Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Ijumaa, 15 Juni 2018

HOTUBA YA MHESHIMIWA UMMY A. MWALIMU (MB) WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO KWENYE SHEREHE YA MAADHIMISHO YA SIKU YA WACHANGIA DAMU DUNIANI MKOANI DODOMA


Waziri wa Afya akiongea na Kanali Ramson Mwaisaka ambaye alishiriki uchangiaji wa damuwakati wa zoezi la uchangiaji damu linalofanyika Nyerere Square katika kilele cha maadhimisho ya siku ya kuchangia damu Duniani.

Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu akisoma kadi ya mchangiaji damu kutoka JKT Dodoma wakati wa zoezi la uchangiaji damu linalofanyika Nyerere Square katika kilele cha maadhimisho ya siku ya kuchangia damu Duniani





Waziri Ummy Mwalimu akiongea na mmoja wa wanawake waliofika kuchangia damu. Damu salama ni nguzo muhimu katika kuokoa vifo vitokanavyo na uzazi kwa akina mama wajawazito nchini wakati wa zoezi la uchangiaji damu linalofanyika Nyerere Square katika kilele cha maadhimisho ya siku ya kuchangia damu Duniani.


HOTUBA YA MHESHIMIWA UMMY A. MWALIMU (MB) WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO KWENYE SHEREHE YA MAADHIMISHO YA SIKU YA WACHANGIA DAMU DUNIANI MKOANI DODOMA TAREHE 14-6-2018


Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma,
Mheshimiwa Mstahiki Meya wa Jiji la Dodoma,
Mkurugenzi wa Tiba-MOHCDGEC,
Mganga Mkuu wa Mkoa-Dodoma,
Meneja wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama,
Waheshimiwa Viongozi wa Serikali na Vyama vya Siasa,
Viongozi wa Dini,
Mwakilishi wa CDC,
Mwakilishi Shirika la Afya Duniani,
Mwakilishi KOICA,
Ndugu  Wachangia Damu, 
Wanahabari,
Wasanii mbalimbali,
Wageni Waalikwa,
Mabibi na Mabwana.

Ndugu Wananchi,
Leo tarehe 14 Juni, 2018 tunaungana na Dunia Kuadhimisha Siku ya Wachangia Damu Duniani.  Hivyo, ninayo furaha kuungana na Watanzania na wananchi wa Dodoma  katika siku hii muhimu  kuwashukuru na  kuwaenzi Wachangia  Damu  wote ambao wamekuwa wakichangia damu, ili kuokoa maisha ya wagonjwa wanaohitaji huduma ya kuongezewa damu. Pamoja na hayo pia ninayo furaha kuona kuwa leo tunazindua Kikundi cha Wachangia Damu Wenye Kundi Adimu la Damu (Rare Blood Group Donor Club) hapa Mkoani Dodoma.
Ndugu Wananchi,
Ni kweli kwamba uchangiaji damu wa hiari bila malipo, ndiyo msingi wa upatikanaji wa damu iliyo salama. Wachangiaji damu wa hiari wanaorudia kuchangia mara kwa mara wapo salama na wanahusishwa na viwango vya chini vya magonjwa ambayo yanaweza kuambukizwa kwa njia ya damu kama virusi vya UKIMWI, homa ya ini na kaswende.  Naomba nitumie fursa hii kwa niaba ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kusema “ASANTENI SANA KWA WOTE AMBAO MMEKUWA MKICHANGIA DAMU KWA HIARI KUOKOA MAISHA YA WATANZANIA WENZETU”.
Ndugu Wananchi,
Kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ni "Jitoe kwa ajili ya mwingine. Changia damu. Okoa Maisha ya mwenzio" (Be there for someone else. Give blood. Share life).  Kauli mbiu ya mwaka huu inalenga kuonyesha mshikamano katika uchangiaji damu, inalenga mambo muhimu ambayo yanaonyesha thamani ya mwanadamu kama heshima, huruma, wema na kuwajali wengine ambavyo ndio msingi wa kuendeleza uchangiaji damu wa hiari bila malipo yoyote.

Ndugu Wananchi,
Huduma za Damu Salama Tanzania Bara zilianza mwaka 1946 kwa utaratibu wa ndugu wa mgonjwa kujitolea damu ya kumuongezea mgonjwa (Family Replacement). Hata hivyo mfumo huu wa kutoa damu kwa utaratibu wa ndugu wa mgonjwa kujitolea damu ulifanya damu kuwa adimu hasa panapotokea dharura.

Tokea kuanzishwa kwa Mpango wa Taifa wa Damu Salama, kumekuwa na ongezeko la ukusanyaji wa chupa za damu kutoka 52,000 (2006) hadi 233,593 (2017). Hata hivyo, ongezeko hili bado halijakidhi mahitaji ya nchi ambayo ni sawa na chupa 520,000 (asilimia moja ya wananchi; kwa takwimu za mwaka 2017 au chupa 10 kwa kila wananchi 1000). Kwa taarifa za Mpango za 2017, Mikoa iliyoongoza kwenye makusanyo ya damu ni Katavi (94% ya malengo), Lindi (79% ya malengo), Pwani (66% ya malengo). Mikoa ambayo haikufanya vizuri ni Songwe (16% ya malengo), Mbeya (20% ya malengo) na Tabora (22% ya malengo). 

Aidha, ili kuendana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano, Mpango wa Taifa wa Damu Salama wakishirikiana na Mikoa na Halmashauri za Wilaya, pamoja na Jeshi la Wananchi Tanzania wameweka lengo la kuongeza ukusanyaji damu kufikia chupa 375,000 mwaka 2018 ikiwa ni ongezeko la asilimia 72.  Vile vile, nimetoa maelekezo kwa Mpango wa Taifa wa Damu Salama kuweka mikakati na kuhakikisha wanakusanya chupa za damu 540,000 (asilimia moja ya wananchi kwa takwimu za mwaka 2018 ambapo inakadiriwa kuwa watanzania watakuwa 54,000,000) ambayo ndio mahitaji ya halisi ya chupa za damu nchini.  Uboreshaji wa huduma za damu salama nchini ni utekelezaji wa ilani ya CCM ya mwaka 2015, ambayo imelenga kuboresha na kuimarisha huduma ya Afya ya uzazi na mtoto nchini; na kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi ifikapo mwaka 2020.

Ili kuweza kufikia malengo haya kwa muda huu mfupi na kuendana na kasi ya Serikali ya Awamu ya Tano, napenda kutoa maelekezo kwa Mpango wa Taifa wa Damu Salama kuimarisha na kuboresha mifumo na utendaji kazi, ikiwa ni pamoja kufanya kazi kwa ukaribu na timu za kukusanya damu za Mikoa na Halmashauri, Timu za Kanda ya Jeshi (TPDF) na Chama cha Msalaba Mwekundu (TRCS).

Aidha, Wizara kwa kushirikiana na OR-TAMISEMI imeanzisha utaratibu wa kuwa na vituo vya benki za damu kwenye ngazi ya Mikoa ili visaidiane na Benki za damu za Kanda katika kuboresha upatikanaji wa damu salama hususani kwa akina mama wajawazito. Hadi sasa Vituo Vidogo vya Damu Salama za Mikoa 9 zimeanzishwa katika Mikoa ya Dar es Salaam, Lindi, Morogoro, Dodoma, Iringa, Kigoma, Shinyanga, Kagera na Mara. Lengo ni kuhakikisha kila Mkoa una Benki ya damu; na kuwa na uwezo wa kutoa huduma ya damu salama kwa kila anayehitaji ndani ya Mkoa. Hii ikiwa ni mojawapo ya jitihada za kuboresha huduma za afya pamoja na kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi. Katika bajeti ya mwaka 2018/2019, Wizara imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Vituo Vidogo vya Damu Salama za Mikoa 5, ikiwemo Mkoa wa Tanga, Ruvuma, Rukwa, Katavi na Geita.

Ndugu Wananchi,
Tumeshuhudia hospitali zetu za rufaa kama Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete, Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Hospitali ya Mifupa MOI, Hospitali ya Mloganzila na nyinginezo zinavyoboresha na kupanua wigo wa huduma za kitaalamu zinazopatikana nchini, kama vile kufanya operesheni za moyo, na kupandikiza figo.  Kuongezeka kwa operesheni hizi kunahitaji damu pamoja na mazao ya damu iliyo salama na ya kutosha, na yenye makundi mbalimbali. Hivyo jitihada zinazofanyika za kuongeza makusanyo ya damu zinaendana na azima ya Serikali kuhakikisha na kufanikisha huduma zote za kibingwa zinatolewa hapa hapa nchini. Kipaumbele kwa Wizara ni kuendelea kuboresha na kuimarisha huduma za kibingwa zitolewazo nchini katika kupunguza idadi ya wagonjwa wanaopewa rufaa ya matibabu nje ya nchi ili kupunguza gharama kubwa ambazo serikali inaingia katika kupeleka wagonjwa nje ya nchi. 

Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Wizara itaboresha upimaji wa kuhakiki usalama wa damu kwa kununua mashine za kisasa kupitia MSD na kusimikwa katika vituo vyetu vya Kanda . Mashine hizi ‘full automated machines’ zitakuwa na uwezo wa kupima sampuli nyingi kwa wakati mmoja. Hii itaongeza ufanisi katika upimaji wa maambukizi ya ukimwi, homa ya ini na kaswende na zitarahisisha upatikanaji wa damu salama kwa wakati katika vituo vya kutolea huduma. 

Vile vile, Wizara itanunua mashine za Apheresis nne (4), ambazo ni maalum na kisasa zinazotumika kukusanya damu na kutengeneza mazao ya damu. Faida za mfumo huu wa kutengeneza mazao ya damu kwa kutumia ‘Apheresis Machine’ utasaidia mchangiaji damu mmoja kuchangia kati ya dozi 2 hadi 3 za chembe sahani “platelets” zilizo katika viwango vya ubora wa juu. Tofauti na mfumo wa sasa ambao unahitaji wachangiaji 6 ili kupata dozi moja ya chembe sahani. Aidha, mashine hizi za apheresis zitawezesha upatikanaji wa mazao ya damu maalum yanayohitajika kutumiwa na madaktari katika kutoa huduma za kibingwa mfano matibabu ya cancer, upasuaji wa mishipa ya fahamu, moyo na upandikizaji wa figo.

Ndugu Wananchi,
Mpango wa Taifa wa Damu Salama (NBTS) umekuwa ukitekeleza mikakati mbalimbali katika usimamizi wa viwango na ubora katika huduma ya damu,  mkakati mmojawapo ni  kusajili Vituo Vyote vya Damu Salama vya Kanda kwenye mchakato wa utambuzi wa Ithibati (Accreditation) kwa kutumia viwango vya Shirika la Kimataifa la “Africa Society for Blood Transfusion” (AfSBT). Mpaka sasa nina taarifa kanda mbili za Kaskazini-Kilimanjaro, Mashariki-Dar-es-salaam, pamoja na Mpango wa Damu Salama Zanzibar, zimefanikiwa kupata vyeti vya utambuzi rasmi kwa kufika daraja la pili la Ithibati inayotolewa na “African Society for Blood Transfusion” (AfSBT) yaani ‘’Step II Certification’’. Nachukua fursa hii kupongeza Menejimenti na Wafanyakazi wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama kwa hatua hii. 
Ninatambua kupata cheti kuna manufaa yafuatayo; ni uthibitisho kuwa serikali kupitia Mpango wa Taifa wa Damu Salama sio tu unaongeza juhudi katika kukusanya damu lakini pia unaendelea kuboresha ubora wa huduma ya damu salama. Kupata vyeti vya utambuzi wa Ithibati utawezesha pia Huduma za Mpango wa Taifa wa Damu Salama kutambulika Kitaifa na Kimataifa; lakini pia utawezesha wananchi kupata huduma bora na kujenga imani kuwa Damu Salama inatoa huduma zinazokidhi viwango vya hali ya juu.
Maelekezo yangu kwa uongozi wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama; ni kuweka mikakati na kuhakikisha vituo vinne (4) vilivyobaki; Kanda ya Ziwa-Mwanza, Nyanda za Juu Kusini-Mbeya, Magharibi-Tabora na Kusini-Mtwara vinapata utambuzi wa Ithibati daraja la pili pia, na hatimaye kupata cheti cha Idhibati kwa huduma zote zinazotolewa na Mpango kwa maana ya kufikia ‘’Full Accreditation’’
Ndugu Wananchi,
Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kupitia Mpango wa Taifa wa Damu Salama umeanzisha Kikundi cha Wachangia Damu Wenye Kundi Adimu la Damu  (Rare Blood Group Donor Club) kama 0-negative, A-negative, B-negative na AB-negative katika kila Mkoa . Lengo ni kuweka msukumo na kuwakutanisha watu wenye kundi adimu la damu na kuwahamasisha wawe wanachangia damu mara kwa mara ili Taifa liwe na akiba ya kutosha ya damu. 

Tunataka kuhakikisha kuwa wagonjwa wenye kundi adimu la damu wanapata huduma za matibabu sawa na wagonjwa wengine na kuhakikisha vifo vyinavyosababishwa na ukosefu wa kundi adimu la damu vinapungua au havitokei kabisa. Hivyo basi nitoe rai kwa wananchi ambao wana kundi adimu la damu watuunge mkono na kujiunga katika klabu hizi. Vile vile, niwaombe Mashirika, Taasisi mbalimbali na vyombo vya habari kuwaelimisha wananchi wote wenye makundi adimu ya damu juu ya umuhimu wa kujiunga katika klabu hizi.

Ndugu Wananchi,
Kabla sijahitimisha napenda kutoa shukrani za dhati kwa Serikali ya Marekani kupitia Shirika la Kuzuia na Kudhibiti Magonjwa Centres for Disease Control and Prevention (CDC), Mfuko wa Dunia wa Magonjwa ya UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria (Global Fund), Shirika la Maendeleo ya Korea Kusini (KOICA) kwa kuendelea kugharimia uimarishaji wa Mpango wa Taifa wa Damu Salama hapa nchini katika masuala ya mfumo wa TEHAMA, viwango na ubora na mchakato wa Ithibati (Accreditation), upatikanaji wa vifaa tiba (equipments and reagents) na mafunzo ya kuwajengea uwezo watumishi. Pia nawashukuru wahisani na wadau wengine ambao kwa njia moja au nyingine wanaendelea kusaidiana na Mpango wa Taifa wa Damu Salama katika kuhakikisha damu inapatikana nchini.

Pia napenda kutambua jukumu na umuhimu wa vyombo vya habari katika juhudi zetu za pamoja za kuelimisha, kuhamasisha na kuongeza idadi ya wachangia damu wa hiari bila malipo.

Napenda kuvisihi vyombo vya habari kuendelea kushirikiana na Mpango wa Taifa wa Damu Salama, kujenga ufahamu wa umuhimu wa kuchangia damu kwa hiari, ili wananchi ambao wamekuwa na imani potofu kuhusu kuchangia damu wabadili imani zao na tabia, ili nao waanze kuchangia damu kwa hiari.

ASANTENI KWA KUNISIKILIZA
CHANGIA DAMU, OKOA MAISHA

0 on: "HOTUBA YA MHESHIMIWA UMMY A. MWALIMU (MB) WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO KWENYE SHEREHE YA MAADHIMISHO YA SIKU YA WACHANGIA DAMU DUNIANI MKOANI DODOMA"