Januari hadi tarehe 19 Juni 2019  jumla ya wagonjwa 4,320 na vifo 4 vilivyotokana na  homa ya Dengue vimetolewa taarifa huku Mkoa wa Dar es salaam ndio unaoongoza kuwa na wagonjwa wengi. Ifuatayo ni idadi ya wagonjwa na vifo kwa mikoa: Dar es salaam 4,029 na vifo 3, Dodoma 3 na kifo 1, Tanga 207 na vifo 0, Pwani 57 na vifo 0, Morogoro 16 na vifo 0, Arusha 3 na vifo 0, Singida 2 na vifo 0, na Kagera 2  na vifo 0. Aidha vifo vilivyotolewa taarifa  ni kutoka  katika hospitali za;   Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma -1, Hindu-Mandal -1 na Hospitali ya  Regency-2.

2.   HATUA ZILIZOCHUKULIWA NA SERIKALI KUDHIBITI UGONJWA HUU
Mheshimiwa Spika, toka kuripotiwa kwa mlipuko wa Dengue, Wizara imeendelea kuimarisha mikakati ya kudhibiti ugonjwa huu, kwanza kwa kuandaa mpango wa dharura wa miezi sita (Mei-Oktoba, 2019) wa kukabiliana na ugonjwa wa Denguenchini. Katika mpango huu yafuatayo yanatekelezwa;
(i)           Kuangamiza mazalia ya mbu wapevu (Adults mosquitoes ) na viluwiluwi nchini ambapo Wizara imeshanunua kiasi cha lita 60,000 za Viuavidudu (biolarvicides) kutoka kwenye kiwanda cha uzalishaji kilichopo Kibaha kwa ajili ya kuangamiza viluwiluwi katika mazalia ya mbu. Kati ya hizi Lita 11,400 zimesambazwa kwenye Halmashauri 5 za mkoa wa Dar es Salaam. Lita 48,600 zinasambazwa kwenye Halmashauri za Mikoa ya Geita (lita 8,092), Kagera (Lita 12,308), Kigoma (7,616), Lindi (9,048) na Mtwara (Lita 11,536). Pia lita zingine 36,000 zimeagizwa ambapo zitasambazwa kwenye Mikoa yenye Mlipuko wa Ugonjwa huu ikwemo Pwani, Morogoro Tanga na Singida. Aidha Wizara imeagiza pia mashine kubwa 6 kwa ajili ya kupulizia mbu wapevu (aina ya Fogging machine) na mashine hizi zinatarajiwa kufika kabla ya mwisho wa mwezi Julai, 2019. Dawa za kunyunyizia nje (aina ya Acteric) lita 2,000 kwa ajili ya kuua mbu wapevu pia zimeagizwa ambazo zitasambazwa katika Mikoa ya Dar es salaam, Pwani na Tanga.
(ii)         Kuunda kikosi kazi cha watalaam cha kushughulikia udhibiti  wa mbu wanaoeneza ugonjwa wa Dengue na Malaria nchini na inategemewa kuwa kikosi kazi hiki kitaimarisha jitihada za udhibiti mbu ndani  ya Mikoa na Halmashauri zote nchini hususan zenye kiwango kikubwa cha maambukizi ya Dengue na Malaria yaani Dar es salaam, Tanga, Pwani, Morogoro, Lindi, Mtwara, Kigoma, Geita na Kagera.
(iii)       Katika kuimarisha uchunguzi na matibabu ya ugonjwa wa Homa ya Dengue, Bohari ya Dawa imeshanunua  vipimo 30,000 vya kupima Homa ya Dengue na awali Wizara ilielekeza Vituo vya umma vya kutolea huduma kutoa huduma ya vipimo vya Dengue kwa utaratibu wa kawaida wa uchangiaji wa gharama za matibabu.

(iv)       Kutengeneza na Kusambaza Mwongozo wa matibabu ya ugonjwa huu kwa ajili ya watoa huduma katika vituo vya kutolea huduma
(v)         Kuimarisha ufuatiliaji wa magonjwa nchi nzima kwa kutumia mfumo uliopo wa ukusanyaji wa taarifa, ambapo tunaendelea kupata taarifa za kila siku juu ya mwenendo wa ugonjwa huu na magonjwa mengine.
(vi)       Kutoa elimu kwa jamii kupitia vyombo vya habari pamoja na ujumbe kwa njia ya mitandao ya kijamii.
Mheshimiwa Spika, kupitia hatua hizi, takwimu za hali ya maambukizi ya ugonjwa wa Dengue zinaonyesha kuwa maambukizi mapya yameanza kupungua kutoka wagonjwa 2494 wa mwezi Mei 2019 hadi wagonjwa 813 kufikia tarehe 19 Juni, 2019.


3.   CHANGAMOTO YA UDHIBITI WA UGONJWA WA HOMA YA DENGUE
Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto mbalimbali katika kudhibiti mlipuko wa Homa ya Dengue nchini. Changamoto hizi  ni pamoja na:
1.   Gharama za kupima Ugonjwa Homa ya Dengue
Ingawa Serikali kupitia Bohari ya Dawa imenunua vipimo moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji na hivyo kuviuza kwa bei nafuu ukilinganisha na gharama inayotozwa kutoka kwenye baadhi ya Hospitali binafsi, bado Wananchi wanashindwa kumudu gharama za uchangiaji matibabu ya ugonjwa wa Homa Dengue

2.   Ushirikishwaji wa Jamii
Jamii bado haijaweza kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa kampeni ya usafi wa mazingira ambayo ni njia kuu ya kudhibiti mazalia ya mbu
3.   Matibabu ya Ugonjwa huu katika vituo vya kutolea huduma
Watoa huduma za Afya kutokufuata kikamilifu miongozo ya matibabu ya ugonjwa wa Homa ya Dengue

4.HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, napenda kulitaarifu Bunge lako tukufu kuwa Wizara imepitia  Miongozo na Kanuni za Kimataifa, ambayo pia ipo katika Sheria  ya Afya ya Jamii  namba 1. ya mwaka 2009 kuweza kupata mwongozo wa namna bora ya utoaji wa matibabu kwa mlipuko wa ugonjwa wa Dengue ambao upo sasa nchini. Kupitia sheria hii, vipo vipengele mbalimbali ambavyo vimeanisha jinsi gani matibabu ya magonjwa ya milipuko mikubwa kama ya Homa ya Dengue inapaswa kutolewa na hii ikiwemo utoaji wa matibabu bure ili  kurahisisha udhibiti wa magonjwa ya milipuko  yasisambae kwa haraka katika jamii.

Mheshimiwa Spika,  kwa kuzingatia sheria hii, Serikali ya Awamu ya tano chini ya Mhe Rais, Dkt John Pombe Magufuli, inayojali wananchi wake, sasa imeamua kuwa vipimo kwa ajili ya Homa ya Dengue vitatolewa  BURE kwenye vituo vya kutolea huduma za Afya vya umma wakati huu wa mlipuko.Aidha, Serikali itaboresha matibabu kwa wagonjwa kwa kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa dawa za kutosha na pia itaendelea kuwajengea uwezo wataalam wa  Afya sambamba na kuboresha mifumo ya ukusanyaji takwimu.

Mheshimiwa Spika,  ili kuhakikisha kuwa tunadhibiti  ugonjwa huu nchini, ninaitaka Mikoa na Halmashauri zote nchini hasa zenye kiwango kikubwa cha maambukizi ya Dengue na Malaria kusimamia kikamilifu kampeni za usafi wa mazingira na kuangamiza mbu kwa kunyunyizia dawa kwa ajili ya kuuwa mbu wapevu na kutokomeza mazalia ya mbu. Aidha natoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na Serikali katika kudhibiti ugonjwa huu kwa kuchukuwa hatua stahiki za kujikinga na ugonjwa huu na kuimarisha usafi wa mazingira na kuangamiza mazalia ya mbu.



UMMY A. MWALIMU
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII,
 JINSIA, WAZEE NA WATOTO

21/06/2019

SERIKALI YAAGIZA KILA KIFO KINACHOTOKEA KUFANYIWA UFUATILIAJI

- Hakuna maoni
Mkurugenzi wa Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi akisisitiza jambo mbele ya 
Wasimamizi wa huduma za Afya katika jiji la Dar es Salaam (RHMT) wakati alipokutana na  kujadiliana mbinu mbali mbali ili kuweza kukabiliana na magonjwa ya mlipuko, hususan magonjwa ya Dengue na Kipindupindu.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt Yudas Ndungile akiyoa maelezo kuhusu hali ya Afya na jitihada za mkoa katika kukabiliana na changamoto za magonjwa ya mlipuko wakati wa kikao cha Mkurugenzi wa Kinga Wizara ya (Wakulia) na wasimamizi wa huduma za Afya katika jiji la Dar es Salaam.

Baadhi ya Wasimamizi wa huduma za Afya katika jiji la Dar es Salaam, wakifuatilia kwa makini maelekezo kutoka Mkurugenzi wa Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi wakati alipokutana na  kujadiliana mbinu mbali mbali ili kuweza kukabiliana na magonjwa ya mlipuko, hususan magonjwa ya Dengue na Kipindupindu.

Mkurugenzi wa Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi (aliyevaa suti) akieleza jambo mbele ya Wasimamizi wa huduma za Afya katika jiji la Dar es Salaam (RHMT) wakati alipokutana na  kujadiliana mbinu mbali mbali ili kuweza kukabiliana na magonjwa ya mlipuko, hususan magonjwa ya Dengue na Kipindupindu.


SERIKALI YAAGIZA KILA KIFO KINACHOTOKEA KUFANYIWA UFUATILIAJI

Na WAMJW- DSM 

Serikali imeagiza Waganga Wakuu wote kuhakikisha wanafanya ufuatiliaji wa kila kifo kitakachotokea katika Hospitali zote nchini ili kubaini chanzo cha vifo hivo jambo litalosaidia kuimarisha mikakati katika kupambana na magonjwa, hususan magonjwa ya milipuko. 

hayo yamesemwa na Mkurugenzi wa Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi leo wakati alipokutana na wasimamizi wa huduma za Afya katika jiji la Dar es Salaam (RHMT) kujadiliana mbinu mbali mbali ili kuweza kukabiliana na magonjwa ya mlipuko, hususan katika kipindi hichi cha milipuko ya magonjwa ya Dengue na Kipindupindu. 

Dkt. Subi amesema kuwa katika vita dhidi ya magonjwa ya mlipuko ni lazima kushirikiana na taasisi nyingine kama vile DAWASA ili kuhakikisha upatikanaji wa maji safi na salama kwa kurekebisha na kuimarisha miundombinu ya maji ambayo yanaweza kuwa moja ya chanzo cha mlipuko wa magonjwa hayo. 

Pia, Dkt Subi amesema kuwa moja ya makubaliano ya kikao hicho ni kuhakikisha inapofika Juni 30, ugonjwa wa Dengue uwe umekwisha katika jiji la Dar es Salaam.

"Wamenihakikishia kwamba inapofika tarehe 30, wamesema mbinu zote inatumika kuhakikisha ugonjwa wa homa ya Dengue unaisha jijini Dar es Salaam au unapungua kwa kiwango ambacho hautoonekana" alisema Dkt Leonard Subi. 

Aidha, Dkt Subi amemwagiza Mganga Mkuu kuhakikisha wanatumia taarifa zote za wagonjwa ambao wanafariki kutoka na magonjwa ya Kipindupindu pamoja na ugonjwa wa homa ya Dengue ili kupata takwimu sahihi ya vifo vinavyosababishwa na magonjwa hayo.

Aliendelea kusema kuwa Serikali imefanikiwa kupambana dhidi ya ugonjwa wa Kipindupindu, huku ikifanikiwa kupunguza maambukizi ya homa ya Dengue kutoka wagonjwa 1000 kwa mpaka kufikia wagonjwa 200 kwa wiki, na jitihada zinaendelea kuchukuliwa ili kuutokomeza kabisa ugonjwa huu.

Mbali na hayo Dkt. Subi alisisitiza kuwa katika mapambano dhidi ya mbu anaesababisha homa ya ugonjwa wa Dengue ni lazima kushirikisha wananchi katika ngazi ya Jamii ili kutoa elimu ya kutosha juu ya namna yakuzuia ugonjwa huu.

Kwa upande mwingine, Dkt. Subi amemwagiza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kuhakikisha anashirikiana na Wakurugenzi ili kutimiza ahadi za kununua mashine za kunyunyizia maazalia ya mbu ambao wanasababisha ugonjwa wa Dengue. 

Hata hivyo, Dkt Subi ameagiza watu wote wanaobainika kutapisha maji machafu katika mazingira kuchukuliwa hatua kali kupitia sheria ya Afya ya jamii ya mwaka 2009.

Nae Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Yudas Ndungile amemshukuru Mkurugenzi wa Kinga kutoka Wizara ya Afya, Dkt Leonard Subi kwa muda aliotenga ili kufahamu kiundani hali ya utendaji kazi katika Sekta ya Afya katika ngazi ya mkoa na ameahidi kutekeleza maagizo yote ili kuendelea kuimarisha Sekta ya Afya.

Mwisho.

Jumatano, 19 Juni 2019

PAMBA ZA KUTOA UCHAFU MASIKIONI ZATAJWA KUSABABISHA MATATIZO YA USIKIVU

- Hakuna maoni
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu akifafanua jambo kutoka kwenye kitabu cha Mpango Mkakati wa Masuala ya Masikio na Usikivu leo Jijini kabla ya kuzindua mpango huo.

Dkt. Bill Austin (kulia) kutoka Taasisi ya Starkey Hearing Foundation akifafanua jambo wakati wa uzinduzi wa Mpango Mkakati wa Masuala ya Masikio na Usikivu leo Jijini Dodoma aliye kushoto ni  mke wake Dkt. Tani Austin.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (katikati) akitazama mtoto Ahmed Said akiwekewa vifaa vya usikivu toka kwa Dkt. Tani Austin wakati wa uzinduzi wa Mpango Mkakati wa Taifa wa Masuala ya Masikio na Usikivu leo Jijini Dodoma.


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (wa pili kutoka kushoto) akizindua rasmi Mpango Mkakati wa Masuala ya Masikio na Usikivu akiwa pamoja na Bwana na Bibi Bill Austin (waliovaa makoti meupe) kutoka Taasisi ya Starkey Hearing Foundation, kutoka kushoto ni Dkt. Grace Maghembe Mkurugenzi wa Tiba kutoka Wizara ya Afya na Daktari Bingwa wa Masikio na Usikivu Dkt Edwin Liyombo (wa pili kutoka kulia)

Wananchi waliojitokeza kupata matibabu ya masikio katika kliniki inayoendeshwa na Taasisi ya Starkey Hearing Foundation leo Jijini Dodoma.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu (kushoto) akifuatilia mtaalam wakati akifunga vifaa vya usikivu kwa mtoto Monica Denis kabla ya kuzindua Mpango Mkakati wa Taifa wa Masuala ya Masikio na Usikivu Jijini Dodoma.


NA WAJMW-DODOMA

Imeelezwa kuwa vijiti na pamba za kusafisha masikio zinasababisha kwa kiasi kikubwa magonjwa ya usikivu yanayopelekea kuwa kiziwi.

Hayo yamebainika leo wakati wataalamu wa afya ya masikio na usikivu kutoka taasisi ya Starkey Foundation for Ear and Healing Care walipomweleza Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakati alipotembelea mabanda ya utoaji wa huduma za masikio na usikivu kwa wananchi mbalimbali jijini Dodoma.

Kufuatia hatua hiyo, Waziri Ummy amewataka wananchi kulinda masikio yao kwa kufuata ushauri wa madaktari na kuacha tabia ya kutumia vifaa vinavyosababisha matatizo ya usikivu kama spika za masikioni na matumizi ya pamba za kutolea uchafu.

“Tatizo la usikivu ni kubwa katika nchi yetu, katika tafiti ndogo ndogo ambazo zimefanyika zinaonesha asilimia 3 ya wanafunzi ambao wako shuleni wana matatizo ya usikivu kwa kiwango fulani lakini pia takwimu zinaonesha kuwa kila watu 100 wenye magonjwa yasiyo ya kuambukiza, 24 kati yao wanakua na matatizo ya usikivu”. Amesema Waziri Ummy.

Aidha, Waziri ummy amesema tafiti zinaonesha pia waathirika wengine wenye matatizo ya usikivu ni wale wanaofanya kazi katika migodi na viwandani hasa viwanda vya nguo ambapo takwimu zinaonyesha asilimia 50 wanakua na matatizo hayo.

Waziri Ummy ameishukuru taasisi ya Starkey Foundation for Ear and Healing Care kwa kutoa huduma za masikio na usikivu nchini huku akisema Serikali imeweka mikakati ya kuimarisha miundombinu, kununua vifaa na kuongeza wataalamu wa huduma za masikio na usikivu, kutoka wataalamu bingwa 11 mwaka 2009 mpaka kufikia wataalamu 46 mwaka 2018.

Hata hivyo Waziri Ummy amesema toka kuanzishwa kwa huduma hizi nchini kumesaidia kuokoa kupunguza idadi ya watoto kupelekwa India, ambapo kila mwaka takribani watoto 13 walikua wanapelekwa India kupata matibabu na mtoto mmoja alikua anagharimu Tsh. Milioni 80 mpaka Milioni 100. Lakini kuanzishwa kwa huduma hizi katika Hospitali ya Muhimbili mwaka 2017, watoto takribani 26 wamepata huduma kwa gharama ya Tsh. Milioni 35 na kuokoa fedha za Serikali kwa zaidi ya asilimia 60.

Kwa upande wake muanzilishi wa taasisi ya Starkey Foundation for Ear and Healing Care Dkt. Bill Austin ameishukuru Serikali ya Tanzania kwa kutoa ushirikiano kwa taasisi hiyo kuendelea kutoa huduma na vifaa vya masikio na usikivu kwa wananchi ambapo ilianza kutoa huduma hizo Jijini Mwanza na kuendelea kutoa huduma Jijini Dodoma.

MWISHO

Jumatatu, 17 Juni 2019

SERIKALI YAENDELEA KUSOGEZA HUDUMA ZA FIGO KWA WANANCHI

- Hakuna maoni
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Faustine Ndugulile akimshukuru Naibu Balozi wa Saudi Arabia baada ya makabidhiano ya mashine 62 za kusafishia damu kwa wagonjwa wa figo, tukio limefanyika leo katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Afya Dkt Faustine Ndugulile akisaini mkataba wa makabidhiano wa mashine 62  za kusafishia damu kwa wagonjwa wa figo zenye thamani ya shilingi Bilion 1.55 zilizotolewa na kituo cha King Salman  Humanitarian and Relief kwa ushirikiano na Naibu Balozi wa Saudi Arabia Bw. Ahmed Bin Saleh Alghamdi, tukio  limefanyika katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es Salaam.

Naibu Balozi wa Saudi Arabia nchini Bw. Ahmed Bin Saleh Alghamdi akisaini mkataba wa makabidhiano wa mashine 62  za kusafishia damu kwa wagonjwa wa figo zenye thamani ya shilingi Bilion 1.55 zilizopokelewa Leo na Naibu Waziri wa Afya Dkt Faustine Ndugulile katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Afya Dkt Faustine Ndugulile akiteta jambo na Naibu Balozi wa Saudi Arabia Bw. Ahmed Bin Saleh Alghamdi wakati wa makabidhiano wa mashine 62  za kusafishia damu kwa wagonjwa wa figo zilizotolewa na kituo cha King Salman  Humanitarian and Relief, tukio  limefanyika katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya mashine za kusafishia damu kwa wagonjwa wa figo zilizotolewa na kituo cha King Salman Humanitarian Aid and Relief kwa kuongozwa na ubalozi wa Saudia Arabia nchini, zilizopokelewa leo na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Faustine Ndugulile katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es Salaam.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Faustine Ndugulile akisisitiza jambo mbele ya Waandishi wa habari (hawapo kwenye picha) wakati wa tukio la kupokea mashine 62  zakusafishia damu kwa wagonjwa wa figo, tukio limefanyika leo katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es Salaam.


SERIKALI YAENDELEA KUSOGEZA HUDUMA ZA FIGO KWA WANANCHI 

Na WAMJW- DSM 

SERIKALI kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto yaendelea kusogeza huduma za matibabu ya figo kwa kupokea jumla ya mashine 62 za kusafishia damu kwa wagonjwa wa figo na kuzisambaza katika Hospitali za Rufaa za mikoa nchini.

Hayo yamejiri mapema leo katika tukio la kupokea mashine hizo kutoka kwa kituo cha King Salman Humanitarian Aid and Relief wakiongozwa na ubalozi wa Saudia Arabia nchini zenye jumla ya shilingi Bilion 1.55, lililoongozwa na Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es Salaam.

Dkt Ndugulile amesema kuwa Serikali inaendelea kusambaza na kuboresha huduma hizi na kwa sasa zinapatikana katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Hospitali ya Rufaa Mbeya, Hospitali ya Bugando, Hospitali ya KCMC na baadhi ya Hospitali binafsi.

"Sisi kama Serikali tumeendelea kuboresha hizi huduma, kwa sasahivi zinapatikana Muhimbili, Hospitali ya Rufaa Mbeya, Hospitali ya Bugando, Hospitali ya KCMC na baadhi ya Hospitali binafsi" alisema   Dkt. Ndugulile 

Aliendelea kusema kuwa, Serikali inaendelea kuboresha huduma hizi licha ya kuwepo changamoto ya idadi kubwa ya wahitaji wa huduma hizi huku akidai kuwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kuna mashine 42 huku zikifanyika sesheni tatu kwa siku, na zinafanyika kwa siku 6 katika kila wiki, 

Aidha, Dkt Ndugulile amesema kuwa, msaada huo wa vifaa vitavyosambazwa katika mikoa tisa nchini ikiweko mikoa ya Tanga, Mwanza, Kigoma, Kagera, Arusha, Iringa, Mtwara, Unguja na Zanzibar, hali itayosaidia kupunguza gharama kwa kuwasogezea wagonjwa huduma hizo.

Mbali na hayo, Dkt. Ndugulile amesema kuwa ndani ya miaka mitatu Serikali imefanikiwa kupunguza magonjwa yakuambukiza kwa asilimia 50%, huku akikiri kuwa bado kuna changamoto kubwa katika kukabiliana na magonjwa yasiyo yakuambukiza kama vile kisukari, presha na figo ambayo kwa kiasi kikubwa yanatokana na mitindo ya maisha.

"Timepiga hatua kubwa sana katika magonjwa yakuambukiza, ambayo tumeyapunguza kwa asilimia 50% ndani ya miaka mitatu, tumepunguza vifo na maambukizi ya Malaria, lakini tumepunguza vile vile maambukizi ya Ukimwi, sasa changamoto inayotukabili ni magonjwa yasiyo yakuambukiza kama, kisukari, presha na magonjwa ya figo"alisema Dkt Ndugulile. 

Akiongea kwa niaba ya kituo cha King Salman Humanitarian Aid and Relief Naibu Balozi wa Saudia Arabia nchini Ahmed Bin Saleh Alghamdi ameipongeza Serikali kupitia Wizara ya Afya kwa jitihada inayoendelea kuchukua katika kutatua changamoto kwenye Sekta ya Afya na ameahidi kuendeleza ushirikiano huo baina ya nchi hizo mbili.

Mwisho.

Ijumaa, 14 Juni 2019

SERIKALI KUONGEZA IDADI VITUO VYA UCHANGIAJI DAMU SALAMA

- Hakuna maoni

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu pamoja na viongozi wa kutoka Wizara ya Afya wakiongea na moja kati ya watu waliojitokeza kuchangia damu, katika Maadhimisho ya Siku ya Wachangia Damu Duniani yaliyofanyika  kitaifa jijini Mwanza, viwanja vya Furahisha.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu akibadilishana mawazo na Mkurugenzi mtendaji wa EMEA Bw. Helmut Butterweck wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wachangia Damu Duniani yaliyofanyika  kitaifa jijini Mwanza, viwanja vya Furahisha.

Baadhi ya picha za Kikundi cha Wasanii wa filamu Tanzania wakionesha igizo kuhusu uhamasishaji kwa jamii juu ya umuhimu wa kuchangia damu, tukio limefanyika kitaifa jijini Mwanza katika viwanja vya Furahisha.

Mashine kubwa zenye gharama inayokadiriwa kuwa dola za kimarekani 600,000 (laki sita) kila moja ambayo ni sawa fedha za Kitanzania bilioni 1.4, zilizozinduliwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu katika Maadhimisho ya Siku ya Wachangia Damu Duniani yaliyofanyika  kitaifa jijini Mwanza, viwanja vya Furahisha.


SERIKALI KUONGEZA IDADI VITUO VYA UCHANGIAJI DAMU SALAMA

Na.WAMJW - Mwanza

SERIKALI kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imetenga Sh. bilioni tano katika mwaka wa fedha 2019/20 zitakazotumika kujenga vituo vidogo vya uchangiaji damu salama katika mikoa 12 nchini.

Hayo yameelezwa leo na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alipozungumza katika Maadhimisho ya Siku ya Wachangia Damu Duniani yaliyofanyika  kitaifa jijini Mwanza, viwanja vya Furahisha.

Sambamba na hilo, Waziri Ummy amezindua mashine mpya ‘full automation’ za kupima maambukizi katika damu na za kupima makundi  ya damu ambapo mashine 24 zimesimikwa kwenye vituo vya kanda sita ikiwamo Dar es Salaam, Mwanza, Tabora, Kilimanjaro, Mtwara na Mbeya.

Amesema kila kituo kimesimikwa mashine nne ikiwa mbili ni za kupima magonjwa yanayoambukizwa kupitia damu na mbili ni za kupima makundi ya damu.

Amesema hatua hiyo imelenga kuimarisha huduma ya uchangiaji damu salama pamoja na kuwezesha kusogeza karibu zaidi huduma za kuongezewa damu salama wagonjwa wenye uhitaji.

“Hadi sasa kuna vituo vidogo vya damu salama nane ambavyo vimeanzishwa Mkoa wa Dar es Salaam, Morogoro, Dodoma, Iringa, Kigoma, Shinyanga, Simiyu, Tabora na Mara.

“Katika mwaka wa fedha 2019/20, tunategemea kujenga vituo vya damu salama katika mikoa 12, imetengwa Sh. bilioni tano, hivi karibuni ujenzi utaanza,” amesema.

Amesema kadri huduma za matibabu ya kibingwa zinavyoboreshwa ikiwamo ya moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete, upandikizaji figo na upasuaji mwengine Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI), Hospitali ya Taifa Muhimbili na Mloganzila, zimepanua wigo wa mahitaji ya upatikanaji wa damu salama.

“Jitihada zinafanyika ili kuongeza wigo wa upatikanaji wa damu salama, kauli mbiu ya mwaka huu inasema ‘Damu Salama kwa Wote’ ni kwa sababu mkutano mkuu wa WHO mwaka huu ulihusu afya kwa wote.

“Tunataka kumfikia kila mtanzania mwenye mahitaji ya damu salama popote alipo tuhakikishe anapata damu salama bila kikwazo chochote. WHO inakadiria katika kila idadi ya watu 1000 zipatikane chupa 10 za damu, Watanzania tunakadiriwa tupo milioni 55 tunapaswa kupata asilimia moja ya idadi hiyo, hivyo chupa 550,000 zinahitajika kila mwaka kutosheleza mahitaji,” amesema.

Akitoa ulinganisho amesema mwaka 2016 zilikusanywa chupa 196,000, mwaka 2017 chupa 233,000 na 2018 idadi imeongezeka kufikia chupa 307,000.

“Kumekuwa na ongezeko la ukusanyaji damu, katika chupa 10 zinazohitajika kupatikana angalau tunapata chupa sita, hivyo nawasihi watanzania wote kujenga utamaduni wa kuchangia damu mara kwa mara ili tuweze kupata inayotosheleza,” amesema.

Aidha, amewataka waganga wakuu wa mikoa na wilaya kuhakikisha wanatekeleza agizo alilowapa la kuandaa kambi za wazi kwa ajili ya uchangiaji damu angalau mara tatu kila mwaka na watenge fedha katika bajeti zao kuwezesha ukusanyaji damu salama.

Awali akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mkuu wa Wilaya ya Ilemela, Steven Lalika amesema walipewa lengo la kukusanya chupa 2000, katika wiki ya uhamasishaji wamefanikiwa kukusanya chupa 3705 kufikia Juni 13 na kwamba lengo la mkoa walikusudia kukusanya chupa 4000.

MWISHO

Jumatano, 12 Juni 2019

MASHINDANO YA TAIFA YA AFYA NA USAFI WA MAZINGIRA YAZINDULIWA JIJINI DODOMA

- Hakuna maoni

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) wakati akitoa taarifa ya uzinduzi wa mashindano ya Afya na usafi wa mazingira mapema leo jijini Dodoma.
Kaimu Mkurugenzi wa kinga Dkt. Khalid Massa (kulia)  akifafanua jambo kuhusiana na mashindano ya taifa ya afya na usafi wa mazingira katika mkutano wa waandishi wa habari uliofanyika jijini Dodoma leo. Kushoto ni Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile




MASHINDANO YA TAIFA YA AFYA NA USAFI WA MAZINGIRA YAZINDULIWA JIJINI DODOMA

NA WAJMW-DODOMA

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imezindua mashindano ya taifa ya afya na usafi wa mazingira yatakayoratibiwa nchi nzima.

Akizungumza mbele ya waandishi wa habari katika ukumbi wa bunge jijini Dodoma, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile amesema lengo la mashindano hayo ni kuinua hali ya afya na usafi wa mazingira katika ngazi ya kaya na taasisi ili kulinda na kuboresha afya ya jamii.

“Mashindano haya yalianza mwaka 1988 ambapo yamekuwa yakifanyika kila mwaka. Kupitia mashindano haya hali ya usafi wa mazingira imeendelea kuimarika mwaka hadi mwaka na kusaidia kupunguza magonjwa ya kuhara kutoka zaidi ya wagonjwa 1,300,000 mwaka 2014 hadi chini ya wagonjwa 70,000 mwaka 2018”. Amesema Dkt. Ndugulile.

Aidha, Naibu Waziri huyo amesema mashindano hayo yamesaidia ujenzi wa madampo ya kisasa katika mikoa ya Dodoma, Mbeya, Arusha, Kigoma na Mtwara. Pia ujenzi wa machinjio ya kisasa katika miji mbalimbali  umeweza kutekelezwa na mashindano.

Dkt. Ndugulile ameongeza kuwa mashindano hayo kwa mwaka 2019 yatahusisha Halmashauri zote 184 ambapo Halmashauri zitakazoshinda ngazi ya mkoa zitashindanishwa kitaifa, pia vipengele viwili vimeongezwa katika mashindano ya mwaka huu.

“Ili kuongeza chachu katika mashindano haya, Wizara imeongeza vipengele viwili ambavyo ni ofisi za Makatibu Tawala wa Mikoa na Taasisi za kibenki. Katika Mkoa Benki itakayoshinda itashindanishwa na mikoa mingine ili kupata mshindi wa kitaifa”. Amesema Dkt. Ndugulile.

Mashindano hayo yataendeshwa na kamati ya taifa ya mashindano ya usafi wa mazingira inayojumuisha wajumbe kutoka wizara na taasisi mbalimbali na pia yatakua  na muundo wa makundi 12 ambapo kila kundi litatoa washindi watatu. Makundi hayo ni Halmashauri za majiji na manispaa, Halmashauri za Miji, Halmashauri za Wilaya, Kijiji bora kinachotekeleza kampeni ya usafi wa mazingira, Hospitali za Rufaa za Mikoa, Hospitali za Rufaa za binafsi, Hoteli, Shule za sekondari na msingi, Shule za serikali za sekondari za bweni, Shule za binafsi za sekondari za bweni, Ofisi za umma na Mabenki.

Dkt. Ndugulile amesema Wizara imepanga kutoa zawadi mbalimbali kwa washindi wa makundi ambapo watapatiwa fedha taslimu, vyeti na vikombe. Mshindi wa juu atatokana na kundi la Halmashauri za wilaya na atapata zawadi ya Shilingi Milioni Hamsini.

Hata hivyo, Dkt. Ndugulile ametoa wito kwa Halmashauri zote nchini kuiga mfano wa Halmashauri ya Wilaya ya Njombe ambayo imewezesha kaya zake zote kuwa na vyoo bora. Naibu Waziri amesema usafi wa mazingira na matumizi ya vyoo bora unaweza kupunguza magonjwa ya kuambukiza kwa zaidi ya asilimia 80 na hivyo kuipunguzia serikali gharama za kununua madawa na kupambana na magonjwa ya milipuko.

MWISHO