Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Ijumaa, 21 Juni 2019

KAULI YA SERIKALI KUHUSU MLIPUKO WA UGONJWA WA HOMA YA DENGUE NCHIN





KAULI YA SERIKALI KUHUSU MLIPUKO WA UGONJWA WA HOMA YA DENGUE NCHINI

1.   UTANGULIZI
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni Na. 49 Ibara ya (1), (2) na (3) ya Kanuni za Kudumu za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Toleo la Mwaka 2016, naomba kutoa Kauli ya Serikali kuhusu mlipuko wa Homa ya Dengue nchini.

Mheshimiwa Spika, ugonjwa wa Dengue sio ugonjwa mpya. Ugonjwa huu ulianza kutolewa taarifa hapa nchini tangu mwaka 2010, na kutolewa tena mwaka 2013, 2014, 2018 na mwaka huu (2019). Kidunia inakadiriwa watu milioni 390 huugua ugonjwa wa homa ya Dengue kila mwaka huku vifo vitokanavyo na ugonjwa huo vikiwa 40,000 kwa mwaka ikilinganishwa na ugonjwa wa Malaria ambapo watu 216 Million huugua ugonjwa huo kwa mwaka huku vifo vikiwa 450,000. Kama ilivyo katika nchi  nyingi duniani zinazoathirika na mlipuko wa ugonjwa huu, mara nyingi hutokea nyakati za mvua hasa katika maeneo ya mijini ambayo kuna mazalia mengi ya mbu kutokana na kutuwama kwa maji. Ugonjwa huu huenezwa na mbu aina ya Aedes ambae ni mbu mweusi mwenye madoadoa meupe ya kung’aa na ambaye hupendelea kuuma hasa wakati wa asubuhi, mchana na jioni.

Mheshimiwa Spika, dalili za ugonjwa huu ni pamoja na homa ya ghafla, kuumwa na kichwa hususan sehemu za macho, maumivu ya viungo na uchovu. Dalili hizi huanza kujitokeza kati siku ya 3 hadi 14 tangu mtu alipoambukizwa virusi vya homa ya Dengue. Wakati mwingine dalili za ugonjwa huu zinaweza kufanana sana na dalili za ugonjwa wa Malaria. Aidha, mara chache hutokea mgonjwa wa homa ya Dengue, anapata vipele vidogovidogo, anavilia damu kwenye ngozi na wengine kutokwa na damu sehemu za fizi, mdomoni, puani, kwenye macho na pia kwenye njia ya haja kubwa au ndogo. 

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2019, ugonjwa huu umeanza kutolewa taarifa katika vituo vya kutolea huduma za Afya hapa nchini kuanzia mwezi Januari hadi tarehe 19 Juni 2019  jumla ya wagonjwa 4,320 na vifo 4 vilivyotokana na  homa ya Dengue vimetolewa taarifa huku Mkoa wa Dar es salaam ndio unaoongoza kuwa na wagonjwa wengi. Ifuatayo ni idadi ya wagonjwa na vifo kwa mikoa: Dar es salaam 4,029 na vifo 3, Dodoma 3 na kifo 1, Tanga 207 na vifo 0, Pwani 57 na vifo 0, Morogoro 16 na vifo 0, Arusha 3 na vifo 0, Singida 2 na vifo 0, na Kagera 2  na vifo 0. Aidha vifo vilivyotolewa taarifa  ni kutoka  katika hospitali za;   Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma -1, Hindu-Mandal -1 na Hospitali ya  Regency-2.

2.   HATUA ZILIZOCHUKULIWA NA SERIKALI KUDHIBITI UGONJWA HUU
Mheshimiwa Spika, toka kuripotiwa kwa mlipuko wa Dengue, Wizara imeendelea kuimarisha mikakati ya kudhibiti ugonjwa huu, kwanza kwa kuandaa mpango wa dharura wa miezi sita (Mei-Oktoba, 2019) wa kukabiliana na ugonjwa wa Denguenchini. Katika mpango huu yafuatayo yanatekelezwa;
(i)           Kuangamiza mazalia ya mbu wapevu (Adults mosquitoes ) na viluwiluwi nchini ambapo Wizara imeshanunua kiasi cha lita 60,000 za Viuavidudu (biolarvicides) kutoka kwenye kiwanda cha uzalishaji kilichopo Kibaha kwa ajili ya kuangamiza viluwiluwi katika mazalia ya mbu. Kati ya hizi Lita 11,400 zimesambazwa kwenye Halmashauri 5 za mkoa wa Dar es Salaam. Lita 48,600 zinasambazwa kwenye Halmashauri za Mikoa ya Geita (lita 8,092), Kagera (Lita 12,308), Kigoma (7,616), Lindi (9,048) na Mtwara (Lita 11,536). Pia lita zingine 36,000 zimeagizwa ambapo zitasambazwa kwenye Mikoa yenye Mlipuko wa Ugonjwa huu ikwemo Pwani, Morogoro Tanga na Singida. Aidha Wizara imeagiza pia mashine kubwa 6 kwa ajili ya kupulizia mbu wapevu (aina ya Fogging machine) na mashine hizi zinatarajiwa kufika kabla ya mwisho wa mwezi Julai, 2019. Dawa za kunyunyizia nje (aina ya Acteric) lita 2,000 kwa ajili ya kuua mbu wapevu pia zimeagizwa ambazo zitasambazwa katika Mikoa ya Dar es salaam, Pwani na Tanga.
(ii)         Kuunda kikosi kazi cha watalaam cha kushughulikia udhibiti  wa mbu wanaoeneza ugonjwa wa Dengue na Malaria nchini na inategemewa kuwa kikosi kazi hiki kitaimarisha jitihada za udhibiti mbu ndani  ya Mikoa na Halmashauri zote nchini hususan zenye kiwango kikubwa cha maambukizi ya Dengue na Malaria yaani Dar es salaam, Tanga, Pwani, Morogoro, Lindi, Mtwara, Kigoma, Geita na Kagera.
(iii)       Katika kuimarisha uchunguzi na matibabu ya ugonjwa wa Homa ya Dengue, Bohari ya Dawa imeshanunua  vipimo 30,000 vya kupima Homa ya Dengue na awali Wizara ilielekeza Vituo vya umma vya kutolea huduma kutoa huduma ya vipimo vya Dengue kwa utaratibu wa kawaida wa uchangiaji wa gharama za matibabu.

(iv)       Kutengeneza na Kusambaza Mwongozo wa matibabu ya ugonjwa huu kwa ajili ya watoa huduma katika vituo vya kutolea huduma
(v)         Kuimarisha ufuatiliaji wa magonjwa nchi nzima kwa kutumia mfumo uliopo wa ukusanyaji wa taarifa, ambapo tunaendelea kupata taarifa za kila siku juu ya mwenendo wa ugonjwa huu na magonjwa mengine.
(vi)       Kutoa elimu kwa jamii kupitia vyombo vya habari pamoja na ujumbe kwa njia ya mitandao ya kijamii.
Mheshimiwa Spika, kupitia hatua hizi, takwimu za hali ya maambukizi ya ugonjwa wa Dengue zinaonyesha kuwa maambukizi mapya yameanza kupungua kutoka wagonjwa 2494 wa mwezi Mei 2019 hadi wagonjwa 813 kufikia tarehe 19 Juni, 2019.


3.   CHANGAMOTO YA UDHIBITI WA UGONJWA WA HOMA YA DENGUE
Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto mbalimbali katika kudhibiti mlipuko wa Homa ya Dengue nchini. Changamoto hizi  ni pamoja na:
1.   Gharama za kupima Ugonjwa Homa ya Dengue
Ingawa Serikali kupitia Bohari ya Dawa imenunua vipimo moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji na hivyo kuviuza kwa bei nafuu ukilinganisha na gharama inayotozwa kutoka kwenye baadhi ya Hospitali binafsi, bado Wananchi wanashindwa kumudu gharama za uchangiaji matibabu ya ugonjwa wa Homa Dengue

2.   Ushirikishwaji wa Jamii
Jamii bado haijaweza kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa kampeni ya usafi wa mazingira ambayo ni njia kuu ya kudhibiti mazalia ya mbu
3.   Matibabu ya Ugonjwa huu katika vituo vya kutolea huduma
Watoa huduma za Afya kutokufuata kikamilifu miongozo ya matibabu ya ugonjwa wa Homa ya Dengue

4.HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, napenda kulitaarifu Bunge lako tukufu kuwa Wizara imepitia  Miongozo na Kanuni za Kimataifa, ambayo pia ipo katika Sheria  ya Afya ya Jamii  namba 1. ya mwaka 2009 kuweza kupata mwongozo wa namna bora ya utoaji wa matibabu kwa mlipuko wa ugonjwa wa Dengue ambao upo sasa nchini. Kupitia sheria hii, vipo vipengele mbalimbali ambavyo vimeanisha jinsi gani matibabu ya magonjwa ya milipuko mikubwa kama ya Homa ya Dengue inapaswa kutolewa na hii ikiwemo utoaji wa matibabu bure ili  kurahisisha udhibiti wa magonjwa ya milipuko  yasisambae kwa haraka katika jamii.

Mheshimiwa Spika,  kwa kuzingatia sheria hii, Serikali ya Awamu ya tano chini ya Mhe Rais, Dkt John Pombe Magufuli, inayojali wananchi wake, sasa imeamua kuwa vipimo kwa ajili ya Homa ya Dengue vitatolewa  BURE kwenye vituo vya kutolea huduma za Afya vya umma wakati huu wa mlipuko.Aidha, Serikali itaboresha matibabu kwa wagonjwa kwa kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa dawa za kutosha na pia itaendelea kuwajengea uwezo wataalam wa  Afya sambamba na kuboresha mifumo ya ukusanyaji takwimu.

Mheshimiwa Spika,  ili kuhakikisha kuwa tunadhibiti  ugonjwa huu nchini, ninaitaka Mikoa na Halmashauri zote nchini hasa zenye kiwango kikubwa cha maambukizi ya Dengue na Malaria kusimamia kikamilifu kampeni za usafi wa mazingira na kuangamiza mbu kwa kunyunyizia dawa kwa ajili ya kuuwa mbu wapevu na kutokomeza mazalia ya mbu. Aidha natoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na Serikali katika kudhibiti ugonjwa huu kwa kuchukuwa hatua stahiki za kujikinga na ugonjwa huu na kuimarisha usafi wa mazingira na kuangamiza mazalia ya mbu.



UMMY A. MWALIMU
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII,
 JINSIA, WAZEE NA WATOTO

21/06/2019

0 on: "KAULI YA SERIKALI KUHUSU MLIPUKO WA UGONJWA WA HOMA YA DENGUE NCHIN"