Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumanne, 23 Oktoba 2018

DKT. NDUGULILE AAGIZA WATUMISHI WA AFYA KUZINGATIA MAADILI YA UTUMISHI WA UMMA KATIKA UTENDAJI WAO.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akikagua ujenzi wa majengo mapya katika kituo cha afya cha Lupiro wilayani Luanga, Mkoa wa Morogoro.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akisikiliza kero kutoka kwa Florence Kilumanga wakati alipotembelea Hospitali ya Mahenge iliyopo wilayani Luanga mkoa wa Morogoro.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile (katikati) akitoa maelekezo kwa Mganga Mkuu wa Wilaya Dkt. Rajabu Risasi (kushoto) wakati alipotembelea Hospitali ya Mahenge iliyopo wilaya ya Ulanga mkoani Morogoro. Kulia ni Mkuu wa Wilaya hiyo Ngollo Malenya.

NA WAMJW-ULANGA


Naibu waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile amewaasa watumishi wa afya nchini kote kuzingatia maadili katika utendaji ili kutoa huduma za afya kwa wananchi kwa kiwango kilicho bora.

Dkt. Ndugulile amesema hayo wakati alipofanya ziara na kukagua hali ya utoaji wa huduma za afya katika Hospitali ya Mahenge iliyopo wilaya ya Luanga mkoani Morogoro.

Katika ziara hiyo, Dkt. Ndugulile alionekana kushangazwa na baadhi ya watoa huduma hospitalini hapo kutozingatia muda wa kuwepo kazini muda wote.

 Amebaini hilo wakati alipotembelea maabara ya Hospitali na kukuta kumbukumbu za mnyororo wa baridi hazijaandikwa ipasavyo, damu na vitendanishi vikiwekwa katika Friji moja na mpangilio mzima wa maabara hiyo kuwa mbovu.

“Niwakumbushe wataalamu wa maabara, taaluma ambazo wamezisoma hazibadiliki hata wakiwa kazini, kuna misingi ya taaluma ambayo tunayo, vitu vidogo kama Temperature Chart vinaonesha umakini na weledi kwa mwana taaluma ambaye tumemkabidhi jukumu lile”. Amesema Dkt. Ndugulile.

Kutokana na hali hiyo, Dkt. Ndugulile aliagiza kuondolewa msimamizi wa maabara Donald Masamaki na kuletwa mtu mwingine atakayezingatia taaluma na weledi katika utoaji wa huduma za maabara na afya kwa ujumla.

Aidha, Dkt. Ndugulile alishangazwa na malalamiko ya wananchi kuhusu wahudumu wa maabara kuwaagiza wagonjwa kwenda kupima Malaria katika vituo vya watu binafsi huku kipimo cha MRDT kikiwepo stoo ya dawa. Kufuatia hali hiyo Naibu Waziri huyo aliagiza Kamat ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya pamoja na Mkuu wa Wilaya hiyo Ngollo Malenya kufuatilia kwa ukaribu na kubaini ukweli wa jambo hilo na wale watakaobainika wachukuliwe hatua.

“Niwakumbushe watu wa maabara, nimkumbushe mganga mfawidhi kuhakikisha kwamba vipimo vyote vinakuwepo Hospitali. Nimepata malalamiko kutoka kwa wananchi, mpaka vipimo vya MRDT vya Malaria watu wanaambiwa wakapime nje”. Ameongeza Dkt. Ndugulile.

Pamoja na hayo, Naibu Waziri aliagiza kufanyiwa marekebisho kwa baadhi ya kasoro zilizoonekana Hospitalini hapo ikiwa ni pamoja na kuagiza kununuliwa mafaili ya kutunzia kumbukumbu za mgonjwa, kujengwa kwa sehemu ya kuchomea taka, kurekebisha mfumo wa mapato na kuiagiza bohari ya dawa (MSD) kuhakikisha dawa zote muhimu zinapatikana Hospitalini hapo.

Katika kuhitimisha ziara yake wilayani Ulanga, Dkt. Ndugulile aliahidi kuipatia Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga gari la wagonjwa (Ambulance) katika mgao unaofuata.

Naibu Waziri Dkt. Ndugulile alihitimisha ziara yake mkoani Morogoro kwa kutembelea kituo cha afya cha Lupiro na kukagua ujenzi wa majengo mapya ya chumba cha kuhifadhia maiti, wodi ya wanawake, maabara na nyumba ya daktari. Huku kwa kiasi kikubwa akionekana kuridhika na ujenzi wa kituo hicho.

0 on: "DKT. NDUGULILE AAGIZA WATUMISHI WA AFYA KUZINGATIA MAADILI YA UTUMISHI WA UMMA KATIKA UTENDAJI WAO."