Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Ijumaa, 26 Januari 2018

TAMKO KUELEKEA MAADHIMISHO YA SIKU YA UKOMA DUNIANI TAREHE 28/01/2018

Naibu Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akisisitiza jambo mbele ya waandishi wa Habari (Hawapo kwenye pich) pindi akitoa taarifa ya siku ya Ukoma Duniani, tukio lililofanyika mapema leo katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es salaam.

Waandishi wa Habari wakifuatilia taarifa kutoka kwa Naibu Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile(Hayupo kwenye picha) katika siku ya Ukoma Duniani, tukio lililofanyika mapema leo katika ofisi ndogo za Wizara ya Afya jijini Dar es salaam.


TAMKO LILILOSOMWA NA NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO, MHE. DKT. FAUSTINE NDUGULILE  (MB) KATIKA KUADHIMISHA SIKU YA UKOMA DUNIANI TAREHE 28/01/2018

Ndugu wanahabari,
Siku ya Ukoma Duniani huadhimishwa ulimwenguni kote kila Jumapili ya mwisho ya mwezi Januari. Kwa mwaka huu, siku hii itaadhimishwa tarehe 28 Januari, 2018. Mwaka huu imetimia  miaka 64 tangu siku hii ilipoasisiwa mnamo mwaka 1954 na mwandishi wa habari mfaransa Raoul Follereau kama njia ya kuelimisha na kuongeza uelewa duniani kuhusu ugonjwa huu wa kale ambao una kinga, unatibika  na mgonjwa kupona kabisa. 

Ndugu wanahabari,
Katika siku hii, Tanzania inaungana na mataifa mengine ulimwenguni kufanya maadhimisho hayo ili kuukumbusha umma na kuuelimisha juu ya uwepo wa ugonjwa huu hatari, athari mbaya za vidonda na ulemavu vinavyotokana na ukoma. Ni dhahiri kuwa ugonjwa wa ukoma umekuwa ukiogopwa sana na kusababisha unyanyapaa mkubwa katika jamii zetu hasa kutokana na ukweli kwamba unasababisha ulemavu wa kudumu  na kwa kiasi kikubwa waathirika hujikuta wakitengwa na kubaguliwa.

Pamoja na kwamba nchi yetu ilifikia viwango vya utokomezaji wa Ukoma kitaifa mnamo mwaka 2006 kwa kiwango cha chini ya mgonjwa 1 kati ya watu 10,000, Ukoma bado unaendelea kuwa tatizo la kiafya miongoni mwa jamii nchini kwetu. Kwa mujibu wa takwimu za Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua kikuu na Ukoma za mwaka 2016, jumla ya wagonjwa  wapya 2,047 waligunduliwa na hivyo kufanya kiwango cha ugunduzi kuwa watu 4 kwa kila watu 100,000. Takwimu hizi zinaifanya Tanzania kuendelea kuwa miongoni mwa nchi  22 zenye wagonjwa wengi wa ukoma duniani.




Takribani mikoa yote nchini mwetu inagundua na kutibu wagonjwa wa ukoma japo kwa viwango tofauti. Hivi sasa bado kuna mikoa kumi ambayo inagundua wagonjwa wapya kila mwaka. Mikoa hiyo ni pamoja na: Lindi, Rukwa, Mtwara, Morogoro, Pwani; Tanga, Geita, Dodoma, Tabora and Kigoma. 
Aidha, bado zipo wilaya 20 ambazo kiwango cha ukubwa wa tatizo la ukoma kipo juu sana na bado hazijafikia lengo la utokomezaji, nazo ni Liwale, Nkasi, Ruangwa, Nanyumbu, Shinyanga manispaa, Kilombero, Mafia, Pangani, Mvomero, Masasi mjini, Lindi vijijini, Kilwa, Mpanda, Nachingwea, Rufiji, Korogwe, Mkinga, Ulanga, Morogoro vijijini na Chato. 

Ndugu wanahabari,
Takwimu za miaka kumi iliyopita, tangu 2007 hadi 2016, zinaonyesha hapa nchini mwetu watoto wapatao 1,456 waligunduliwa na kutibiwa ukoma. Ugonjwa wa Ukoma miongoni mwa watoto ni dalili ya kuwa bado kuna maambikizi mapya katika baadhi ya maeneo nchini mwetu.  Miongoni mwa hawa, watoto 73  waligunduliwa wakiwa tayari wamepata ulemavu wa kudumu; yaani wakiwa tayari wamekatika baadhi ya viungo vyao na wengine kuhitaji kutumia viungo bandia na kiasi kikubwa kuwa tegemezi maisha yao yote. 

Ndugu wanahabari,
Kauli mbiu katika maadhimisho ya mwaka huu inasema “TOKOMEZA ULEMAVU MIONGONI MWA VIJANA WETU”.  ‘ZERO DISABILITIES IN GIRLS AND BOYS” Kila mmoja wetu anahitajika kushiriki kikamilifu kupambana na ukoma, hususani katika halmashauri ambazo zina wagonjwa wengi na hazijafikia viwango vya utokomezaji. Juhudi zetu tuzielekeze katika kuwagundua wagonjwa mapema wakiwa bado wapo katika hatua za awali za ugonjwa, ili kuzuia maabukizi katika jamii hususan miongoni mwa watoto na vijana wetu kabla ugonjwa haujawa mkubwa na kusababisha ulemavu. 





Ndugu wanahabari,
Dalili ya awali kabisa za ugonjwa wa Ukoma ni baka au mabaka kwenye ngozi yasiyo na hisia na yenye rangi ya shaba. Kwa kawaida hayawashi wala hayaumi. Mabaka haya hukosa hisia ya joto, mguso au maumivu. Dalili nyingine za ukoma ni pamoja na vijinundu (vijifundo) kwenye ngozi hasa usoni na masikioni, uvimbe na maumivu kwenye mishipa ya fahamu, ganzi kwenye mikono na miguu, vidonda au kuungua moto katika mikono na miguu bila kusikia maumivu yoyote,  
Athari za Ukoma ambazo pia watu hufikiri ni dalili ni pamoja na kukatika vidole vya mikono na miguu na upofu; athari hizi ni matokeo ya kuchelewa kuanza matibabu. 


Ndugu wanahabari,
Zipo hatua zinazochukuliwa na serikali yetu ya awamu ya tano kudhibiti ukoma nchini. Hatua hizo ni pamoja na:
Kuendesha   kampeni za uibuaji wa wagonjwa wapya ngazi ya  jamii kwa kuwashirikisha watoa huduma ngazi ya jamii ( Leprosy Elimination Campaigns) hasa katika wilaya zenye kiwango kikubwa cha wagonjwa wa Ukoma,
Utekelezaji wa mpango wa majaribio wa utoaji wa dawa kinga ngazi ya kaya kwa ajili ya kuzuia maambukizi ya ukoma (Leprosy Post-Exposure Prophylaxis). Mpango huu unafanyika katika wilaya za Nanyumbu, Liwale na Kilombero ambapo umeonesha mafanikio makubwa katika kuzuia kuenea kwa ukoma katika jamii,
Utekelezaji wa maazimio ya Bangkok (the Bangkok Declaration Special Fund (BDSF) kwa ajili ya kuhamasisha uibuaji wa wagonjwa wa ukoma mapema na kutatua changamoto wanazokabiliana nazo watu walioathirika na ukoma.  Zoezi hili linatekelezwa kwenye wilaya za Mkinga, Muheza – Tanga na Chato mkoani Geita,
Utekelezaji wa shughuli za kuzuia ulemavu unaotokana na ukoma ikiwemo kutathmini wagonjwa wenye vidonda, kufanya upasuaji maalumu, huduma za kitaalamu za macho, utoaji wa viungo bandia pamoja na viatu maalum,
Kuagiza na kusambaza dawa za kutosha za ugonjwa wa ukoma nchi nzima.
Kutoa elimu kwa umma kuhusu dalili na tiba ya ukoma.


Ndugu wanahabari,
Pamoja na hatua zanazochukuliwa na serikali na mafanikio zipo changamoto.  Miongoni mwa changamoto zinazotukabili ni pamoja na jamii kuendelea kushikilia imani potofu juu ya ukoma kuwa ni ugonjwa wa kurithi au kulogwa na wagonjwa kuchelewa kujitokeza kupata matibabu hadi wanapopata ulemavu. Ukoma ni ugonjwa wa kuambukizwa unaosababishwa na vimelea vinavyoshambulia mishipa ya fahamu na huambukizwa kwa njia ya hewa pekee.

Nitoe rai kwa jamii, wazazi na walezi kuwa sote tujenge tabia ya kuchunguza miili yetu na ya watoto wetu. Endapo utaona mojawapo ya dalili za Ukoma, unashauriwa kwenda kwenye kituo cha tiba kilicho karibu nawe kwa uchunguzi bila kuchelewa. Hii itawawezesha wataalam wa afya kuchunguza na kubainisha kama mgonjwa ana ukoma ili apate tiba sahihi mapema na hivyo kuzuia maambukizi na ulemavu wa kudumu unaoweza kuzuilika.
Tiba ya Ukoma inapatikana nchini kote na hutolewa bila malipo kwa wagonjwa wote. Nirudie tena kuwa, pale tunapoona mabadiliko yoyote yanajitokeza kwemye miili yetu twende mapema katika vituo vyetu vya huduma kuchunguzwa ili tupate matibabu stahili. 

Ndugu wanahabari,
Aidha, napenda kuwashukuru wanahabari,  watoa huduma katika vituo vya afya kwa juhudi wanazofanya kila siku kuhakikisha ugonjwa huu si tatizo la kiafya tena nchini. 

Pia  nachukua nafasi hii kwa niaba ya serikali ya awamu ya tano ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kuyashukuru mashirika mbalimbali ya ndani na nje kama vile Norvatis Foundation ya Uswisi, Germany Leprosy and Tuberculosis Relief Association (GLRA) ya Ujerumani, Nippon Foundation chini ya  Sasakawa Memorial Health Initiative ya Japani na Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa michango yao katika mapambano dhidi ya ugonjwa wa ukoma hapa nchini Tanzania. 

“TOKOMEZA UKOMA KUZUIA ULEMAVU MIONGONI MWA VIJANA WETU”.  

Asanteni sana kwa kunisikiliza.

0 on: "TAMKO KUELEKEA MAADHIMISHO YA SIKU YA UKOMA DUNIANI TAREHE 28/01/2018"