Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumanne, 6 Februari 2018

TIBA MTANDAO KUBORESHA HUDUMA ZA AFYA NCHINI



Na WAMJWW. Dom
Serikali imejipanga kutumia tiba mtandao kuboresha huduma za afya nchini kwenye hospitali zote za ngazi ya taifa, rufaa na wilaya ili kuwawezesha wagonjwa waishio sehemu mbali mbali nchini kupata huduma za afya kwa wakati na kwa ufanisi.

Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Mpoki Ulisubisya wakati akifungua kongamano la ubunifu na utekelezaji wa huduma za tiba mtandao Tanzania lililofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa jengo la LAPF, Dodoma.

Dkt. Ulisubisya amesema kuwa lengo la kongamano hilo ni kuwakutanisha watendaji wakuu wa hospitali za taifa nchini, madaktari bingwa wa sekta ya Afya, wakuu wa taasisi zinazoshughulika na sekta ya Afya, Wizara ya TAMISEMI, Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano; taasisi nyingine za Serikali; sekta binafsi na wabia wa maendeleo ili kujadiliana na kuwa na uelewa wa pamoja wa kufanikisha utekelezaji wa huduma za tiba mtandao ili kuboresha huduma za afya nchini.

Amesema kuwa tiba mtandao itawezesha na kuongeza ufanisi katika kufanya uchunguzi, utoaji wa tiba na madawa kwa wagonjwa wanaosumbuliwa na magonjwa mbalimbali yasiyoambukiza na yanayotokana na ajali za barabarani.
“Hadi hivi sasa ni asilimia 37 tu ya wagonjwa wa kifua kikuu ndio wanaotambulika na kupatiwa huduma na Wizara ya Afya katika hospitali mbalimbali nchini. Hivyo, tiba mtandao itawezesha upatikanaji wa wagonjwa na ufikishaji wa huduma kwao kwa wagonjwa wengine asilimia 63”, alifafanua Dkt. Ulisubisya.

Aliongeza kuwa tiba mtandao itapunguza gharama za wagonjwa na wanaowahudumia kusafiri kufuata madaktari. Aidha, amewataka wakuu hao wa taasisi kuwaruhusu wataalamu wao, wa Wizara ya TAMISEMI na wa Wizara ya Afya, kushiriki mafunzo ya tiba mtandao ili kuongeza ufanisi wao katika kuhudumia wagonjwa.

Amewataka wataalamu wa afya na wakuu wa taasisi zinazohusika na masuala ya afya kununua vifaa tiba vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) vyenye viwango na ubora unaohitajika ili kuwezesha tiba mtandao na manunuzi hayo yazingatie na kufuata ununuzi wa pamoja wa huduma na bidhaa za Serikali.
Vifaa vya kisasa vya TEHAMA vinavyohusika na tiba mtandao vitawawezesha wataalamu kufanya uchunguzi kwa mgonjwa, kupata majibu ya uhakika na kumpatia mgonjwa tiba inayostahili na ya uhakika. 
Aidha, amemuelekeza Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF), Eng. Ulanga, ambao ndio waanadaji na waratibu wa kongamano hilo, kushirikiana na TTCL kuhakikisha kuwa tiba mtandao inapatikana katika hospitali zote za rufaa na hospitali ambazo zina changamoto ya kijiografia ya kufikika kwa urahisi.

0 on: " TIBA MTANDAO KUBORESHA HUDUMA ZA AFYA NCHINI"