Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumamosi, 13 Oktoba 2018

UMEZAJI DAWA NDIYO SULUHISHO KAMILI KATIKA KUDHIBITI MAGONJWA YALIYOKUWA HAYAPEWI KIPAUMBELE.

Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma, Bi. Christina Mndeme (aliyesimama) akisema jambo katika Semina ya uraghibishaji na uhamasishaji wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele iliyojumuisha Wakuu wa Wilaya pamoja wataalam mbalimbali toka Mamlaka za Serikali za Mitaa za Mkoa wa Ruvuma (hawapo pichani)

Kaimu Meneja wa Mpango wa Kudhibiti Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbe Kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bwana Oscar Kaitaba (aliyesimama) akiongea na washiriki wa Semina ya uraghibishaji na uhamasishaji wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele iliyojumuisha Wakuu wa Wilaya pamoja wataalam mbalimbali toka Mamlaka za Serikali za Mitaa za Mkoa wa Ruvuma (hawapo pichani)

Mratibu wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Mkoa wa Ruvuma Dkt. Charles Hinju (aliyesimama) akitoa mada katika Semina ya Uraghibishaji na uhamasishaji wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele kwa Viongozi wa Wilaya na Wataalam toka Mamlaka za Serikali za Mitaa Mkoa wa Ruvuma.
Viongozi pamoja na wataalam toka Mamlaka za Serikali za Mitaa Mkoa wa Ruvuma wakisikiliza mada katika Semina ya Uraghibishaji na uhamasishaji wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele iliyofanyika katika Ukumbi wa Mipango Mkoani Ruvuma.

Na WAMJW - RUVUMA

Pamoja na juhudi zinazofanywa na Serikali na wadau mbalimbali katika kudhibiti magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele, mwamko wa wananchi wa Mkoa wa Ruvuma kutumia kingatiba bado upo chini hivyo kukwamisha malengo yaliyokusudiwa.
Hayo yamesemwa na Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Bi. Christina Mndeme alipokuwa akifungua semina ya uraghibishaji na uhamasishaji wa kudhibiti magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele kwa Wakuu wa Wilaya pamoja na wataalam wa Mamlaka za Serikali za Mitaa za Mkoa wa Ruvuma iliyofanyika katika ukumbi wa mipango Oktoba 13, 2018.
Mkuu huyo wa Mkoa aliyataja magonjwa ambayo bado yanaendelea kusumbua wananchi mkoani humo kuwa ni; Usubi, Minyoo ya tumbo pamoja na kichocho huku akiwapongeza wataalam kwa kufanikiwa kwa kiasi kikubwa kudhibiti magonjwa ya Vikope (trakoma), Matende pamoja na Mabusha.
Bi. Mndeme amesema kuwa sehemu kubwa ya jamii bado haijahamasika kumeza dawa kutokana na uelewa mdogo wa athari za magonjwa hayo huku wananchi wengi bado wakiwa na imani potofu juu ya dawa hizo.
“Magonjwa haya yamekuwa yakiathiri rika zote katika jamii, tumeona Watoto wakishindwa kwenda shuleni na kusababisha taaluma kushuka huku kwa watu wazima wakipata ulemavu wa kudumu hivyo kushusha nguvu kazi ya Taifa” alisema Bi Mndeme.
Naye Meneja wa Mpango wa Kudhibiti Magonjwa Yaliyokuwa Hayapewi Kipaumbele kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bwana Oscar Kaitaba, amesema kuwa lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa magonjwa hayo yanadhibitiwa kikamilifu hivyo kuwaomba wataalam walioshiriki semina hiyo kusaidia Serikali katika kuelimisha na kuhamasiha jamii kutumia kingatiba ili kudhibiti magonjwa hayo.
“Njia bora ya kudhibiti magonjwa haya ni kuhakikisha wananchi katika maeneo tunayotoka wanakunywa dawa zinazopatikana katika hospitali zetu” Alisema Bwana Kaitaba.
Kwa upande wake Mratibu magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Mkoa wa Ruvuma Dkt. Charles Hinju amesema shughuli ya kuhamasisha wananchi kumeza kingatiba bado inaendelea kutolewa licha ya changamoto wanazokutana nazo.
“Kwa mwaka 2016 jumla ya watu 1,052,907 kati ya 1,420,317 walipata kingatiba sawa na asilimia 74 huku kwa mwaka 2017 watu 1,192,390 kati ya 1,413,751 walipata kingatiba sawa na asilimia 84.3” alisema DKt. Hinju.
Dkt. Hinju amezitaja changamoto za kuchelewa kwa dawa na rasilimali fedha kuwa zinaathiri ufanisi wa kazi huku pia Halmashauri nyingi hazitengi fedha ili kufanikisha kazi ya kukabiliana na magonjwa hayo.
Akifunga semina hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Bi. Christina Mndeme ameishukuru Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa kuandaa Mpango huo wa kudhibiti magonjwa hayo na kuishauri Wizara kuandaa vipindi maalum kwenye vyombo vya habari ili kuhamasisha jamii kumeza dawa za kutibu magonjwa hayo huku akiwataka wataalam katika maeneo wanayotoka kuelimisha jamii kuachana na imani potofu juu ya dawa hizo.
Aidha Mkuu huyo wa Mkoa amewataka Waganga Wakuu wa Wilaya kuwa na takwimu sahihi za idadi ya watu wanaofika katika vituo vya afya na hospitali ili kusaidia katika maombi ya dawa toka bohari kuu ya dawa.

MWISHO

0 on: "UMEZAJI DAWA NDIYO SULUHISHO KAMILI KATIKA KUDHIBITI MAGONJWA YALIYOKUWA HAYAPEWI KIPAUMBELE."