Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumatatu, 23 Oktoba 2017

SERIKALI YAONGEZA VITUO 100 KWA AJILI YA KUTOA HUDUMA ZA UCHUNGUZI NA MATIBABU YA AWALI YA SARATANI YA MLANGO WA KIZAZI NCHINI




Ndugu wanahabari,
Tanzania ni mojawapo ya nchi za kusini mwa Afrika zinazokadiriwa kuwa na  idadi kubwa ya wagonjwa na vifo vingi vitokanavyo na Saratani.  Takribani wagonjwa wapya 50,000 kila mwaka wanagundulika kuwa na Saratani, na idadi hii inakadiriwa kuongezeka kwa asilimia hamsini (50%) ifikapo mwaka 2020.

Taarifa kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road kwa kipindi cha mwaka 2006 hadi 2015 zinaonyesha kwamba aina za Saratani zinazoongoza hapa nchini ni kama ifuatavyo; Saratani ya mlango wa kizazi (34%),Saratani ya Ngozi (kaporsis Sarcoma)(13%), Saratani ya matiti (12%), Saratani ya mfumo wa njia ya chakula (10%), Saratani ya Kichwa na shingo (7%), Saratani ya Matezi (6%), Saeatani ya Damu (4%), Saratani ya Kibofu cha mkojo (3%),Saratani ya ngozi (3%), Saratani ya Macho (2%), na saratani ya tezi dume (2%).  Mbaya zaidi, asilimia 80 ya  wagonjwa wote hao wanafika Ocean Road wakiwa katika hatua za mwisho za  ugonjwa na kufanya matokeo ya matibabu kutokuwa mazuri.


Ndugu wanahabari,
Kupitia takwimu hizi ni dhahiri kuwa Saratani ya Mlango wa Kizazi husababisha vifo vingi kwa wanawake, ikifuatiwa na saratani ya matiti. Na kama ilivyo kwa saratani nyingine, asilimia 80 ya wanawake wanaougua saratani hiiwanafika katika vituo vya kutolea huduma za afya kwa ajili ya tiba wakiwa katika hatua za mwisho za ugonjwa, ambapo hufanya  matibabu kutokuwa na matokeo mazuri. Aidha Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kutibu wagonjwa  hawa.  Saratani ya Mlango wa kizazi inatibika endapo itagundulika mapema sambamba na kusaidia kupunguza gharama za matibabu ambazo Serikali, familia na mgonjwa wamekuwa wakikabiliana nazo.

Tangu mwaka 2008, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ilianza kutoahuduma ya uchunguzi kwa kutumia siki(acetic acid) na matibabu ya mabadiliko ya awali ya saratani ya mlango wa kizazi kwa kutumia tiba mgando (cryotherapy).Kwa kushirikiana na wadau mbalimbali, Wizara imeshaanzisha vituo 459 (vituo 343 vya serikali na 116 vya mashirika na watu binafsi) vinavyotoa huduma ya uchunguzi na matibabu ya mabadiliko ya awali ya Saratani ya Mlango wa Kizazi. Wizara inawapongeza na kuwashukuru wadauwote wanaoshiriki katika kuimarisha upatikanaji wa huduma hizi. Kipekee tungependa kutambau mchango wa Jhpiego, ICAP, EGPAF, THPS, Marie Stope, PSI, Umati, MEWATA, T Marc na WAMA.  Tunawashukuru sana!

Ndugu  wanahabari,
Katika kuhakikisha tunaongeza upatikanaji wa huduma za uchunguzi na matibabu ya awali ya Saratani ya Mlango wa Kizazi, Wizara ya Afya imekuja na mkakati wa kuboresha huduma hizi kwakununuamashine 100  za tiba mgando  (cryotherapy) na mashine  9 za upasuaji mdogo (LEEP) ambazo zitatumika kwa ajili ya matibabu ya awali ya saratani kwa wanawake watakaofanyiwa uchunguzi na kukutwa na mabadiliko ya awali ya saratani ya mlango wa kizazi. Pia tumenunua mitungi 173 ya gesi ya ‘’carbon dioxide‘’ itakayowezesha mashine hizo kufanya kazi. Vilevile, tumeshatoa mafunzo ya kuwajengea uwezo watoa huduma ili kuweza kutoa huduma hizi bila vikwazo. Vifaa hivi vimekwishawasili nchini na vinaanza kusambazwa katika vituo vya Tiba 100 nchini kuanzia kesho. Vifaa hivyo vitasambazwa katika mikoa 10, halmashauri 31 ambazo tumebaini zina vituo vichache vya kutolea huduma  hizi ukilinganisha na Mikoa mingine. Mikoa hii ni Mara, Singida, Geita, Dodoma, Tanga, Arusha, Manyara, Ruvuma, Lindi na Mtwara.

Ndugu  wanahabari,
Kupitia hatua hii, Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais, Mhe Dr. John Pombe Magufuli inaongeza idadi ya vituo vinavyotoa huduma za uchunguzi na matibabu ya awali ya saratani kutoka vituo 343 (2015) hadi vituo 443 (2017). Huduma hizi zinapatikana katika Hospitali zote za Rufaa za Kanda na Mikoa, Hospitali zote za Wilaya, na baadhi ya Vituo vya Afya na Zahanati.


Ndugu wanahabari,
Kupitia kwenu, napenda kuwahimiza wanawake kujitokeza kwa wingi kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya awali ya Saratani ya Mlango wa Kizazi katika vituo hivi. Huduma hizi zinatolewa katika kliniki ya afya ya mama na mtoto kila siku na bila malipo yoyote. Aidha ninavielekeza vituo vyote vya umma nchinikutenga siku maalumu katika kila mwezi ambayo kituo kitahamasisha wanawake kuja kwa wingi kupata huduma hizi. Na kwa kuwa mwezi wa Octoba kila mwaka ni mwezi wa uhamasishaji wa upimaji wa saratani ya matiti duniani kote,  nitumie fursa hii kutoa rai kwa wananchi hasa wanawake wenzangu kuhudhuria vituoni kupata huduma za uchunguzi mapema. Wananchi wengi wamekuwa wakipoteza maisha aidha kwa kutofahamu au uelewa mdogo kuhusu saratani.

Ndugu wananchi,
Aidha, katika kuhakikisha huduma hizi zinakuwa endelevu, nazielekeza halmashauri zote kutenga fedha za kutosha kuhakikisha huduma hizi zinaingizwa kwenye mipango yao ya bajeti ya vituo na halmashauri. Pia ni lazima wahakikishe mashine hizi zinatunzwa na kufanyiwa ukarabati inapobidi.Kwa upande wetu Wizara ya Afya, tutaendelea kusimamia ubora wa huduma zinazotolewa kulingana na miongozi, kujenga uwezo wa watoa huduma. Vilevile, tutahakikisha mafundi sanifu tiba wanapatiwa uelewa na nyezo za kufanya matengenezo madogo na ukarabati wa mashine hizi kwa kushirikiana na Halmashauri husika.

Kwa ujumla, Serikali  itaendelea kuhakikisha vituo zaidi vinaanzishiwa huduma hii ili ipatikane karibu zaidi na wananchi hasa wa vijijini. Vilevile, tutahakikisha tunapanua huduma za Rufaa za Matibabu ya saratani  nchini kwa kuhakikisha huduma za Tiba kwa kutumia dawa (Chemotherapy ) na Mionzi (Radiotherapy) zinapatikana katika  Hospitali za Rufaa za Kanda- Mbeya, Bugando na KCMC ili kupunguza msongano wa wagonjwa katika Hospitali ya Ocean Road, Dar es salaam.

ASANTENI  KWA KUNISIKILIZA

0 on: "SERIKALI YAONGEZA VITUO 100 KWA AJILI YA KUTOA HUDUMA ZA UCHUNGUZI NA MATIBABU YA AWALI YA SARATANI YA MLANGO WA KIZAZI NCHINI"