Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Rayson. Onyesha machapisho yote
Inaonyesha machapisho yaliyo na lebo Rayson. Onyesha machapisho yote

Jumanne, 1 Desemba 2020

WANAOFANYA MAPENZI NA WASICHANA WENYE UMRI MDOGO WAONYWA

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akihutubia Wananchi kwenye maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa Kimataifa, Tujumuike Pamoja".

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akitoa taarifa ya hali ya maambukizi ya virusi vya UKIMWI mbele ya mgeni rasmi (Hayupo kwenye picha) wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro.

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akiteta jambo na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro. 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akipeana mkono na Mkurugenzi wa TACAIDS Dkt. leonard Maboko baada ya kuhutubia wananchi, wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro. 
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akipata taarifa kutoka kwa Mkuu wa kitengo cha tiba na matunzo Dkt. Anath Rwebemberwa katika banda la Mpango wa Taifa wa kupambana na UKIMWI (NACP) ulio chini ya Wizara ya Afya, maendeleo ya jamii, jinsia, Wazee na watoto.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe na Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi wakiwa na Mkurugenzi wa Kinga Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi (watano kutoka kushoto) Meneja NACP Dkt. Beatrecy Mutayoba (wamwisho), wakwanza kushoto ni Mkuu wa kitengo cha tiba na matunzo Dkt. Anath Rwebemberwa na wapili kushoto ni Mkuu wa kitengo cha Kinga (NACP) Dkt. Magreth Kagashe.


Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa akiwa na viongozi wengine Wakiserikali, wakati wa maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa Kimataifa, Tujumuike Pamoja".


WANAOFANYA MAPENZI NA WASICHANA WENYE UMRI MDOGO WAONYWA. 

Na Rayson Mwaisemba WAMJW- Kilimanjaro 

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa ametoa onyo kali kwa wanaofanya mapenzi (ngono) na wasichana wenye umri mdogo, hali inayosababisha kuwaharibia malengo yao ya baadae. 

Mhe. Kassim Majaliwa ameyasema hayo leo wakati akiwahutubia wananchi kwenye maadhimisho ya siku ya Ukimwi Duniani yaliyofanyika katika uwanja wa Mandela Moshi, Mkoani Kilimanjaro yenye kauli mbiu ya "Mshikamano wa Kimataifa, Tujumuike Pamoja".

"Nataka niwakumbushe na kutoa tahadhari kwa wale watu wazima mnaofanya mapenzi na vijana wadogo wa kike, ole wenu, ole wenu, ole wenu " ameyasema Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa.
Alisema kuwa, takwimu za maambukizi mapya ya VVU zinaonesha kwamba asilimia 40 ya maambukizi hutokea kwa vijana na katika hao asilimia 80 ni vijana wa kike, huku akiweka wazi kuwa, vijana ni kundi linalokabiliwa na changamoto ya maambukizi mapya ya VVU nchini.

Aliendelea kusema, kundi la vijana na hasa wa kike lipo kwenye hatari kubwa zaidi ya kupata maambukizi mapya, huku akidai uchambuzi wa kimazingira kuhusu takwimu hizi unaonesha kuwa sababu za vijana kuwa katika hatari ya maambukizi mapya ya VVU ni pamoja na kuanza ngono katika umri mdogo, vijana wadogo wa kike kuwa na mahusiano ya kingono na wanaume wenye umri mkubwa Matumizi yasiyo sahihi na endelevu ya mipira ya kike na kiume.

Aidha, Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa, ametoa wito kwa vijana kujitambua na kuthamini maisha yao kwa kujikinga na maambukizi mapya ya VVU, huku akiwakumbusha kuwa vijana ndio nguvu kazi ya Taifa, na kuwataka wale wanaoishi na VVU waendelee kutumia dawa za ARV kwa ufuasi sahihi bila kuacha ili kufubaza VVU na kuimarisha afya zao. 

"Natoa wito kwa vijana kujitambua na kuthamini maisha yao kwa kujikinga na maambukizi mapya ya VVU kwa kuwa ninyi ni nguvu kazi na Taifa linawategemea. Na wale wanaoishi na VVU waendelee kutumia dawa za ARV kwa ufuasi sahihi bila kuacha ili kufubaza VVU na kuimarisha afya zao", alisema Mhe. Kassim Majaliwa Majaliwa. 

Nae Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe amesema kuwa, Tanzania na Dunia kwa ujumla imepiga hatua kubwa katika jitihada za kukabiliana na janga la VVU na UKIMWI.

Aliendelea kusema kuwa, kama nchi inavyoelekea kufikia malengo ya Tisini Tatu, changamoto, na vipaumbele vimeendelea kubadilika kutokana na mafanikio ya mwitikio wa mapambano.
Takwimu zinaonesha kuwa wanaume, watoto, vijana wanaopevuka na vijana wadogo, na watu wanaofanya tabia hatarishi, wako nyuma kutambua hali zao, ufuasi hafifu wa tiba, na ufubazaji wa VVU usioridhisha. 

Hata hivyo, Prof. Mabula Mchembe amesema kuwa, Serikali inaendelea na jukumu la kutafiti, kuandika na kusambaza taarifa za kitaalamu zinazochambua na kutoa masuluhisho ya changamoto zitazotumika kuhuisha sera, miongozo na taratibu za huduma na afua za VVU na UKIMWI. 

"Tunalo jukumu sasa, la kutafiti, kuandika na kusambaza taarifa za kitaalamu zinazochambua na kutoa masuluhisho ya changamoto hizi ili sasa yatumike kuhuisha sera, miongozo na taratibu za huduma na afua za VVU na UKIMWI", amesema Prof. Mchembe 

Mwisho.

Ijumaa, 27 Novemba 2020

HAKIKISHENI UKOMA UNATOKOMEA NCHINI TANZANIA.

Mkurugenzi wa huduma za kinga Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi akisisitiza jambo mbele ya Waganga Wakuu wa Mkoa na Waratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma wakati wa kuhitimisha Mkutano wa mwaka wa Kifua Kikuu na Ukoma uliofanyika Jijini Dodoma.

Mkurugenzi msaidizi wa Idara ya Afya, Ustawi wa Jamii na Lishe TAMISEMI Dkt. Paul Chawote akieleza jambo wakati wa kuhitimisha Mkutano wa mwaka wa Kifua Kikuu na Ukoma uliofanyika Jijini Dodoma.

Meneja Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua Kikuu na Ukoma nchini Dkt. Zuweina Kondo Sushy akifuatilia neno kutoka kwa Mkurugenzi wa huduma za kinga Wizara ya Afya (hayupo kwenye picha) wakati wa kuhitimisha Mkutano wa mwaka wa Kifua Kikuu na Ukoma uliofanyika Jijini Dodoma.

Waganga Wakuu wa Mikoa na Waratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma wakimkaribisha mgeni rasmi (hayupo kwenye picha), wakati wa kuhitimisha Mkutano wa mwaka wa Kifua Kikuu na Ukoma uliofanyika Jijini Dodoma.



Na Rayson Mwaisemba WAMJW- DOM 

Mkurugenzi wa kinga Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Leonard Subi ametoa wito kwa Waganga Wakuu wa mikoa wote kutumia mbinu mbali mbali ili kuutokomeza ugonjwa wa ukoma na Kifua Kikuu nchini Tanzania. 

Dkt. Subi ametoa wito huo leo wakati akifunga Mkutano wa mwaka wa Mpango wa taifa wa kudhibiti kifua Kikuu na ukoma uliohudhuriwa na Waganga wakuu na Waratibu wa kifua Kikuu na ukoma ngazi ya Mkoa, uliofanyika Jijini Dodoma. 

"Tumieni kila liwezekanalo ugonjwa wa ukoma uishe nchini Tanzania, kwa Waganga Wakuu wa Mkoa ambao Halmashauri zenu bado zina maambukizi ya ukoma jipeni ndani ya miaka mitano ugonjwa wa ukoma utoweke nchini " amesema Dkt. Subi. 

Dkt. Subi amesema kuwa, ni muhimu kwa viongozi kutumia takwimu ili kuwasaidia katika kufanya maamuzi sahihi na kwa wakati katika utekelezaji wa majukumu yao, jambo litalosaidia kutokomeza maambukizi ya ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma nchini. 

Aidha, Dkt. Subi ametoa agizo kwa Waganga Wakuu wa mikoa wote kuhakikisha maelekezo na maazimio yaliyotokana na Mkutano huo yatolewe kwa maandishi kwa Halmashauri zote nchini ikiwa ni sehemu ya mikakati ya kutokomeza ugonjwa wa Ukoma na Kifua Kikuu.

Mbali na hayo, Dkt. Subi ameagiza kuendelea kutoa elimu ya Afya kwa umma kwa wananchi kupitia vyombo vya habari kama vile radio za jamii, mitandao ya jamii, ili kuwakinga wananchi wetu dhidi ya maambukizi ya magonjwa ikiwemo ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma. 

"Toeni elimu ya Afya kwa wananchi, wananchi waelimishwe kuhusu magonjwa mbali mbali katika Jamii ikiwemo ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma, wekeni utaratibu wa vipindi vya Afya kwenye radio za mikoa yenu" amesema Dkt. Subi. 

Kwa upande wake Mkurugenzi msaidizi wa Idara ya Afya na Ustawi wa Jamii na Lishe TAMISEMI Dkt. Paul Chawote amemhakikishia Mgeni rasmi kusimamia utekelezaji wa maazimio ya Mkutano huo ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kutokomeza maambukizi ya ugonjwa wa Kifua Kikuu na ukoma nchini. 

"Sisi kama Ofisi ya Rais TAMISEMI tumejipanga kusimamia utekelezaji wa maazimio yote ambayo yametokana na Mkutano huo ili kupambana dhidi ya ugonjwa wa Kifua Kikuu na Ukoma nchini "amesema Dkt. Çhawote. 

Mwisho

Jumatano, 25 Novemba 2020

PROF. MCHEMBE AWAAGIZA WATAALAMU WA SEKTA YA AFYA KUFIKIRIA HUDUMA BORA NA NAFUU KWA WANANCHI

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akifungua Mkutano wa saba wa Afya uliohudhuriwa na Wadau mbali mbali wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Mkurugenzi Idara ya Afya ustawi wa Jamii na Lishe Dkt. Ntuli Kapologwe akimkaribisha mgeni rasmi, Katibu Mkuu Wizara ya Afya Prof. Mabula Mchembe (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa saba wa afya, uliohudhuriwa na Wadau mbali mbali wa afya nchini, Jijini Dodoma

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akipita katika banda la NIMR kujionea shughuli zinazoendelea, wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa saba wa Afya uliohudhuriwa na Wadau mbali mbali wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Wadau mbali mbali wa masuala ya Afya waliohudhuria Mkutano wa saba wa masuala ya Afya unaoendelea Jijini Dodoma kujadili namna bora ya kuboresha huduma za Afya nchini.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akiwa na Wadau mbali mbali wa Afya wakati wa  Mkutano wa saba wa Afya unaoendelea Jijini Dodoma.



PROF. MCHEMBE AWAAGIZA WATAALAMU WA SEKTA YA AFYA KUFIKIRIA HUDUMA BORA NA NAFUU KWA WANANCHI

Na Rayson Mwaisemba, WAMJW - DOM 

KATIBU Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe ametoa wito kwa Wataalamu wa Sekta ya Afya nchini kuhakikisha wanafikiria namna ya utoaji huduma bora na kwa gharama nafuu ili wananchi wenye hali zote waweze kuzimudu.

Wito huo ameutoa leo, wakati akifungua Mkutano wa saba wa Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Watumishi kutoka Wizara ya Afya, Ofisi ya Rais TAMISEMI na Wadau mbali mbali wanaojihusisha na masuala ya Afya nchini.

"Ni wajibu wetu sisi, tukiwa kwenye Mkutano huu wa wa Afya kuwaza vyema tunamsaidiaje mwananchi wa hali ya chini kupata huduma bora, zenye unafuu na zinazofikika kila sehemu bila kumuumiza mwananchi" alisema Prof. Mchembe.

Hata hivyo, Prof. Mchembe amesema kuwa, Wizara ya Afya itaendelea kutoa ushirikiano kwa Wadau wote ili kufanikisha utoaji huduma bora na nafuu kwa wananchi, huku akiweka wazi kuwa kama Serikali itatendea kazi mapendekezo na ushauri utakaotokana na Mkutano huo. 

Aidha, Prof. Mchembe amesisitiza kuwa, ni muhimu mijadala itayoendelea katika Mkutano huo kuhakikisha inapita kwenye malengo ya Wizara yakiwemo kupunguza vifo vya mama na mtoto, kupunguza maambukizi ya VVU, TB, Ukoma, 

Mbali na hayo, Prof. Mabula Mchembe amewataka Wataalamu hao kujadili masuala ya kupunguza magonjwa yasiyo yakuambukiza ambayo yanaongeza mzigo kwa Serikali kutokana na gharama za kuyatibu magonjwa hayo, yanayotokana na mtindo wa maisha ikiwemo matumizi ya pombe kupita kiasi, kutofanya mazoezi. 

Naye, Mkurugenzi Idara ya Afya ustawi wa Jamii na Lishe kutoka TAMISEMI Dkt. Ntuli Kapologwe amesema kuwa, Serikali imefanya maboresho mengi sana katika miaka saba iliyopita, huku akiweka wazi kuwa mambo yatakayojadiliwa katika kikao hicho yataendana na mpango mkakati wa Sekta afya unaosimamiwa na Serikali kupitia Wizara ya Afya. 

Pia, Dkt.Kapologwe amesema kuwa, kama wasimamizi wa Sera watahakikisha maazimio yatakayotoka kwenye kikao hicho yanaingizwa kwenye mipango ya utekelezaji kwenye Hospitali zote ngazi ya Wilaya, Halmashauri na zahanati kwa utekelezaji zaidi. 

"Katika kikao hiki, pamoja na maelekezo ambayo utayatoa, sisi tukiwa kama wasaidizi wako tutahakikisha, maelekezo yako pamoja na maazimio utakayotoa katika kikao hiki, tunaenda kuyaingiza katika mipango yetu katika Hospitali za Mikoa, Halmashauri na Zahanati" amesema Dkt. Ntuli Kapologwe. 

Mwisho

Jumanne, 24 Novemba 2020

KUELEKEA MPANGO MKAKATI WA TANO WA SEKTA YA AFYA, SERIKALI YAJIDHATITI KUSOGEZA ZAIDI HUDUMA KWA WANANCHI.

Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe akifungua Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa Tathmini ya Utekelezaji katika Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Wadau wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Naibu Katibu Mkuu TAMISEMI anaeshughulikia masuala ya Afya Dkt. Dorothy Gwajima akieleza jambo wakati wa ufunguzi  wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa Tathmini ya Utekelezaji katika Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Wadau wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi akimkaribisha mgeni  rasmi Katibu Mkuu Wizara  ya Afya Prof. Mabula Mchembe (hayupo kwenye picha) wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Wadau wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Wakurugenzi kutoka Wizara ya Afya wakiteta jambo wakati  wa ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliohudhuriwa na Wadau wa Sekta ya Afya nchini, Jijini Dodoma.

Baadhi ya Wakurugenzi wasaidizi kutoka Wizara ya Afya  walioshiriki katika ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Baadhi ya Wadau waliohudhuria ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Wakurugenzi kutoka Wizara ya Afya na Wadau wa Sekta ya Afya nchini walio hudhuria  ufunguzi wa Mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya uliofanyika Jijini Dodoma.

Picha ya pamoja ikiongozwa na Katibu Mkuu Wizara  ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe, akiwa na Sekretarieti ya mkutano wa 21 wa Kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya.



Na, Rayson Mwaisemba WAMJW- DOM 

SERIKALI, kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeendelea kujidhatiti katika kuboresha utoaji huduma za Afya kwa wananchi ikiwemo kupunguza vifo vya mama na mtoto, uboreshaji wa huduma za chanjo, upatikanaji wa vifaa na vifaa tiba. 

Hayo yamesemwa leo na Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Prof. Mabula Mchembe wakati akifungua Mkutano wa 21 wa kitaalam wa tathmini ya utekelezaji katika Sekta ya Afya ulioandaliwa kwa pamoja na Wizara yake na Ofisi ya Rais TAMISEMI ukishirikisha Wadau mbalimbali wa Sekta ya Afya nchini unaoendelea Jijini Dodoma.

Prof. Mchembe amesema kuwa, kikao hicho kina umuhimu mkubwa sana katika Wizara na Sekta ya Afya kwa ujumla kwa sababu ndio kinachoweza kuweka mikakati ya nini kifanyike miaka mitano ijayo, baada ya kupitia mikakati ya miaka mitano iliyopita na kuona mafanikio na changamoto zake.

"Kama Serikali tumefanikiwa kuboresha katika kupunguza vifo vya mama na mtoto,  huduma za chanjo, vifaa na vifaa tiba pamoja na uboreshaji wa utoaji huduma zinazotolewa na Watumishi wa Afya" amesema Prof. Mchembe. 

Aidha,  Prof. Mchembe amesema mpango mkakati wa tano unaoenda kuanza ni matokeo ya ule wa nne ambapo unaangazia mafanikio, na kuboresha maeneo yaliyokuwa na changamoto na kuweka mikakati madhubuti ya kuboresha Sekta ya Afya. 

Naye Naibu Katibu Mkuu anayeshughulikia masuala ya Afya kutoka ofisi ya Rais TAMISEMI Dkt. Dorothy Gwajima amesema kuwa, kama wasimamiaji wa utekelezaji wa Sera katika ngazi za Mikoa na Mamlaka za mitaa wapo tayari kutekeleza maagizo na miongozo itayotolewa kupitia kikao hicho cha tathmini ya Sera kilichohudhuriwa na Wadau wote wa Sekta ya Afya nchini. 

"Katibu Mkuu Wizara ya Afya ameeleza mambo mengi, sisi tupo kama Wadau ambao tunasimamia utekelezaji kwenye ngazi ya Mikoa na Mamlaka ya Serikali za Mitaa tunasubiri maelekezo  na miongozo ya Kisera ili kwenye kipindi cha miaka mitano ijayo tuweze kutekeleza kwa kasi ile ile" alisema Dkt. Gwajima. 

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Sera na Mipango Wizara ya Afya Bw. Edward Mbanga amesema kuwa, kikao hicho cha Sera hupokea mambo yote katika Sekta ya Afya yaliyofanyiwa tathmini na yaliyokubalika kuwa ndio yatakuwa malengo na muelekeo wa Sekta ya Afya nchini. 

Mwisho.

Ijumaa, 21 Agosti 2020

TUSHIRIKIANE KUPAMBANA DHIDI YA MAGONJWA YASIYO AMBUKIZA - MGANGA MKUU WA SERIKALI.

- Hakuna maoni

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi (watatu kutoka kushoto) akikagua taarifa za mgonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Kaskazini KCMC, pindi alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma katika Hospitali hiyo.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi (watatu kutoka kushoto) akipokea taarifa za hali ya mgonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Kaskazini KCMC, pindi alipofanya ziara ya kukagua hali ya utoaji huduma katika Hospitali hiyo.

Kiwanda cha uzalishaji mitungi ya oksijeni kilichopo katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya kaskazini KCMC. 

Baadhi ya mashine za uzalishaji wa gesi ya oksijeni inazotumika katika matibabu  ya wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya kanda ya kaskazini KCMC.


TUSHIRIKIANE KUPAMBANA DHIDI YA MAGONJWA YASIYO AMBUKIZA - MGANGA MKUU WA SERIKALI.

Na WAMJW- KILIMANJARO

MGANGA Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi ametoa wito kwa watoa huduma za Afya kushirikiana kwa pamoja kwa kutoa elimu, katika mapambano dhidi ya magonjwa yasiyo ambukiza yanayosababishwa na mtindo wa maisha ikiwemo ulaji usiofaa, matumizi ya vileo na kutofanya mazoezi.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Makubi ametoa rai hiyo wakati alipotembelea Hospitali ya Rufaa ya kanda ya Kaskazini KCMC kukagua hali ya utoaji huduma za Afya katika Hospitali hiyo kwa wananchi.

Prof. Makubi amesema kuwa, ni muhimu watoa huduma za afya kuungana kwa pamoja kushirikiana kwa kutoa elimu kwa wananchi kuhusu magonjwa yasiyo ambukiza (NCD), kwa njia ya kuwafuata wagonjwa katika maeneo yao, jambo ambalo litasaidia kupunguza mzigo wa wagonjwa katika hospitali za Rufaa nchini.

"Mshirikiane kwa pamoja kutoa Elimu ya ufahamu, na kupima angalau mara 2 kwa mwaka juu ya  magonjwa yasiyo ambukiza  kupitia njia ya kuwafuata wateja katika maeneo yao na kuwafanyia upimaji (outreach program)" alisema Prof. Makubi.

Hata hivyo, Prof. Makubi ametoa rai kwa watoa huduma za afya kuhakikisha wanatoa huduma kwa wakati kwa wagonjwa ili kuepusha msongamano unaoweza sababisha mlipuko wa magonjwa mengine katika hospitali na kupunguza usumbufu kwa wagonjwa.

Aidha, Prof. Makubi ameridhishwa kwa kiasi kikubwa hali ya utoaji huduma katika Hospitali hiyo, huku akiwataka kuongeza jitihada ili kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi na kupunguza malalamiko yanayoweza kuepukika kwa urahisi.

"Mimi kwa KCMC, sipati malalamiko mengi sana, simamìeni katika ubora huo, na mhakikishe mnaongeza Juhudi zaidi, na kwa hilo nawapongèza sana sana" alisema Prof. Abel Makubi.

Hata hivyo, Prof. Makubi amewapongeza watumishi wa Hospitali ya KCMC wakiongozwa na Mkurugenzi wao Prof. Gileard Masenga kwa kuanzisha mradi wa uzalishaji wa gesi ya oksijeni, jambo linalosaidia kuongeza mapato na kuokoa kiasi kikubwa cha pesa ambacho kingetumika kununua mitungi ya gesi, na pesa hizo kuelekezwa katika kuboresha huduma kwa wananchi.

Naye, Mkurugenzi wa huduma za tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Grace Maghembe amewataka watumishi kutobweteka, katika kuwahudumia wananchi, licha ya kazi nzuri ambayo inaendelea kufanywa na uongozi kwa kushirikiana na Mkoa.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa uhakika ubora huduma Wizara ya Afya Dkt. Eliakim Eliud amewataka watoa huduma kuhakikisha wanafuata miongozo ya kujikinga ya utoaji huduma (IPC guidelines) wakati wa kuhudumia wagonjwa ili kujikinga wao na wagonjwa wanaowahudumia.

Mwisho.

Alhamisi, 20 Agosti 2020

HATUNA UHABA WA CHANJO NCHINI- DKT. LEONARD SUBI

- Hakuna maoni

Mkurugenzi wa Tiba Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na watoto Dkt. Leonard Subi, akisisitiza jambo mbele ya Waandishi wa habari wakati alipofanya ziara katika ghala la chanjo lililopo katika Hospitali ta Rufaa ya Mkoa wa Dodoma-General.


HATUNA UHABA WA CHANJO NCHINI: DKT. LEONARD SUBI

Na. Catherine Sungura,WAMJW-Dodoma

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imesema kuwa, haina upungufu wa chanjo wa aina yeyote hivyo kuwataka wazazi/walezi kuwapeleka watoto wao kuwapatia chanjo katika vituo vya kutolea huduma za afya.

Hayo yamesemwa leo na Mkurugenzi wa Kinga kutoka Wizara ya Afya Dkt. Leonard Subi wakati alipotembelea ghala ya kuhifadhia chanjo iliyopo hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma kukagua hali ya chanjo katika mkoa huo.

Dkt. Subi amesema kuwa, chanjo zote aina tisa ambazo zinakinga dhidi ya magonjwa kumi na tatu zipo kwenye ghala hilo“tulikua na upungufu wa aina mbili za chanjo nchini kati ya tisa ambazo tumekuwa tukizitoa lakini, sasa hivi chanjo zote zipo, kwani zimeshawasili hapa nchini na usambazaji unaendelea”, amesema Dtk. Subi

Hata hivyo Dkt. Subi amesema kuwa, upungufu huo wa chanjo ulitokea baada ya Dunia kukumbwa na janga la mlipuko wa ugonjwa wa COVID-19 ambapo anga zote zilifungwa kwani chanjo husafirishwa kwa mnyororo baridi, kwahiyo huitaji usafiri wa anga.

“Tunamshukuru Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kwa kulifungua anga la Tanzania ambapo,  chanjo sasa zimeanza kuingia nchini na hadi sasa mikoa kumi na tatu(13) chanjo hizi zimeshapokelewa kati ya mikoa 26, na mikoa mingine kumi na tatu  ya Tanzania Bara usambazaji unaendelea kupitia Bohari ya Dawa (MSD)”.

Aidha, Dkt. Subi alisema kuwa, usambazaji wa chanjo hizo mbili ambazo wananchi walikua wanazikosa, umeshaanza na watazipata kwa uhakika, huku akielekeza bohari ya dawa nchini (MSD) kuhakikisha chanjo zote  zimefika katika mikoa iliyosalia ya Tanzania Bara ifikapo mwishoni mwa wiki hii.

“Waganga Wakuu wa Mikoa na Halmashauri wote nchini hakikisheni chanjo hizo mnazipeleka kwenye vituo vyetu  vya kutolea huduma za afya na muwajulishe wananchi kwamba chanjo zipo na zinapatikana bila malipo yeyote, wazazi na walezi pelekeni watoto wenu kupata chanjo katika mikoa yenu”Alisisitiza Dkt. Subi.

Kwa upande wa taarifa iliyotolewa na moja ya chombo cha habari hapa nchini kwa kukosekana kwa chanjo ya kuzuia kuhara (Rota) Dkt. Subi alifafanua kuwa, nchi ya Tanzania haijawahi kukosa chanjo hiyo,huku akiweka bayana kuwa, chanjo zilizopungua kwa mwezi mmoja na nusu ni chanjo ya Polio na Surua-Rubella hali iliyosababishwa na mlipuko wa Covid-19 Duniani, huku akisisitiza kuwa serikali imekua ikinunua chanjo hizo kutoka nchi za Ulaya na Asia.

Aliendelea kusema kuwa, Serikali inaendelea kutoa fedha za chanjo, na kuweka wazi kuwa hadi sasa  imetoa zaidi ya  shilingi bilioni 18 kwa ajili ya ununuzi wa chanjo  na kuifanya  Tanzania kuendelea kuwa katika kiwango cha juu cha utoaji wa chanjo kwa zaidi ya asilimia 98 kwa miaka sita mfululizo.

Hata hivyo, Dkt. Subi amesema kuwa, Tanzania haijawahi kupata mgonjwa wa kupooza tangu mwaka 1996, jambo linalotokana na  uwepo wa hali nzuri ya upatikanaji wa chanjo, huku akidai kuwa nchi ya Tanzania tayari imepata cheti cha utambuzi kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) mwaka 2015.

 

MWISHO.