Jumanne, 23 Oktoba 2018

DKT. NDUGULILE AAGIZA WATUMISHI WA AFYA KUZINGATIA MAADILI YA UTUMISHI WA UMMA KATIKA UTENDAJI WAO.
Jumanne, Oktoba 23, 2018
-
Hakuna maoni
![]() |
| Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akikagua ujenzi wa majengo mapya katika kituo cha afya cha Lupiro wilayani Luanga, Mkoa wa Morogoro. |
Jumatatu, 22 Oktoba 2018
MAAFISA AFYA WATAKIWA KUSIMAMIA USAFI WA MAZINGIRA ILI KUTOKOMEZA MALARIA
Jumatatu, Oktoba 22, 2018
-
Hakuna maoni
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy
Mwalimu akisisitiza jambo mbele ya Wabunge wa kamati ya Huduma za Jamii
na Wadau wa Masuala ya Afya (hawapo kwenye picha) katika uzinduzi wa
taarifa ya utafiti wa Viashiria vya Malaria nchini.
Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya
TAKWIMU Dkt. Albina Chuwa akionesha Kitabu cha Taarifa ya Takwimu za Viashiria vya Ugonjwa wa Malaria mbele ya Wabunge wa Kamati ya Huduma za Jamii na Wadau wa Masuala ya Afya wakati wa uzinduzi wa
taarifa ya utafiti wa Viashiria vya Malaria nchini.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakioneshana jambo na Mkurugenzi Mkuu wa Ofisi ya Taifa ya TAKWIMU Dkt. Albina Chuwa (wakatikati).
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy
Mwalimu akikata utepe kuashiria uzinduzi rasmi wa taarifa ya utafiti wa
Viashiria vya Malaria nchini uliofanyika leo jijini Dar es salaam.
Wabunge wa Kamati ya Huduma za Jamii na Wadau wa Masuala ya Afya
wakifuatilia taarifa ya Utafiti ya Viashiria vya ugonjwa wa Malaria
nchini iliyokuwa ikisomwa na Mgeni rasmi Waziri wa Afya Mhe. Ummy
Mwalimu (hayupo kwenye Picha) jijini Dar es salaam.
Picha ya pamoja ikiongozwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakati wa uzinduzi wa taarifa
ya utafiti wa Viashiria vya Malaria nchini.
MAAFISA AFYA WATAKIWA KUSIMAMIA USAFI WA MAZINGIRA ILI KUTOKOMEZA MALARIA
Na WAMJW – Dar Es Salaam.
Waziri
wa Afya, Maendeleo ya Jamii, jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu
amewaagiza Maafisa Afya nchini kusimamia kwa ukamilifu usafi wa
mazingira katika jamii ili kutokomeza ugonjwa wa Malaria.
Waziri
Ummy ametoa agizo hilo leo Oktoba 22, 2018 wakati akizindua Taarifa ya
Utafiti wa Viashiria vya Ugonjwa wa Malaria wa Mwaka 2017 katika Ukumbi
wa Karimjee jijini Dar Es Salaam
“Nawaagiza Maafisa
Afya, badala ya kupoteza muda mwingi wa kukagua migahawa, bucha za
nyama na sehemu ambazo wanajua zinaleta fedha, tunataka pia wajikite
katika kusimamia usafi wa mazingira katika Kata, Vijiji na Mitaa
yetu”Alisema Mhe. Ummy.
Katika kuhakikisha hali ya
usafi wa mazingira inakuwa endelevu, Waziri Ummy ameagiza Mabalaza yote
ya Halmashauri nchini kuweka Sheria na adhabu kali kwa wote ambao
wamekuwa wagumu katika kushiriki katika usafi wa mazingira huku Waganga
Wakuu wa Halmashauri zote nchini kuhakikisha wanasimamia vyema
utekelezaji wa kanuni na sheria za afya na usafi wa mazingira jambo
ambalo litaibua chachu ya ushindi katika mapambano dhidi ya Ugonjwa wa
Malaria.
“Niyatake
Mabalaza ya Hamashauri kuweka hatua kali, sheria kali na adhabu kali kwa
wote ambao hawashiriki katika usafi wa mazingira” alisema Waziri Ummy.
Licha
ya hivyo Waziri Ummy alisema kuwa Serikali kupitia Wizara inaendelea
kutekeleza Mpango endelevu wa ugawaji vya ndarua kupitia wanafunzi wa
shule za msingi, kupitia Kliniki za wajawazito na watoto, ambayo
hujulikana kama Chandarua Kliniki huku hadi sasa jumla ya vyandarua
milioni 31 vimeshagawiwa nchini kote.
Aidha, Waziri
Ummy alisema kuwa Matokeo ya mpango endele u wa ugawaji wa vyandarua
yameonesha kuwa asilimia 78 ya kaya nchini Tanzania zinamiliki angalau
chandarua kimoja chenye dawa, Katika utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto
na Viashiria vya Malaria wa mwaka 2015-16, ni asilimia 66 tu za kaya
zilikuwa zinamiliki angalau chandarua kimoja chenye dawa huku Umiliki wa
vyandarua vyenye dawa ni wa kiwango cha juu kwa kaya za mijini
(asilimia 81) ikilinganishwa na kaya za vijijini (asilimia 77).
Kwa
upande mwingine Waziri Ummy alitaja Halmashauri zenye maambukizi ya
kiwango cha juu ni pamoja na Kakonko 30.8%, Kasulu DC 27.6%, Kibondo DC
25.8%, Uvinza 25.4%, Kigoma DC 25.1%, Buhigwe 24%, Geita DC 22.4%,
Nanyamba TC 19.5%, Muleba DC 19.4%, Mtwara DC 19.1%, huku Halmashauri
zenye maambukizi ya kiwango cha chini ya asilimia 0.1 ni Mbulu TC,
Mbulu DC, Hanang, Hai, Siha, Moshi MC, Mwanga, Kondoa TC, Meru DC,
Arusha CC, Arusha DC, Munduli, Ngorongoro, Rombo DC
MWISHO
Ijumaa, 19 Oktoba 2018

DKT. NDUGULILE AAHIDI UJENZI WA HOSPITALI MPYA YA WILAYA YA RUFIJI.
Ijumaa, Oktoba 19, 2018
-
Hakuna maoni
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akikagua dawa zilizopo katika stoo ya Hospitali ya Utete wilayani Rufiji kuhakikisha kama zina nembo ya serikali wakati wa muendelezo wa ziara yake katika mkoa wa Pwani.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile ameahidi ujenzi wa Hospitali mpya ya Utete ili kuboresha huduma za afya wilayani Rufiji.
Dkt. Ndugulile amesema hayo wakati alipokuwa anaendelea na ziara katika Mkoa wa Pwani ambapo alionekana kutoridhishwa na majengo ya Hospitali hiyo kongwe iliyojengwa kipindi cha ukoloni na majengo yake yakionekana chakavu.
"Naomba niwe balozi wenu, nimejionea mwenyewe majengo ya Hospitali hii, kwa kweli ni chakavu sana” alisema Dkt. Ndungulile na kuendelea “sasa baada ya nyinyi kuomba serikali ifanye ukarabati wa Hospitali hii, mimi nitahakikisha tunapata pesa ya kujenga Hospitali mpya"
Aidha, Dkt. Ndugulile alionekana kutoridhishwa na nyumba wanazoishi madaktari wa Hospitali hiyo huku zikionekana kuwa chakavu zinazohatarisha maisha ya watu wanaoishi humo na kuahidi kuzifanyia ukarabati ikiwa ni pamoja na kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga nyumba mpya za kisasa.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Rufiji Juma Abdallah amesema hali ya watumishi katika sekta ya afya siyo nzuri hasa kwa wenye taaluma mbalimbali. Amesema kuna upungufu wa asilimia 49 ya watumishi wenye ujuzi unaohitajika, huku akifafanua upungufu mkubwa katika kada ya wauguzi.
"Katika kada ya wauguzi tuna upungufu wa wauguzi 146, Madaktari 4, madaktari wasaidizi 11, wataalam wa mionzi 15, wataalam wa maabara 8, ustawi wa jamii 5, maafisa afya 12, makatibu wa afya 3 na watunza kumbukumbu za Hospitali 10". Amesema Mkuu huyo wa wilaya.
Pia amesema wilaya hiyo haina daktari bingwa wa aina yeyote na mtaalamu wa mionzi baada ya aliyekuwepo kuondoka mara baada ya kuripoti kwa maelezo kuwa mazingira ya Rufiji siyo rafiki kwake.
Kwa upande wa hali ya upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi, Mkuu wa Wilaya hiyo amesema upatikanaji wa wake ni wa wastani. Hadi kufikia mwezi Septemba 30, 2018 dawa zinazofuatiliwa Tracer Medicine upatikanaji wake ni asilimia 90.6 na dawa zingine upatikanaji wake ni kwa zaidi ya asilimia 55.
Kufuatia hali hiyo, Naibu Waziri amemuagiza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Pwani Dkt. Yudas Ndungile kuhakikisha anatafuta mtaalam wa mionzi kutoka Wilaya nyingine ili kutoa huduma katika wilayani humo. Aidha Dkt. Ndugulile ameahidi kufanyia kazi suala hilo la upungufu wa watumishi hao muhimu.
Wakati huo huo Dkt. Ndugulile alihitimisha ziara yake katika Mkoa wa Pwani kwa kutembelea vituo vya afya vya Ikwiriri ambacho kimekamilisha ujenzi ya Wodi ya watoto, wodi ya Wanawake, jengo la kuhifadhia maiti na jengo la kufulia nguo.
Kwa upande wa kituo cha afya Kibiti, Naibu Waziri huyo ameonekana kutoridhika na huduma za afya zinazotolewa katika kituo hicho na kuona kuna ubadhirifu wa fedha za umma katika ujenzi wa miundombinu ya maabara, wodi na chumba cha upasuaji huku akiagiza kamati ya ulinzi na usalama kuchunguza na kuwachukulia hatua wote watakaobainika na ubadhirifu wa fedha za umma.
Katika kuhitimisha ziara yake katika Mkoa wa Pwani Dkt. Ndugulile alitembelea ujenzi wa kituo cha Bungu kwa lengo la kukagua miundombinu na hali ya utoaji huduma za afya, ambapo aliridhishwa na maendeleo ya kituo hicho na kuahidi serikali kuendelea kusaidia katika ujenzi huo lengo likiwa ni kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi.
MWISHO
Jumatano, 17 Oktoba 2018

MARUFUKU MGONJWA KWENDA KUNUNUA DAWA NJE IKIWA DAWA ZIPO
Jumatano, Oktoba 17, 2018
-
Hakuna maoni
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt.
Faustine Ndugulile (katikati) akisikiliza maelezo kutoka kwa Fundi
msanifu wa wilaya ya Mafia Ramadhan Madenge kuhusiana na mchoro wa kituo
cha afya cha Kilongwe.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt.
Faustine Ndugulile (katikati) akisikiliza maelezo kutoka kwa Mwenyekiti
wa kijiji cha Kifinge Hamis Omary (kushoto) wakati alipotembelea kuona
maendeleo ya ujenzi wa zahanati ya kijiji hicho.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt.
Faustine Ndugulile (kushoto) akionesha moja ya dawa za serikali wakati
alipofanya ziara kuona hali ya utoaji wa huduma za afya katika Hospitali
ya wilaya ya Mafia kuona.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt.
Faustine Ndugulile akisikiliza maelezo kutoka kwa mganga mkuu wa wilaya
ya Mafia Dkt. Zuberi Mzige kuhusiana na mchoro wa jengo la huduma kwa
wagonjwa wa bima ya afya wakati wa ziara katika Hospitali ya Wilaya
hiyo.
MARUFUKU MGONJWA KWENDA KUNUNUA DAWA NJE IKIWA DAWA ZIPO.
Na WAMJW-MAFIA
SERIKALI
kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
imepiga marufuku kwa watoa dawa kuwaandikia wagonjwa kwenda kununua
kwenye maduka binafsi ikiwa kwenye kituo kuna dawa na vifaa tiba vya
kutosha.
Hayo yamezemwa
na Naibu Waziri wa Afya , Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto
Dkt. Faustine Ndugulile wakati alipotembelea Hospitali ili kuangalia
hali ya utoaji huduma Wikayani Mafia .
"Nauagiza
uongozi wa hospitali ya wilaya ya Mafia mkoani Pwani kuwarudishia
wagonjwa wote gharama za vifaa tiba na dawa walizonunua katika maduka
binafsi ambazo zinapatikana Hospitalini hapo" alisema Dkt. Ndugulile.
Aidha
Dkt. Ndugulile amesema kuwa amebaini baadhi ya wagonjwa walioandikiwa
kwenda kununua dawa na vifaa tiba katika maduka binafsi huku baadhi ya
dawa hizo zikiwepo katika stoo ya kuhifadhia dawa.
Dkt.
Ndugulile amemuagiza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri na Mganga Mkuu
wa Wilaya ahakikishe wanawarudishia wagonjwa wote gharama walizotumia
kununua dawa nje ya Hospitali hiyo.
Pia
Dkt. Ndugulile alishangazwa na Hospitali hiyo kutokuwa na dawa na vifaa
tiba muhimu huku serikali ikiwa imetenga kiasi cha Tsh. Bilioni 270
kuanzia mwaka 2015/16 kutoka bilioni 31 za hapo awali, ikiwa na lengo la
kuhakikisha dawa zote zinapatikana katika Hospitali na vituo vyote vya
afya nchini.
Vikevike
Dkt. Ndugulile ameuagiza uongozi wa wilaya ya Mafia kuhakikisha bajeti
ya dawa inapitiwa yakinifu na kutekelezwa ili kuepuka changamoto ambazo
zinaweza kuepukika za ukosefu wa dawa na vifaa tiba muhimu na kuleta
usumbufu kwa wakazi wa wilaya hiyo.
Amebaini
upungufu huo wa dawa na vifaa tiba baada ya kutembelea wodi za watoto
na akina mama waliojifungua na kuelezwa na baadhi ya wagonjwa hao
kununua dawa na vifaa tiba vya kusaidia kujifungua nje ya Hopitali hali
ambayo imekua kero kwa wagonjwa wanaoenda kutibiwa katika Hospitali
hiyo.
Wakati huo huo Dkt.
Ndugulile amesitisha ukarabati wa jengo la wagonjwa wa bima baada ya
kuona kuna ubadhirifu wa fedha ambao hauendani na mazingira halisi ya
ukarabati huo.
Pamoja na
hayo Dkt. Ndugulile amefanya ziara katika kituo cha afya cha Kilongwe
na zahanati ya kifinge na kutoridhishwa na maendeleo ya vituo hivyo
huku akibaini utaratibu usiofaa wa manunuzi ya vifaa vya ujenzi na
kuamuru Halmashauri hiyo ifuate utaratibu wa manunuzi wa Force Account.
Sambamba
na hilo Dkt. Ndugulile alisitisha mara moja ukarabati wa jengo katika
zahanati hiyo huku akiagiza kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya
ikishirikiana na kamati ya ujenzi kufuatilia uhalisia wa gharama hiyo.
Kwa
upande wake Mkuu wa Wilaya ya Mafia Shaibu Mnunduma amemshukuru Naibu
waziri huyo kufanya ziara kisiwani humo huku akiahidi kuzifanyia kazi
changamoto zote zilizobainika ili kutoa huduma bora za afya kwa wananchi
wa wilaya hiyo.
Naye
Fundi msanifu wa Wilaya ya Mafia Ramadhan Madenge alisema kuwa kuna
ukarabati wa jengo hilo unagharimu takribani Tsh. Milioni 94.
Jumamosi, 13 Oktoba 2018

DKT NDUGULILE AGAWA KADI ZA BIMA YA AFYA KWA WASANII ZAIDI YA 100
Jumamosi, Oktoba 13, 2018
-
Hakuna maoni
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt Faustine Ndungulile akisema jambo katika mkutano wa Umoja wa Wasanii wa Muziki uliofanyika katika
ukumbi wa NSSF Ilala, Jijini Dar es salaam.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto (katiki mstari wa chini) katika picha ya pamoja na wadau wa mkutano Umoja wa Wasanii wa Muziki uliofanyika katika ukumbi wa NSSF Ilala, Jijini Dar es salaam huku akiwa ameshika sampuli za kadi ya bima ya afya.
Wadau wa mkutano wa Umoja wa Wasanii wa Muziki wakisikiliza mada.
Na. WAMJW - DAR ES SALAAM.
Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe Dkt Faustine Ndugulile, leo tarehe 13/10/2018 ameshiriki katika mkutano wa Umoja wa Wasanii wa Muziki uliofanyika katika ukumbi wa NSSF Ilala, Jijini Dar es salaam.
Akizungumza kabla ya kukabidhi Kadi hizo za bima ya Afya Mhe Ndugulile mewataka wasanii kutumia vipaji vyao kuelimisha jamii hususani katika masuala mbalimbali yanayohusu jamii kama unyanyasaji wa kijinsia na unyanyasaji wa watoto.
Vilevile amewahasa wasanii kuzingatia maadili ya taifa katika kufanya kazi zao kwani wapo waimbaji ambao wamekuwa wakikiuka maadili na nyimbo zao zinapofungiwa wanalalamika bila kujua kuwa wao ndio wenye makosa.
Akijibu ombi la wasanii kuwapa kipaumbele cha bei nafuu ya bima ya afya, Mhe. Ndugulile amesema kuwa kwa kuzingatia kuwa kugharamia huduma za afya ni changamoto, serikali imetoa maelekezo kwa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) kuweka vifurushi rafiki kwa wananchi wa kawaida vitakavyoendana na mahitaji ya mwananchi mmoja mmoja kuchagua kulingana na Mahitaji yake.
Aidha, Mhe Ndugulile amesema serikali ikitoa sera mpya ya afya itamtaka kila mwananchi kujiunga na bima ya afya kwa lazima ili watu wote waweze kupata matibabu kwa urahisi pindi wanapoenda katika vituo vya kutolea huduma za afya.
Akizungumzia matibabu bure kwa wazee, Mhe Ndugulile amesisitiza kuwa katika Sera Mpya ya Afya itakayotolewa na serikali itaboresha zaidi na kuweka utaratibu mzuri wa kuwahudumia wazee kwani kutokana na utafititi uliofanywa na Wizara, magonjwa mengi ya wazee ni yale ambayo yanajulikana na mara nyingi si ya kuambukiza.
Pia amewataka Mfuko wa Bima ya Afya (NHIF) na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) kuendelea kubaini changamoto na kufanya maboresho ya namna bora zaidi ya kuwapatia bima za afya wananchi hasa wale ambao hawako katika mfumo rasmi wa ajira.
UMEZAJI DAWA NDIYO SULUHISHO KAMILI KATIKA KUDHIBITI MAGONJWA YALIYOKUWA HAYAPEWI KIPAUMBELE.
Jumamosi, Oktoba 13, 2018
-
Hakuna maoni
Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Bi. Christina Mndeme (aliyesimama) akisema jambo katika Semina ya uraghibishaji na uhamasishaji wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele iliyojumuisha Wakuu wa Wilaya pamoja wataalam mbalimbali toka Mamlaka za Serikali za Mitaa za Mkoa wa Ruvuma (hawapo pichani)
Kaimu Meneja wa Mpango wa Kudhibiti Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbe Kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bwana Oscar Kaitaba (aliyesimama) akiongea na washiriki wa Semina ya uraghibishaji na uhamasishaji wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele iliyojumuisha Wakuu wa Wilaya pamoja wataalam mbalimbali toka Mamlaka za Serikali za Mitaa za Mkoa wa Ruvuma (hawapo pichani)
Mratibu wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Mkoa wa Ruvuma Dkt. Charles Hinju (aliyesimama) akitoa mada katika Semina ya Uraghibishaji na uhamasishaji wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele kwa Viongozi wa Wilaya na Wataalam toka Mamlaka za Serikali za Mitaa Mkoa wa Ruvuma.
Viongozi pamoja na wataalam toka Mamlaka za Serikali za Mitaa Mkoa wa Ruvuma wakisikiliza mada katika Semina ya Uraghibishaji na uhamasishaji wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele iliyofanyika katika Ukumbi wa Mipango Mkoani Ruvuma.
Na WAMJW - RUVUMA
Pamoja na juhudi zinazofanywa na
Serikali na wadau mbalimbali katika kudhibiti magonjwa yaliyokuwa hayapewi
kipaumbele, mwamko wa wananchi wa Mkoa wa Ruvuma kutumia kingatiba bado upo
chini hivyo kukwamisha malengo yaliyokusudiwa.
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa
Ruvuma Bi. Christina Mndeme alipokuwa akifungua semina ya uraghibishaji na
uhamasishaji wa kudhibiti magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele kwa Wakuu wa
Wilaya pamoja na wataalam wa Mamlaka za Serikali za Mitaa za Mkoa wa Ruvuma
iliyofanyika katika ukumbi wa mipango Oktoba 13, 2018.
Mkuu huyo wa Mkoa aliyataja
magonjwa ambayo bado yanaendelea kusumbua wananchi mkoani humo kuwa ni; Usubi,
Minyoo ya tumbo pamoja na kichocho huku akiwapongeza wataalam kwa kufanikiwa
kwa kiasi kikubwa kudhibiti magonjwa ya Vikope (trakoma), Matende pamoja na
Mabusha.
Bi. Mndeme amesema kuwa sehemu
kubwa ya jamii bado haijahamasika kumeza dawa kutokana na uelewa mdogo wa
athari za magonjwa hayo huku wananchi wengi bado wakiwa na imani potofu juu ya
dawa hizo.
“Magonjwa haya yamekuwa yakiathiri
rika zote katika jamii, tumeona Watoto wakishindwa kwenda shuleni na
kusababisha taaluma kushuka huku kwa watu wazima wakipata ulemavu wa kudumu
hivyo kushusha nguvu kazi ya Taifa” alisema Bi Mndeme.
Naye Meneja wa Mpango wa Kudhibiti
Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya
Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bwana Oscar Kaitaba, amesema kuwa lengo la
Serikali ni kuhakikisha kuwa magonjwa hayo yanadhibitiwa kikamilifu hivyo
kuwaomba wataalam walioshiriki semina hiyo kusaidia Serikali katika kuelimisha
na kuhamasiha jamii kutumia kingatiba ili kudhibiti magonjwa hayo.
“Njia bora ya kudhibiti magonjwa
haya ni kuhakikisha wananchi katika maeneo tunayotoka wanakunywa dawa zinazopatikana
katika hospitali zetu” Alisema Bwana Kaitaba.
Kwa upande wake Mratibu magonjwa
yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Mkoa wa Ruvuma Dkt. Charles Hinju amesema
shughuli ya kuhamasisha wananchi kumeza kingatiba bado inaendelea kutolewa licha
ya changamoto wanazokutana nazo.
“Kwa mwaka 2016 jumla ya watu 1,052,907 kati ya 1,420,317 walipata kingatiba sawa na asilimia 74 huku
kwa mwaka 2017 watu 1,192,390 kati ya 1,413,751
walipata kingatiba sawa na asilimia 84.3” alisema DKt. Hinju.
Dkt. Hinju amezitaja changamoto za
kuchelewa kwa dawa na rasilimali fedha kuwa zinaathiri ufanisi wa kazi huku pia
Halmashauri nyingi hazitengi fedha ili kufanikisha kazi ya kukabiliana na
magonjwa hayo.
Akifunga semina hiyo, Mkuu wa Mkoa
wa Ruvuma Bi. Christina Mndeme ameishukuru Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto kwa kuandaa Mpango huo wa kudhibiti magonjwa hayo na
kuishauri Wizara kuandaa vipindi maalum kwenye vyombo vya habari ili kuhamasisha
jamii kumeza dawa za kutibu magonjwa hayo huku akiwataka wataalam katika maeneo
wanayotoka kuelimisha jamii kuachana na imani potofu juu ya dawa hizo.
Aidha Mkuu huyo wa Mkoa amewataka
Waganga Wakuu wa Wilaya kuwa na takwimu sahihi za idadi ya watu wanaofika
katika vituo vya afya na hospitali ili kusaidia katika maombi ya dawa toka
bohari kuu ya dawa.
MWISHO
Alhamisi, 11 Oktoba 2018

TAARIFA KWA UMMA
Alhamisi, Oktoba 11, 2018
-
Hakuna maoni
JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO
WIZARA YA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO
TANGAZO KWA UMMA
Katibu
Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
(Afya) anawatangazia watumishi wote waliopata udahili wa kusoma masomo
ya Shahada ya Uzamili (Masters Degree) katika fani za Afya kwa mwaka
2018/2019, kwamba Wizara inaanza kupokea maombi ya Ufadhili kwa mwaka
2018/2019. Maombi haya yatawasilishwa kwa njia ya kielektroniki kwa
kujisajili kupitia fomu zilizopo kwenye tovuti ya Wizara www.moh.go.tz (https://sponsorship.moh.go.tz ).Maombi
yatakayofanyiwa kazi ni yale yaliyowasilishwa kwa njia ya mfumo huu tu,
hivyo waombaji waliowasilisha maombi yao kabla ya tangazo hili
wanapaswa kurudia kuomba kupitia utaratibu huu.
Ufadhili huu ni kwa ajili ya kulipiwa ada ya mafunzo (Tuition fee), pamoja na posho ya utafiti (Dissertation allowance).
Vigezo vitakavyotumika kuchagua ni hivi vifuatavyo :
Kuwasilishwa kwa maombi rasmi ya ufadhili kwa njia ya mfumo (online application)
Mwombaji kuwa Raia wa Tanzania.
Awe amedahiliwa Chuoni kuanza masomo kwa mwaka wa kwanza 2018/2019
Kipaumbele kitatolewa kwa:
Watumishi
wa Serikali waliomo kwenye sekta ya Afya wanaofanya kazi katika vituo
vilivyoko Wilayani/Mikoani hususani katika Hospitali za Rufaa za Mikoa
ambao baada ya mafunzo watarudi kuendelea kufanya kazi katika vituo vyao
vya awali, au watapangiwa vituo vya kazi sehemu nyingine yeyote nchini
Waombaji
waliodahiliwa katika fani ambazo ni za msingi katika utoaji wa huduma
za rufaa katika Hospitali za Rufaa za Mikoa. Nyanja hizo ni
Anaesthisiology, Surgery, Neurosurgery, Obstetrics and Gynaecology,
Orthopaedics Surgery, Emergency Medicine, Paediatrics, Internal
Medicine, Critical Care in Nursing na Midwifery and Womens Health,
Radio-pharmacy,Epidemiology and Lab.Management
Waombaji
waliodahiliwa katika nyanja za Ubingwa/Ubingwa wa Juu (Specialities na
Super-specialities) zenye umuhimu mkubwa katika Hospitali za Kitaifa
(kama Cardiology, Nephrology,Opthalmology, Radiography na Oncology)
ili kujenga uwezo wa ndani ya nchi katika jitihada za kupunguza wagonjwa
wa rufaa wanaotibiwa nje ya nchi.
Aidha, mwombaji atatakiwa aambatanishe nyaraka zifuatazo wakati wa kufanya maombi:
Barua ya ruhusa ya masomo kutoka kwa mwajiri wake
Barua ya udahili kutoka chuoni
Cheti cha taaluma
Cheti cha kuzaliwa
Mwisho wa kupokea maombi haya ni tarehe 10/11/2018.
Imetolewa na:
Katibu Mkuu,
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
Chuo Kikuu Dodoma,
Kitivo cha Sanaa na Sayansi ya Maendeleo ya Jamii
S.L.P 743
DODOMA
11/10/20

WAGONJWA WA MACHO 300 NCHINI WAFANYIWA UPASUAJI NDANI YA SIKU TANO
Alhamisi, Oktoba 11, 2018
-
Hakuna maoni
Jisajili kwenye:
Machapisho (Atom)



















