Like us on Facebook

Inaendeshwa na Blogger.

Tafuta katika Blogu Hii

Kumbukumbu la Blogu

Instagram

visitors

display number of visitors

Popular Posts

Pages

Flickr Images

Jumatatu, 27 Novemba 2017

HOTUBA YA MHE. DR FAUSTINE NDUGULILE (MB)






HOTUBA YA MHE. DR FAUSTINE NDUGULILE (MB) NAIBU WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII JINSIA WAZEE NA WATOTO KATIKA MKUTANO WA MWAKA WA MPANGO WA TAIFA WA KUDHIBITI KIFUA KIKUU NA UKOMA TAREHE 27 NOV -1 DISEMBA, 2017 MKOANI DODOMA

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Muhammad Bakari Kambi,
Mkurugenzi wa Kinga Dkt. Neema Rusibamayila,
Naibu Meneja Mpango, Dkt. Liberate Mleoh,
Wadau wa Maendeleo kutoka mashirika mbali mbali ya kitaifa na kimataifa,
Waratibu wa Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua Kikuu na Ukoma ngazi ya Taifa,
Waratibu wa  Kifua kikuu na Ukoma wa Mikoa na wilaya
Wageni wetu waalikwa.
Mabibi na Mabwana
Awali ya yote napenda niwapongeze kwa juhudi zenu za dhati kabisa katika kutekeleza majukumu yenu ili kuhakikisha kuwa magonjwa ya kifua kikuu na ukoma yanadhibitiwa na kuwa si tatizo la kiafya kwa watanzania.
Kama mnavyofahamu tatizo la kifua kikuu katika nchi yetu ni kubwa.  Kwa mujibu wa ripoti ya Shirika la Afya Duniani (WHO) ya kifua kikuu ya mwaka 2017, Tanzania ni miongoni mwa nchi 30 duniani zenye kiwango kikubwa cha ugonjwa wa Kifua kikuu. Inakadiriwa kuwa katika kila watanzania laki moja (100,000) watu mia mbili themanini na saba (287) wanaugua kifua kikuu kwa mwaka. Utafiti wa kutathmini ukubwa wa tatizo la Kifua kikuu nchini uliofanyika mwaka 2012/13 ulibaini kuwa kifua kikuu bado ni tatizo kubwa katika maeneo ya vijijini na kwa wazee wenye umri zaidi ya miaka 60.
Vile vile, kutokana na ripoti ya kifua kikuu ya Shirika la Afya Duniani ya mwaka 2017, Tanzania inakadiriwa kuwa na asilimia 1.3 ya wagonjwa wapya na asilimia 6.2 ya wagonjwa waliokwishatumia dawa za Kifua kikuu wana Kifua kikuu sugu. Takwimu hizi zinaweka makadirio ya kuwepo wagonjwa 830 wa kifua kikuu sugu kwa mwaka 2016. Maambukizi mseto ya Kifua kikuu na UKIMWI ni tatizo kubwa nchini ambapo asilimia 34 ya wagonjwa wa kifua kikuu wana maambukizi ya VVU na asilimia 91 ya wagonjwa hao walianzishiwa dawa za kufubaza VVU (ARV).
Kwa upande wa ugonjwa wa ukoma ni wazi kuwa ukubwa wa tatizo la ukoma unaendelea kupungua. Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) za mwaka 2016 inaonyesha kuwa tuna chini ya mgonjwa mmoja (0.4) katika kila watu 10,000.

Ndugu washiriki,
Miongoni mwa mafanikio katika mapambano dhidi ya kifua kikuu nchini ni kuwa wagonjwa wote wanaoanzishiwa matibabu, asilimia 90 wanapona kabisa, na asilimia 78 kati ya hao wanapatiwa matibabu katika ngazi ya jamii. Vile vile asilimia 71 ya wagonjwa wa Kifua kikuu sugu wanatibiwa na kupona kabisa.
Hata hivyo changamoto kubwa tuliyonayo hapa nchini ni kuweza kuwaibua wagonjwa wote wa Kifua kikuu cha kawaida na Kifua kikuu sugu ambapo kwa takwimu za sasa zinaonyesha kuwa tunashindwa kuwafikia wagonjwa takriban 85,000 wa Kifua kikuu na 600 wa Kifua kikuu sugu kwa mwaka. Vile vile mpaka sasa tumekwishagundua wagonjwa wawili wa kifua kikuu sugu zaidi (XDR-TB) kwa miaka ya 2014 (ameshapona kabisa) na 2017 yuko kwenye matibabu.

NdugU Washiriki
Wizara kupitia Mpango inatekeleza Mpango Mkakati wa miaka mitano wa Kudhibiti Kifua kikuu na Ukoma (2015-2020). Mikakati iliyowekwa ili kukabiliana nazo ni pamoja na:-
·        Kuhakikisha dawa za kutibu Kifua kikuu zinaendelea kupatikana wakati wote na bila malipo yoyote
·        Kuimarisha uwezo wa vituo vya ugunduzi wa Kifua kikuu  kwa kutumia teknolojia mpya ya vipimo kwa kutumia vinasaba vya GeneXpert MTB/RIF,
·        Kuimarisha uwezo wa maabara za kikanda zilizopo Dodoma, (Dodoma Hospitali) Mwanza, (Bugando) Mbeya (Mbeya Rufaa) na Kilimanjaro (Kibong’oto),
·        Kushirikisha sekta binafsi katika mapambano dhidi ya Kifua kikuu ikiwemo maduka ya dawa muhimu, famasi na hospitali binafsi katika kuibua wagonjwa wa Kifua kikuu,
·        Kuimarisha mikakati ya uibuaji wagonjwa wa Kifua kikuu kutoka kwa wachimbaji wadogo wadogo wa madini na jamii zinazowazunguka kwa kushirikiana na wadau mbali mbali,
·        Uboreshaji wa huduma za uibuaji wa wagonjwa kupitia ushirikishwaji wa vitengo vyote katika vituo vya kutolea huduma za afya,
·        Kushirikisha jamii katika kuibua wahisiwa wa Kifua kikuu na Ukoma na kuwapeleka kwenye vituo vya kutolea huduma za afya kwa uchunguzi na tiba
·        Kuimarisha mikakati ya uibuaji watoto wenye maambukizi ya Kifua kikuu na kuanzisha dawa mpya za Kifua kikuu kwa watoto,
·        Kugatua huduma za Kifua kikuu sugu kwa kushirikisha vituo vingine zaidi ya Hospitali ya Magonjwa ya Kuambukiza ya  Kibong’oto na kuanzisha  matibabu ya muda mfupi ya Kifua kikuu sugu kutoka miezi 24 hadi miezi 9,
·        Kuimarisha mfumo wa ukusanyaji wa taarifa za Mpango kwa mfumo wa kielektroniki.
Kwa upande wa ugonjwa wa Ukoma, ni wazi kuwa, ukubwa wa tatizo la ugonjwa huo linapungua kila mwaka na waathirika wengi bado tunawapata wakiwa tayari wamepata ulemavu. Kuna watanzania wenzetu takribani 300 kila mwaka hupata ulemavu wa kudumu utokanao na ukoma; ulemavu huu unazuilika kabisa. Takwimu za Mpango za mwaka 2015 zinaainisha kuwa wilaya ambazo bado zina wagonjwa wengi wa ukoma ni Masasi, Nanyumbu, Namtumbo, Liwale, Ruangwa, Mkinga, Kilombero, Chato na Nkasi.  Hivyo basi ni jukumu letu sote kuongeza juhudi za kupambana na Ukoma kwa kuongeza ubunifu katika kutafuta njia na mbinu mpya za kuhakikisha wagonjwa wanagunduliwa mapema na kupatiwa matibabu kwa wakati.  
Miongoni mwa mafanikio yaliyopatikana katika kudhibiti Ukoma nchini ni pamoja na:
·        Asilimia 95 ya wenye Ukoma hafifu na asilimia 93 ya wenye ukoma mkali walioanzishiwa matibabu walipona kabisa

Ndugu Waratibu,
Nitoe rai kwa mikoa na wilaya kushirikisha wadau wote katika kutekeleza mikakati iliyoainishwa na Mpango ambayo inalenga kutimiza malengo ya kitaifa ya kudhibiti Kifua kikuu kitaifa na kidunia. 
Ni matumaini yangu kwamba mkutano huu utakuwa ni chachu ya kuibua changamoto tulizo nazo, kujifunza kutoka kwa kila mmoja wetu na hivyo basi kuweza kuimarisha mipango na mikakati yetu ili tuwapatie wananchi huduma bora na endelevu. Ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha wagonjwa wenye Kifua kikuu na ukoma wanaibuliwa na kupatiwa matibabu kwa wakati. Kila mtumishi atimize wajibu wake.
Napenda kusisitiza na kuwaasa juu ya utekelezaji bora wa kazi za Mpango na matumizi sahihi ya fedha zinazofadhiliwa na wadau wetu wa maendeleo na kuzitolea taarifa kwa wakati ili kuendana na kasi ya Serikali ya awamu ya tano, yaani “HAPA KAZI TU



Ndugu Waratibu,
Serikali inapenda kuchukua fursa hii kuwashukuru wadau wa maendeleo kama vile Global Fund ATM, Shirika la Afya Duniani (WHO) Serikali ya Marekani kupitia USAID na mashirika yanayotekeleza shughuli za Kifua kikuu nchini kwa juhudi zao za kuisaidia serikali katika kupambana na magonjwa haya. Mchango wenu ni muhimu sana katika kuhakikisha mikakati tuliyojiwekea inatekelezwa kwa ufanisi na  kwa wakati.

Ndugu washiriki, Mabibi na Mabwana
Nichukue fursa hii kutamka kuwa mkutano huu wa Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Kifua kikuu na Ukoma kwa mwaka 2017 umefunguliwa rasmi.
Mungu ibariki Africa Mungu ibariki Tanzania Asanteni kwa kunisikiliza.

0 on: "HOTUBA YA MHE. DR FAUSTINE NDUGULILE (MB)"