Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Habari Picha. Onyesha machapisho yote
Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Habari Picha. Onyesha machapisho yote

Alhamisi, 20 Agosti 2020

HATUNA UHABA WA CHANJO NCHINI- DKT. LEONARD SUBI

- Hakuna maoni

Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto Dkt. Leonard Subi, akisisitiza jambo mbele ya Waandishi wa habari wakati alipofanya ziara katika ghala la chanjo lililopo katika Hospitali ta Rufaa ya Mkoa wa Dodoma-General.


HATUNA UHABA WA CHANJO NCHINI: DKT. LEONARD SUBI

Na. Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesema kuwa, haina upungufu wa chanjo wa aina yeyote hivyo kuwataka wazazi/walezi kuwapeleka watoto wao kuwapatia chanjo katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi wakati alipotembelea ghala ya kuhifadhia chanjo iliyopo hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma kukagua hali ya chanjo katika mkoa huo.

Dkt. Subi amesema kuwa, chanjo zote aina tisa ambazo zinakinga dhidi ya magonjwa kumi na tatu zipo kwenye ghala hilo“tulikua na upungufu wa aina mbili za chanjo nchini kati ya tisa ambazo tumekuwa tukizitoa lakini, sasa hivi chanjo zote zipo, kwani zimeshawasili hapa nchini na usambazaji unaendelea”, amesema Dtk. Subi

Hata hivyo Dkt. Subi amesema kuwa, upungufu huo wa chanjo ulitokea baada ya Dunia kukumbwa na janga la mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19 ambapo anga zote zilifungwa kwani chanjo husafirishwa kwa mnyororo baridi, kwahiyo huitaji usafiri wa anga.

“Tunamshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa kulifungua anga la Tanzania ambapo,  chanjo sasa zimeanza kuingia nchini na hadi sasa mikoa kumi na tatu(13) chanjo hizi zimeshapokelewa kati ya mikoa 26, na mikoa mingine kumi na tatu  ya Tanzania Bara usambazaji unaendelea kupitia Bohari ya Dawa (MSD)”.

Aidha, Dkt. Subi alisema kuwa, usambazaji wa chanjo hizo mbili ambazo wananchi walikua wanazikosa, umeshaanza na watazipata kwa uhakika, huku akielekeza bohari ya dawa nchini (MSD) kuhakikisha chanjo zote  zimefika katika mikoa iliyosalia ya Tanzania Bara ifikapo mwishoni mwa wiki hii.

“Waganga Wakuu wa Mikoa na Halmashauri wote nchini hakikisheni chanjo hizo mnazipeleka kwenye vituo vyetu  vya kutolea huduma za afya na muwajulishe wananchi kwamba chanjo zipo na zinapatikana bila malipo yeyote, wazazi na walezi pelekeni watoto wenu kupata chanjo katika mikoa yenu”Alisisitiza Dkt. Subi.

Kwa upande wa taarifa iliyotolewa na moja ya chombo cha habari hapa nchini kwa kukosekana kwa chanjo ya kuzuia kuhara (Rota) Dkt. Subi alifafanua kuwa, nchi ya Tanzania haijawahi kukosa chanjo hiyo,huku akiweka bayana kuwa, chanjo zilizopungua kwa mwezi mmoja na nusu ni chanjo ya Polio na Surua-Rubella hali iliyosababishwa na mlipuko wa Covid-19 Duniani, huku akisisitiza kuwa serikali imekua ikinunua chanjo hizo kutoka nchi za Ulaya na Asia.

Aliendelea kusema kuwa, Serikali inaendelea kutoa fedha za chanjo, na kuweka wazi kuwa hadi sasa  imetoa zaidi ya  shilingi bilioni 18 kwa ajili ya ununuzi wa chanjo  na kuifanya  Tanzania kuendelea kuwa katika kiwango cha juu cha utoaji wa chanjo kwa zaidi ya asilimia 98 kwa miaka sita mfululizo.

Hata hivyo, Dkt. Subi amesema kuwa, Tanzania haijawahi kupata mgonjwa wa kupooza tangu mwaka 1996, jambo linalotokana na  uwepo wa hali nzuri ya upatikanaji wa chanjo, huku akidai kuwa nchi ya Tanzania tayari imepata cheti cha utambuzi kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) mwaka 2015.

 

MWISHO.

Jumatatu, 3 Agosti 2020

WAUGUZI NA WAKUNGA WATAKIWA KUTUMIA UTAALAMU WAO KWA AJILI YA USTAWI WA TAIFA

- Hakuna maoni




Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto-Idara Kuu Afya Edward Mbanga akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi kwenye ukumbi wa Cathedral jijini Dodoma.

Kaimu Katibu Mkuu, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsai, wazee na Watoto akiongea na viongozi  hao wakati wa kikao cha mafunzo ambapo aliwataka kuweka dhamira na malengo  ya dhati  katika kuboresha maadili katika taaluma ya uuguzi na ukunga.

Muuguzi Mkuu kutoka Ofisi ya Rais-TAMISEMI Charles Kadugushi akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi, Jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Idara ya Uuguzi na Ukunga kutoka Wizara ya Afya Bi. Ziana Sellah akiongea na Wauguzi Wakuu wa Wilaya nchini wakati wa ufunguzi wa kikao kazi cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi, Jijini Dodoma.

Msajili wa Baraz a la Uuguzi na Ukunga Agnes Mtawa akiwasilisha mada wakati wa kikao kazi hicho kinachofanyika jijini Dodoma.

Picha ya pamoja ya mgeni rasmi na wasajili wa mabaraza ya kitaaluma yaliyopo chini ya wizara ya afya.

Mgeni rasmi akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wauguzi wakuu wa Wilaya mara baada ya ufunguzi.


WAUGUZI NA WAKUNGA WATAKIWA KUTUMIA UTAALAMU WAO KWA AJILI YA USTAWI WA TAIFA

Na.Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Wauguzi na Wakunga nchini wametakiwa kutoa huduma kwa kuzingatia miongozo iliyopo wakati wakitoa huduma kwa weledi ili kufikia malengo na matumaini ya wateja kwa ajili ya ustawi wa Taifa.

Rai hiyo imetolewa leo na Kaimu Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto – Idara Kuu ya Afya Bw. Edward Mbanga wakati wa ufunguzi wa  kikao kazi  cha kuwajengea uwezo wa kusimamia maadili na utendaji kazi wauguzi wakuu wa wilaya kinachofanyika jijini Dodoma.

Bw. Mbanga amesema  kuwa wauguzi na wakunga ndio watendaji wakuu katika vituo vya afya kwenye ngazi ya jamii hadi Taifa hivyo uwajibikaji mzuri na utawala bora utaboresha utendaji hali itayosaidia kufikia malengo mbalimbali waliyojiwekea katika ngazi zote.

"Viongozi mnatakiwa kuwa wabunifu, wachapa kazi, wenye nidhamu na mfano bora wa kuigwa katika utekelezaji wa majukumu yenu,kwahiyo  ni lazima msimamie utoaji wa huduma uliyo mzuri na wenye heshima na utu.”Alisema

Aidha, Kaimu Katibu Mkuu huyo aliwakumbusha  washiriki hao kuwa, suala la huduma za uuguzi na ukunga ni suala la  ubinadamu zaidi na kuvaa viatu vya wagonjwa wao.

“Hakuna aliyegongwa muhuri wa kuugua  au kuwa mgonjwa akalazwa ,sisi sote ni wagonjwa watarajiwa kwahiyo kama ambavyo sisi tungependa kuuguzwa vizuri, kijibiwa kwa kauli nzuri basi tuhakikishe tunasimamia maadaili ya kazi”.Alisisitiza Mbanga.

Hatahivyo alisema kuwa, Serikali inawahakikishia itaendelea kufanya kazi pamoja na waauguzi  kwa kutoa miongozo thabiti na kuhakikisha upatikanaji wa nyenzo muhimu katika hospitali na vituo vya kutolea huduma ya afya na kuboresha mazingira ya kazi yaliyo bora na salama.

Aliendelea kusema kuwa, hivi karibuni kumekuwa na malalamko  mbalimbali ya kiutendaji  na kitaaluma kutoka kwa wateja  wanaofika kupata huduma za afya na hivyo kuleta taswira mbaya  kwa taaluma yao na kuonyesha hakuna usimamizi mzuri wa utoaji huduma za uuguzi na ukunga.

“Tungependa  wateja wetu watoe sifa  badala ya malalamiko hivyo kikao hiki mje na mipango ya kuondokana na malalamiko kwani taaluma yenu ni zaidi taaluma." alisema.

Hata hivyo, amewakumbusha  viongozi hao kuwa mstari wa mbele kupambana dhidi  ya rushwa na kuhakikisha inatokomezwa katika maeneo yao ya kazi kwani rushwa imekuwa ikilalamikiwa na kuripotiwa katika kada ya afya nchini.

-MWISHO-

Ijumaa, 17 Julai 2020

PROF. MCHEMBE AWATAKA WAFAMASIA KUSIMAMIA MAADILI

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Prof. Mabula Mchembe akiongea na wafamasia na wadau wa mnyororo wa ugavi na usambazaji wa bidhaa za afya (hawapo pichani) wakati akifungua kikao kinachoendelea mkoani Morogoro.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Prof. Mabula Mchembe akiwa na Mtendaji Mkuu wa Wakala wa ununuzi Serikalini Prof. Geraldine wakifuatilia moja ya mada zilizokua zinawasilishwa katika kikao cha wadau wa mnyororo wa ugavi wa bidhaa za afya nchini.
Mfamasia Mkuu Ndg. Daud Msasi akitolea ufafanuzi moja ya hoja wakati akiwasilisha mada katika kikao cha wafamasia na wadau wa mnyororo wa ugavi na usambazaji wa bidhaa za afya kinachoendelea Mkoani Morogoro.

Picha za Wafamasia na Wadau mbalimbali waliohudhuria kikao cha Wadau wa mnyororo wa ugavi na usambazaji wa bidhaa za afya kutoka Sekta mbalimbali za Serikali na Binafsi waliokutana Mkoani Morogoro.


Na WAJMW-MOROGORO

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe amewataka Wafamasia nchini kote kuzingatia maadili na kutumia taaluma waliyonayo ili kutoa huduma bora kwa wananchi.

Prof. Mchembe amesema hayo wakati akifungua semina inayojumuisha Wadau wa mnyororo wa ugavi na usambazaji wa bidhaa za afya kutoka Sekta mbalimbali za Serikali na Binafsi waliokutana Mkoani Morogoro.

“Ninawataka Wafamasia wote mbadilike kulingana na mazingira yaliyopo, hivi sasa nchi imeingia kwenye uchumi wa kati, hii inamaana mboreshe utaalamu wenu ili kukidhi mahitaji ya nchi. Corona imekuja na faida kubwa, imetufanya sasa tunaweza kutengeneza Vitakasa mikono vyetu (Hand Sanitizer) na barakoa jambo ambalo hapo awali halikuwepo”. Amesema Katibu Mkuu Prof. Mchembe.

Prof. Mchembe amesisitiza kuboreshwa kwa huduma za dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya zikiwemo Zahanati na vituo vya afya vya umma kuhakikisha dawa zote muhimu zinapatikana ili mwananchi anapofika kupata huduma asikose dawa na kulazimika kwenda kununua kwenye maduka ya watu binafsi.

Aidha, Prof. Mchembe amewataka wataalamu hao kutochagua vituo vya kazi kwani kwa kufanya hivyo wanaweza kuwa wanadidimiza taaluma yao kwa kufanya kazi maeneo ambayo hayana vifaa.
“Rais wetu ana nia njema katika kuboresha huduma za afya nchini, utakuta Hospitali fulani ina vifaa vizuri sana vya kufanyia kazi lakini haina wataalam wa kuvitumia”. Amesema Katibu Mkuu huyo.

Katika kutatua changamoto hizo Katibu Mkuu Mchembe amemuagiza Mfamasia Mkuu wa Serikali Ndg. Daud Msasi kuweka muongozo mzuri katika kuwapangia vituo vya kazi Wafamasia na wataalam wengine ili wananchi waweze kupata huduma bora za afya popote walipo.

Pia Prof. Mchembe amesisitiza matumizi ya data katika kutoa huduma na kutunza kumbukumbu kupitia mifumo ya GOTHOMIS na mingineyo ili kurahisisha utoaji wa huduma na kutunza rekodi za wagonjwa na pia kuweka mnyororo wa huduma zote za Hospitali kuwa katika hali nzuri.

Kwa upande wake Mfamasia Mkuu wa Serikali Ndg. Daud Msasi amewataka wadau waliohudhuria katika kikao hicho kuhakikisha mnyororo wa ugavi wa bidhaa za afya unatekelezwa ipasavyo kwa kuzingatia mambo ya msingi ambayo ni Pamoja na uzuiaji wa kukua kwa madeni yasiyolipika, nyaraka za mali za serikali zitunzwe vizuri, matumizi ya miongozo ili kuepika gharama zisizo za lazima, uwepo wa maduka ya dawa yanayojiendesha bila kuathiri huduma nyingine Pamoja na kuweka taarifa zilizo sahihi.

MWISHO



Ijumaa, 10 Julai 2020

SERIKALI YAAGIZA KUBORESHWA KWA VIWANGO VYA HUDUMA KATIKA HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA DODOMA

- Hakuna maoni


Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akikagua wodi ya wanaume iliyoko hospitali ya rufaa ya mkoa Dodoma.Kushoto ni Muuguzi Mfawidhi wa hospitali hiyo Stanley Mahumbo.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akikagua duka la dawa la Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.
Mganga Mkuu wa Serikali akitazama moja ya faili la   mgonjwa aliolazwa kwenye wodi hiyo ambapo alibaini mapungufu.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akiangalia moja ya mashine zilizopo kwenye maabara ya hospitali hiyo.

Na. WAMJW-Dodoma

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi ameuagiza Uongozi wa  Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma kuboresha huduma za tiba kwa wananchi wanaofika kupata huduma za afya katika hospitali hiyo.

Prof. Makubi ametoa maagizo hayo kufuatia ziara ya kushtukiza aliyoifanya kwenye Hospitali hiyo na kushuhudia changamoto mbalimbali ikiwemo baadhi ya wagonjwa kuchelewa kupewa huduma, Madaktari bingwa kutowaona wagonjwa kwa wakati na huduma za vipimo kuchelewa.

“Yapo mazuri tumeona mnayofanya kwa wananchi na tunawapongeza, ila lazima kuangalia upande wa pili ambao wananchi wanayataka, kwa yale mapungufu tuliyoyaona tungependa kuona yanaboreshwa haraka ili hospitali hii iwe ya mfano kwa hospitali zote za rufaa za mikoa kwa kutoa huduma zilizo bora”.

Prof. Makubi amesema hospitali hiyo inatakiwa kuonesha mfano kuanzia utoaji wa huduma bora kwa mteja pamoja, kupunguza muda wa wagonjwa kusubiri huduma, upatikanaji wa wauguzi na mabingwa wanapohitajika na usafi wa wodi kwani ndiyo chachu ya wananchi wengi kufika hapo na kupata huduma kabla hawajapewa rufaa ya kwenda Hospitali kubwa kama Benjamin Mkapa.

Aidha, Mganga Mkuu huyo ameutaka uongozi na watumishi wa hospitali hiyo kutambua majukumu yao  kwa kuonesha kuwajali wananchi  wote na kuwataka kuweka utaratibu usio na usumbufu kwa wagonjwa na kupatiwa huduma kwa wakati.

Prof. Makubi alionyesha kusikitishwa alipokuta wodini  baadhi ya wagonjwa wamelazwa na hawajaonwa na Mabingwa kwa zaidi ya siku tatu, wauguzi wakiwa hawajaambatana na madaktari katika kuzungukia wagonjwa huku madaktari wa vitendo (interns)  wakifanya “procedures” peke yao bila uangalizi na baadhi ya  wagonjwa wengine wakiwa wamelazwa chini wakati vitanda viko wazi pamoja na mazingira ya wodi hayakuwa ya kuridhisha na kukosekana kwa mpangilio wa vifaa (5S)

 “Lazima watumishi mjitambue mko wapi kwani awamu hii ni ya kuwajali wanyonge na kufanya kazi  kwa bidii ndio kanuni ya awamu hii hapa kazi tu”. Alisisitiza Prof. Makubi.

Prof. Makubi ameelekeza madaktari wa hospitali hiyo kufanya kazi kwa ushirikiano na wauguzi katika kuwahudumia wagonjwa katika wodi, kuleta mabadiliko kwa kutengeneza miongozo mbalimbali ya kusimamia huduma na kuacha kufanya kazi kwa mazoea ili kila mwananchi anayefika hospitalini hapo ahudumiwe kwa wakati na huduma inayostahili.

Kwa upande mwingine Mganga Mkuu huyo wa Serikali ameitaka hospitali hiyo kuboresha idara ya huduma kwa wateja (Customer Care) kwani hakuna mgonjwa anayependa kuchelewa kupata huduma hivyo lazima kutoa huduma bora na zinazohitajika kwa wananchi wote.

Prof. Makubi ameelekeza Uongozi wa Hospitali kuhakikisha mashine za maabara ambazo zimeishiwa vitendanishi, zinaanza kufanya kazi haraka.

"Ni vizuri mkapunguza muda wa kusubiri majibu ya vipimo vya damu, X-ray, ultrasound, na Moyo na vipimo vingine".Alielekeza Prof. Abel Makubi.

Prof. Makubi aliagiza Hospitali zote nchini zifanyie kazi changamoto alizoziona hapo Dodoma, na akaagiza Idara ya ukaguzi wa huduma bora kutoka wizarani wafanye ufuatiliaji wa utoaji wa huduma mikoani,  wilayani na Vituo vya afya kila mwezi na kutoa taarifa kwake.

"KUTOA HUDUMA ZA AFYA ZA UHAKIKA NI JUKUMU LETU"-PROF. MAKUBI

- Hakuna maoni

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akiongea na wataalam kutoka Wizara ya Afya na TAMISEMI wakati wa kujadili utoaji wa huduma bora za afya kwenye vituo vya afya,hospitali za halmashauri na rufaa zilizojengwa kukarabatiwa na Serikali
Mkurugenzi wa huduma za Afya, Lishe na Ustawi wa Jamii-TAMISEMI Dkt. Ntuli Kapologwe akiongea wakati wa kikao hicho.
Mkurugenzi wa Idara ya Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi akiwasilisha mada wakati wa kikao baina ya Wizara ya Afya na TAMISEMI














Na. WAMJW-Dodoma

Serikali imefanikiwa kutimiza dhamira ya kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji na uwiano wa kutosha katika utoaji huduma za afya pamoja na kuhakikisha wananchi wanapata huduma za afya za uhakika na wakati.

Hayo yamesemwa leo na Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi wakati akifungua kikao kati ya Wizara ya Afya na Ofisi ya Rais-TAMISEMI cha kujadili utoaji huduma bora za afya kwenye vituo vya afya, Hospitali za Halmashauri na Rufaa zilizojengwa na kukarabatiwa na serikali ya awamu ya tano.

“Sisi kama wataalam tunawajibu wa kuendeleza chachu ya maendeleo  yaliyofikiwa na kuhakikisha vituo hivi vinafunguliwa kwa kuzingatia utaratibu unaotakiwa na kuendelea kutoa huduma vikiwa na vifaa vyote muhimu na wataalam wenye weledi na stadi katika kupambana na magonjwa na kupunguza vifo vinavyozuilika”.Amesema Prof. Makubi.

Prof. Makubi ameongeza kuwa mafanikio hayo yamepatikana kufuatia sekta ya afya kuchukua jukumu la kufanya ukarabati wa ujenzi katika vituo vya kutolea huduma za afya ambapo iliweka kipaumbele kwenye vituo vya afya vya msingi ili kuviwezesha kutoa huduma za dharura za uzazi na mtoto mchanga.

“Tumejenga hospitali mpya za wilaya 99, kutoka hospitali 70 za awamu ya kwanza zimekamilika na nyingi zimeanza kutoa huduma hata hivyo serikali imeongeza kujenga hospitali nyingine 29 na fedha zake zimetengwa tayari”. Ameongeza Prof. Makubi.

Awali akiongea kwa niaba ya Naibu katibu Mkuu wa Afya TAMISEMI, Mkurugenzi wa huduma za Afya, Lishe na ustawi wa jamii Dkt. Ntuli Kapologwe amesema kuwa kikao hicho kina lengo la kuwa na muelekeo mzuri wa sekta ya afya hivyo ushirikiano wa pamoja kati ya Wizara hizo mbili ni muhimu katika kufanikisha na kusukuma mbele sekta hiyo nchini.

Naye Mkurugenzi wa huduma za kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi amesema kuwa vituo vya afya 570 vilivyojengwa na kukarabatiwa na Serikali vimeweza kuboresha huduma za afya na kuzuia vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga huku vikiwa na uwezo wa kutoa huduma za dharura kama upasuaji.

MWISHO

Alhamisi, 2 Julai 2020

WAZIRI UMMY ARIDHISHWA NA KASI YA UJENZI WA HOSPITALI YA KANDA MTWARA

- Hakuna maoni
Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akiongozana na Mkuu wa Mkoa wa Mtwara Bw. Gelasius Byakanwa wakikagua ujenzi wa Hospitali mpya ya kanda ya kusini inayojengwa Mkoani Mtwara.

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akisikiliza maelezo kutoka kwa msanifu majengo anayesimamia mradi wa ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya kanda ya kusini wakati alipotembelea Hospitali hiyo kuona hali ya ujenzi.

Waziri wa Afya Mhe. Ummy Mwalimu akiwa na Mbunge wa Mtwara vijijini Mhe. Hawa Ghasia wakitembelea ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya kanda ya kusini iliyopo Mtwara.


Sehemu ya jengo la Hospitali ya Rufaa ya Mikoa ya kusini inayoendelea na ujenzi.

Na. WAJMW-Mtwara

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu ametembelea ujenzi wa Hospitali mpya ya Rufaa ya Mikoa ya kusini iliyopo mkoani Mtwara na kuridhishwa na kasi ya ujenzi wa Hospitali hiyo.

Waziri Ummy ameonekana kuridhidhishwa na ujenzi wa Hospitali hiyo ambao umefikia asilimia 80 na inagharimu Shilingi Bilioni 15.8 mpaka kukamilika kwake.

"Kukamilika kwa Hospitali hii kutasaidia kupunguza rufaa kwa wananchi wa mikoa ya kusini kwenda kutafuta huduma za kibingwa Muhimbili, MOI au JKCI, huduma zote zitakua zinapatikana hapa". Amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy amesema lengo la Wizara ya Afya ni kuona huduma zinaanza kutolewa katika Hospitali hiyo kabla ya kuanza kampeni za uchaguzi mwaka huu kwani ilikua ni ahadi ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli alipopita mwaka 2015 kuomba kura na Hospitali hiyo ipo kwenye utekelezaji wa ilani ya Chama cha Mapinduzi.

"Hatutaki watu wa Mtwara na mikoa ya kusini kwa ujumla muende Dar Es Salaam kwa ajili ya kufuata huduma za CT-Scan, huduma za madaktari bingwa ikiwemo upasuaji wa mifupa, mishipa ya fahamu, Madaktari wa watoto na uzazi. Huduma zote hizi zitapatikana hapa mara baada ya ujenzi wa Hospitali hii kukamilika". Amesema Waziri Ummy.

Waziri Ummy amesema kwa ujumla hali ya sekta ya Afya mkoani Mtwara ni nzuri ambapo katika kipindi cha miaka mitano Hospitali mpya za Wilaya tatu zimejengwa ambazo ni Nanguluwe, Nanyamba pamoja na Masasi. Aidha, vituo vya Afya vinane vimejengwa katika Mkoa huo katika kipindi hicho na kufanya idadi kufikia vituo 23 kutoka 15 wakati Rais Magufuli anaingia madarakani.

Jumanne, 23 Juni 2020

UGONJWA WA CORONA USIWE KIGEZO CHA WATOTO KUKOSA CHANJO

- Hakuna maoni
Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma ya Afya ya Uzazi na Watoto, Dk.Ahmad Makuwani akisema jambo kwa wanahabari (hawapo pichani) wakati wa semina ya huduma za chanjo.
Afisa Programu ya Chanjo wa Mpango wa Taifa wa Chanjo kutoka Wizara ya Afya, Lotalis Gadau akisema jambo kwa waandishi wa habari wa mikoa ya Singida na Dodoma wakati wa semina ya huduma za chanjo nchini
Afisa Programu ya Chanjo wa Mpango wa Taifa wa Chanjo kutoka Wizara ya Afya, Lotalis Gadau (aliyesimama) akisema jambo wa waandishi wa habari wa mikoa ya Singida na Dodoma kwenye semina ya huduma za chanjo Tanzania.

Waandishi wa habari wa mikoa ya Singida na Dodoma wakisikiliza wasilisho la mada wakati wa semina ya huduma za chanjo nchini.

Picha ya pamoja na Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma ya Afya ya Uzazi na Watoto, Dk.Ahmad Makuwani  watalaam pamoja na wanahabari wa Mkoa wa Dodoma.


Picha ya pamoja na Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma ya Afya ya Uzazi na Watoto, Dk.Ahmad Makuwani  watalaam pamoja na wanahabari wa Mkoa wa Singida.



 Na WAMJW - Dodoma

Serikali imeitaka jamii kuhakikisha watoto wanapata chanjo kipindi hichi chenye maambukizi ya Virusi vya Corona (Covid-19) ili wapate kinga ya magonjwa mengine.

Rai hiyo imetolewa na Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma ya Afya ya Uzazi na Watoto, Dk.Ahmad Makuwani kwenye semina ya waandishi wa habari wa Mikoa ya Singida na Dodoma kuhusu huduma za chanjo nchini.

Amesema maambukizi ya Corona kwasasa yamepungua na kuwataka watanzania kutotumia ugonjwa huo kama sababu ya kutowapeleka watoto kupata chanjo.

“Tulikuwa tunaenda vizuri lakini hivi karibuni idadi ya watoto na wasichana wanaopaswa kupata chanjo ya mlango wa kizazi imepungua, hizi chanjo ni muhimu sana jamii ipeleke watoto kwenye vituo wapate chanjo” amesema Dkt. Makuwani.

Amebainisha kuwa Tanzania imepiga hatua kwasasa katika utoaji wa huduma za chanjo huku akidai kuwa kuna vituo zaidi ya 600 vinavyofanya uchunguzi wa saratani ya mlango wa kizazi.

“Tunaamini mtatumia weledi wenu kuelimisha jamii kuhusu huduma ya chanjo mbalimbali zinazotolewa, wahimizeni wananchi kule vijijini wapeleke watoto wao kwa kuwa chanjo inatolewa kwenye vituo vya kutolea huduma" amesema Dkt Makuwani.

Amesisitiza kuwa waandishi waendelea kuhamasisha wananchi kunawa mikono kwa kuwa imesaidia kupunguza kasi ya magonjwa ya mlipuko ikiwemo kipindupindu.

Awali, akizungumzia hali ya huduma za chanjo nchini, Ofisa Programu ya Chanjo wa Mpango wa Taifa wa Chanjo kutoka Wizara ya Afya, Lotalis Gadau, alisema pamoja na jitihada za kuhakikisha magonjwa yanayizuilika kwa chanjo yanapewa kipaumbele kwa kuwapatia watoto chanjo lakini bado kuna jamii hazichanji watoto.

“Baadhi ya chanjo kiwango kipo chini ya kiwango kinachotakiwa, chanjo ya Surau na Rubella kitaifa tuna asilimia 76% ambayo iko chini ya kiwango cha utoaji wa huduma za chanjo ambayo inatakiwa kuwa asilimia 90” alisema Bi. Gadau kupitia tathmini ambazo hufanywa na Wizara kuona hali ya huduma za chanjo.

“Kuwepo kwa ugonjwa wa Corona sio sababu ya kutopeleka watoto kupata chanjo kwasababu wakichanjwa inasaidia kuwakinga na magonjwa mengi zaidi” amesisitiza Bi. Gadau.

Amesema kuwa Wizara imekuwa ikifanya usimamizi elekezi wa huduma za chanjo katika kipindi ambacho mlipuko wa ugonjwa wa corona ulivyoanza na shule kufungwa kuona hali ya utoaji wa chanjo ya kuzuia saratani ya mlango wa kizazi (HPV) kwenye jamii ambapo wananchi wengi wamekuwa wakiogopa kwenda kwenye vituo vya kutolea huduma za afya wakiogopa maambukizi na kuihamasisha jamii kwenda kupeleka watoto wao kupata chanjo hizo muhimu huku wakizingatia tahadhari za kujikinga na ugonjwa wa corona.

Mwisho


Ijumaa, 19 Juni 2020

WAZIRI UMMY AZINDUA MWONGOZO WA MATIBABU YA SIKOSELI

- Hakuna maoni
Waziri Ummy Mwalimu akiwa na Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi wakikata utepe kuzindua muongozo wa tiba ya wagonjwa wa Sikoseli nchini

Waziri Ummy Mwalimu akimsikiliza mmoja wa watoto waliozaliwa na Sikoseli wakati wa maadhimisho ya siku ya sikoseli duniani.

Waziri Ummy Mwalimu akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili Prof. Lawrence Museru muongozo wa matibabu ya sikoseli mara baada ya kuzindua.



Picha ya Pamoja na Madaktari wa Watoto

Picha ya pamoja na Watoto wenye ugonjwa wa Sikoseli

WAMJW- Dar es Salaam



Serikali imezindua mwongozo wa Taifa wa matibabu kwa watu wenye ugonjwa wa sikoseli, huku ikiagiza kuanzishwa kwa kliniki maalumu za kuchunguza ugonjwa huo katika ngazi ya wilaya na mikoa ili kuhakikisha watu wengi hasa watoto wanafikiwa.

Akizindua mwongozo huo leo, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu amesema kuanzishwa kwa kliniki katika ngazi za wilaya na mikoa itasaidia watu mbalimbali kupata huduma ya utambuzi ya ugonjwa wa sikoseli karibu na maeneo wanayoishi.

“Naagiza vipimo vya utambuzi kupelekwa kwenye ngazi ya wilaya na mikoa ili kila mtu aweze kuchunguzwa kama ana tatizo la sikoseli". Amesema Waziri Ummy.

Pia, Waziri ameshauri upatikanaji salama wa damu kwa ajili ya watu wenye tatizo la ugonjwa sikoseli ili kuondoa changamoto ya tiba kwa wagonjwa mbalimbali.

Waziri wa Ummy ameshauri wananchi kufanya uchunguzi wa afya zao mapema ili kubaini kama wana ugonjwa huo kwani endapo watabaini itawasaidia kuanza matibabu mapema.

 Katika hatua nyingine, Waziri wa Afya amewataka wadau wa ugonjwa huo kupunguza gharama za dawa kwani wagonjwa wengi hawezi kuzinunua.

“Naagiza pia dawa ya sikoseli ziingizwe katika Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) ili iwe rahisi kupatika kwa wagonjwa wengi". Amesema Waziri Ummy.

Nae Mganga Mkuu wa Serikali, Prof. Abel Makubi amesema Serikali imefikia hatua kubwa ya kuanzishwa kwa mwongozo wa Taifa wa matibabu kwa wagonjwa wa sikoseli kwa kuwa utazuia vifo vingi.

Amesema vifo vingi vinavyotokana na ugonjwa wa sikoseli, vinaweza kuzuilika endapo utagundulika mapema kwa watoto wachanga.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Prof. Lawrence Museru amesema katika kliniki ya wagonjwa wa sikoseli, watoto 50 hadi 70 wamekuwa wakipatiwa matibabu ya ugonjwa huo wakati kwa mwezi ni wagonjwa 211 hadi 300.

“Katika kliniki ya watu wazima, kwa siku wanaonwa wagonjwa 30 hadi 40 na kwa mwezi wagonjwa 160 hadi 200 wanatibiwa hapa Muhimbili". Amesema Prof. Museru.

Prof. Museru amesema watoto wenye ugonjwa huo wamekuwa wakipata tatizo la kupumua, damu kuganda mwilini na kiharusi.

Kauli mbiu ya mwaka huu, “Huduma Bora kwa Kila Mhitaji; Chukua hatua, panua wigo.”

MWISHO